Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA 16

Kukusanyika Pamoja kwa Ajili ya Ibada

Kukusanyika Pamoja kwa Ajili ya Ibada

WAZO KUBWA KATIKA SURA HII

Inaeleza historia ya mikutano yetu na faida ya kuhuzuria mikutano

1. Wakati wanafunzi walikusanyika pamoja walipokea musaada gani, na sababu gani walihitaji musaada huo?

MUDA kidogo tu kisha Yesu kufufuliwa, wanafunzi walikusanyika pamoja ili kutiana moyo. Lakini, kwa sababu waliogopa maadui wao, walifunga milango. Bila shaka, woga ambao walikuwa nao uliisha wakati Yesu aliwatokea na kuwaambia hivi: ‘Mupokee roho takatifu’! (Soma Yohana 20:19-22.) Kisha, siku fulani, mitume walikusanyika tena pamoja, na Yehova akawamwangia roho takatifu. Bila shaka walipokea nguvu ambayo iliwasaidia kufanya kazi ya kuhubiri ambayo walipaswa kufanya!​—Mdo. 2:1-7.

2. (a) Yehova anatupatia nguvu namna gani, na sababu gani tunahitaji nguvu hiyo? (b) Sababu gani mupango wa kufanya Ibada ya Familia ni wa lazima sana? (Ona maelezo mengine na kisanduku “ Ibada ya Familia,” , katika ukurasa wa 175.)

2 Leo pia, tunapambana na hali kama zile za ndugu zetu wa wakati wa mitume. (1 Pet. 5:9) Kama mitume, wakati fulani sisi pia tunaogopa wanadamu. Ili tuendelee kufanya kazi yetu ya kuhubiri, tunahitaji nguvu kutoka kwa Yehova. (Efe. 6:10) Yehova anatupatia sehemu kubwa ya nguvu hiyo kupitia mikutano yetu. Kila juma tunapata pendeleo la kuhuzuria mikutano miwili yenye kujenga sana; ni kusema, Hotuba ya Watu Wote na Funzo la Munara wa Mulinzi, na katikati ya juma mukutano wenye kuitwa Utumishi na Maisha ya Mukristo. * Pia, kila mwaka tunafurahia matukio ine ya maana sana, ni kusema, mukusanyiko wa eneo, mikusanyiko miwili ya muzunguko, na Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Sababu gani ni jambo la maana sana tuhuzurie mikutano hiyo yote? Ni maendeleo gani tulifanya kuhusu mikutano ambayo tunafanya leo? Kuhuzuria ao kutohuzuria mikutano hiyo, kunaonyesha nini juu yetu?

Sababu Gani Tunakusanyika Pamoja?

3, 4. Yehova anaomba watu wake wafanye nini? Toa mifano.

3 Kuanzia zamani Yehova amekuwa akiamuru watu wake wakusanyike pamoja ili wamuabudu. Kwa mufano, katika mwaka wa 1513 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, Yehova alipatia taifa la Israeli Sheria yake. Na katika Sheria hiyo kulikuwa sheria ambayo iliwaomba Waisraeli washike sabato ya kila juma ili kila familia ipate nafasi ya kumuabudu Yehova na kujifunza Sheria yake. (Kum. 5:12; 6:4-9) Wakati Waisraeli walishika amri hiyo, familia zao zilitiwa nguvu na taifa lote liliendelea kuwa safi na nguvu kiroho. Lakini, wakati Waisraeli walishindwa kushika Sheria, kama vile kukusanyika kwa ukawaida ili kumuabudu Yehova, walipoteza baraka zake.​—Law. 10:11; 26:31-35; 2 Nya. 36:20, 21.

4 Tufikirie pia mufano ambao Yesu alituachia. Yeye alizoea kuenda kwenye hekalu kila siku ya Sabato. (Lu. 4:16) Hata kisha Yesu kufa na kufufuliwa, wanafunzi wake waliendelea na zoezi ya kukusanyika pamoja hata kama hawakuombwa tena kushika Sabato. (Mdo. 1:6, 12-14; 2:1-4; Rom. 14:5; Kol. 2:13, 14) Kwenye mikutano hiyo, Wakristo walitolewa maagizo na walitiana moyo. Pia kwenye mikutano hiyo, walimutolea Yehova zabihu za sifa kupitia sala zao, maelezo yao, na nyimbo.​—Kol. 3:16; Ebr. 13:15.

