Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 13

Wahubiri wa Ufalme Wanapeleka Kesi Mahakamani

Wahubiri wa Ufalme Wanapeleka Kesi Mahakamani

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Kama Yesu alivyotabiri, watu wake wanakabili upinzani kutoka kwa watu wanaotumia sheria kuzuia kazi yao ya kuhubiri

1, 2. (a) Viongozi wa kidini walifanikiwa kufanya jambo gani kuhusu kazi ya kuhubiri, hata hivyo mitume walitendaje? (b) Kwa nini mitume walikataa kutii amri ya kuacha kuhubiri?

NI MUDA mfupi tu baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Kutaniko la Kikristo limeanzishwa majuma machache tu huko Yerusalemu. Shetani anaona huo ndio wakati mwafaka wa kulishambulia kutaniko hilo. Anataka kuliangamiza kabla halijawa imara. Haraka, Shetani apanga njama hivi kwamba viongozi wa kidini wanapiga marufuku kazi ya kuhubiri Ufalme. Hata hivyo, mitume wanaendelea kuhubiri kwa ujasiri, na wanaume na wanawake wengi ‘wanamwamini bwana.’—Mdo. 4:18, 33; 5:14.

Mitume walishangilia “kwa sababu walikuwa wamehesabiwa kuwa wenye kustahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake”

2 Kwa ghadhabu, wapinzani wanawashambulia tena—wakati huu wanawatupa mitume wote gerezani. Hata hivyo, wakati wa usiku, malaika wa Yehova anafungua milango ya gereza, na kufikia mapambazuko mitume walikuwa nje wakihubiri! Wanakamatwa tena na kupelekwa mbele ya watawala, ambao wanawashutumu mitume kwa kuvunja sheria ya kuacha kuhubiri. Mitume wanajibu hivi kwa ujasiri: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” Watawala wanakasirika sana hivi kwamba wanataka “kuwaangamiza” mitume. Lakini kwa wakati huo unaofaa, Gamalieli, mwalimu wa sheria aliyeheshimika sana anawaonya hivi watawala hao: “Jiangalieni . . . Msijiingize katika mambo ya watu hawa, bali waacheni.” Kwa kushangaza, watawala hao wanakubali ushauri huo na kuwaacha mitume waende zao. Wanaume hao waaminifu wanafanya nini? Bila woga, wanaendelea “bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.”—Mdo. 5:17-21, 27-42; Met. 21:1, 30.

3, 4. (a) Shetani amefanikiwa kutumia mbinu gani kwa muda mrefu ili kuwashambulia watu wa Mungu? (b) Tutazungumzia nini katika sura hii na zile mbili zinazofuata?

3 Kesi hiyo ya mahakamani iliyofanywa mwaka wa 33 W.K. ilikuwa ya kwanza kuwasilishwa na wenye mamlaka waliopinga kutaniko la Kikristo, hata hivyo haikuwa ya mwisho. (Mdo. 4:5-8; 16:20; 17:6, 7) Katika nyakati zetu, bado Shetani anawaongoza wapinzani wa ibada safi kuwachochea wenye mamlaka kupiga marufuku kazi yetu ya kuhubiri. Wapinzani wametoa mashtaka mbalimbali dhidi ya watu wa Mungu. Kwanza wanasema tunavuruga amani, yaani, tunafanya fujo. Pili wanasema sisi ni wachochezi; pia, kwamba sisi ni wafanyabiashara, yaani, wachuuzi. Inapofaa, ndugu zetu wameenda mahakamani kuthibitisha mashtaka hayo kuwa ya uwongo. Kesi hizo zimekuwa na matokeo gani? Kesi zilizoamuliwa makumi ya miaka iliyopita zimekuathirije wewe binafsi? Acheni tuchunguze kesi kadhaa ili kuona jinsi ambavyo zimesaidia “katika kutetea na kuithibitisha kisheria habari njema.”—Flp. 1:7.

4 Katika sura hii tutachunguza jinsi ambavyo tumetetea haki yetu ya kuwa na uhuru wa kuhubiri. Sura mbili zinazofuata zitazungumzia baadhi ya hatua za kisheria tulizochukua katika jitihada zetu za kuendelea kutokuwa sehemu ya ulimwengu na kuishi kulingana na viwango vya Ufalme.

Wafanya Fujo—Au Wateteaji Washikamanifu wa Ufalme wa Mungu?

5. Kwa nini wahubiri wa Ufalme walikamatwa mwishoni wa miaka ya 1930, na wale waliokuwa wakiongoza waliamua kuchukua hatua gani?

