Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA 12

Tengenezo Linalotumikia “Mungu wa Amani”

Tengenezo Linalotumikia “Mungu wa Amani”

WAZO KUBWA KATIKA SURA HII

Hatua kwa hatua, Yehova anasaidia watu wake kufuata utaratibu wa tengenezo

1, 2. Katika Mwezi wa 1, 1895, gazeti Munara wa Mulinzi lilifanyiwa mabadiliko gani, na ndugu walisema nini kuhusu jambo hilo?

WAKATI John A. Bohnet, mwanafunzi mwenye bidii, alipata gazeti Munara wa Mulinzi la Mwezi wa 1, 1895, alifurahia sana jambo ambalo aliona juu ya gazeti hilo. Gazeti hilo lilikuwa na jalada mupya lenye maandishi meusi sana, na lilikuwa na picha ambayo inaonyesha munara wenye kuwa na taa juu yake. Munara huo unapatikana juu ya bahari yenye zoruba ya upepo, na taa yake inatuma mwangaza wake katika anga lenye giza. Tangazo katika gazeti hilo kuhusu picha hiyo mupya lilikuwa na kichwa “Vazi Letu Mupya.”

2 Ndugu Bohnet alipendezwa sana, na kwa hiyo, alimuandikia Ndugu Russell barua yenye kusema hivi: “Ni furaha sana kuona namna MUNARA unaonekana vizuri sana. Unapendeza sana.” Ndugu John H. Brown, ambaye alikuwa pia mwanafunzi mwaminifu wa Biblia, aliandika hivi kuhusu jalada hilo: “Ni lenye kuvutia sana. Na musingi wa munara huo unaonekana kuwa nguvu kabisa, hata kama mawimbi na upepo wa zoruba yanaupiga.” Jalada hilo mupya la gazeti lilikuwa ndio badiliko la kwanza ambalo ndugu waliona mwaka huo, lakini ilikuwa ni mwanzo tu. Katika Mwezi wa 11, walijulishwa badiliko lingine kubwa sana. Jambo la kupendeza ni kwamba, badiliko hilo lilizungumuzia pia bahari yenye zoruba.

3, 4. Ni tatizo gani ambalo lilirekebishwa katika gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 15 Mwezi wa 11, 1895, na gazeti hilo lilitangaza mabadiliko gani makubwa?

3 Gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 15 Mwezi wa 11, lilikuwa na habari ndefu ambayo ilionyesha wazi tatizo fulani: Muvurugo ulio kama mawimbi yenye kusukumwa na zoruba kubwa ulikuwa unavuruga amani ambayo ilikuwa katika tengenezo la Wanafunzi wa Biblia. Mabishano kati ya ndugu ili kujua ni nani anastahili kuongoza katika kutaniko yalizidi kuongezeka. Ili kusaidia ndugu waone kwamba ni jambo la maana waondoe roho ya kushindana ambayo inagawanya watu, habari hiyo ya Munara wa Mulinzi ililinganisha tengenezo na mashua. Ilionyesha waziwazi kwamba ndugu ambao wanaongoza wameshindwa kutayarisha tengenezo ambalo linalinganishwa na mashua ambayo inapambana na zoruba ya upepo mukali. Sasa wangepaswa kufanya nini?

4 Habari ya gazeti hilo ilionyesha kwamba katika mashua, kapiteni hapaswe kukosa vyombo ambavyo vinaweza kutumiwa ili kuokoa uzima na kwamba wafanyakazi wa mashua wanapaswa kuwa tayari kufunga milango ya kushuka ndani ya mashua wakati zoruba kali inatokea. Vilevile, ndugu ambao wanaongoza tengenezo walipaswa kuhakikisha kwamba makutaniko yote yametayarishwa ili kupambana na hali ambazo zinafanana na zoruba ya upepo mukali. Ili kutimiza jambo hilo, gazeti hilo lilitangaza mabadiliko makubwa. Lilitoa maagizo kwamba kuanzia mwezi huo, “katika kila kutaniko, wazee wanapaswa kuchaguliwa” ili “kuwa waangalizi wa kundi ao kondoo wa Yehova.”​—Mdo. 20:28.