Wanafunzi wa Yesu walikusanyika pamoja ili kutiana moyo na kutiana nguvu

5. Sababu gani tunahuzuria mikutano kila juma na pia mikusanyiko kila mwaka? (Ona pia kisanduku “ Mikusanyiko ya Kila Mwaka Ambayo Inaunganisha Watu wa Mungu” katika ukurasa wa 176.)

5 Leo pia, wakati tunahuzuria mikutano yetu ya kila juma na mikusanyiko yetu ya kila mwaka, tunaonyesha kwamba tunaunga mukono Ufalme wa Mungu. Pia, tunatiwa nguvu na roho takatifu, na tunatia wengine moyo kupitia imani yetu. Na jambo la maana sana, inatutolea nafasi ya kumuabudu Yehova kupitia sala zetu, maelezo yetu, na nyimbo. Ni kweli kwamba mikutano yetu inaweza kuwa tofauti kidogo na mikutano ambayo Waisraeli walikuwa wanafanya na pia ile ya Wakristo wa wakati wa mitume. Hata hivyo, tunapata faida ileile ambayo walipata wakati tunakusanyika pamoja. Ni maendeleo gani tumefanya kuhusu mikutano ambayo tunafanya leo?

Mikutano Yetu ya Kila Juma Inatuchochea Kuwa na “Upendo na Matendo Mazuri”

6, 7. (a) Mikutano yetu ina kusudi gani? (b) Ni nini ambayo inaonyesha kwamba kila kikundi cha Wanafunzi wa Biblia kilikuwa na programu yake ya kufanya mikutano?

6 Wakati Ndugu Charles Taze Russell alianza kutafuta kweli katika Neno la Mungu, aliona kwamba ni jambo la lazima kukusanyika pamoja na watu ambao walikuwa pia na kusudi hilo. Katika mwaka wa 1879, Ndugu Russell aliandika hivi: “Katika muji wa Pittsburgh, mimi na watu wengine tumefanya kikundi cha kujifunza Biblia. Tulipanga kukusanyika pamoja kila Siku ya Yenga ili kuchunguza Maandiko.” Wasomaji wa gazeti Munara wa Mulinzi walitiwa moyo kukusanyika pamoja. Katika mwaka wa 1881, ndugu katika muji wa Pittsburgh, na wa Pennsylvania, walikuwa wanakusanyika pamoja kila Siku ya Yenga na Siku ya Tatu. Gazeti Munara wa Mulinzi la Mwezi wa 9, 1895 lilionyesha kwamba kusudi la mikutano hiyo ilikuwa kuchochea “undugu, upendo na ushirika [muungano] kati ya ndugu na dada,” na kuwapatia wote ambao walihuzuria nafasi ya kutiana moyo.​—Soma Waebrania 10:24, 25.

7 Kwa miaka mingi, kila kikundi cha Wanafunzi wa Biblia kilikuwa na programu yake ya mikutano na kilijipangia ni mara ngapi kilipaswa kufanya mikutano. Kwa mufano, katika mwaka wa 1911 kikundi kimoja cha Wanafunzi wa Biblia katika Amerika kiliandika barua ambayo ilisema hivi: “Kila juma tunafanya karibu mikutano tano.” Walikuwa wanafanya mikutano hiyo kila Siku ya Kwanza, Siku ya Tatu, Siku ya Tano, na kila Siku ya Yenga mara mbili. Barua ingine ambayo ilitumwa na kikundi fulani cha Afrika, ambayo ilichapishwa katika mwaka wa 1914, ilisema hivi: “Tunafanya mikutano yetu mara mbili kwa mwezi, tunaanza Siku ya Tano mupaka siku ya Yenga.” Hata hivyo, kisha muda fulani namna ya kufanya mikutano ilianza kubadilika na kuwa namna ambavyo inafanywa leo. Acha basi tuchunguze kwa ufupi historia ya kila mukutano.