5 Mwishoni mwa miaka ya 1930, majiji na majimbo nchini Marekani yalitaka kuwalazimisha Mashahidi wa Yehova kuwa na vibali au leseni ili kushiriki katika huduma. Lakini ndugu zetu hawakuomba leseni hizo. Leseni inaweza kufutwa, na waliamini kwamba hakuna serikali iliyokuwa na mamlaka ya kuwazuia Wakristo kutii amri ya Yesu ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme. (Marko 13:10) Kwa sababu hiyo, mamia ya wahubiri wa Ufalme walikamatwa. Kwa hiyo, ndugu waliokuwa wakiongoza katika tengenezo waliamua kwenda mahakamani. Walitaka kuonyesha kwamba serikali ilikuwa imezuia kinyume cha sheria haki ya Mashahidi ya kuabudu kwa uhuru. Katika mwaka wa 1938, kulitukia kisa fulani ambacho kilisababisha kufunguliwa kwa kesi muhimu. Ni nini kilichotukia?

6, 7. Familia ya Cantwell ilikabili jambo gani?

6 Asubuhi ya Jumanne Aprili 26, 1938, Newton Cantwell, mwenye umri wa miaka 60, mke wake, Esther, na watoto wao Henry, Russell, na Jesse—wote watano walikuwa mapainia wa pekee—walienda kuhubiri katika jiji la New Haven, Connecticut. Kwa kweli, walitarajia kukaa huko kwa zaidi ya siku moja. Kwa nini? Walikuwa wamekamatwa mara kadhaa, hivyo walitambua kwamba huenda wangekamatwa tena. Hata hivyo, jambo hilo halikuivunja moyo familia ya Cantwell kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Walitumia magari mawili kufika New Haven. Newton aliendesha gari la familia lililobeba machapisho ya Biblia na gramafoni, na Henry mwenye umri wa miaka 22 aliendesha gari lenye vipaaza-sauti. Kwa kweli, kama walivyotarajia, baada ya saa kadhaa walikamatwa na polisi.

7 Kwanza, Russell, mwenye umri wa miaka 18, alikamatwa, kisha Newton na Esther. Akiwa mbali kidogo, Jesse, mwenye umri wa miaka 16, aliwaona wazazi na ndugu yake wakikamatwa na polisi. Henry alikuwa akihubiri upande mwingine wa mji, hivyo, Jesse aliachwa peke yake. Hata hivyo, alichukua gramafoni yake na kuendelea kuhubiri. Wanaume wawili Wakatoliki walikubali Jesse awachezee hotuba ya Ndugu Rutherford iliyokuwa na kichwa “Maadui.” Lakini walipokuwa wakisikiliza hotuba hiyo, wanaume hao walikasirika sana na wakataka kumpiga Jesse. Kwa upole, aliondoka, lakini baada ya muda mfupi polisi akamkamata. Kwa hiyo, yeye pia alipelekwa rumande. Polisi hawakumfungulia Dada Cantwell mashtaka, lakini walimshtaki Ndugu Cantwell na vijana wake. Hata hivyo, waliachiliwa huru kwa dhamana siku hiyohiyo.

8. Kwa nini mahakama ilimpata Jesse Cantwell na hatia ya kusababisha fujo?

8 Miezi michache baadaye, mnamo Septemba 1938, familia ya Cantwell ilifikishwa mahakamani huko New Haven. Newton, Russell, na Jesse walishtakiwa kwa kosa la kuomba michango bila kuwa na leseni. Licha ya kukata rufaa mara kadhaa katika Mahakama Kuu ya Connecticut, Jesse alipatikana na hatia ya kuwachochea watu wavuruge amani, yaani, alisababisha fujo. Kwa nini? Kwa sababu wale Wakatoliki wawili waliosikiliza hotuba ya Ndugu Rutherford walitoa ushahidi mahakamani kwamba hotuba hiyo ilitukana dini yao na kuwakasirisha. Ili kupinga uamuzi huo usiofaa wa mahakama, ndugu wenye madaraka katika tengenezo walikata rufaa katika Mahakama Kuu ya Marekani, ambayo ndiyo mahakama kuu zaidi katika nchi hiyo.

9, 10. (a) Mahakama Kuu Zaidi ya Marekani ilitoa uamuzi gani katika kesi ya familia ya Cantwell? (b) Tunafaidikaje na uamuzi huo mpaka sasa?

