Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 15

Kupigania Uhuru wa Kuabudu

Kupigania Uhuru wa Kuabudu

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Jinsi ambavyo Kristo amewasaidia wafuasi wake wapiganie kutambuliwa kisheria na haki ya kutii sheria za Mungu

1, 2. (a) Ni nini kinachothibitisha uraia wako wa Ufalme wa Mungu? (b) Kwa nini nyakati fulani Mashahidi wa Yehova wamelazimika kupigania uhuru wa ibada?

JE, WEWE ni raia wa Ufalme wa Mungu? Ukiwa Shahidi wa Yehova, bila shaka wewe ni raia! Na ni nini kinachothibitisha uraia wako? Si pasipoti, wala hati nyingine ya serikali. Badala yake, uraia wako unathibitishwa na jinsi unavyomwabudu Yehova Mungu. Ibada ya kweli inahusisha mengi zaidi ya yale unayoamini. Inahusisha yale unayofanya, yaani, utii wako kwa sheria za Ufalme wa Mungu. Kwetu sote, ibada yetu inagusa kila sehemu ya maisha yetu, kutia ndani namna tunavyolea watoto wetu na tunavyotenda tunapokabili masuala fulani ya afya.

2 Hata hivyo, si kila mara ulimwengu tunamoishi huheshimu uraia wetu wenye thamani au matakwa yake. Baadhi ya serikali zimejaribu kuzuia ibada yetu au hata kuifutilia mbali. Nyakati fulani, raia wa Kristo wamelazimika kupigania uhuru wao ili waishi kupatana na sheria za Mfalme wa Kimasihi. Je, hilo linashangaza? Hapana. Katika nyakati za Biblia, mara nyingi watu wa Yehova walilazimika kupigania uhuru wao wa kumwabudu Yehova.

3. Watu wa Mungu walipigania jambo gani katika siku za Malkia Esta?

3 Kwa mfano, katika siku za Malkia Esta, watu wa Mungu walilazimika kupigana ili waendelee kuishi. Kwa nini? Hamani, Waziri Mkuu aliyekuwa mwovu alipendekeza kwa Mfalme Ahasuero wa Uajemi kwamba Wayahudi wote wanaoishi chini ya utawala wa mfalme wauawe kwa sababu “sheria zao ni tofauti na zile za watu wengine wote.” (Esta 3:8, 9, 13) Je, Yehova aliwaacha watumishi wake? Hapana. Alibariki jitihada za Esta na Mordekai walipomsihi mfalme wa Uajemi awalinde watu wa Mungu.—Esta 9:20-22.

4. Tutachunguza nini katika sura hii?

4 Namna gani leo? Kama tulivyoona katika sura iliyotangulia, nyakati nyingine, serikali zimewapinga Mashahidi wa Yehova. Katika sura hii, tutazungumzia baadhi ya njia ambazo serikali hizo zimejaribu kutumia ili kuzuia ibada yetu. Tutakazia sehemu tatu: (1) haki yetu ya kutambuliwa tukiwa tengenezo na haki yetu ya kuchagua jinsi tutakavyoabudu, (2) uhuru wetu wa kuchagua matibabu yanayopatana na kanuni za Biblia, na (3) haki ya wazazi ya kulea watoto kulingana na viwango vya Yehova. Katika kila sehemu, tutaona jinsi ambavyo raia washikamanifu wa Ufalme wa Kimasihi wamepambana kishujaa ili kulinda uraia wao wenye thamani na jinsi ambavyo jitihada zao zimebarikiwa.

Kupigania Kutambuliwa Kisheria na Kupewa Uhuru wa Msingi

5. Kutambuliwa kisheria kuna manufaa gani kwa Wakristo wa kweli?

5 Je, tunahitaji kutambuliwa kisheria na serikali za wanadamu ili tumwabudu Yehova? Hapana. Hata hivyo, kutambuliwa kisheria kunafanya iwe rahisi kuendeleza ibada yetu—kwa mfano, kukutana kwa uhuru kwenye Majumba yetu ya Ufalme na Majumba yetu ya Kusanyiko, kuchapisha na kuingiza nchini machapisho yanayotegemea Biblia, na kuwahubiria jirani zetu habari njema waziwazi, pasipo kizuizi chochote. Katika nchi nyingi, Mashahidi wa Yehova wamesajiliwa kisheria na wanafurahia uhuru uleule wa kuabudu ambao wafuasi wa dini nyingine zinazotambuliwa kisheria wanafurahia. Hata hivyo, ni nini ambacho kimetokea wakati ambapo serikali zimekataa kututambua kisheria au kujaribu kuzuia uhuru wetu wa msingi?