8. Taja tungo fulani za hotuba ambazo zilitumiwa hapo mwanzo?

8 Hotuba ya Watu Wote. Katika mwaka wa 1880, mwaka mumoja kisha Ndugu Russell kuanza kuchapisha gazeti Munara wa Mulinzi, aliamua kufuata mufano wa Yesu wa kuhubiri. Kwa hiyo, alipanga kufanya safari ya kuhubiri mahali mbalimbali. (Lu. 4:43) Wakati huo Ndugu Russell alianzisha mupango wa Hotuba ya Watu Wote ambayo tunafanya leo. Kuhusu safari hiyo, gazeti Munara wa Mulinzi lilisema kwamba Ndugu Russell “atafurahi kutoa hotuba za watu wote ambazo zinazungumuzia ‘Mambo ambayo yanahusu Ufalme wa Mungu.’” Katika mwaka wa 1911, makutaniko yalikuwa yameanzishwa katika inchi nyingi. Kwa hiyo, kila kutaniko lilitiwa moyo kutuma wasemaji wenye ufundi katika maeneo ya karibu-karibu ili kutoa hotuba sita mufululizo ambazo zilikuwa zinazungumuzia habari kama vile hukumu na zabihu ya ukombozi. Mwisho wa kila hotuba, wahuzuriaji walijulishwa jina la musemaji wa juma ambalo linafuata na pia kichwa cha hotuba ambayo atatoa.

9. Kwa miaka mingi, Hotuba ya Watu Wote imefanyiwa mabadiliko gani, na namna gani unaweza kutegemeza mukutano huo?

9 Katika mwaka wa 1945, gazeti Munara wa Mulinzi lilitangaza kuanzishwa kwa kampanye ya Hotuba ya Watu Wote ambayo itatolewa duniani pote. Kampanye hiyo ilikuwa na hotuba munane mufululizo ambazo zilizungumuzia “matatizo makubwa ya wakati huo.” Kwa miaka mingi, wasemaji walitoa hotuba ambazo zilitayarishwa na mutumwa mwaminifu, lakini pia walitoa hotuba ambazo walitayarisha wao wenyewe. Hata hivyo, katika mwaka wa 1981, wasemaji wote waliombwa kutumia plan ambazo zilitumwa katika makutaniko. * Pia kwa miaka mingi Hotuba za Watu Wote zilikuwa na sehemu ya maonyesho ao ya kuuliza maulizo. Lakini, katika mwaka wa 1990, maagizo mapya yalitolewa, na wasemaji walipaswa sasa kutoa hotuba zao bila sehemu ya maonyesho ao ya kuuliza maulizo. Mwezi wa 1, 2008 mabadiliko mengine yalitokea. Dakika za hotuba ya watu wote zilipunguzwa. Hotuba hiyo ilipaswa sasa kutolewa kwa dakika 30 kuliko kutolewa kwa dakika 45. Hata ikiwa Hotuba ya Watu Wote imebadilika-badilika, wakati hotuba zinatayarishwa vizuri zinaendelea kutusaidia tuwe na imani yenye nguvu katika Neno la Mungu. Pia zinaendelea kutufundisha mambo mbalimbali kuhusu Ufalme wa Mungu. (1 Tim. 4:13, 16) Unawaalika kwa furaha watu ambao unajifunza nao Biblia ao watu wengine ambao si Mashahidi, ili wao pia wafike kusikiliza hotuba hizo za maana sana ambazo zinazungumuzia habari za Biblia?

10-12. (a) Funzo la Munara wa Mulinzi limefanyiwa mabadiliko gani? (b) Ni vizuri ujiulize maulizo gani?