9 Kuanzia Machi 29, 1940, Jaji Mkuu Charles E. Hughes na majaji wenzake nane walisikiliza hoja zilizowasilishwa na Ndugu Hayden Covington, wakili wa Mashahidi wa Yehova. * Wakili wa jimbo la Connecticut alipowasilisha hoja zake ili kuthibitisha kwamba Mashahidi walikuwa wanafanya fujo, jaji mmoja aliuliza hivi: “Je, si kweli kwamba ujumbe ambao Kristo Yesu alitangaza haukupendwa na watu wengi?” Wakili wa jimbo alijibu: “Ni kweli haukupendwa, na, ikiwa nakumbuka vizuri, Biblia yangu inataja pia kilichompata Yesu kwa kutangaza ujumbe huo.” Jibu lake lilifunua mambo mengi sana! Bila kujua, wakili huyo aliwahusianisha Mashahidi na Yesu, na serikali na wale waliomhukumu Yesu. Mei 20, 1940, kwa kauli moja Mahakama hiyo ilitoa uamuzi uliowaunga mkono Mashahidi.

Hayden Covington (mbele, katikati), Glen How (kushoto), na wengine wakiondoka mahakamani baada ya kushinda kesi

10 Uamuzi huo wa Mahakama ulikuwa na faida gani? Haki ya uhuru wa kuabudu ililindwa nchini kote hivi kwamba bunge, serikali za majimbo, au serikali za mitaa hazingeweza kuzuia uhuru wa kidini. Zaidi ya hayo, Mahakama hiyo haikumpata Jesse na ‘hatia ya kuvuruga amani na utulivu.’ Kwa hiyo, uamuzi wa mahakama ulionyesha wazi kwamba Mashahidi wa Yehova hawavurugi amani ya umma. Huo ulikuwa ushindi muhimu sana wa kisheria kwa watumishi wa Mungu! Tunafaidikaje na uamuzi huo mpaka sasa? Mwanasheria ambaye ni Shahidi anasema: “Haki ya uhuru wa kuabudu bila hofu ya kuwekewa vizuizi inatupa nafasi ya kuwaambia watu ujumbe wa tumaini mahali popote tunapoishi.”

Wachochezi—Au Watangazaji wa Kweli?

Trakti Quebec’s Burning Hate for God and Christ and Freedom Is the Shame of All Canada

11. Ndugu zetu nchini Kanada walifanya kampeni gani, na kwa nini?

11 Katika miaka ya 1940, Mashahidi wa Yehova nchini Kanada walikabili upinzani mkali. Hivyo, katika mwaka wa 1946, ili kuwajulisha watu kwamba serikali ilikuwa ikizuia haki ya kuabudu kwa uhuru, ndugu zetu walifanya kampeni ya siku 16 ya kugawa trakti yenye kichwa Quebec’s Burning Hate for God and Christ and Freedom Is the Shame of All Canada (Chuki Kali ya Quebec Kuelekea Mungu, Kristo, na Uhuru, Ni Aibu kwa Kanada Yote). Trakti hiyo yenye kurasa nne ilifunua ghasia zilizochochewa na viongozi wa kidini, ukatili wa polisi, na jeuri za wafanya-ghasia dhidi ya ndugu zetu katika jimbo la Quebec. Trakti hiyo ilisema, “Mashahidi wa Yehova wanaendelea kutiwa mbaroni kinyume cha sheria. Mashtaka karibu 800 yamefunguliwa dhidi ya mashahidi wa Yehova huko Greater Montreal.”

12. (a) Wapinzani walitendaje kampeni ya kusambaza trakti ilipoanza? (b) Ndugu zetu walishtakiwa kwa kosa gani? (Ona pia maelezo ya chini.)

12 Waziri Mkuu wa Quebec, Maurice Duplessis, akishirikiana na Kadinali Villeneuve wa Kanisa Katoliki, waliipinga kampeni hiyo kwa kutangaza “vita visivyo na huruma” dhidi ya Mashahidi. Idadi ya walioshtakiwa iliongezeka haraka kutoka 800 hadi 1,600. Dada mmoja painia alisema, “Polisi walitukamata mara nyingi sana.” Mashahidi ambao walikamatwa wakigawa trakti walishtakiwa kwa kosa la kuchapisha “maandishi yenye uchochezi.” *