5. (a) Sababu gani mupango wa kuanza kuwachagua wazee wa kutaniko ilikuwa hatua ya kusonga mbele ambayo ilichukuliwa pa wakati unaofaa? (b) Ni maulizo gani tutachunguza?

5 Mupango huo wa kuanza kuwachagua wazee wa kutaniko ulionekana kuwa ni hatua ambayo ilichukuliwa pa wakati unaofaa. Ulisaidia kuwe na makutaniko yenye nguvu na yenye kutumika kwa utaratibu. Mupango huo ulisaidia ndugu zetu kushinda magumu yaliyo kama mawimbi ambayo yalichochewa na Vita ya Kwanza ya Ulimwengu. Miaka ambayo ilifuata, mabadiliko mengine kuhusu namna ya kuongoza mambo katika tengenezo yalisaidia watu wa Mungu wawe wenye kustahili kumutumikia Yehova vizuri zaidi. Ni unabii gani wa Biblia ulitabiri mabadiliko hayo? Ni mabadiliko gani kuhusu utaratibu wa kuongoza mambo katika tengenezo umejionea? Umepata faida gani kwa sababu ya mabadiliko hayo?

‘Nitatia Amani Kuwa Kama Waangalizi Wako’

6, 7. (a) Andiko la Isaya 60:17 linamaanisha nini? (b) Maneno “waangalizi”na “wagawa-kazi” yanaonyesha nini?

6 Kama tulivyojifunza katika Sura ya 9, nabii Isaya alitabiri kwamba Yehova atabariki watu wake kwa kuwafanya wawe wengi. (Isa. 60:22) Lakini, Yehova aliahidi kwamba atafanya hata zaidi ya hilo. Katika unabii huohuo, alisema hivi: ‘Badala ya shaba nitaingiza zahabu, na badala ya chuma nitaingiza feza, na badala ya miti, shaba, na badala ya mawe, chuma; nami nitaweka amani kuwa [kama] waangalizi wako na uadilifu kuwa [kama] wagawa-kazi wako.’ (Isa. 60:17) Unabii huo unamaanisha nini? Unabii huo unatimia namna gani katika tengenezo leo?

kuweka kitu fulani mahali pa kitu kingine ni mabadiliko. Hata hivyo, unabii huo hauseme kama kitu fulani kibaya kitabadilika na kuwa kizuri. Lakini, kitu fulani kizuri kitakuwa kizuri zaidi

7 Unabii wa Isaya unaonyesha kwamba kitu fulani kingechukua mahali pa kitu kingine. Ni kweli kwamba kuweka kitu fulani mahali pa kitu kingine ni mabadiliko. Hata hivyo, ona kwamba unabii huo hauseme kama kitu fulani kibaya kitabadilika na kuwa kizuri. Lakini, unasema kwamba kitu fulani kizuri kitakuwa kizuri zaidi. Kubadilisha shaba iwe zahabu ni mabadiliko ao maendeleo kabisa. Ni hivyo pia kuhusu mabadiliko ya vile vitu vingine ambavyo vinatajwa katika andiko hilo. Kwa hiyo, kupitia maneno hayo, Yehova alitabiri kwamba hali ya watu wake itabadilika na kuwa muzuri hatua kwa hatua. Unabii huo unazungumuzia mabadiliko ya namna gani? Kwa sababu unabii unataja “waangalizi” na “wagawa-kazi,” Yehova anaonyesha kwamba mabadiliko yatakuja hatua kwa hatua katika namna ambayo watu wake wanatunzwa na kufuata utaratibu wa tengenezo.