10 Funzo la Munara wa Mulinzi. Katika mwaka wa 1922, ndugu ambao waliitwa wapelerin (waangalizi wenye kusafiri) walitumwa na Watch Tower Society ili kutoa hotuba na kuongoza kazi ya kuhubiri katika makutaniko mbalimbali. Ndugu hao walipendekeza kuwe na Funzo la Munara wa Mulinzi katika makutaniko yote kila juma. Pendekezo lao lilikubaliwa na kuanzia mwaka huo makutaniko yalianza kufanya funzo la Munara wa Mulinzi katikati ya juma ao Siku ya Yenga.

Funzo la Munara wa Mulinzi, Ghana, Mwaka wa 1931

11 Gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 15 Mwezi wa 6, 1932, lilitoa maagizo mengine ambayo yalionyesha namna funzo la Munara wa Mulinzi linapaswa kuongozwa. Gazeti hilo lilionyesha kwamba ndugu mumoja anapaswa kuongoza funzo hilo, kwa kufuata namna funzo hilo linaongozwa katika Beteli. Ndugu wengine watatu walipaswa kukaa kwenye viti vya mbele ili wasaidiane kusoma mafungu. Wakati huo habari za kujifunza hazikuwa na sehemu ya maulizo. Kwa hiyo, ndugu ambaye alikuwa anaongoza, aliwaomba wasikilizaji watokeze maulizo juu ya habari ambayo walikuwa wanajifunza. Kisha angeweza kuomba wale ambao wanapenda kutoa majibu wafanye hivyo. Ikiwa wasikilizaji walihitaji kuelewa jambo fulani vizuri zaidi, ndugu huyo angeweza kutoa maelezo “mafupi na yenye kufasiria mambo waziwazi.”

12 Hapo mwanzo, kila kutaniko liliruhusiwa kujifunza habari ambayo watu wengi walichagua katika gazeti fulani. Lakini, gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 15 Mwezi wa 4, 1933, liliomba kila kutaniko litumie gazeti la karibuni. Katika mwaka wa 1937, makutaniko yote yaliagizwa kujifunza gazeti Munara wa Mulinzi Siku ya Yenga. Gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 15 Mwezi wa 4, 1942 lilitoa maagizo mengine. Kupita maagizo hayo, funzo hilo liliongozwa kama tunavyofanya leo. Kwanza, gazeti hilo lilionyesha kwamba maulizo yatapatikana mwisho wa kila ukurasa na kwamba maulizo hayo yanapaswa kutumiwa na ndugu anayeongoza. Pia, lilionyesha kwamba funzo linapaswa kuchukua saa moja. Tena, gazeti hilo liliwatia ndugu moyo wajibu kwa kutumia “maneno yao wenyewe” wala si kusoma majibu katika vifungo. Funzo la Munara wa Mulinzi linaendelea kuwa njia ya maana sana ambayo mutumwa mwaminifu anatumia ili kututolea chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. (Mt. 24:45) Kwa hiyo, ni vizuri kila mumoja wetu ajiulize hivi: ‘Ninatayarisha funzo la Munara wa Mulinzi kila juma? Ninajikaza kutoa majibu ikiwa inawezekana?’

13, 14. Eleza historia ya Funzo la Biblia la Kutaniko. Na ni mambo gani unafurahia kuhusu mukutano huo?

13 Funzo la Biblia la Kutaniko. Katikati ya miaka ya 1890, kisha tu kutolewa kwa mabuku ya kitabu L’Aurore du Millénium, Ndugu H. N. Rahn, Mwanafunzi wa Biblia ambaye alikuwa anaishi katika muji wa Baltimore, Maryland, Amerika, alipendekeza kuwe na vikundi vya kujifunza Biblia, kupitia kitabu L’Aurore du Millénium. Mwanzoni, mikutano hiyo ilikuwa inafanywa katika nyumba za ndugu. Wakati huo ilikuwa tu ni kujaribu. Lakini, Mwezi wa 9, 1895, vikundi vya kujifunza Biblia kupitia kitabu L’Aurore du Millénium vilipatikana katika miji mingi ya Amerika (États-Unis). Kwa hiyo, gazeti Munara wa Mulinzi la mwezi huo, liliagiza Wanafunzi wote wa Biblia waanze kufanya mikutano hiyo. Gazeti hilo lilisema kwamba ndugu ambaye anaongoza mukutano huo anapaswa kuwa musomaji muzuri. Alipaswa kusoma sentensi ao musemwa na kisha kuwaomba wahuzuriaji watoe maelezo. Kisha kusoma na kuzungumuzia sentensi zote katika kila fungu, ndugu anayeongoza alipaswa kusoma maandiko yote ambayo yalitajwa. Mwisho wa kila sura, kila mutu ambaye alihuzuria alipaswa kusema kwa kifupi mambo ambayo alijifunza.