13. Ni nani waliokuwa wa kwanza kushtakiwa kwa kosa la uchochezi, na mahakama ilitoa uamuzi gani?

13 Katika mwaka wa 1947, Ndugu Aimé Boucher na binti zake Gisèle, mwenye umri wa miaka 18, na Lucille, mwenye umri wa miaka 11, walikuwa wa kwanza kufikishwa mahakamani kwa mashtaka ya uchochezi. Walikuwa wamegawa trakti ya Quebec’s Burning Hate karibu na shamba lao lililokuwa kwenye milima iliyo kusini ya jiji la Quebec City, lakini ilikuwa vigumu sana kuwazia familia hiyo ikifanya fujo. Ndugu Boucher alikuwa mwanaume mnyenyekevu na mpole aliyelima shamba lake dogo na mara kwa mara alienda mjini kwa gari lake la kukokotwa na farasi. Hata hivyo, familia yake ilikuwa imevumilia baadhi ya mateso ambayo yalitajwa katika trakti hiyo. Hakimu wa mahakama hiyo aliyewachukia Mashahidi, alikataa kukubali ushahidi uliothibitisha kwamba familia ya Boucher haikuwa na hatia. Badala yake, alikubali ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka kwamba trakti hiyo ilichochea uhasama na hivyo familia ya Boucher ilipaswa kupatikana na hatia. Hivyo, kulingana na hakimu huyo, ni hatia kusema ukweli! Aimé na Gisèle walipatikana na hatia ya kusambaza maandishi ya uchochezi, na hata Lucille mwenye umri wa miaka 11, alitupwa gerezani kwa siku mbili. Akina ndugu walikata rufaa katika Mahakama Kuu ya Kanada, ambayo ndiyo mahakama kuu zaidi nchini humo, nayo ikakubali kusikiliza kesi hiyo.

14. Ndugu zetu huko Quebec walitendaje wakati wa miaka ya mateso?

14 Hata hivyo, ndugu na dada zetu huko Quebec waliendelea kuhubiri ujumbe wa Ufalme kwa ujasiri licha ya mashambulizi yasiyokoma na yenye jeuri—na mara nyingi walipata matokeo mazuri sana. Katika kipindi cha miaka minne baada ya kuanza kwa ile kampeni ya kugawa trakti mwaka wa 1946, idadi ya Mashahidi huko Quebec iliongezeka kutoka 300 hadi 1,000! *

15, 16. (a) Mahakama Kuu ya Kanada ilitoa uamuzi gani katika kesi ya familia ya Boucher? (b) Ushindi huo ulikuwa na matokeo gani kwa ndugu zetu na kwa watu wengine?

15 Mnamo Juni 1950, jopo kamili la Mahakama Kuu ya Kanada, lililokuwa na mahakimu tisa, lilisikiliza kesi ya Aimé Boucher. Miezi sita baadaye, Desemba 18, 1950, Mahakama hiyo ilitoa uamuzi uliotuunga mkono. Kwa nini? Ndugu Glen How, wakili wa Mashahidi, alieleza kwamba mahakama ilikubali hoja iliyotolewa na akina ndugu kwamba “uchochezi” unahusisha kuchochea jeuri au uasi dhidi ya serikali. Lakini, trakti hiyo “haikuwa na uchochezi wa aina hiyo na kwa hiyo ilikuwa njia halali ya kujieleza kwa uhuru.” Ndugu How aliongezea hivi: “Nilijionea jinsi ambavyo Yehova alitupatia ushindi.” *

16 Uamuzi huo wa Mahakama Kuu ulikuwa ushindi mkubwa kwa Ufalme wa Mungu. Uliondoa msingi wa kesi nyingine 122 zilizokuwa zinasubiri kusikilizwa ambazo Mashahidi walikuwa wameshtakiwa kwa kosa la kusambaza maandishi ya uchochezi huko Quebec. Zaidi ya hilo, uamuzi huo wa Mahakama ulimaanisha kwamba raia wote wa Kanada na nchi zote za Jumuiya ya Madola sasa walikuwa na uhuru wa kulalamika ikiwa serikali ingetumia vibaya mamlaka yake. Pia ushindi huo wa Quebec ulikomesha mashambulizi ya makanisa na serikali dhidi ya uhuru wa Mashahidi wa Yehova. *

Wachuuzi—Au Watangazaji Wenye Bidii wa Ufalme wa Mungu?

17. Baadhi ya serikali zinajaribu kuzuia kazi yetu ya kuhubiri jinsi gani?

17 Kama ilivyokuwa kwa Wakristo wa karne ya kwanza, watumishi wa Yehova leo “si wachuuzi wa neno la Mungu.” (Soma 2 Wakorintho 2:17.) Hata hivyo, baadhi ya serikali zinajaribu kuzuia huduma yetu kwa kutumia sheria zinazodhibiti biashara. Acheni tuchunguze kesi mbili ambazo zilishughulikia suala la ikiwa Mashahidi wa Yehova ni wachuuzi au wahubiri.