8. (a) Ni nani ameleta mabadiliko hayo mazuri ambayo yalitabiriwa katika unabii wa Isaya? (b) Tunapata faida gani kupitia mabadiliko hayo? (Soma kisanduku “ Alikubali kwa Unyenyekevu Kurekebishwa.”)

8 Ni nani amefanya utaratibu huo wa mambo katika tengenezo usonge mbele? Yehova anasema hivi: ‘Nitaingiza zahabu,’ ‘Nitaingiza feza,’ na “Nitatia amani.” Kwa kweli, mabadiliko hayo mazuri kuhusu utaratibu wa tengenezo ambao unapaswa kufuatwa katika makutaniko hayakuletwa na nguvu za wanadamu, lakini na Yehova mwenyewe. Na zaidi sana, tangu Yesu atiwe kuwa Mufalme, Yehova ameleta mabadiliko hayo mazuri kupitia Mwana wake. Tunapata faida gani kupitia mabadiliko hayo? Pia andiko hilo la Isaya linaonyesha kwamba matokeo ya mabadiliko hayo mazuri itakuwa “amani” na “uadilifu [haki].” Wakati tunakubali uongozi wa Mungu na tunafanya mabadiliko, matokeo ni kwamba tutakuwa na amani kati yetu, na kupenda kufanya yaliyo haki kunatuchochea kumutumikia Yehova, ambaye mutume Paulo alisema kwamba ni “Mungu wa amani.”​—Flp. 4:9.

9. Ni nini inapaswa kuwa musingi wa utaratibu na umoja katika kutaniko, na sababu gani?

9 Mutume Paulo aliandika pia juu ya Yehova, hivi: ‘Mungu si Mungu wa muchafuko, bali ni wa amani.” (1 Kor. 14:33) Ona kwamba Biblia haiseme kwamba muchafuko (ao muvurugo) haupatane na utaratibu, lakini inaonyesha kwamba haupatane na amani. Sababu gani? Fikiria jambo hili: Utaratibu tu hauwezi kuleta hali za amani. Fikiria mufano huu, kikundi fulani cha maaskari wanaweza kutembea kwa utaratibu wakati wanaenda kwenye vita. Lakini utaratibu unawaongoza kwenye vita, si kwenye amani. Kwa hiyo, kila mara sisi Wakristo tunapaswa kukumbuka jambo hili: Tengenezo lolote lenye utaratibu ambalo halijengwe juu ya amani hata lifanye siku ngapi mwisho tu litaanguka. Tofauti na hilo, amani ambayo inatoka kwa Mungu inasaidia kuwe na utaratibu ambao unadumu. Kwa hiyo, sisi ni wenye furaha sana kuona kwamba tengenezo letu linaongozwa na kusafishwa na “Mungu anayetoa amani”! (Rom. 15:33) Amani ambayo inatoka kwa Mungu ndio musingi wa utaratibu na umoja ambao tunafurahia sana katika makutaniko duniani pote.—Zab. 29:11.

10. (a) Katika miaka ya mwanzo-mwanzo ni mabadiliko gani ambayo yalifanyika katika tengenezo? (Soma kisanduku “ Maendeleo Katika Namna ya Kuweka Wachungaji.”) (b) Ni maulizo gani ambayo tutachunguza sasa?

10 Kisanduku chenye kichwa “ Maendeleo Katika Namna ya Kuweka Wachungaji,”kinatuonyesha kwa kifupi faida ambazo tulipata kupitia mabadiliko ambayo yalifanywa ili kuwe na utaratibu katika tengenezo katika miaka ya mwanzo-mwanzo. Lakini, ni mabadiliko gani ya ‘feza kuwa zahabu’ ambayo Yehova ameleta kupitia Mufalme wetu hivi karibuni? Namna gani mabadiliko hayo kuhusu waangalizi yalitia nguvu amani na umoja wetu katika makutaniko ya duniani pote? Namna gani mambo hayo mawili yanakusaidia kumutumikia “Mungu wa amani”?