14 Jina la mukutano huo limebadilishwa mara kwa mara. Wakati fulani uliitwa Funzo la Biblia la Waberoya, jina ambalo lilitokana na Waberoya ambao walikuwa wanachunguza Maandiko kwa uangalifu. (Mdo. 17:11) Kisha, funzo hilo liliitwa Funzo la Kitabu la Kutaniko. Leo, linaitwa Funzo la Biblia la Kutaniko, na kutaniko lote linakusanyika pamoja katika Jumba la Ufalme, wala si katika vikundi mbalimbali katika nyumba za ndugu. Kwa muda wa miaka mingi, tulitumia vitabu na broshua mbalimbali ili kufanya funzo hilo, na hata habari mbalimbali za gazeti Munara wa Mulinzi. Tangu zamani, wale wote ambao walihuzuria mukutano huo walitiwa moyo kutoa maelezo wakati wa funzo. Mukutano huo umetusaidia sana kuelewa vizuri Neno la Mungu Biblia. Je, unatayarisha mukutano huo kwa ukawaida, na unajikaza kutoa majibu wakati wa funzo?

15. Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi yana kusudi gani?

15 Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi. Wakati mupango wa Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi ulichukuliwa, Ndugu Carey Barber ambaye wakati huo alikuwa anatumikia kwenye makao makubwa ya Brooklyn, New York, alisema hivi: “Siku ya Kwanza tarehe 16 Mwezi wa 2, 1942, ndugu wote wa familia ya Beteli walialikwa kujiandikisha kwenye masomo ambayo tunaita leo, Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi.” Ndugu Barber, ambaye kisha alitumikia katika Baraza Lenye Kuongoza, alisema kwamba masomo hayo ni kati ya “mipango ya maana sana yenye kuonyesha namna Yehova anahangaikia watu wake katika siku zetu.” Masomo hayo yalisaidia sana ndugu waongeze ufundi wao wa kufundisha na wa kuhubiri. Kwa hiyo, kuanzia mwaka wa 1943, kijitabu Cours pour le ministère théocratique, kiligawanywa hatua kwa hatua katika makutaniko duniani pote. Gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 1 Mwezi wa 6, 1943, lilisema kwamba Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi yalianzishwa ili kusaidia watu wa Mungu, “wajizoeze ili kuwa mashahidi wenye ufundi katika kutangaza Ufalme.”​—2 Tim. 2:15.

16, 17. Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi yana kusudi tu la kutoa ufundi wa kufundisha? Fasiria jibu lako.

16 Mwanzoni, ndugu wengi waliogopa sana kutoa hotuba mbele ya watu wengi. Ndugu Clayton Woodworth, Jr., ambaye baba yake alikuwa kati ya ndugu ambao walifungwa bure pamoja na ndugu Rutherford mwaka wa 1918, alikumbuka namna alijisikia wakati alitoa kipindi chake kwa mara ya kwanza kwenye masomo hayo katika mwaka wa 1943. Alisema hivi: “Ilikuwa vigumu sana kwangu kutoa hotuba. Nilisikia kama vile ulimi wangu umeongezeka, kinywa kilinikauka kabisa, na sauti yangu ilianza kubadilika-badilika.” Hata hivyo, wakati uwezo wa kufundisha wa ndugu Clayton uliendelea kuwa muzuri, alipata mapendeleo mengi ya kutoa hotuba mbele ya watu. Masomo yalimusaidia kuwa na ufundi wa kufundisha, lakini pia yalimusaidia katika mambo mengine. Yalimusaidia aone kwamba unyenyekevu ni sifa ya maana sana na pia kumutegemea Yehova. Ndugu Clayton alisema tena hivi: “Nilifikia kuelewa kwamba, kuwa musemaji haiko ndilo jambo la maana. Lakini, ikiwa musemaji anatayarisha hotuba yake vizuri na anamutegemea Yehova, wasikilizaji watamusikiliza kwa furaha na watajifunza jambo fulani.”