6. Mashahidi wa Yehova nchini Australia walikabili hali gani ngumu katika miaka ya 1940?

6 Australia. Mapema katika miaka ya 1940, gavana mkuu wa Australia aliona mafundisho yetu kuwa yana “ubaguzi” kuelekea vita. Hivyo tukapigwa marufuku. Mashahidi hawakuweza kukutana na kuhubiri waziwazi, Betheli ilifungwa, na Majumba ya Ufalme yakatwaliwa. Ilikuwa kosa kuwa na machapisho yetu yanayotegemea Biblia. Baada ya kuendeleza utendaji wao kwa siri kwa miaka kadhaa, mwishowe Mashahidi wa Australia walipata kitulizo. Juni 14, 1943, Mahakama Kuu ya Australia iliondoa marufuku hiyo.

7, 8. Eleza jitihada za kupigania uhuru wa kuabudu ambazo ndugu zetu nchini Urusi wamefanya kwa miaka mingi.

7 Urusi. Mashahidi wa Yehova walikuwa chini ya marufuku ya Kikomunisti kwa makumi ya miaka lakini hatimaye walisajiliwa mwaka wa 1991. Baada ya kuvunjika kwa ule uliokuwa Muungano wa Sovieti, tulitambuliwa kisheria katika Shirikisho la Urusi mwaka wa 1992. Hata hivyo, baada ya muda mfupi, baadhi ya wapinzani—hasa wale walioshirikiana na Kanisa Othodoksi la Urusi—walianza kuingiwa na wasiwasi kwa sababu ya idadi yetu iliyokuwa ikiongezeka kwa kasi sana. Wapinzani walifungua mashtaka matano ya jinai dhidi ya Mashahidi wa Yehova kati ya mwaka wa 1995 na 1998. Kila wakati, mwendesha-mashtaka hakupata uthibitisho wowote wa kosa. Watu hao walioazimia kutupinga walifungua kesi ya madai katika mwaka wa 1998. Mwanzoni, Mashahidi walishinda kesi hiyo, lakini wapinzani walikata rufaa dhidi ya uamuzi huo na Mashahidi wakashindwa katika rufaa hiyo Mei 2001. Kesi ilianza kusikilizwa upya mwezi Oktoba mwaka huohuo, na katika mwaka wa 2004, uamuzi ulifikiwa wa kufutilia mbali shirika lililosajiliwa kisheria ambalo Mashahidi wanatumia jijini Moscow na kupiga marufuku utendaji wake.

8 Wimbi la mateso lilifuata. (Soma 2 Timotheo 3:12.) Mashahidi walinyanyaswa na kushambuliwa. Mashahidi walinyang’anywa machapisho yao ya kidini; na wakazuiliwa kujenga au kukodi mahali pa ibada. Hebu wazia jinsi ndugu na dada zetu walivyohisi walipokabili hali hiyo ngumu! Mashahidi walikuwa wamepeleka kesi yao katika Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR) mwaka wa 2001, na wakawasilisha habari zaidi katika Mahakama hiyo mwaka wa 2004. Mnamo mwaka wa 2010, ECHR ilifikia uamuzi wake. Mahakama hiyo iliona waziwazi kwamba chuki ya kidini ndiyo iliyosababisha Urusi iwapige marufuku Mashahidi na iliamua kwamba hakukuwa na sababu ya kuunga mkono maamuzi ya mahakama za chini, kwani hakukuwa na uthibitisho wowote kwamba Mashahidi wamefanya makosa. Mahakama hiyo ilisema kwamba marufuku hiyo ilikusudiwa kuwanyang’anya Mashahidi haki zao za kisheria. Uamuzi wa Mahakama ulitetea haki ya Mashahidi ya kuwa na uhuru wa kidini. Ingawa serikali ya Urusi haijatekeleza uamuzi wa ECHR, watu wa Mungu katika nchi hiyo wamepata ujasiri mkubwa kutokana na ushindi huo.

Titos Manoussakis (Ona fungu la 9)

9-11. Nchini Ugiriki, watu wa Yehova wamejitahidi jinsi gani kupata uhuru wa kuabudu pamoja, na kumekuwa na matokeo gani?

