Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 17

Kuwazoeza Wahudumu wa Ufalme

Kuwazoeza Wahudumu wa Ufalme

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Jinsi ambavyo shule za kitheokrasi zinawatayarisha wahudumu wa Ufalme kutimiza migawo yao

1-3. Yesu aliipanuaje kazi ya kuhubiri, na hilo linatokeza maswali gani?

KWA miaka miwili, Yesu alihubiri kotekote Galilaya. (Soma Mathayo 9:35-38.) Alitembelea majiji na vijiji vingi, akifundisha katika masinagogi na kuhubiri habari njema ya Ufalme. Mahali popote alipohubiri, umati ulimiminika kwake. “Mavuno ni mengi” Yesu akasema, na wafanyakazi zaidi walihitajika.

2 Yesu alipanga kuipanua kazi ya kuhubiri. Jinsi gani? Kwa kuwatuma mitume wake 12 “kuhubiri ufalme wa Mungu.” (Luka 9:1, 2) Huenda mitume hao walijiuliza jinsi ambavyo wangeifanya kazi hiyo. Kabla ya kuwatuma, kwa upendo Yesu aliwapa kitu ambacho Baba yake wa mbinguni alikuwa amempa—mazoezi.

3 Maswali mengi sasa yanakuja akilini: Yesu alipata mazoezi gani kutoka kwa Baba yake? Yesu aliwapa mitume wake mazoezi gani? Namna gani leo—je, Mfalme wa Kimasihi amewazoeza wafuasi wake kutimiza huduma yao? Ikiwa ndivyo, amefanya hivyo jinsi gani?

“Kama Vile Baba Alivyonifundisha, Ndivyo Ninavyosema”

4. Yesu alifundishwa na Baba yake lini na wapi?

4 Yesu alikubali waziwazi kwamba alifundishwa na Baba yake. Wakati wa huduma yake, Yesu alisema: “Kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.” (Yoh. 8:28) Yesu alifundishwa lini na wapi? Kwa wazi, mazoezi yake yalianza mara tu Yesu—akiwa Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu—alipoumbwa. (Kol. 1:15) Akiwa kando ya Baba yake mbinguni, Mwana alimsikiliza na kumtazama “Mfundishaji Mkuu” kwa miaka mingi sana. (Isa. 30:20) Matokeo yakawa kwamba Mwana alipata elimu isiyo na kifani kuhusu sifa, kazi, na makusudi ya Baba yake.

5. Baba alimpa Mwana maagizo gani kuhusu huduma ambayo angefanya duniani?

5 Wakati ulipofika, Yehova alimfundisha Mwana wake kuhusu huduma ambayo angefanya duniani. Ona unabii ambao ulieleza uhusiano kati ya Mfundishaji Mkuu na Mwana wake mzaliwa wa kwanza. (Soma Isaya 50:4, 5.) Unabii huo unasema kwamba Yehova alimwamsha Mwana wake “asubuhi baada ya asubuhi.” Maneno hayo yanatoa wazo la mwalimu anayemwamsha mwanafunzi wake asubuhi na mapema ili amfundishe. Kitabu kimoja cha marejeo ya Biblia kinasema hivi: “Ni kana kwamba Yehova . . . anampeleka shuleni kama mwanafunzi na kumfundisha mambo atakayohubiri na jinsi atakavyohubiri.” Katika “shule” hiyo iliyokuwa mbinguni, Yehova alimfundisha Mwana wake “jambo la kutangaza na la kusema.” (Yoh. 12:49) Baba alimpa pia Mwana wake maagizo ya jinsi ya kufundisha. * Alipokuwa duniani, Yesu alitumia vizuri mazoezi hayo katika huduma yake na pia aliyatumia kuwazoeza wafuasi wake kutimiza huduma yao.

6, 7. (a) Yesu aliwapa mitume wake mazoezi gani, na mazoezi hayo yaliwatayarisha kwa ajili ya kazi gani? (b) Yesu amehakikisha kwamba wafuasi wake leo wamepata mazoezi gani?