Namna Kristo Anaongoza Kutaniko

11. (a) Kujifunza Maandiko kulisaidia kuelewa jambo gani? (b) Ndugu wa baraza linaloongoza waliazimia kufanya nini?

11 Tangu mwaka wa 1964 mupaka mwaka wa 1971, ndugu wa baraza lenye kuongoza walijifunza sana habari fulani za Biblia, kama vile, habari kuhusu namna kutaniko la Kikristo la wakati wa mitume lilikuwa linafanya kazi. * Kuhusu utaratibu wa kuongoza mambo katika tengenezo, walijifunza kwamba wakati wa mitume makutaniko hayakuwa yanasimamiwa na muzee mumoja ao mwangalizi mumoja, lakini na baraza la wazee. (Soma Wafilipi 1:1; 1 Timotheo 4:14.) Wakati jambo hilo lilieleweka vizuri zaidi, ndugu wa baraza linaloongoza walielewa kwamba ni Mufalme wao, Yesu, ndiye alikuwa anawaongoza ili wafanye mabadiliko kuhusu utaratibu wa kuongoza mambo katika tengenezo la watu wa Mungu, na ndugu hao waliazimia kufuata muongozo wa Mufalme. Mara moja walifanya mabadiliko ili tengenezo lifuate kabisa mupango wa kuwekwa kwa wazee kama vile Biblia inaonyesha. Ni mabadiliko gani fulani yalifanywa mwanzo-mwanzo ya miaka ya 1970?

12. (a) Ni mabadiliko gani ambayo yalifanyika katika baraza linaloongozwa lenyewe? (b) Fasiria namna Baraza Linaloongoza linafanya kazi leo. (Soma kisanduku “ Namna Baraza Linaloongoza Linasimamia Kazi ya Ufalme,” ukurasa wa 130.)

12 Badiliko la kwanza lilianzia kwenye Baraza Lenye Kuongoza lenyewe. Mupaka wakati huo, kikundi cha ndugu hao watiwa-mafuta kilifanyizwa na ndugu saba ambao pia walikuwa ndio kikundi cha viongozi wa shirika la Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania. Lakini, katika mwaka wa 1971, ndugu wengine waliongezwa kwenye Baraza Lenye Kuongoza, na wakawa 11. Tangu wakati huo ndugu wa baraza linaloongoza hawakuwa tena kikundi cha viongozi wa shirika la kisheria la Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania. Hakuna ndugu wa Baraza Lenye Kuongoza ambaye anajiona kuwa wa maana sana kuliko wengine. Pia kila mwaka walianza kubadilishana usimamizi kwa kufuata utaratibu wa herufi ya kwanza ya jina la kila mumoja wao.

13. (a) Ni mupango gani ambao uliendelea kufanya kazi kwa muda wa miaka 40? (b) Katika mwaka wa 1972, ndugu wa Baraza Linaloongoza walifanya nini?

13 Badiliko la pili lilifanyika katika kila kutaniko. Namna gani? Tangu mwaka wa 1932 mupaka mwaka wa 1972, ni ndugu mumoja tu ndiye alikuwa mwangalizi katika kutaniko. Mupaka mwaka wa 1936, mwangalizi huyo alikuwa anaitwa kiongozi wa utumishi (directeur de service). Kisha, jina lilibadilishwa na kuwa mutumishi wa kikundi, kisha akaitwa mutumishi wa kutaniko na mwishowe akaitwa mwangalizi wa kutaniko. Ndugu hao ambao waliwekwa, walihangaikia kwa bidii hali njema ya kiroho ya kundi ao kondoo wa Mungu. Kwa kawaida mwangalizi wa kutaniko alikuwa anafanya maamuzi kuhusu kutaniko bila kuwauliza watumishi wengine wa kutaniko. Lakini, katika mwaka wa 1972, ndugu wa Baraza Linaloongoza walitayarisha njia kwa ajili ya mabadiliko ya maana sana. Ilikuwa ni mabadiliko gani?