17 Katika mwaka wa 1959 dada pia walialikwa kwenye masomo hayo. Dada Edna Bauer anakumbuka wakati alisikia tangazo hilo kwenye mukusanyiko ambao alihuzuria. Anasema hivi: “Ninakumbuka namna dada walifurahi sana kisha kusikia tangazo hilo. Mupango huo uliwafungulia njia.” Kwa miaka mingi, ndugu na dada walifaidika na mupango huo kwa kujiandikisha kwenye Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi na kufundishwa na Yehova. Leo, tunaendelea kupata mazoezi kama hayo kwenye mukutano wetu wa katikati ya juma.​—Soma Isaya 54:13.

18, 19. (a) Mukutano wa Utumishi unafanywa kwa kufuata mufano wa nani? (b) Sababu gani tunaimba kwenye mikutano yetu? (Ona kisanduku “ Kuimba Kuhusu Ile Kweli.”)

18 Mukutano wa Utumishi. Kuanzia mwaka wa 1919, mikutano ilifanywa ili kupanga namna ya kufanya mahubiri. Lakini wakati huo, si watu wote katika kutaniko ndio walihuzuria mikutano hiyo. Ni wale tu ambao walikuwa wanagawanyia watu vichapo. Lakini, kuanzia mwaka wa 1923, Mukutano wa Utumishi ulikuwa unafanywa mara moja kwa mwezi, na kutaniko lote liliombwa kuhuzuria mukutano huo. Katika mwaka wa 1928, makutaniko yalitiwa moyo kufanya Mukutano wa Utumishi kila juma. Na katika mwaka wa 1935, gazeti Munara wa Mulinzi lilitia makutaniko moyo yatumie habari ambazo zilikuwa zinapatikana katika L’instructeur (ambayo kisha iliitwa L’informateur na kisha ikaitwa Huduma Yetu ya ufalme). Kisha, kila kutaniko lilianza kufanya mukutano huo kila juma.

19 Leo, kwenye mukutano wetu wa katikati ya juma tunapata muongozo wenye kufaa ili kutimiza kazi yetu ya kuhubiri. (Mt. 10:5-13) Ikiwa unastahili kupewa buku la mukutano, je unasoma na kutumia mashauri ambayo yanapatikana ndani wakati unaenda katika mahubiri?

Mukutano Ulio wa Maana Zaidi Katika Mwaka

Kuanzia wakati wa mitume, Wakristo wanakusanyika pamoja kila mwaka ili kufanya Ukumbusho wa kifo cha Kristo (Ona fungu la 20)

20-22. (a) Sababu gani tunafanya Ukumbusho wa kifo cha Kristo? (b) Wakati tunahuzuria Ukumbusho wa kila mwaka, tunapata faida gani?

20 Yesu aliwaambia wanafunzi wake waendelee kukumbuka kifo chake mupaka atakapofika. Ukumbusho wa kifo cha Kristo unapaswa kufanywa mara moja kwa mwaka kama vile Sikukuu ya Pasaka ilikuwa inafanywa. (1 Kor. 11:23-26) Kila mwaka, mamilioni ya watu wanahuzuria mukutano huo. Mukutano huo unakumbusha watiwa-mafuta pendeleo ambalo wamepewa la kutawala na Yesu katika Ufalme. (Rom. 8:17) Na unawapa kondoo wengine nafasi ya kuonyesha heshima yao na ushikamanifu wao kwa Mufalme wa Ufalme wa Mungu.​—Yoh. 10:16.