6 Kama ilivyotajwa mwanzoni mwa sura hii, Yesu aliwapa mitume wake mazoezi gani? Katika Mathayo sura ya 10, aliwapa maagizo hususa kwa ajili ya huduma ya shambani, kutia ndani mambo yafuatayo: eneo ambalo wangehubiri (mstari wa 5, 6), ujumbe ambao wangehubiri (mstari wa 7), uhitaji wa kumtumaini Yehova (mstari wa 9, 10), jinsi ya kuwafikia wenye nyumba (mstari wa 11-13), jinsi ya kutenda watu wanapokataa ujumbe (mstari wa 14, 15), na jinsi ya kukabiliana na mateso (mstari wa 16-23). * Mazoezi ambayo Yesu aliwapa mitume wake yaliwatayarisha ili waongoze kazi ya kuhubiri habari njema katika karne ya kwanza W.K.

7 Namna gani leo? Yesu, Mfalme wa Ufalme wa Mungu, amewapa wafuasi wake mgawo muhimu zaidi, yaani, kuhubiri “hii habari njema ya ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14) Je, Mfalme ametuzoeza jinsi ya kufanya kazi hiyo muhimu sana? Ndiyo! Akiwa mbinguni, Mfalme amehakikisha kwamba wafuasi wake wamezoezwa jinsi ya kuhubiri nje ya kutaniko na jinsi ya kutimiza majukumu ya pekee ndani ya kutaniko.

Kuwazoeza Wahudumu Kuwa Waeneza-Injili

8, 9. (a) Kusudi kuu la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi lilikuwa nini? (b) Mkutano wa katikati ya juma umekusaidiaje kuwa na matokeo zaidi katika huduma yako?

8 Tangu zamani, tengenezo la Yehova limetumia makusanyiko na mikutano ya kutaniko kama vile Mkutano wa Utumishi, ili kuwazoeza watu wa Mungu kwa ajili ya huduma. Hata hivyo, kuanzia miaka ya 1940, ndugu waliokuwa wakiongoza katika makao makuu walianza kuandaa mazoezi kupitia shule mbalimbali.

9 Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Kama tulivyoona katika sura iliyotangulia, shule hiyo ilianza mwaka wa 1943. Je, kusudi la shule hiyo lilikuwa kuwazoeza tu wanafunzi ili waweze kutoa hotuba nzuri katika mikutano ya kutaniko? Hapana. Tangu zamani, kusudi kuu la shule hiyo lilikuwa kuwazoeza watu wa Mungu kutumia zawadi yao ya kusema ili kumsifu Yehova katika huduma. (Zab. 150:6) Shule hiyo iliwasaidia ndugu na dada wote ambao walijiandikisha wawe wahudumu wa Ufalme wenye matokeo mazuri. Sasa wanapata mazoezi kama hayo kwenye mkutano wa katikati ya juma.

10, 11. Ni nani sasa wanaoweza kuandikishwa katika Shule ya Gileadi, na shule hiyo ina kusudi gani?

10 Shule ya Gileadi. Shule ya Gileadi ilianza Jumatatu, Februari 1, 1943. Mwanzoni, shule hiyo ilikusudiwa iwazoeze mapainia na watumishi wengine wa wakati wote kwa ajili ya utumishi wa umishonari mahali popote ulimwenguni. Lakini kuanzia Oktoba 2011, wanaoandikishwa katika shule hiyo ni wale ambao tayari wako katika utumishi wa pekee wa wakati wote, kama vile mapainia wa pekee, waangalizi wanaosafiri na wake zao, Wanabetheli, na wamishonari walio shambani ambao hawajahudhuria shule hiyo.

11 Kusudi la masomo ya Shule ya Gileadi ni nini? Ndugu mmoja ambaye amefundisha shule hiyo kwa miaka mingi anajibu: “Ni kuimarisha imani ya wanafunzi kupitia kujifunza kwa kina Neno la Mungu na kuwasaidia wasitawishe sifa za kiroho ambazo zitawasaidia kukabiliana na magumu katika migawo yao. Pia, kusudi kuu la masomo hayo ni kuwachochea wanafunzi washiriki zaidi katika kazi ya kueneza injili.”—Efe. 4:11.

12, 13. Shule ya Gileadi imekuwa na matokeo gani katika kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote? Toa mfano.

12 Shule ya Gileadi imekuwa na matokeo gani katika kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote? Tangu mwaka wa 1943, zaidi ya ndugu na dada 8,500 wamezoezwa katika shule hiyo, * na wamishonari waliozoezwa katika Shule ya Gileadi wametumikia katika nchi zaidi ya 170 ulimwenguni. Wamishonari hao hutumia vizuri mazoezi waliyopata, na hivyo wanaweka mfano mzuri kwa kuwa na bidii katika huduma na wanawazoeza wengine kufanya vivyo hivyo. Katika visa vingi, wamishonari waliongoza kazi ya kuhubiri katika maeneo yaliyokuwa na wahubiri wachache wa Ufalme.