18, 19. Wenye mamlaka nchini Denmark walijaribu jinsi gani kuzuia kazi ya kuhubiri?

18 Denmark. Oktoba 1, 1932, serikali ilipitisha sheria iliyosema kwamba ni kinyume cha sheria kuuza machapisho bila leseni ya uchuuzi. Hata hivyo, ndugu zetu hawakuomba leseni hizo. Siku iliyofuata, wahubiri watano walienda kuhubiri katika mji wa Roskilde, ulio umbali wa zaidi ya kilomita 30 magharibi ya jiji la Copenhagen. Ilipofika jioni, mhubiri mmoja anayeitwa August Lehmann, hakuwepo. Alikuwa amekamatwa kwa sababu ya kuuza bidhaa bila leseni.

19 Desemba 19, 1932, August Lehmann alifikishwa mahakamani. Alikubali kwamba alikuwa akiwapa watu machapisho yanayotegemea Biblia, lakini akakataa kwamba alikuwa mchuuzi. Mahakama ilikubaliana naye. Ilieleza hivi: “Mshtakiwa . . . ana uwezo wa kujitegemeza kifedha, na hajapata faida yoyote ya kifedha wala hana nia ya kupata faida hiyo, badala yake utendaji wake umemfanya apoteze pesa.” Ikiwaunga mkono Mashahidi, mahakama hiyo iliamua kwamba kazi ya Lehmann haipaswi “kuhusianishwa na biashara.” Hata hivyo, wapinzani wa watu wa Mungu walikuwa wameazimia kuzuia kazi ya kuhubiri nchini kote. (Zab. 94:20) Mwendesha-mashtaka wa serikali alikata rufaa katika Mahakama Kuu ya nchi hiyo. Ndugu zetu walifanya nini?

20. Mahakama Kuu ya Denmark ilitoa uamuzi gani, na ndugu zetu walitendaje?

20 Juma lililotangulia kusikilizwa kwa kesi hiyo katika Mahakama Kuu, Mashahidi nchini Denmark waliongeza bidii yao katika kazi ya kuhubiri. Jumanne ya Oktoba 3, 1933, Mahakama Kuu ilitangaza uamuzi wake. Ilikubaliana na uamuzi wa mahakama ya chini kwamba August Lehmann hakuwa amevunja sheria. Uamuzi huo ulimaanisha kwamba Mashahidi wangeendelea kuhubiri kwa uhuru. Ili kumshukuru Yehova kwa ushindi huo wa kisheria, ndugu na dada waliongeza hata zaidi bidii yao ya kuhubiri. Tangu uamuzi huo utolewe, ndugu zetu nchini Denmark wamekuwa wakihubiri bila kizuizi chochote kutoka serikalini.

Mashahidi wenye ujasiri nchini Denmark katika miaka ya 1930

21, 22. Mahakama Kuu ya Marekani ilitoa uamuzi gani katika kesi ya Ndugu Murdock?

21 Marekani. Jumapili Februari 25, 1940, painia anayeitwa Robert Murdock, Jr., na Mashahidi wengine saba walikamatwa walipokuwa wakihubiri katika jiji la Jeannette lililo karibu na Pittsburgh, katika jimbo la Pennsylvania. Walishtakiwa kwa kosa la kutokuwa na leseni ya kugawa machapisho. Alipokata rufaa, Mahakama Kuu ya Marekani ilikubali kusikiliza kesi hiyo.

22 Mei 3, 1943, Mahakama Kuu ilitangaza uamuzi wake, ambao uliwatetea Mashahidi. Mahakama hiyo ilipinga sheria ya kuwa na leseni kwa sababu kufanya hivyo kulikuwa sawa na “kuwatoza watu pesa ili wafurahie haki inayotolewa na Katiba ya serikali.” Mahakama ilibatilisha sheria hiyo ya jiji kwa sababu “ilizuia uhuru wa kusambaza habari na uhuru wa kuabudu.” Alipokuwa akizungumzia maoni ya mahakimu wengi, Jaji William O. Douglas alisema kwamba kazi ya Mashahidi wa Yehova “inahusisha mengi zaidi ya kuhubiri; inahusisha mengi zaidi ya kugawanya machapisho ya kidini. Inahusisha mambo yote mawili.” Aliongezea hivi: “Kazi hiyo ya kidini ina umuhimu sawa . . . na ibada inayofanywa makanisani na mahubiri yanayofanywa jukwaani.”

