Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 16

Kukusanyika Pamoja kwa Ajili ya Ibada

Kukusanyika Pamoja kwa Ajili ya Ibada

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Kuchunguza historia na umuhimu wa mikutano yetu

1. Wanafunzi walipokusanyika pamoja walipata msaada gani, na kwa nini walihitaji msaada huo?

MUDA mfupi baada ya Yesu kufufuliwa, wanafunzi wake walikusanyika pamoja ili kutiana moyo. Hata hivyo, walifunga milango kwa sababu ya kuogopa maadui wao. Woga wao ulitoweka Yesu alipotokea katikati yao na kuwaambia: “Pokeeni roho takatifu”! (Soma Yohana 20:19-22.) Baadaye, mitume walikusanyika tena pamoja, na Yehova akawamiminia roho takatifu. Walipata nguvu za kufanya kazi ya kuhubiri iliyokuwa mbele yao!—Mdo. 2:1-7.

2. (a) Yehova anatupatia nguvu jinsi gani, na kwa nini tunahitaji nguvu hizo? (b) Kwa nini mpango wa Ibada ya Familia ni muhimu sana? (Ona maelezo ya chini na sanduku “ Ibada ya Familia,” ukurasa wa 175.)

2 Tunakabiliana na hali ileile ambayo ndugu zetu wa karne ya kwanza walikabili. (1 Pet. 5:9) Nyakati nyingine, huenda baadhi yetu tukaogopa wanadamu. Na tunahitaji nguvu ambazo Yehova hutoa ili tuvumilie katika kazi ya kuhubiri. (Efe. 6:10) Yehova hutoa kiasi kikubwa cha nguvu hizo kupitia mikutano yetu. Leo tuna fursa ya kuhudhuria mikutano miwili kwa juma—Mkutano wa Watu Wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi, na Mkutano wa katikati ya juma unaoitwa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo. * Pia, tunafurahia matukio manne kila mwaka—kusanyiko la eneo, makusanyiko mawili ya mzunguko, na Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Kwa nini ni muhimu tuhudhurie mikutano hiyo yote? Mikutano ya siku za kisasa ilianzaje? Na mtazamo wetu kuhusu mikutano unafunua nini kutuhusu?

Kwa Nini Tukusanyike Pamoja?

3, 4. Yehova anataka watu wake wafanye nini? Toa mifano.

3 Tangu zamani Yehova amewataka watu wake wakusanyike pamoja ili kumwabudu. Kwa mfano, katika mwaka wa 1513 K.W.K. Yehova alilipa taifa la Israeli Sheria yake, na Sheria hiyo ilitia ndani Sabato ya kila juma ili kwamba kila familia iweze kumwabudu na kufundishwa Sheria hiyo. (Kum. 5:12; 6:4-9) Waisraeli walipofuata amri hiyo, familia ziliimarishwa na taifa lote kwa ujumla lilibaki likiwa safi na imara kiroho. Taifa hilo lilipokataa kufuata Sheria, na kupuuza matakwa kama vile kukusanyika kwa ukawaida ili kumwabudu Yehova, walipoteza kibali cha Mungu.—Law. 10:11; 26:31-35; 2 Nya. 36:20, 21.

4 Fikiria pia mfano ambao Yesu aliweka. Alikuwa na desturi ya kwenda katika sinagogi kila juma siku ya Sabato. (Luka 4:16) Baada ya Yesu kufa na kufufuliwa, wanafunzi wake waliendelea na desturi ya kukusanyika pamoja kwa ukawaida licha ya kwamba hawakuwa tena chini ya sheria ya Sabato. (Mdo. 1:6, 12-14; 2:1-4; Rom. 14:5; Kol. 2:13, 14) Kwenye mikutano hiyo, Wakristo wa karne ya kwanza walifundishwa na kutiwa moyo, na pia walimtolea Mungu dhabihu za sifa kupitia sala, maelezo yao, na nyimbo.—Kol. 3:16; Ebr. 13:15.

Wanafunzi wa Yesu walikusanyika pamoja ili kuimarishana na kutiana moyo

5. Kwa nini tunahudhuria mikutano ya kila juma na makusanyiko ya kila mwaka? (Ona pia sanduku “ Makusanyiko ya Kila Mwaka Ambayo Huwaunganisha Watu wa Mungu,” ukurasa wa 176.)