9 Ugiriki. Katika mwaka wa 1983, Titos Manoussakis alikodi chumba kimoja katika jiji la Heraklion, Krete, ili kikundi kidogo cha Mashahidi wa Yehova kikutane hapo kwa ajili ya ibada. (Ebr. 10:24, 25) Hata hivyo, baada ya muda mfupi, kasisi mmoja wa Othodoksi alipeleka malalamiko yake polisi, akipinga chumba hicho kutumiwa na Mashahidi kwa ajili ya ibada. Kwa nini? Kwa sababu tu imani ya Mashahidi ni tofauti na ile ya Kanisa Othodoksi! Polisi walimfungulia mashtaka Titos Manoussakis na Mashahidi wengine watatu wa eneo hilo. Walitozwa faini na kuhukumiwa kifungo cha miezi miwili gerezani. Wakiwa raia washikamanifu wa Ufalme wa Mungu, Mashahidi waliona uamuzi huo wa mahakama kuwa ulikiuka uhuru wao wa kuabudu, hivyo wakapeleka kesi yao katika mahakama nyingine nchini humo na hatimaye wakaipeleka ECHR.

10 Mwishowe, mwaka wa 1996, Mahakama hiyo ilitoa uamuzi ambao wapinzani wa ibada safi hawakutazamia. Mahakama hiyo ilieleza kwamba “kulingana na sheria ya Ugiriki, Mashahidi wa Yehova wanafafanuliwa kuwa ‘dini inayojulikana’” na kwamba uamuzi wa mahakama za chini “ulikiuka moja kwa moja uhuru wao wa ibada.” Mahakama hiyo iliendelea kusema kwamba haukuwa wajibu wa serikali ya Ugiriki “kuamua ikiwa mafundisho ya dini au njia ambayo dini inatumia kueleza imani hiyo ni halali.” Hukumu dhidi ya Mashahidi ikabatilishwa, na uhuru wao wa ibada ukatetewa!

11 Je, ushindi huo ulisuluhisha mambo nchini Ugiriki? Inasikitisha kwamba haikuwa hivyo. Katika mwaka wa 2012, kesi kama hiyo ambayo ilichukua karibu miaka 12, mwishowe ilisuluhishwa katika mji wa Kassandreia, Ugiriki. Katika kesi hiyo upinzani ulianzishwa na askofu wa Othodoksi. Baraza la Serikali, ambalo ndilo mahakama ya juu zaidi ya Ugiriki, ilisuluhisha jambo hilo kwa kuwapa ushindi watu wa Mungu. Uamuzi huo ulitaja kwamba katiba ya Ugiriki inawapa watu uhuru wa kidini na kupinga dai linalotolewa mara kwa mara kwamba Mashahidi wa Yehova ni dini isiyojulikana. Mahakama hiyo ilisema hivi: “Mafundisho ya ‘Mashahidi wa Yehova’ hayajafichwa na, kwa hiyo, yanaonyesha wazi kwamba wao ni dini inayojulikana.” Washiriki wa kutaniko dogo katika mji wa Kassandreia wanashangilia kwamba sasa wanaweza kukutana kwa ajili ya ibada katika Jumba lao la Ufalme.

12, 13. Nchini Ufaransa, wapinzani wamejaribu jinsi gani kutunga “matatizo kwa njia ya amri,” na kukawa na matokeo gani?

12 Ufaransa. Baadhi ya wapinzani wa watu wa Mungu wametumia mbinu ya ‘kutunga matatizo kwa njia ya amri.’ (Soma Zaburi 94:20.) Kwa mfano, katika miaka ya 1990, idara ya utozaji kodi nchini Ufaransa ilianza kukagua mapato ya Association Les Témoins de Jéhovah (ATJ), mojawapo ya mashirika ya kisheria ambayo Mashahidi wa Yehova wanatumia nchini Ufaransa. Waziri wa bajeti alifunua kusudi halisi la ukaguzi huo: “Ukaguzi huo unaweza kusababisha tuombe agizo la mahakama ili kuuza mali zote za shirika hilo na kulipa deni, au lifunguliwe mashtaka ya uhalifu . . . , ambayo huenda yakadhoofisha utendaji wa shirika au kukomesha utendaji wake katika eneo letu.” Ingawa matokeo ya ukaguzi huo yalionyesha kwamba hakuna kosa lolote lililofanywa, idara ya utozaji kodi ilitoza shirika la ATJ kodi kubwa sana. Ikiwa mbinu hiyo ingefanikiwa, basi ingebidi ndugu zetu wafunge ofisi ya tawi na kuuza majengo ili kulipa kodi hiyo kubwa sana. Lilikuwa pigo kubwa sana, lakini watu wa Mungu hawakukata tamaa. Mashahidi hao walipinga kwa nguvu zote uamuzi huo usio wa haki, mwishowe mwaka wa 2005, walipeleka kesi hiyo ECHR.