23. Kwa nini ushindi wa mahakamani wa mwaka wa 1943 ni muhimu sana kwetu leo?

23 Uamuzi huo wa Mahakama Kuu ulikuwa ushindi muhimu sana wa kisheria kwa watu Mungu. Ulithibitisha wazi kwamba sisi ni wahudumu wa Kikristo, na si wafanyabiashara. Katika siku hiyo ya kukumbukwa mwaka wa 1943, Mashahidi wa Yehova walishinda kesi 12 kati ya kesi 13 katika Mahakama Kuu, kutia ndani kesi ya Murdock. Uamuzi huo wa mahakama umekuwa kielelezo cha kufuatwa katika kesi za karibuni ambazo wapinzani wamepinga tena haki yetu ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme hadharani na nyumba kwa nyumba.

“Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala Kuliko Wanadamu”

24. Tunatendaje serikali zinapopiga marufuku kazi yetu ya kuhubiri?

24 Tukiwa watumishi wa Yehova, tunathamini sana serikali zinapotupatia haki ya kisheria ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme kwa uhuru. Hata hivyo, serikali inapopiga marufuku kazi yetu ya kuhubiri, tunabadili mbinu zetu na kuendelea kuhubiri kwa njia yoyote ile. Kama mitume walivyofanya, “lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Mdo. 5:29; Mt. 28:19, 20) Wakati huohuo, tunakata rufaa mahakamani ili marufuku dhidi ya kazi yetu iondolewe. Fikiria mifano miwili.

25, 26. Ni matukio gani yaliyofanya kesi iwasilishwe katika Mahakama Kuu nchini Nikaragua, na kulikuwa na matokeo gani?

25 Nikaragua. Novemba 19, 1952, Donovan Munsterman mmishonari na mtumishi wa tawi alienda katika Ofisi ya Uhamiaji iliyo Managua, mji mkuu wa Nikaragua. Alikuwa ameagizwa aende kumwona Kapteni Arnoldo García, msimamizi wa ofisi hiyo. Kapteni huyo alimwambia Donovan kwamba Mashahidi wa Yehova nchini Nikaragua walikuwa “wamekatazwa kuendelea kuhubiri mafundisho yao na kuendeleza shughuli zao za kidini.” Alipoulizwa sababu, Kapteni García alieleza kwamba Mashahidi hawakuwa na kibali cha kuhubiri kutoka serikalini na ilidaiwa kwamba walikuwa wakomunisti. Ni nani waliotoa madai hayo? Viongozi wa Kanisa Katoliki.

Akina ndugu nchini Nikaragua wakati wa marufuku

26 Mara moja, Ndugu Munsterman alikata rufaa katika Wizara ya Dini na pia kwa Rais Anastasio Somoza García, lakini rufaa hiyo haikukubaliwa. Kwa hiyo, akina ndugu walibadili mbinu yao. Walifunga Jumba la Ufalme, wakaanza kukutanika kwenye vikundi vidogo, na wakaacha mahubiri ya barabarani, lakini bado walihubiri ujumbe wa Ufalme. Wakati huohuo, walituma ombi katika Mahakama Kuu ya Nikaragua wakitaka Mahakama hiyo itoe amri ya kuondolewa kwa marufuku hiyo. Magazeti ya habari yaliripoti marufuku hiyo na ombi hilo, na Mahakama Kuu ilikubali kusikiliza kesi hiyo. Kukawa na matokeo gani? Juni 19, 1953, Mahakama Kuu ilichapisha uamuzi uliokubaliwa kwa kauli moja uliowaunga mkono Mashahidi. Mahakama iligundua kwamba marufuku hiyo ilikuwa ikivunja haki ya kikatiba ya uhuru wa kusema, dhamiri, na uhuru wa kufuata imani ya kidini. Pia iliamuru kwamba uhusiano kati ya serikali ya Nikaragua na Mashahidi urudishwe kama ulivyokuwa awali.

27. Kwa nini watu wa Nikaragua walishangazwa na uamuzi wa Mahakama, na ndugu walikuwa na maoni gani kuhusu ushindi huo?

27 Wananchi wa Nikaragua walishangaa kwamba Mahakama Kuu iliwatetea Mashahidi. Kabla ya kesi hiyo, viongozi wa kidini walikuwa na uvutano mkubwa sana hivi kwamba Mahakama iliogopa kuzozana nao. Pia, maofisa wa serikali walikuwa na mamlaka kubwa hivi kwamba ilikuwa nadra sana kwa Mahakama kupinga maamuzi yao. Ndugu zetu walikuwa na uhakika kwamba walishinda kesi hiyo kwa sababu walipata ulinzi kutoka kwa Mfalme wao na pia kwa sababu waliendelea kuhubiri.—Mdo. 1:8.