5 Sisi pia, tunapohudhuria mikutano yetu ya kila juma, makusanyiko ya kila mwaka, tunaonyesha kwamba tunaunga mkono Ufalme wa Mungu, tunatiwa nguvu na roho takatifu, na kuwatia moyo wengine kwa maelezo yanayoonyesha imani yetu. Jambo muhimu zaidi ni kwamba tuna fursa ya kumwabudu Yehova kupitia sala zetu, maelezo, na nyimbo. Utaratibu wa mikutano yetu huenda ukawa tofauti na ule ambao Waisraeli na Wakristo wa karne ya kwanza walifuata, lakini mikutano yetu ina umuhimu uleule. Mikutano yetu ya siku za kisasa ilianzaje?

Mikutano ya Kila Juma Ambayo Huchochea “Upendo na Matendo Mazuri”

6, 7. (a) Mikutano yetu ina kusudi gani? (b) Mikutano ilitofautianaje kati ya kikundi kimoja na kingine?

6 Ndugu Charles Taze Russell alipoanza kuitafuta kweli katika Neno la Mungu, aliona umuhimu wa kukusanyika pamoja na wale waliokuwa na lengo kama lake. Mwaka wa 1879, Russell aliandika hivi: “Mimi, pamoja na wale nilioshirikiana nao huko Pittsburgh, tulipanga na kuendeleza darasa la biblia kwa ajili ya kuchunguza Maandiko, tukikusanyika kila Jumapili.” Wasomaji wa Zion’s Watch Tower walitiwa moyo wakusanyike pamoja, na kufikia mwaka wa 1881, mikutano ilikuwa ikifanywa huko Pittsburgh, Pennsylvania, kila Jumapili na Jumatano. Toleo la Novemba 1895 la Mnara wa Mlinzi lilisema kwamba kusudi la mikutano hiyo ilikuwa kusitawisha “ushirika wa Kikristo, upendo na ushirikiano” na wale waliohudhuria walipata fursa ya kutiana moyo.—Soma Waebrania 10:24, 25.

7 Kwa miaka mingi, utaratibu na mara ambazo mikutano hiyo ilifanywa zilitofautiana kati ya kikundi kimoja cha Wanafunzi wa Biblia na kingine. Kwa mfano, barua iliyoandikwa na kikundi kimoja nchini Marekani ambayo ilichapishwa mwaka wa 1911 ilisema hivi: “Tunafanya angalau mikutano mitano kila juma.” Walifanya mikutano hiyo siku za Jumatatu, Jumatano, Ijumaa, na mara mbili siku ya Jumapili. Barua nyingine kutoka kikundi kimoja barani Afrika iliyochapishwa mwaka wa 1914 ilisema hivi: “Tunafanya mikutano mara mbili kwa mwezi, tunaanza Ijumaa na kumaliza Jumapili.” Hata hivyo, baadaye, utaratibu tunaofuata leo katika mikutano yetu ulianzishwa. Chunguza kwa ufupi historia ya kila mkutano.

8. Baadhi ya hotuba za mapema zilizungumzia habari gani?

8 Mkutano wa Watu Wote. Katika mwaka wa 1880, mwaka mmoja baada ya Ndugu Russell kuanza kuchapisha gazeti Zion’s Watch Tower, alifuata mfano uliowekwa na Yesu na akaanza safari ya kuhubiri. (Luka 4:43) Kwa kufanya hivyo, Ndugu Russell aliweka kielelezo cha mkutano ambao leo unaitwa Mkutano wa Watu Wote. Likitangaza safari hiyo, gazeti Mnara wa Mlinzi lilisema kwamba Russell “angependa kuhutubia mikutano ya hadhara kuhusu ‘Mambo yanayohusiana na ufalme wa Mungu.’” Katika mwaka wa 1911, baada ya madarasa au makutaniko, kuanzishwa katika nchi nyingi, kila darasa lilitiwa moyo kumchagua msemaji anayestahili kwenda katika maeneo ya karibu na kutoa mfululizo wa hotuba sita zilizozungumzia habari kama vile hukumu na fidia. Mwishoni mwa kila hotuba, jina la msemaji na kichwa cha hotuba ya juma lililofuata kilitangazwa.