13 Mahakama hiyo ilitoa uamuzi wake Juni 30, 2011. Ilieleza kwamba haki ya kuwa na uhuru wa kidini inapaswa kuizuia serikali, isipokuwa katika visa vigumu zaidi, kuchunguza kwa undani uhalali wa imani za kidini au jinsi imani hizo zinavyoonyeshwa. Zaidi ya hilo, Mahakama hiyo ilieleza hivi: “Kodi hiyo . . . ingekomesha mapato muhimu ya shirika hilo na hivyo kuwazuia wafuasi wake kufanya ibada yao kwa uhuru na njia inayofaa.” Mahakama hiyo ilifikia uamuzi kwa kauli moja ambao uliwaunga mkono Mashahidi wa Yehova! Mashahidi wa Yehova walifurahi sana serikali ya Ufaransa iliporudisha kodi iliyolitoza shirika la ATJ pamoja na riba na, kutekeleza agizo la Mahakama kwa kurudisha mali ya ofisi ya tawi ambayo serikali ilikuwa inamiliki.

Unaweza kusali kwa ukawaida kwa ajili ya ndugu na dada zako wa kiroho ambao wanateseka kwa sababu ya ukosefu wa haki za kisheria

14. Unaweza kushiriki jinsi gani katika kupigania uhuru wa ibada?

14 Kama Esta na Mordekai wa zamani, watu wa Yehova leo wanapigania uhuru wa kumwabudu Yehova kwa njia ambayo ameamuru. (Esta 4:13-16) Je, unaweza kushiriki katika mapambano hayo? Ndiyo. Unaweza kusali kwa ukawaida kwa ajili ya ndugu na dada zako wa kiroho ambao wanateseka kwa sababu ya ukosefu wa haki za kisheria. Sala hizo zinaweza kuwa msaada wenye nguvu sana kwa ndugu na dada zetu walio chini ya hali ngumu na mateso. (Soma Yakobo 5:16.) Je, Yehova anajibu sala hizo? Ushindi tunaopata mahakamani unaonyesha kwamba kwa kweli anafanya hivyo!—Ebr. 13:18, 19.

Uhuru wa Kuchagua Matibabu Yanayopatana na Imani Yetu

15. Ni mambo gani ambayo watu wa Mungu huzingatia kuhusiana na matumizi ya damu?

15 Kama tulivyoona katika Sura ya 11, raia wa Ufalme wa Mungu wamepokea mwongozo wa Maandiko ulio wazi kuhusu kuepuka matumizi mabaya ya damu, ambayo yamekuwa jambo la kawaida sana leo. (Mwa. 9:5, 6; Law. 17:11; soma Matendo 15:28, 29.) Ingawa hatukubali kutiwa damu mishipani, kadiri inavyowezekana tunataka matibabu bora zaidi kwa ajili yetu na wapendwa wetu maadamu matibabu hayo hayapingani na sheria za Mungu. Mahakama za juu za mataifa mengi zimetambua kwamba watu wana haki ya kuchagua au kukataa matibabu wakiongozwa na dhamiri na imani yao ya kidini. Hata hivyo, katika baadhi ya nchi, watu wa Mungu wamekabili hali ngumu kuhusiana na jambo hilo. Fikiria mifano kadhaa.

16, 17. Dada mmoja nchini Japani alipata matibabu gani ambayo yalimshtua sana, na sala zake zilijibiwa jinsi gani?

16 Japani. Misae Takeda, mwanamke mwenye umri wa miaka 63 nchini Japani, alihitaji kufanyiwa upasuaji mkubwa. Akiwa raia mshikamanifu wa Ufalme wa Mungu, alimweleza waziwazi daktari wake kwamba alitaka matibabu yasiyohusisha damu. Hata hivyo, miezi mingi baadaye, alishtuka alipojua kwamba alikuwa ametiwa damu mishipani wakati wa upasuaji. Akihisi kwamba alidanganywa na haki zake kukiukwa, Dada Takeda alifungua kesi dhidi ya madaktari na hospitali hiyo Juni 1993. Mwanamke huyo mpole na mnyenyekevu alikuwa na imani thabiti. Alitoa ushahidi kwa ujasiri mbele ya mahakama iliyokuwa imejaa watu, na akasimama kizimbani kwa zaidi ya saa moja licha ya kwamba alikuwa dhaifu kiafya. Alifika mahakamani kwa mara ya mwisho mwezi mmoja tu kabla ya kifo chake. Je, hatuvutiwi na ujasiri na imani yake? Dada Takeda alisema kwamba siku zote alimwomba Yehova abariki pambano lake. Alikuwa na uhakika kwamba sala zake zingejibiwa. Je, zilijibiwa?