13 Fikiria kilichotokea nchini Japani kazi ya kuhubiri hadharani ilipokoma wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Kufikia Agosti 1949, kulikuwa na wahubiri wasiozidi kumi nchini Japani. Hata hivyo, kufikia mwishoni mwa mwaka huo, wamishonari 13 waliozoezwa Gileadi walikuwa wakihubiri kwa bidii nchini humo. Wamishonari wengine wengi walitumwa baadaye. Mwanzoni, wamishonari walihubiri tu katika majiji makubwa, lakini baadaye walihamia majiji mengine. Wamishonari hao waliwatia moyo wanafunzi wao na wengine wawe mapainia. Bidii hiyo ya wamishonari ilikuwa na matokeo mazuri sana. Sasa, kuna watangazaji wa Ufalme zaidi ya 216,000 nchini Japani, na karibu asilimia 40 wanatumikia wakiwa mapainia! *

14. Shule za kitheokrasi ni uthibitisho wenye nguvu wa nini? (Ona pia sanduku “ Shule Zinazowazoeza Wahudumu wa Ufalme,” ukurasa wa 188.)

14 Shule nyingine za kitheokrasi. Shule ya Utumishi wa Painia, Shule ya Biblia ya Wenzi wa Ndoa Wakristo, na Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja zimewasaidia wanafunzi kukua kiroho na kuongoza kwa bidii katika kazi ya kueneza injili. * Shule hizo zote za kitheokrasi ni uthibitisho wenye nguvu kwamba Mfalme wetu amewapa wafuasi wake vifaa kamili ili watimize huduma yao.—2 Tim. 4:5.

Kuwazoeza Akina Ndugu Kushughulikia Majukumu ya Pekee

15. Wanaume walio na majukumu kutanikoni wanataka kumwiga Yesu katika njia gani?

15 Kumbuka unabii wa Isaya ulisema kwamba Yesu alifundishwa na Mungu. Katika “shule” hiyo iliyokuwa mbinguni, Mwana alijifunza “jinsi ya kumjibu neno yeye aliyechoka.” (Isa. 50:4) Yesu alitumia mafunzo hayo; alipokuwa duniani aliwaburudisha wale ‘waliotaabika na kulemewa na mizigo.’ (Mt. 11:28-30) Wakimwiga Yesu, wanaume walio na majukumu kutanikoni wanataka kuwaburudisha ndugu na dada zao. Ili kutimiza hilo, shule kadhaa zimeanzishwa ili kuwasaidia ndugu wanaostahili waweze kuwatumikia waamini wenzao kwa njia nzuri zaidi.

16, 17. Shule ya Huduma ya Ufalme ina kusudi gani? (Ona pia maelezo ya chini.)

16 Shule ya Huduma ya Ufalme. Darasa la kwanza la shule hiyo lilianza Machi 9, 1959, huko South Lansing, New York. Waangalizi wanaosafiri na pia watumishi wa kutaniko walialikwa wahudhurie masomo hayo ya mwezi mmoja. Baadaye, masomo hayo yaliyokuwa katika Kiingereza, yalitafsiriwa katika lugha nyingine, na hatua kwa hatua shule hiyo ilianza kuwazoeza akina ndugu ulimwenguni pote. *

Ndugu Lloyd Barry akifundisha Shule ya Huduma ya Ufalme nchini Japani, 1970

17 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1962, kilisema hivi kuhusu kusudi la Shule ya Huduma ya Ufalme: “Katika ulimwengu huu wenye shughuli nyingi, mwangalizi katika kutaniko la mashahidi wa Yehova anapaswa kuwa mtu anayeweza kupanga maisha yake vizuri ili aweze kuwapa wote kutanikoni uangalifu unaofaa na kuwa baraka kwao. Wakati huohuo hapaswi kuipuuza familia yake kwa sababu ya kutaniko, bali anapaswa kuwa na utimamu wa akili. Watumishi wa kutaniko ulimwenguni pote wamepewa fursa nzuri ya kukutanika pamoja katika Shule ya Huduma ya Ufalme ili wapate mazoezi ambayo yatawasaidia kufanya yale ambayo Biblia inasema mwangalizi anapaswa kutimiza!”—1 Tim. 3:1-7; Tito 1:5-9.