9. Mkutano wa Watu Wote umebadilikaje kadiri miaka ilivyopita, na unawezaje kuunga mkono mkutano huo?

9 Katika mwaka wa 1945, gazeti Mnara wa Mlinzi lilitangaza kuanzishwa kwa kampeni ya ulimwenguni pote ya Mkutano wa Watu Wote uliotia ndani mifululizo ya hotuba nane za Biblia zilizozungumzia “matatizo yaliyopaswa kushughulikiwa haraka wakati huo.” Kwa miaka mingi, wasemaji walitumia habari walizopewa na mtumwa mwaminifu na pia walijitayarishia mihtasari yao wenyewe. Hata hivyo, mwaka wa 1981, wasemaji wote walielekezwa watoe hotuba zinazotegemea mihtasari ambayo makutaniko yalitumiwa. * Kabla ya mwaka wa 1990, baadhi ya mihtasari ya hotuba za watu wote ilihusisha mazungumzo pamoja na wasikilizaji au maonyesho; lakini katika mwaka huo maagizo yalibadilishwa, na kuanzia wakati huo na kuendelea, mihtasari hiyo ilitolewa kwa njia ya hotuba tu. Badiliko lingine lilifanywa Januari 2008, muda wa hotuba za watu wote ulipopunguzwa kutoka dakika 45 hadi dakika 30. Hata ingawa hotuba za watu wote zimefanyiwa mabadiliko, hotuba zilizotayarishwa vizuri zinaendelea kujenga imani katika Neno la Mungu na kutufundisha mambo mbalimbali yanayohusu Ufalme wa Mungu. (1 Tim. 4:13, 16) Je, unawaalika kwa shauku wale wote unaowafanyia ziara za kurudia na watu wengine ambao si Mashahidi kuja kusikiliza hotuba hizo muhimu zinazotegemea Biblia?

10-12. (a) Funzo la Mnara wa Mlinzi limefanyiwa mabadiliko gani? (b) Ingefaa ujiulize maswali gani?

10 Funzo la Mnara wa Mlinzi. Katika mwaka wa 1922, ndugu waliojulikana kama mapilgrimu—wahudumu waliotumwa na shirika la Watch Tower Society ili kutoa hotuba makutanikoni na kuongoza katika kazi ya kuhubiri—walipendekeza kwamba kuwe na mkutano wa kawaida wa kujifunza gazeti Mnara wa Mlinzi. Pendekezo hilo lilikubaliwa, na mwanzoni mafunzo ya Mnara wa Mlinzi yalifanywa katikati ya juma au Jumapili.

Funzo la Mnara wa Mlinzi, nchini Ghana, 1931

11 Gazeti Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 1932, lilitoa mwongozo zaidi jinsi ambavyo mkutano huo ulipaswa kufanywa. Ikitumia funzo lililofanywa Betheli kama kielelezo, makala hiyo ilieleza kwamba ndugu alipaswa kuongoza mkutano huo. Ndugu watatu wangekaa mbele na kusoma mafungu kwa zamu. Wakati huo makala hazikuwa na maswali, hivyo kiongozi wa funzo aliambiwa awaombe wasikilizaji waulize maswali kuhusu habari iliyokuwa ikizungumziwa. Kisha angewaalika wasikilizaji kujibu maswali hayo. Ikiwa ufafanuzi zaidi ulihitajika, aliyekuwa anaongoza aliambiwa atoe maelezo “mafupi na yaliyo wazi.”