17 Miaka mitatu baada ya kifo cha Dada Takeda, Mahakama Kuu ya Japani ilifikia uamuzi ambao ulimuunga mkono—ilikubali kwamba lilikuwa kosa kumtia damu mishipani kinyume na maagizo yake hususa. Uamuzi uliofanywa Februari 29, 2000, ulieleza kwamba “haki ya kuamua” katika visa kama hivyo “lazima iheshimiwe kama haki za kibinafsi.” Kwa sababu ya jitihada za Dada Takeda za kupigania uhuru wa kuchagua matibabu yanayopatana na dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia, sasa Mashahidi nchini Japani wanaweza kutibiwa bila woga wa kutiwa damu mishipani kwa lazima.

Pablo Albarracini (Ona fungu la 18 to 20)

18-20. (a) Mahakama moja ya rufaa nchini Argentina iliungaje mkono haki mtu ya kukataa kutiwa damu mishipani kupitia mwelekezo wa kitiba? (b) Kuhusu matumizi mabaya ya damu, tunaweza kuonyesha jinsi gani ujitiisho kwa uongozi wa Kristo?

18 Argentina. Raia wa Ufalme wanaweza kujitayarisha jinsi gani iwapo uamuzi kuhusu matibabu unahitaji kufanywa wakiwa katika hali ya kupoteza fahamu? Kama Pablo Albarracini alivyofanya, tunaweza kubeba hati yetu ya kisheria ambayo itazungumza kwa niaba yetu. Mnamo Mei 2012, Pablo alipigwa risasi mara kadhaa na watu waliokuwa wakijaribu kuiba eneo fulani. Alilazwa hospitalini akiwa amepoteza fahamu kwa hiyo hangeweza kueleza msimamo wake kuhusiana na suala la kutiwa damu mishipani. Hata hivyo, alikuwa na kadi yake ya mwelekezo wa kitiba ambayo alikuwa amejaza kikamili na kutia sahihi miaka minne mapema. Ingawa hali yake ilikuwa mbaya na baadhi ya madaktari walihisi kwamba ili kuokoa uhai wake, lazima atiwe damu mishipani, madaktari hao walikuwa tayari kuheshimu maagizo yake. Hata hivyo, baba ya Pablo, ambaye hakuwa Shahidi wa Yehova, alitafuta agizo la mahakama ili kubatilisha maagizo ya mwana wake.

19 Wakili aliyemwakilisha mke wa Pablo alikata rufaa mara moja. Baada ya saa chache, mahakama ya rufaa ilibatilisha agizo la mahakama hiyo ya chini na kuamuru kwamba maagizo ya mgonjwa, kama yalivyoelezwa kwenye kadi ya mwelekezo wa kitiba, yanapaswa kuheshimiwa. Baba ya Pablo alikata rufaa katika Mahakama Kuu ya Argentina. Hata hivyo, Mahakama Kuu haikuona “sababu ya kutilia shaka kwamba [maelezo ya Pablo yaliyo kwenye kadi ya mwelekezo wa kitiba ambayo aliagiza kwamba asitiwe damu mishipani] yaliandikwa akiwa na ufahamu, kusudi na uhuru.” Mahakama hiyo ilieleza hivi: “Kila mtu mzima ana uwezo wa kutoa maelekezo mapema kuhusu afya [yake], na anaweza kukubali au kukataa aina fulani ya matibabu . . . Daktari anayemtibu anapaswa kufuata maelekezo hayo.”

Je, umejaza kadi yako ya mwelekezo wa kitiba?

20 Sasa Ndugu Albarracini amepona kabisa. Yeye na mke wake wanafurahi kwamba alikuwa amejaza kadi hiyo ya mwelekezo wa kitiba. Kwa kuchukua hatua hiyo rahisi—lakini muhimu—alionyesha kwamba anajitiisha chini ya Kristo, Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Je, wewe na familia yako mmejaza kadi hiyo?

April Cadoreth (Ona fungu la 21 hadi 24)

21-24. (a) Mahakama Kuu ya Kanada ilitoa uamuzi gani usio wa kawaida kuhusu vijana na matumizi ya damu? (b) Kesi hiyo inaweza kuwatiaje moyo vijana wanaomtumikia Yehova?

21 Kanada. Kwa ujumla, mahakama zinatambua kwamba wazazi wana haki ya kuamua matibabu bora kwa ajili ya watoto wao. Nyakati nyingine, mahakama zimeamua kwamba uamuzi wa vijana waliokomaa kuhusiana na matibabu unapaswa kuheshimiwa. Ndivyo ilivyokuwa kwa April Cadoreth. Akiwa na umri wa miaka 14, April alilazwa hospitali kwa sababu alikuwa anavuja sana damu ndani ya mwili. Miezi michache mapema, alikuwa amejaza kadi ya Mwelekezo wa Mapema Kuhusu Tiba iliyokuwa na maagizo hususa kwamba asitiwe damu mishipani hata katika hali ya dharura. Daktari aliyekuwa akimtibu aliamua kupuuza maagizo yaliyo wazi ya April na akatafuta agizo la mahakama ili amtie damu mishipani. Alitiwa mishipani pakiti tatu za damu bila hiari yake. Baadaye April alililinganisha tukio hilo na kubakwa.