14. (a) Mupango gani mupya ulianza kutumika tangu tarehe 1 Mwezi wa 10, 1972? (b) Namna gani kila muratibu wa baraza la wazee anatumikisha shauri lililo katika Wafilipi 2:3?

14 Kuliko kuwa na mwangalizi mumoja tu katika kutaniko, sasa ndugu wengine ambao walitimiza sifa ambazo zinaombwa na Maandiko waliweza pia kuwekwa kuwa wazee kwa kufuata utaratibu wa kiteokrasi. Wote pamoja walifanyiza baraza la wazee ili kuchunga kutaniko la kwao. Mupango huo mupya wa kuwa na baraza la wazee ulianza kutumika kuanzia tarehe 1 Mwezi wa 10, 1972. Leo, muratibu wa baraza la wazee hajione kuwa wa maana sana kuliko wazee wengine, lakini anajiona kuwa ‘mudogo zaidi.’ (Lu. 9:48) Ndugu hao wanyenyekevu ni baraka kabisa kwa ndugu wote duniani pote!—Flp. 2:3.

Ni wazi kwamba, kwa hekima Mufalme wetu amewapatia wafuasi wake wachungaji ambao walihitaji kwa wakati unaofaa

15. (a) Mupango wa kuwa na baraza la wazee katika makutaniko umeleta faida gani? (b) Ni nini inaonyesha kwamba Mufalme wetu anatenda kwa busara?

15 Mupango wa kila muzee kutimiza daraka lake katika baraza la wazee umeonekana kuwa wenye faida kubwa. Fikiria faida hizi tatu: Ya kwanza na ya maana sana, ni kwamba mupango huo unasaidia wazee wote kutambua kwamba Yesu ndiye Kichwa cha kutaniko, hata ikiwa wanatimiza madaraka gani mazito katika kutaniko lao. (Efe. 5:23) Ya pili, andiko la Methali 11:14 linasema hivi: “Kwa wingi wa washauri kuna wokovu [matokeo mazuri].” Kwa hiyo, wakati wazee wanatia mawazo pamoja kuhusu mambo ambayo yanataka kuharibu hali nzuri ya kutaniko na kufikiria mawazo ya kila mumoja, wanasaidiwa kufikia maamuzi ambayo yanapatana na kanuni za Biblia. (Met. 27:17) Maamuzi kama hayo Yehova anayabariki, na yanakuwa na matokeo mazuri. Ya tatu, kwa sababu kuna ndugu wenye kustahili kabisa ambao ni wazee, tengenezo limekuwa na uwezo wa kupambana na ulazima ambao unazidi kuongezeka wa kusimamia na wa uchungaji katika makutaniko. (Isa. 60:3-5) Fikiri kidogo: Katika mwaka wa 1971 tulikuwa na makutaniko zaidi ya 27000. Katika mwaka wa 2013 makutaniko hayo yaliongezeka kufikia hesabu ya makutaniko zaidi ya 113000 hivi! Ni wazi kwamba kwa hekima, Mufalme wetu amewapatia wafuasi wake wachungaji ambao walihitaji kwa wakati unaofaa.—Mika 5:5.

‘Kuwa Mifano kwa Kundi’

16. (a) Wazee wa kutaniko wana daraka gani? (b) Namna gani Wanafunzi wa Biblia walifikiria shauri la Yesu kuhusu ‘kuchunga kondoo’?