28, 29. Ni badiliko gani lililotukia nchini Zaire katikati ya miaka ya 1980?

28 Zaire. Katikati ya miaka ya 1980, kulikuwa na Mashahidi 35,000 hivi katika nchi ya Zaire, ambayo sasa ni Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Ili kushughulikia kazi ya Ufalme iliyokuwa ikiongezeka kwa kasi, ofisi ya tawi ilikuwa ikijenga majengo mapya. Mnamo Desemba 1985, kusanyiko la kimataifa lilifanywa katika mji mkuu, Kinshasa, na wajumbe 32,000 kutoka sehemu mbalimbali za ulimwengu walijaa kwenye uwanja wa jiji hilo. Lakini hali ya watumishi wa Yehova ilianza kubadilika. Ni nini kilichotukia?

29 Ndugu Marcel Filteau, mmishonari kutoka Quebec, Kanada, ambaye aliteswa wakati wa utawala wa Duplessis, alikuwa akitumikia Zaire wakati huo. Alisimulia yaliyotukia: “Machi 12, 1986, ndugu waliokuwa wakiongoza walipokea barua iliyosema kwamba shirika la Mashahidi wa Yehova la Zaire halikuwa halali.” Marufuku hiyo ilitiwa sahihi na aliyekuwa rais wa nchi hiyo, Mobutu Sese Seko.

30. Halmashauri ya Tawi ilihitaji kufanya uamuzi gani mzito, na iliamua kufanya nini?

30 Siku iliyofuata redio ya taifa ilitangaza hivi: “Huu ndio mwisho wa Mashahidi wa Yehova nchini [Zaire].” Mara moja wakaanza kuteswa. Majumba ya Ufalme yaliharibiwa, na ndugu zetu walinyang’anywa mali zao, wakakamatwa, wakafungwa na kupigwa. Hata watoto wa Mashahidi waliwekwa gerezani. Oktoba 12, 1988, serikali ilitaifisha mali za tengenezo letu, na kikosi cha jeshi kiliishi kwenye majengo ya ofisi ya tawi. Ndugu waliokuwa wakiongoza walikata rufaa kwa Rais Mobutu, lakini hawakujibiwa. Wakati huo Halmashauri ya Tawi ilihitaji kufanya uamuzi mzito, “Je, tukate rufaa katika Mahakama Kuu au tusubiri?” Timothy Holmes, ambaye alikuwa mmishonari na mratibu wa Halmashauri ya Tawi wakati huo, anasema hivi, “Tulimwomba Yehova atupe hekima na mwongozo.” Baada ya kusali na kujadiliana, Halmashauri ya Tawi iliona kwamba huo haukuwa wakati unaofaa wa kuchukua hatua za kisheria. Badala yake, walikazia fikira kuwaimarisha akina ndugu na kutafuta mbinu za kuendeleza kazi ya kuhubiri.

“Wakati wa kesi hiyo, tuliona jinsi ambavyo Yehova anaweza kubadili mambo”

31, 32. Mahakama Kuu ya Zaire ilifanya uamuzi gani wenye kushangaza, na ulikuwa na matokeo gani kwa ndugu zetu?

31 Miaka kadhaa ilipita. Mateso dhidi ya Mashahidi yakapungua, na watu wakaanza kuheshimu haki za binadamu nchini humo. Halmashauri ya Tawi iliona kwamba huo ulikuwa wakati unaofaa wa kukata rufaa katika Mahakama Kuu ya Sheria ya Zaire ili kupinga marufuku hiyo. Jambo la kushangaza ni kwamba Mahakama Kuu ilikubali kusikiliza kesi hiyo. Kisha, Januari 8, 1993, karibu miaka saba baada ya rais kuamuru marufuku hiyo, Mahakama iliamua kwamba uamuzi wa serikali dhidi ya Mashahidi ulikuwa kinyume cha sheria na marufuku hiyo ikaondolewa. Hebu wazia jambo hilo! Mahakimu hao walihatarisha maisha yao kwa kufutilia mbali amri ya rais wa nchi! Ndugu Holmes anasema hivi: “Wakati wa kesi hiyo, tuliona jinsi ambavyo Yehova anaweza kubadili mambo.” (Dan. 2:21) Ushindi huo uliimarisha imani ya ndugu zetu. Walihisi kwamba Mfalme, Yesu, alikuwa amewaongoza watu wake kujua wakati na jinsi ya kuchukua hatua.