12 Mwanzoni, kila kutaniko liliruhusiwa kuchagua toleo la gazeti ambalo wengi walitaka kujifunza. Hata hivyo, gazeti Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1933 lilipendekeza kwamba makutaniko yote yatumie toleo la karibuni. Katika mwaka wa 1937, mwongozo ulitolewa kwamba funzo hilo linapaswa kufanywa siku ya Jumapili. Marekebisho zaidi yaliyotokeza utaratibu wa mkutano tunaofuata leo, yalichapishwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 1942. Kwanza, gazeti hilo lilitangaza kwamba sehemu ya chini ya kila ukurasa katika makala ya funzo itakuwa na maswali, na maswali hayo ndiyo yanayopaswa kutumiwa. Kisha, likasema kwamba mkutano huo ulipaswa kufanywa kwa saa moja. Na pia liliwatia moyo wale waliokuwa wakitoa majibu kujieleza “kwa maneno yao wenyewe” badala ya kusoma sehemu fulani ya fungu. Funzo la Mnara wa Mlinzi linaendelea kuwa njia kuu ambayo mtumwa mwaminifu anatumia kutoa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. (Mt. 24:45) Inafaa kila mmoja wetu ajiulize: ‘Je, ninatayarisha funzo la Mnara wa Mlinzi kila juma? Na je, ninajitahidi kutoa maelezo inapowezekana?’

13, 14. Eleza historia ya Funzo la Biblia la Kutaniko, na jambo unalofurahia kuhusu mkutano huo.

13 Funzo la Biblia la Kutaniko. Mwanzoni mwa miaka ya 1890, baada ya mabuku kadhaa ya Millennial Dawn kutolewa, Ndugu H. N. Rahn, Mwanafunzi wa Biblia aliyeishi katika jiji la Baltimore, Maryland, Marekani, alipendekeza kuwe na “Vikundi vya Mapambazuko” kwa ajili ya kujifunza Biblia. Mwanzoni, mikutano hiyo ambayo mara nyingi ilifanywa katika nyumba za watu, ilikuwa ya majaribio. Hata hivyo, kufikia Septemba 1895, kulikuwa na Vikundi vya Mapambazuko katika majiji mengi ya Marekani. Hivyo, gazeti Mnara wa Mlinzi la mwezi huo lilipendekeza kwamba wanafunzi wote wa ile kweli wafanye mikutano hiyo. Lilielekeza kwamba yule aliyekuwa akiongoza alipaswa kuwa msomaji mzuri. Alipaswa kusoma sentensi na kisha asubiri waliohudhuria watoe maelezo. Baada ya kusoma kila sentensi katika fungu na kuzizungumzia, alipaswa kusoma maandiko yalionyeshwa. Mwishoni mwa sura, kila mtu aliyehudhuria alieleza kwa ufupi mambo yaliyozungumziwa.

14 Jina la mkutano huo lilibadilishwa mara kadhaa. Lilibadilishwa na kuitwa Vikundi vya Kiberoya kwa Ajili ya Funzo la Biblia, likirejelea Waberoya wa karne ya kwanza ambao walichunguza Maandiko kwa uangalifu. (Mdo. 17:11) Baada ya muda, jina hilo lilibadilishwa na kuwa Funzo la Kitabu la Kutaniko. Sasa mkutano huo unaitwa Funzo la Biblia la Kutaniko, na kutaniko zima hukutanika pamoja katika Jumba la Ufalme badala ya kukutana kwenye vikundi katika nyumba za watu. Kwa miaka mingi, vitabu, broshua, na hata makala za gazeti Mnara wa Mlinzi zimetumiwa kwa ajili ya funzo hilo. Tangu mwanzoni, wote waliohudhuria walitiwa moyo kushiriki katika mkutano huo. Mkutano huo umechangia sana kuongeza ujuzi wetu wa Biblia. Je, unajitayarisha kwa ukawaida na kushiriki katika mkutano huo kadiri uwezavyo?

15. Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ina kusudi gani?

15 Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Carey Barber, ambaye wakati huo alikuwa akitumikia katika makao makuu huko Brooklyn, New York, alisema hivi: “Jumatatu usiku, Februari 16, 1942, ndugu wote katika familia ya Betheli ya Brooklyn walialikwa wajiandikishe katika shule ambayo baadaye ilikuja kuitwa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.” Ndugu Barber, ambaye miaka mingi baadaye alikuja kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, aliifafanua shule hiyo kuwa “mojawapo ya njia muhimu sana ambazo Yehova ametumia kuwafundisha watu wake katika siku za kisasa.” Shule hiyo ilifanikiwa sana kuwasaidia akina ndugu kuboresha ustadi wao wa kufundisha na kuhubiri, hivi kwamba kuanzia mwaka wa 1943, kijitabu Course in Theocratic Ministry kilitolewa hatua kwa hatua katika makutaniko ulimwenguni pote. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Juni 1, 1943, lilisema kwamba Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ilikusudiwa kuwasaidia watu wa Mungu “kujizoeza wenyewe ili wawe mashahidi wazuri katika kuutangaza Ufalme.”—2 Tim. 2:15.