18. Watu wote wa Mungu wananufaikaje na Shule ya Huduma ya Ufalme?

18 Watu wote wa Mungu wamenufaika na Shule ya Huduma ya Ufalme. Kwa njia gani? Wazee na watumishi wa huduma wanapofuata yale waliyojifunza katika shule hiyo, wanamwiga Yesu na kuwaburudisha waamini wenzao. Bila shaka, sisi huthamini sana mzee au mtumishi wa huduma anayejali anapotuambia neno lenye fadhili, anapotusikiliza, au anapotutembelea ili kututia moyo! (1 The. 5:11) Kwa kweli, wanaume hao ni baraka kwa makutaniko yao!

19. Halmashauri ya Ufundishaji inasimamia shule gani nyingine, na ni nini kusudi la shule hizo?

19 Shule nyingine za kitheokrasi. Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Linaloongoza inasimamia shule nyingine ambazo huwazoeza ndugu wenye majukumu katika tengenezo. Kusudi la shule hizo ni kuwasaidia ndugu wenye majukumu—wazee wa kutaniko, waangalizi wanaosafiri, na washiriki wa Halmashauri za Tawi—kutimiza majukumu yao mengi kwa njia yenye matokeo zaidi. Masomo hayo yanayotegemea Biblia huwatia moyo akina ndugu wadumishe hali yao ya kiroho na kufuata kanuni za Kimaandiko wanaposhughulika na kondoo wenye thamani ambao Yehova amewakabidhi wawatunze.—1 Pet. 5:1-3.

Darasa la kwanza la Shule ya Mazoezi ya Kihuduma nchini Malawi

20. Kwa nini Yesu angeweza kusema kwamba sisi sote ‘tunafundishwa na Yehova,’ nawe umeazimia kufanya nini?

20 Ni wazi kwamba Mfalme wa Kimasihi amehakikisha kwamba wafuasi wake wanazoezwa vizuri. Mazoezi hayo yote yalianzia kwa Yehova ambaye alimzoeza Mwana wake, kisha Mwana wake amewazoeza wafuasi wake. Kwa sababu hiyo, Yesu angeweza kusema kwamba sisi sote ‘tunafundishwa na Yehova.’ (Yoh. 6:45; Isa. 54:13) Acheni tuazimie kutumia kikamili mazoezi ambayo Mfalme wetu ametuandalia—iwe ni katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, mikutano mingine ya kutaniko, au shule nyingine zilizozungumziwa katika sura hii. Na tukumbuke kwamba kusudi kuu la mazoezi hayo yote ni kutusaidia tuwe imara kiroho ili tutimize kwa ukamili huduma yetu.

^ fu. 5 Tunajuaje kwamba Baba alimfundisha Mwana jinsi ya kufundisha? Fikiria hili: Mifano mingi ambayo Yesu alitumia alipokuwa akifundisha ilitimiza unabii uliotolewa karne nyingi kabla ya kuzaliwa kwake. (Zab. 78:2; Mt. 13:34, 35) Ni wazi kwamba Yehova, Mtungaji wa unabii huo, aliamua tangu zamani kwamba Mwana wake angetumia mifano kufundisha.—2 Tim. 3:16, 17.

^ fu. 6 Miezi kadhaa baadaye, Yesu ‘aliwachagua wengine 70 na kuwatuma wawili-wawili’ wakahubiri. Pia aliwapa mazoezi.—Luka 10:1-16.

^ fu. 12 Baadhi ya wanafunzi wamehudhuria Shule ya Gileadi zaidi ya mara moja.

^ fu. 13 Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ambavyo wamishonari waliozoezwa Gileadi wamekuwa na matokeo mazuri katika kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote, ona sura ya 23 ya kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu.

^ fu. 14 Shule ya Biblia ya Wenzi wa Ndoa Wakristo na Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja zimeunganishwa na kuwa shule moja inayoitwa Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme.

^ fu. 16 Sasa wazee wote hunufaika na Shule ya Huduma ya Ufalme ambayo huwa na vipindi vyenye urefu mbalimbali na hufanywa kila baada ya miaka michache. Tangu mwaka wa 1984, watumishi wa huduma pia wamezoezwa katika shule hiyo.