16 Huko nyuma katika miaka ya mwanzo-mwanzo ya Wanafunzi wa Biblia, wazee walikuwa wamekwisha kuelewa kwamba wana daraka la kusaidia ndugu wenzao wabaki watumishi wa Mungu. (Soma Wagalatia 6:10.) Katika mwaka wa 1908, gazeti Munara wa Mulinzi lilitoa habari ambayo ilizungumuzia shauri la Yesu, linalosema: “Chunga kondoo wangu wadogo.” (Yoh. 21:15-17) Habari hiyo iliwaambia wazee wa kutaniko hivi: “Ni lazima sana kufikiria sana agizo la Bwana wa kazi la kuchunga kondoo. Tunapaswa kuona kazi ya kulisha na kutunza vizuri wafuasi wa Bwana kuwa ni pendeleo kubwa kabisa.” Katika mwaka wa 1925, gazeti Munara wa Mulinzi lilikazia tena umaana wa kuwa wachungaji kwa kuwakumbusha wazee hivi: “Kanisa la Mungu ni kanisa lake, . . . na atawaomba wote walio na madaraka watoe hesabu juu ya pendeleo lao la kutumikia ndugu zao.”

17. Ni nini imesaidia wazee kuwa wachungaji wenye ufundi ao uwezo?

17 Namna gani tengenezo la Yehova liliwasaidia wazee wageuze ufundi wao wa uchungaji kuwa ‘feza pahali pa chuma’? Tengenezo liliwatolea mazoezi. Katika mwaka 1959, wazee walihuzuria Masomo ya Huduma ya Ufalme ya kwanza kwa ajili ya wazee. Katika kipindi fulani cha masomo hayo walijifunza habari iliyosema: “Kuhangaikia Ndugu Kipekee.” Wazee walitiwa moyo “kuwa na programu ya kutembelea wahubiri nyumbani kwao.” Kipindi hicho kilionyesha njia mbalimbali ambazo wachungaji wanaweza kutumia ili kazi hiyo ya uchungaji iwe yenye kujenga. Katika mwaka wa 1966, Masomo ya Huduma ya Ufalme yenye mambo mapya yalianzishwa. Yalizungumuzia habari iliyosema “Umaana wa Kazi ya Uchungaji.” Ni nini ilikuwa jambo la maana katika kipindi cha masomo hayo? Wazee walijifunza kwamba wale ambao wanaongoza katika kutaniko “wanapaswa kutolea kondoo ao kundi la Mungu musaada ambao linahitaji kwa upendo, bila kusahau watu wa nyumba zao na kazi ya kuhubiri.” Katika miaka ya hivi karibuni, wazee wamehuzuria masomo mengine zaidi. Mazoezi hayo ambayo tengenezo la Yehova limeendelea kutoa, yamekuwa na matokeo gani? Leo, kutaniko la Kikristo lina maelfu ya ndugu wenye kustahili ambao wanafanya kazi ya wachungaji wa kiroho.

Masomo ya Huduma ya Ufalme katika inchi ya Ufilipino, mwaka wa 1966

18. (a) Wazee wamepewa kazi gani nzito? (b) Sababu gani Yehova na Yesu wanawapenda wazee wenye kuchunga kondoo kwa bidii?

18 Mupango wa kuwa na wazee umewekwa na Yehova kupitia Mufalme wetu, Yesu, ili kutimiza kazi fulani nzito. Ni kazi gani hiyo? Ni kazi ya kuongoza kondoo wa Mungu katika kipindi hiki kibaya zaidi cha historia ya wanadamu. (Efe. 4:11, 12; 2 Tim. 3:1) Yehova na Yesu wanawapenda sana wazee ambao wanatumika kwa bidii kwa sababu ndugu hao wanatii shauri la Maandiko ambalo linasema: ‘Mulichunge kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu kwa kupenda, kwa hamu, kwa kuwa vielelezo [mifano] kwa kundi.’ (1 Pet. 5:2, 3) Tuchunguze sasa njia mbili kati ya njia mbalimbali ambazo waangalizi Wakristo ni mifano ya kuiga kwa lile kundi, na namna njia hizo mbili zinasaidia sana kuwe na amani na furaha katika kutaniko.