16, 17. Je, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ilifundisha ustadi wa kufundisha tu? Eleza.

16 Mwanzoni, wengi waliona ilikuwa vigumu kutoa hotuba mbele ya watu wengi. Clayton Woodworth, Jr., ambaye baba yake alifungwa isivyo haki pamoja na Ndugu Rutherford na wengine mwaka wa 1918, alikumbuka jinsi alivyohisi alipojiunga na shule hiyo mwaka wa 1943. Ndugu Woodworth alisema hivi: “Ilikuwa vigumu kwangu kutoa hotuba, ulimi wangu ulionekana kana kwamba umekuwa mrefu, mdomo wangu ulikauka, na sauti yangu ikabadilika.” Hata hivyo, uwezo wa Clayton ulipoendelea kuboreshwa, alipata mapendeleo mengi ya kutoa hotuba mbele za watu. Shule hiyo ilimfundisha mambo mengi zaidi ya ustadi wa kufundisha. Ilimfundisha umuhimu wa unyenyekevu na kumtegemea Yehova. Alisema hivi: “Nilikuja kutambua kwamba haitoshi tu kuwa msemaji. Bali ikiwa msemaji atajitayarisha vizuri na kumtegemea Yehova, wasikilizaji watafurahia kumsikiliza na watajifunza jambo fulani.”

17 Katika mwaka wa 1959, akina dada walialikwa kujiandikisha katika shule hiyo. Dada Edna Bauer anakumbuka akisikia tangazo hilo likitolewa kwenye kusanyiko alilohudhuria. Alisema hivi: “Nakumbuka jinsi akina dada walivyosisimka. Sasa walikuwa na fursa nyingi.” Kwa miaka mingi ndugu na dada wengi walitumia fursa hiyo kujiandikisha katika shule ya Huduma ya Kitheokrasi ili wafundishwe na Yehova. Leo, tunaendelea kupata mazoezi hayo katika mkutano wa katikati ya juma.—Soma Isaya 54:13.

18, 19. (a) Leo sisi hupata mwongozo unaofaa wa kuhubiri jinsi gani? (b) Kwa nini sisi huimba kwenye mikutano yetu? (Ona sanduku “ Kuimba Kuhusu Kweli.”)

18 Mkutano wa Utumishi. Hata kabla ya mwaka wa 1919, mikutano ilikuwa ikifanywa ili kupanga utumishi wa shambani. Wakati huo, si wote katika kutaniko waliohudhuria mikutano hiyo—ni wale tu waliohusika moja kwa moja kugawa machapisho. Karibu muda wote wa mwaka wa 1923, Mkutano wa Utumishi ulifanywa mara moja kwa mwezi, na wote katika darasa, au kutaniko walipaswa kuhudhuria. Kufikia mwaka wa 1928, makutaniko yalihimizwa kufanya Mkutano wa Utumishi kila juma, na katika mwaka wa 1935, gazeti Mnara wa Mlinzi liliyatia moyo makutaniko yote yatumie habari zilizochapishwa katika kijitabu Director (baadaye kiliitwa Informant na kisha, Huduma Yetu ya Ufalme) katika Mkutano wa Utumishi. Punde si punde, mkutano huo ukaanza kufanywa kwa ukawaida katika kila kutaniko.

19 Leo sisi hupata mwongozo unaofaa wa jinsi ya kuhubiri katika Mkutano wa katikati ya juma. (Mt. 10:5-13) Ikiwa unastahili kupata nakala ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo, je, unaisoma na kutumia mapendekezo yanayotolewa unaposhiriki katika huduma?

Mkutano Muhimu Zaidi Katika Mwaka

Tangu karne ya kwanza W.K., Wakristo wamekusanyika pamoja kila mwaka ili kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo (Ona fungu la 20)

20-22. (a) Kwa nini sisi hukumbuka kifo cha Yesu? (b) Unapata faida gani kwa kuhudhuria Ukumbusho wa kila mwaka?