Mashahidi katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wanafurahia kumwabudu Yehova kwa uhuru

32 Marufuku ilipoondolewa, ofisi ya tawi iliruhusiwa kuleta wamishonari, kujenga majengo mapya ya ofisi ya tawi, na kuingiza nchini machapisho yanayotegemea Biblia. * Ni shangwe iliyoje kwa watumishi wa Mungu ulimwenguni pote kuona jinsi ambavyo Yehova analinda hali ya kiroho ya watu wake!—Isa. 52:10.

“Yehova Ni Msaidizi Wangu”

33. Tunajifunza nini kwa kuchunguza kifupi kesi kadhaa?

33 Kujikumbusha baadhi ya kesi za kisheria kunathibitisha kwamba Yesu ametimiza ahadi yake: “Nitawapa ninyi kinywa na hekima, ambayo wapinzani wenu wote wakiwa pamoja hawataweza kushindana nayo wala kubisha.” (Soma Luka 21:12-15.) Nyakati nyingine, Yehova amewatumia akina Gamalieli wa siku hizi kuwalinda watu wake au amewaongoza mahakimu na wanasheria wenye ujasiri watetee haki. Yehova amezifanya silaha za wapinzani wetu kuwa butu. (Soma Isaya 54:17.) Upinzani hauwezi kuzuia kazi ya Mungu.

34. Kwa nini ushindi tuliopata ni wa pekee sana, na hilo linathibitisha nini? (Ona pia sanduku “ Ushindi Muhimu Katika Mahakama Kuu Ambao Ulisaidia Kuhubiriwa kwa Ufalme.”)

34 Kwa nini ushindi mbalimbali wa kesi tuliopata ni wa pekee sana? Fikiria jambo hili: Mashahidi wa Yehova si watu mashuhuri wala hawana uvutano mkubwa. Hatupigi kura, hatuungi mkono kampeni za kisiasa, au kuwashawishi viongozi wa kisiasa. Isitoshe, Mashahidi ambao wamepeleka kesi katika mahakama kuu wanaonekana kuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Mdo. 4:13) Hivyo, kwa maoni ya kibinadamu, mahakama hazina sababu ya kutusaidia kwa kutoa uamuzi unaowapinga wapinzani wetu wenye nguvu kidini na kisiasa. Hata hivyo, mara nyingi mahakama zimetoa uamuzi unaotuunga mkono! Ushindi wetu unathibitisha kwamba tunatembea “machoni pa Mungu, kwa kushirikiana na Kristo.” (2 Kor. 2:17) Hivyo basi, kama mtume Paulo, tunatangaza hivi: “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa.”—Ebr. 13:6.

^ fu. 9 Kesi hiyo ya Cantwell v. State of Connecticut (Cantwell Dhidi ya Jimbo la Connecticut) ilikuwa ya kwanza kati ya kesi 43 zilizowasilishwa katika Mahakama Kuu ya Marekani ambazo Ndugu Hayden Covington angekuwa wakili wa akina ndugu. Alikufa mwaka wa 1978. Mjane wake, Dorothy, alibaki mwaminifu hadi kifo mwaka wa 2015 akiwa na umri wa miaka 92.

^ fu. 12 Mashtaka hayo yalitegemea sheria iliyotungwa mwaka wa 1606. Iliruhusu wasaidizi wa mahakama kumtia mtu hatiani ikiwa walihisi kwamba maneno yake yalichochea uhasama—hata kama yalikuwa ya kweli.

^ fu. 14 Mwaka wa 1950, kulikuwa na watumishi wa wakati wote 164 huko Quebec—kutia ndani wahitimu wa Gileadi 63 waliokubali kwa hiari mgawo wa kwenda huko licha ya kujua kwamba wangepata upinzani mkali.

^ fu. 15 Ndugu W. Glen How alikuwa wakili jasiri, ambaye kuanzia mwaka wa 1943 hadi mwaka wa 2003, alitumia ustadi mkubwa kuwasaidia Mashahidi wa Yehova kushinda kesi nyingi sana nchini Kanada na katika nchi nyingine.

^ fu. 16 Kwa habari zaidi kuhusu kesi hiyo, ona makala “Vita Si Yenu Bali Ni ya Mungu” katika gazeti Amkeni! la Aprili 22, 2000, ukurasa wa 18-24.

^ fu. 32 Mwishowe kikosi cha jeshi kiliyahama majengo ya ofisi ya tawi; hata hivyo majengo mapya yalijengwa katika eneo lingine.