Namna Wazee Wanachunga Kundi la Mungu Leo

19. Tunajisikia namna gani kuhusu wazee ambao wanatusindikiza katika mahubiri?

19 Njia ya kwanza: Wazee wanatumika pamoja na ndugu katika kutaniko. Muandikaji wa Injili Luka alisema hivi kuhusu Yesu: ‘Akasafiri kutoka muji mupaka muji na kutoka kijiji mupaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Na wale kumi na wawili walikuwa pamoja naye.’ (Lu. 8:1) Kama vile Yesu alihubiri pamoja na mitume wake, wazee ambao ni mifano ya kuiga leo wanatumika pamoja na ndugu wa kutaniko katika kazi ya kuhubiri. Wanaelewa kwamba kwa kufanya hivyo, wanasaidia sana ili kuwe na roho nzuri katika kutaniko. Namna gani ndugu katika kutaniko wanajisikia kuhusu wazee kama hao? Dada mumoja anayeitwa Jeannine, ambaye ana miaka zaidi ya 80, alisema hivi: “Kutumika pamoja na muzee katika utumishi wa shambani kunanipatia nafasi nzuri ya kuzungumuza naye na kumujua vizuri zaidi.” Ndugu Steven, aliye na miaka zaidi ya 30, anasema hivi: “Wakati muzee anatumika pamoja na mimi katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba, ninajisikia kwamba anapenda kunisaidia. Kupata musaada kama huo kunanifanya niwe mwenye furaha sana.”

Kama vile muchungaji anatafuta kondoo aliyepotea, vilevile wazee wanajikaza kutafuta ndugu ambao wameacha kutaniko

20, 21. Namna gani wazee wanaweza kuiga muchungaji anayezungumuziwa katika mufano wa Yesu? Toa mufano. (Soma pia kisanduku “ Kazi ya Uchungaji ya Kila Juma Yenye Matokeo.”)

20 Njia ya pili: Tengenezo la Yehova limewazoeza wazee ili waweze kuhangaikia wale ambao wameacha kutaniko. (Ebr. 12:12) Sababu gani wazee wanapaswa kusaidia ndugu walio wazaifu kiroho, na namna gani wanaweza kuwasaidia? Tutapata jibu kupitia mufano wa Yesu wa muchungaji na kondoo aliyekuwa amepotea. (Soma Luka 15:4-7.) Wakati muchungaji aliona kwamba kondoo moja haonekane katika kondoo wengine, alienda kumutafuta kondoo huyo. Ungefikiri kwamba alikuwa na kondoo huyo tu. Namna gani wazee wa Kutaniko wanaiga mufano wa muchungaji huyo leo? Kama vile muchungaji huyo aliona kondoo aliyekuwa amepotea kuwa kitu cha bei sana machoni pake, ndivyo wazee wanaona wale ambao wameacha kutaniko. Wazee hawapaswe kufikiri kwamba kutafuta na kusaidia wazaifu hao kuwa ni kupoteza wakati. Tena, kama vile muchungaji anaamua ‘kuenda kumutafuta kondoo aliyekuwa amepotea mupaka amupate,’ vilevile wazee wanachukua hatua ya kwanza ya kutafuta na kusaidia wale walio wazaifu.

21 Muchungaji alifanya nini wakati alimupata yule kondoo? Alimukamata polepole na ‘kumuweka kwenye mabega’ na kumurudisha katika kondoo wengine. Vilevile, maneno yenye kutoka katika moyo wa muzee mwenye kuhangaikia wazaifu, yanaweza kumuinua ndugu aliye muzaifu kiroho na kumusaidia arudie katika kutaniko. Hilo ndilo jambo lilimufikia ndugu Victor, ambaye anaishi katika Afrika. Ndugu huyo alikuwa ameacha kutaniko kwa miaka mingi. Anaeleza: “Kwa muda wa miaka munane ambayo sikuwa tena nakusanyika wala kuhubiri, wazee walijaribu kuendelea kunisaidia.” Ni jambo gani kabisa ambalo liligusa moyo wake? Anafasiria: “Siku moja, ndugu John, muzee wa kutaniko ambaye tulihuzuria pamoja Masomo ya Mapainia, alinitembelea na kunionyesha picha fulani ambazo tulikamatwa pamoja wakati wa Masomo hayo ya Mapainia. Picha hizo zilinikumbusha mambo mengi yenye kupendeza sana na nikaanza kukumbuka furaha ambayo nilikuwa nayo wakati nilikuwa ninamutumikia Yehova.” Muda kidogo tu, kisha ndugu John kumutembelea Victor, [Victor] alirudilia tena kutaniko. Leo hii Victor ni painia tena. Kwa kweli, wazee wa kutaniko ambao wanatuhangaikia wanafanya tuwe na furaha sana.​—2 Kor. 1:24. *