21 Ndugu Russell pamoja na wenzake, waliona umaana wa kukumbuka Chakula cha Mangaribi cha Bwana na walijua kwamba ukumbusho unapaswa kufanywa mara moja tu kwa mwaka. Gazeti Munara wa Mulinzi la Mwezi wa 4, 1880, lilisema hivi : “Kwa miaka fulani sasa, hapa Pittsburgh, tumekuwa na zoea la kufanya Pasaka [Ukumbusho] na kula mufano wa mwili na kunywa mufano wa damu ya Bwana.” Kisha, mikusanyiko ilianza kufanywa wakati mumoja na ukumbusho. Ripoti ya kwanza ambayo ilionyesha tukio hilo ni ile ya mwaka wa 1889. Ripoti hiyo ilionyesha kwamba, watu 225 walihuzuria na watu 22 walibatizwa.

22 Leo, hatufanye tena Ukumbusho kuwa sehemu ya programu ya mukusanyiko. Lakini, tunawaalika watu wa kila mahali ambapo tunaishi waje kuhuzuria Ukumbusho pamoja na sisi kwenye Jumba letu la Ufalme ao mahali pengine. Katika mwaka wa 2013, watu zaidi ya milioni 19 walikumbuka kifo cha Yesu. Ni pendeleo kubwa sana kuhuzuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu, na pia kualika watu wengine wawe pamoja na sisi wakati wa mangaribi hiyo ya pekee sana. Unajikaza kwa furaha kualika watu wengi zaidi kwenye Ukumbusho kila mwaka?

Kuhuzuria Kwetu Mikutano ao Kutohuzuria Kunaonyesha Nini?

23. Namna gani tunaona agizo ambalo linatuomba kukusanyika pamoja?

23 Wakristo waaminifu wa Yehova hawaone agizo ambalo linawaomba kukusanyika pamoja kuwa muzigo. (Ebr. 10:24, 25; 1 Yoh. 5:3) Kwa mufano, mufalme Daudi alipenda kuenda katika nyumba ya Yehova ili kuabudu. (Zab. 27:4) Na alifurahi zaidi wakati alifanya hivyo pamoja na wengine ambao walikuwa wanamupenda Mungu. (Zab. 35:18) Fikiria pia mufano wa Yesu. Hata wakati alikuwa angali kijana mudogo, alitamani sana kuwa katika nyumba ya Baba yake ili kuabudu.—Lu. 2:41-49.

Tamaa yetu kubwa ya kukusanyika pamoja inafunua wazi kwamba Ufalme wa Mungu ni jambo la kweli kwa kila mumoja wetu

24. Wakati tunahuzuria mikutano, tunapata nafasi gani mbalimbali?

24 Wakati tunahuzuria mikutano tunaonyesha kwamba tunamupenda Yehova na kwamba tunapenda kuwatia moyo ndugu na dada zetu. Tena wakati tunahuzuria mikutano, tunaonyesha kwamba tunatamani kujua namna raia wa Ufalme wa Mungu wanapaswa kuishi, kwa sababu mazoezi kama hayo tunayapata kwanza kupitia mikutano na mikusanyiko. Zaidi ya hayo, mikutano yetu inatusaidia kuwa na ufundi na nguvu ambazo tunahitaji ili kuendelea kufanya kazi ya maana zaidi ambayo Ufalme wa Mungu unatimiza leo, ni kusema, kufanya na kuzoeza wanafunzi wa Mufalme Yesu Kristo. (Soma Mathayo 28:19, 20.) Ni wazi kwamba, tamaa yetu kubwa ya kukusanyika pamoja inafunua wazi kwamba Ufalme wa Mungu ni jambo la kweli kwa kila mumoja wetu. Na tuendelee kila siku kuona mikutano yetu kuwa ya maana sana!

^ fu. 2 Zaidi ya mikutano yetu ya kutaniko, kila familia ao kila Mukristo anatiwa moyo kuwa na programu ya kufanya ibada ya familia ao funzo la pekee.

^ fu. 9 Kufikia mwaka wa 2013, tengenezo limetolea wasemaji plan za hotuba ya watu wote zaidi ya 180.