22 April na wazazi wake walifungua kesi mahakamani ili kupata haki. Baada ya miaka miwili, kesi hiyo ilipelekwa katika Mahakama Kuu ya Kanada. Ingawa April alishindwa kesi hiyo ya kutetea haki zake za kikatiba, Mahakama hiyo iliamuru hospitali ilipe gharama za kesi hiyo na kufikia uamuzi uliomuunga mkono yeye na vijana wengine ambao wanataka kutumia haki yao ya kujiamulia matibabu watakayopewa. Mahakama hiyo ilieleza hivi: “Inapohusu matibabu, vijana wenye umri usiozidi miaka 16 wanapaswa kuruhusiwa kutoa maoni yao kuhusu uamuzi wa matibabu fulani hususa ili kuonyesha kwamba wana kiasi fulani cha uhuru wa kufikiri na wamekomaa.”

23 Kesi hiyo ni muhimu katika maana ya kwamba Mahakama ya Juu ilizungumzia haki za kikatiba za vijana. Kabla ya uamuzi huo, mahakama yoyote nchini Kanada ilikuwa na uwezo wa kuidhinisha matibabu ya mtoto mwenye umri usiozidi miaka 16, maadamu mahakama iliona kwamba matibabu hayo yalikuwa kwa manufaa ya mtoto huyo. Lakini baada ya uamuzi huo, mahakama haiwezi kuidhinisha matibabu ya aina yoyote kwa ajili ya vijana wenye umri usiozidi miaka 16 pasipo kwanza kuwapa nafasi ya kuonyesha kwamba wamekomaa vya kutosha kujifanyia maamuzi.

“Kujua kwamba nilishiriki kwa kiasi fulani kulitukuza jina la Mungu na kumthibitisha Shetani kuwa mwongo kumenifanya niwe na furaha sana”

24 Je, kesi hiyo iliyochukua miaka mitatu ilikuwa na manufaa yoyote? Kulingana na maoni ya April, “Ndiyo!” Sasa akiwa painia wa kawaida na mwenye afya nzuri, anasema hivi: “Kujua kwamba nilishiriki kwa kiasi fulani kulitukuza jina la Mungu na kumthibitisha Shetani kuwa mwongo kumenifanya niwe na furaha sana.” Kisa cha April kinaonyesha kwamba vijana wetu wanaweza kuwa na msimamo thabiti, wakijithibitisha wenyewe kuwa raia wa kweli wa Ufalme wa Mungu.—Mt. 21:16.

Uhuru wa Kulea Watoto Kulingana na Viwango vya Yehova

25, 26. Ni hali gani ambayo nyakati fulani inatokea wazazi wanapotalikiana?

25 Yehova amewapa wazazi wajibu wa kulea watoto wao kulingana na viwango vyake. (Kum. 6:6-8; Efe. 6:4) Mgawo huo ni mgumu, lakini huenda ukawa mgumu zaidi wazazi wanapotalikiana. Maoni kuhusu namna ya kuwalea watoto yanaweza kutofautiana kabisa. Kwa mfano, mzazi ambaye ni Shahidi anaona kwamba mtoto anapaswa kulelewa kulingana na viwango vya Kikristo, lakini mzazi asiye Shahidi huenda asikubaliane na maoni hayo. Bila shaka, mzazi ambaye ni Shahidi anapaswa kutambua kwa heshima kwamba ingawa huenda talaka ikavunja uhusiano wa wenzi wa ndoa, uhusiano wa mzazi na mtoto unabaki.

26 Huenda mzazi ambaye si Shahidi akaiomba mahakama impe haki ya kulea mtoto au watoto ili adhibiti malezi yao ya kidini. Baadhi ya watu wanadai kwamba kulelewa kama Shahidi wa Yehova kuna madhara. Huenda wakasema kwamba watoto hao hawatasherehekea siku ya kuzaliwa na sikukuu nyingine, na wanapohitaji matibabu ya dharura, hawatatiwa damu mishipani ili “kuokoa uhai.” Jambo la kupendeza ni kwamba mahakama nyingi zinazingatia masilahi ya mtoto badala ya kuamua kwa kutegemea ikiwa dini ya mzazi ina madhara. Acheni tuchunguze mifano kadhaa.

27, 28. Mahakama Kuu ya Ohio ilishughulikiaje dai lililotolewa kwamba kumlea mtoto kama Shahidi wa Yehova kunamdhuru?