Maendeleo Katika Kazi ya Uchungaji Yanasaidia Tuwe na Umoja Wenye Nguvu

22. Namna gani uadilifu na amani vinatia nguvu umoja wa kutaniko la Kikristo? (Soma pia kisanduku “ )Tulishangaa Sana.”)

22 Kama tulivyoona, Yehova alitabiri kwamba watu wake watakuwa na uadilifu (haki) na amani tele katikati yao. (Isa. 60:17) Sifa hizo mbili zinafanya makutaniko yawe na umoja wenye nguvu. Namna gani? Kuhusu haki (ao uadilifu), Biblia inasema kwamba, ‘Mungu ni Yehova mumoja.’ (Kum. 6:4) Kanuni zake za haki zinabadilika kulingana na kutaniko fulani la inchi fulani? Hapana, kanuni zake kuhusu yaliyo sawa na yaliyo makosa ni moja, na ni kanuni zilezile kwa ajili ya “makutaniko yote ya watakatifu.” (1 Kor. 14:33) Kwa hiyo, kutaniko linaweza kuzaa matunda ikiwa tu ndugu wanatii kanuni za Mungu. Kuhusu amani, Mufalme wetu anapenda tuwe na amani katika kutaniko, lakini anapenda pia tuwe watu “wanaofanya amani.” (Mt. 5:9) Kwa hiyo, ‘tunafuatilia mambo yanayofanya kuwe na amani.’ Wakati kunatokea magumu kati yetu tunakuwa wa kwanza kumuendea ndugu ili kumaliza magumu yetu. (Rom. 14:19) Kwa kufanya hivyo, tunasaidia kuwe amani na umoja katika kutaniko.—Isa. 60:18.

23. Sisi watumishi wa Yehova tunafurahia jambo gani leo?

23 Huko zamani katika Mwezi wa 11, 1895, wakati gazeti Munara wa Mulinzi lilitangaza kwa mara ya kwanza mupango wa kuwa na muzee katika kutaniko, ndugu ambao walikuwa wanaongoza walionyesha pia tamaa ya mioyo yao. Ni tamaa gani hiyo? Walitamani sana, na kusali ili mupango huo mupya wa utaratibu wa tengenezo usaidie watu wa Mungu ‘wafikie umoja katika imani.’ Wakati tunaangalia miaka ambayo imepita, sisi ni wenye furaha sana kuona kwamba kazi ya kusafisha ambayo Yehova alifanya kupitia Mufalme wetu kuhusu mambo ya uchungaji katika tengenezo, imetia nguvu umoja wetu katika ibada. (Zab. 99:4) Matokeo ni haya: leo watu wote wa Yehova duniani pote wanafurahi kuona tunatembea “katika roho ileile,” tunafuata “hatua zilezile,” na tunamutumikia “Mungu wa amani” “bega kwa bega.”​—2 Kor. 12:18; soma Sefania 3:9.

^ fu. 11 Matokeo ya kazi ya kutafuta habari ambayo walifanya yalitolewa katika kitabu Auxiliaire pour une meilleure intellingence de la Bible.

^ fu. 21 Soma habari “Wazee wa Kutaniko ‘Ni Wafanyakazi Wenzetu kwa Furaha Yetu,’” ilitolewa katika gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 15 Mwezi wa 1, 2013