20 Wafuasi wa Yesu waliambiwa wakumbuke kifo chake hadi atakapowasili. Kama ilivyokuwa kwa sherehe ya Pasaka, Ukumbusho wa kifo cha Kristo ni tukio linalofanywa mara moja kwa mwaka. (1 Kor. 11:23-26) Kila mwaka mamilioni ya watu huhudhuria mkutano huo. Unawakumbusha watiwa-mafuta kuhusu pendeleo lao la kuwa warithi wa Ufalme. (Rom. 8:17) Na unawachochea kondoo wengine kumheshimu sana Mfalme wa Ufalme wa Mungu na kuwa washikamanifu kwake.—Yoh. 10:16.

21 Ndugu Russell na wenzake walitambua umuhimu wa kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana na walijua kwamba ulipaswa kufanywa mara moja kwa mwaka. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Aprili 1880 lilisema hivi: “Kwa miaka kadhaa imekuwa desturi ya wengi wetu hapa Pittsburgh . . . kukumbuka Pasaka [Ukumbusho] na kula mifano ya mwili na damu ya Bwana wetu.” Punde si punde, makusanyiko yalianza kufanywa baada ya Ukumbusho. Rekodi ya kwanza kuchukuliwa kwa ajili ya tukio kama hilo ilikuwa mwaka wa 1889, ambapo watu 225 walihudhuria na 22 wakabatizwa.

22 Leo, hatufanyi tena Ukumbusho kuwa sehemu ya programu ya kusanyiko, badala yake tunawaalika watu wote katika jamii tunayoishi waungane nasi katika Jumba la Ufalme au kumbi tulizokodi. Katika mwaka wa 2013, watu zaidi za milioni 19 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Ni pendeleo kama nini kuhudhuria Ukumbusho na pia kuwaalika wengine kuungana nasi katika usiku huo mtakatifu! Je, unawaalika kwa shauku watu wengi kadiri unavyoweza kwenye Ukumbusho wa kila mwaka?

Mtazamo Wetu Unafunua Nini?

23. Una maoni gani kuhusu mikutano yetu?

23 Watumishi washikamanifu wa Yehova hawaoni maagizo ya kukusanyika pamoja kuwa mzigo. (Ebr. 10:24, 25; 1 Yoh. 5:3) Kwa mfano, Mfalme Daudi alipenda kwenda kwenye nyumba ya Yehova ili kuabudu. (Zab. 27:4) Alifurahia hasa kufanya hivyo akiwa na watu wengine waliompenda Mungu. (Zab. 35:18) Fikiria pia mfano wa Yesu. Hata alipokuwa mtoto, alitamani sana kuwa katika nyumba ya ibada ya Baba yake.—Luka 2:41-49.

 Tamaa yetu ya kukusanyika pamoja inafunua kwamba Ufalme wa Mungu ni halisi kwetu

24. Tunapata fursa gani tunapohudhuria mikutano?

24 Tunapohudhuria mikutano, tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova na tunatamani kuwajenga waamini wenzetu. Pia tunaonyesha hamu yetu ya kujifunza jinsi ya kuishi tukiwa raia wa Ufalme wa Mungu, kwa sababu tunapata mazoezi hayo kwenye mikutano na makusanyiko. Kwa kuongezea, mikutano yetu inatupatia ustadi na nguvu tunazohitaji ili tuendelee kuvumilia katika kazi muhimu inayofanywa na Ufalme wa Mungu leo, yaani, kuwafanya watu kuwa wanafunzi wa Mfalme Yesu Kristo na kuwazoeza. (Soma Mathayo 28:19, 20.) Bila shaka, tamaa yetu ya kukusanyika pamoja inafunua kwamba Ufalme wa Mungu ni halisi kwetu. Acheni sikuzote tuthamini mikutano yetu!

^ fu. 2 Mbali na mikutano yetu ya kila juma, kila familia au mtu mmoja-mmoja wanatiwa moyo kutenga wakati wa kuwa na funzo la kibinafsi au ibada ya familia.

^ fu. 9 Kufikia mwaka wa 2013, mihtasari zaidi ya 180 ya hotuba za watu wote ilikuwa imetolewa.