27 Marekani. Katika mwaka wa 1992, Mahakama Kuu ya Ohio iliendesha kesi ambayo baba mmoja ambaye si Shahidi wa Yehova alidai kwamba kulelewa kama Shahidi wa Yehova kungemdhuru mvulana wake. Mahakama ya chini ilikubaliana naye, hivyo ikampa baba huyo haki ya kumlea. Mama wa mvulana huyo, Jennifer Pater, alipewa haki ya kumtembelea, lakini aliagizwa kwamba “asimfundishe mtoto huyo imani za Mashahidi wa Yehova kwa njia yoyote ile.” Agizo hilo la mahakama ya chini lilihusisha mambo mengi sana kwani lingeweza kumaanisha kwamba Dada Pater hangeweza hata kuzungumza na mwanaye, Bobby, kuhusu Biblia au viwango vyake vya maadili! Je, unaweza kuwazia jinsi alivyohisi? Jennifer alifadhaika sana, lakini anasema kwamba alijifunza kuwa na subira na kumngojea Yehova atende. Anasema hivi, “Siku zote Yehova alikuwa pamoja nami.” Wakili wake, akisaidiwa na tengenezo la Yehova, alikata rufaa katika Mahakama Kuu ya Ohio.

28 Mahakama hiyo ilipinga uamuzi wa mahakama ya chini, na kusema kwamba “wazazi wana haki ya msingi ya kuwaelimisha watoto wao, kutia ndani haki ya kuwafundisha maadili na viwango vya dini.” Mahakama hiyo ilieleza kwamba mahakama ya chini haikuwa na haki ya kumnyima mzazi haki ya kulea kwa sababu ya dini isipokuwa kuwe na uthibitisho kwamba viwango vya maadili vya Mashahidi wa Yehova vingemdhuru mtoto huyo kimwili na kiakili. Mahakama hiyo haikupata ushahidi wowote unaothibitisha kwamba imani ya dini ya Mashahidi inaweza kuathiri vibaya afya ya kiakili na ya kimwili ya mtoto huyo.

Mahakama nyingi zimewaunga mkono wazazi Wakristo na kuwapa haki ya kulea watoto wao

29-31. Kwa nini dada mmoja nchini Denmark alinyang’anywa haki ya kumlea binti yake, na Mahakama Kuu Zaidi ya Denmark iliamua nini kuhusu jambo hilo?

29 Denmark. Anita Hansen alikabiliana na tatizo kama hilo wakati mume wake wa zamani alipoomba mahakama impe haki ya kumlea Amanda, mtoto wao mwenye umri wa miaka saba. Ingawa katika mwaka wa 2000 mahakama ya wilaya ilimpa Dada Hansen haki ya kumlea, baba ya Amanda alikata rufaa katika mahakama ya juu, ambayo ilibatilisha uamuzi wa mahakama ya wilaya na akapewa haki ya kumlea mtoto huyo. Mahakama hiyo ilieleza kwamba kwa kuwa wazazi hao walikuwa na maoni yanayopingana kuhusu maisha kwa sababu ya mafundisho yao ya kidini, baba angefaa zaidi kuamua dini atakayolelewa binti yao. Hivyo, Dada Hansen alipoteza haki ya kumlea Amanda kwa sababu ya kuwa Shahidi wa Yehova!

30 Alipokuwa akipitia hali hiyo ngumu, nyakati fulani Dada Hansen alifadhaika sana hivi kwamba hakujua asali kuhusu nini. Anasema hivi: “Lakini, maneno yaliyo kwenye Waroma 8:26 na 27 yalinifariji sana. Siku zote niliona kwamba Yehova alielewa kile nilichomaanisha. Siku zote alinitazama na hajawahi kuniacha.”—Soma Zaburi 32:8; Isaya 41:10.

31 Dada Hansen alikata rufaa katika Mahakama Kuu Zaidi ya Denmark. Katika uamuzi wake, Mahakama hiyo ilieleza hivi: “Suala kuhusu malezi linapaswa kuamuliwa hasa baada ya kuchanganua masilahi ya mtoto.” Isitoshe, Mahakama hiyo ilisema kwamba uamuzi kuhusu haki ya kumlea mtoto unapaswa kuamuliwa kwa kutegemea jinsi ambavyo mzazi anashughulikia matatizo, na si kwa msingi wa “mafundisho na msimamo” wa Mashahidi wa Yehova. Dada Hansen alifurahi sana Mahakama hiyo ilipotambua kwamba yeye ni mzazi mzuri na kumrudishia haki ya kumlea Amanda.

32. Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu imewalinda jinsi gani wazazi Mashahidi dhidi ya ubaguzi?

32 Nchi mbalimbali barani Ulaya. Katika visa fulani, kesi kuhusu masuala ya kulea watoto zimepelekwa katika mahakama za kimataifa baada ya mahakama kuu za nchi kutoa uamuzi usiofaa. Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR) imeshughulikia suala hilo pia. Katika visa viwili, Mahakama ya ECHR ilikubali kwamba mahakama za chini katika nchi mbalimbali zilikuwa zimewatendea kwa njia tofauti wazazi Mashahidi na wasio Mashahidi kwa msingi wa dini. Mahakama hiyo ilisema kwamba huo ulikuwa ubaguzi, na ikaamua kwamba “uamuzi unaotolewa ukitegemea tofauti za kidini tu haukubaliki.” Mama mmoja Shahidi ambaye alinufaishwa na uamuzi huo wa Mahakama ya ECHR alieleza hivi, “Niliumia sana niliposhtakiwa kwa kuwadhuru watoto wangu, kwani mimi niliona kwamba nilikuwa nikiwapa mafunzo bora zaidi, yaani, kuwalea wawe Wakristo.”

33. Wazazi Mashahidi wanaweza kutumiaje kanuni ya Wafilipi 4:5?

33 Bila shaka, wazazi Mashahidi wanajitahidi kuwa na usawaziko wanapokabili matatizo ya kisheria yanayohusu haki zao za kukazia viwango vya Biblia katika mioyo ya watoto wao. (Soma Wafilipi 4:5.) Kama vile wanavyothamini kupewa haki ya kuwazoeza watoto wao katika njia ya Mungu, wao pia wanatambua kwamba mzazi asiye Shahidi, ana haki ya kutimiza wajibu wake akiwa mzazi kama angependa kufanya hivyo. Mzazi ambaye ni Shahidi anaonaje jukumu lake la kumzoeza mtoto?

34. Wazazi Wakristo leo wanaweza kunufaika jinsi gani kutokana na mfano wa Wayahudi wa siku za Nehemia?

34 Tunajifunza jambo fulani kutokana na mfano mmoja katika siku za Nehemia. Wayahudi walifanya kazi kwa bidii ili kurekebisha na kujenga kuta za Yerusalemu. Walijua kwamba kufanya hivyo kungewalinda wao na familia zao dhidi ya maadui waliowazunguka. Kwa sababu hiyo, Nehemia aliwahimiza hivi: “Mpigane kwa ajili ya ndugu zenu, wana wenu na binti zenu, wake zenu na nyumba zenu.” (Neh. 4:14) Wayahudi hao walikuwa na sababu nzuri ya kupigana. Vivyo hivyo leo, wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova wanajitahidi sana kuwalea watoto wao katika njia ya kweli. Wanajua kwamba watoto wao wanakabiliwa na uvutano mwingi sana usiofaa shuleni na katika ujirani. Huenda uvutano huo ukapenya nyumbani kupitia vyombo vya habari. Wazazi, msisahau kamwe kwamba mna kila sababu ya kupigana kwa ajili ya wana na binti zenu ili kuwaandalia mazingira salama ambayo yatawasaidia wasitawi kiroho.

Uwe na Hakika Kwamba Yehova Atategemeza Ibada ya Kweli

35, 36. Mashahidi wa Yehova wamepata manufaa gani kwa sababu ya kupigania haki zetu za kisheria, na wewe umeazimia kufanya nini?

35 Bila shaka, Yehova amebariki jitihada za tengenezo lake leo za kupigania haki ya kuabudu kwa uhuru. Kwa kupigania haki zao za kisheria, mara nyingi watu wa Mungu wametoa ushahidi mkubwa mahakamani na ushahidi mkubwa hata zaidi kwa watu wote. (Rom. 1:8) Faida nyingine ya ushindi huo mwingi wa kisheria ni kwamba umelinda haki za raia wengi ambao si Mashahidi. Hata hivyo, tukiwa watu wa Mungu, hatubadili mfumo wa kijamii; wala kujitetea kana kwamba tumefanya makosa. Zaidi ya yote, Mashahidi wa Yehova wamepigania haki zao za kisheria mahakamani ili kuthibitisha na kuendeleza ibada safi.—Soma Wafilipi 1:7.

36 Na tusipuuze kamwe yale tunayojifunza kutokana na imani ya wale ambao wamepigania uhuru wa kumwabudu Yehova! Acheni sisi pia tubaki waaminifu, tukiwa na hakika kwamba Yehova anaitegemeza kazi yetu na anaendelea kutupa nguvu ya kufanya mapenzi yake.—Isa. 54:17.