Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA 17

Wahubiri wa Ufalme Wanapewa Mazoezi

Wahubiri wa Ufalme Wanapewa Mazoezi

WAZO KUBWA KATIKA SURA HII

Namna masomo mbalimbali ya kiteokrasi imetayarisha wahubiri wa Ufalme kutimiza migao yao

1-3. Yesu alichukua mipango gani ili kazi ya kuhubiri ifike mahali pote, na tunaweza kujiuliza maulizo gani?

YESU alihubiri katika muji wote wa Galilaya kwa muda wa miaka mbili. (Soma Mathayo 9:35-38.) Alitembelea miji na vijiji mbalimbali ili kufundisha katika masinagogi na kuhubiri kuhusu habari njema ya Ufalme. Kila mahali ambako alikuwa anahubiri, watu wengi sana walikuja kumusikiliza. Ndio sababu Yesu alisema kwamba “mavuno ni mengi,” na kwamba kuna lazima ya wafanyakazi wengi.

2 Yesu alichukua mipango ili kazi ya kuhubiri ifike kila mahali. Alifanya hivyo namna gani? Aliwatuma mitume wake 12 ili “kuhubiri ufalme wa Mungu.” (Lu. 9:1, 2) Inawezekana mitume walijiuliza namna gani wangeweza kutimiza kazi hiyo. Mbele ya kuwatuma, kwa upendo Yesu aliwapatia jambo fulani ambalo baba yake alikuwa amemupatia, ni kusema, aliwapatia mazoezi.

3 Kwa hiyo, tunaweza kujiuliza: Yesu alipata mazoezi gani kutoka kwa Baba yake? Yesu aliwapatia mitume wake mazoezi gani? Tuseme nini kuhusu wafuasi wa Masiya Mufalme leo, amewapa mazoezi ili kutimiza kazi yao? Ikiwa jibu ni ndiyo, amefanya hivyo namna gani?

“Kama Vile Baba Alivyonifundisha, Ndivyo Ninavyosema”

4. Ni wapi na ni wakati gani Yesu alifundishwa na Baba yake?

4 Yesu alionyesha waziwazi kwamba alifundishwa na Baba yake. Wakati alikuwa anahubiri, Yesu alisema hivi: “Kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema.” (Yoh. 8:28) Ni wapi na ni wakati gani Yesu alifundishwa? Ni wazi kwamba, Yesu alianza kufundishwa na Mungu kisha tu kuumbwa. (Kol. 1:15) Kwa sababu Mwana huyo muzaliwa wa kwanza wa Mungu alikuwa pembeni ya Baba yake huko mbinguni, alikuwa na miaka mingi sana ya kumusikiliza na kumutazama ‘Mufundishaji [huyo] Mukubwa.’ (Isa. 30:20) Kwa hiyo, Yesu alijifunza mengi juu ya sifa, kazi, na makusudi ya Baba yake.

5. Ni nini Baba alimufundisha mwana wake kuhusu kazi ambayo angetimiza hapa duniani?

5 Kwa wakati uliofaa, Yehova alimufundisha Mwana wake kuhusu kazi ambayo angetimiza hapa duniani. Acha tuchunguze unabii ambao unaonyesha uhusiano ambao Mufundishaji Mukubwa alikuwa nao pamoja na Mwana wake muzaliwa wa kwanza. (Soma Isaya 50:4, 5.) Unabii huo unasema kwamba Yehova alikuwa anamuamusha Mwana wake “asubuhi baada ya asubuhi.” Maneno hayo ya mufano, yanatusaidia kufikiria mwalimu ambaye anamuamusha mwanafunzi wake asubuhi sana ili kumufundisha. Kitabu kimoja ambacho kinafasiria Biblia kinasema hivi: “Ni kama vile Yehova . . . anamupeleka kwenye masomo, kama vile wanamupeleka mwanafunzi kwenye masomo, na anamufundisha namna ya kuhubiri na pia mambo ya kuhubiri.” Kwenye “masomo” hayo ya mbinguni Yehova alimufundisha Mwana wake “jambo la kutangaza na la kusema.” (Yoh. 12:49) Pia, Yehova alimupatia Mwana wake mazoezi kuhusu namna ya kufundisha. * Wakati Yesu alikuwa hapa duniani, alitumia vizuri mazoezi ambayo alipewa kwa kutimiza kazi yake ya kuhubiri. Lakini pia, alitumia mazoezi hayo kwa kuwazoeza wanafunzi wake watimize kazi yao.

6, 7. (a) Yesu aliwapatia mitume wake mazoezi gani, na mazoezi hayo yaliwasaidia kufanya nini? (b) Yesu amehakikisha kwamba wafuasi wake hapa duniani wapewe mazoezi gani?

6 Kama vile imeonyeshwa mwanzoni mwa sura hii, ni mazoezi gani Yesu aliwapatia mitume wake? Kulingana na Mathayo sura ya 10, Yesu aliwapatia maagizo kuhusu kazi ya kuhubiri, kama vile: mahali pa kuhubiri (mustari wa 5, na wa 6), habari ya kuhubiri (mustari wa 7), ulazima wa kumutegemea Yehova (mustari wa 9, na wa 10), namna ya kuanza mazungumuzo na watu (mustari wa 11-13, namna wangefanya ikiwa watu wanakataa kuwasikiliza (mustari wa 14, na wa 15), na namna ya kufanya ikiwa wanateswa kwa sababu ya imani yao (mustari wa 16-23). * Maagizo hayo yenye kuwa wazi ambayo Yesu aliwapatia mitume wake, yaliwasaidia kuwa kwenye mustari wa mbele ao kuongoza kazi ya kuhubiri habari njema wakati wao.

7 Tuseme nini juu ya siku zetu? Yesu ambaye ni Mufalme wa Ufalme wa Mungu amepatia wafuasi wake kazi ya lazima sana kuliko zote, ni kazi ya kuhubiri ‘hii habari njema ya Ufalme katika dunia yote inayoikaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.’ (Mt. 24:14) Mufalme, ametuzoeza ili tutimize kazi hii ya lazima sana kuliko zote? Bila shaka, ndiyo! Mufalme iko mbinguni; kutoka huko anahakikisha kwamba wafuasi wake wanapokea mazoezi kuhusu namna ya kuhubiri inje ya kutaniko na pia kuhusu namna ya kutimiza migao ya pekee katika kutaniko.

Wahubiri Wanazoezwa ili Kuwa Waeneza-Injili

8, 9. (a) Ni nini kusudi kubwa la Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi? (b) Namna gani Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi yamekusaidia uwe na matokeo mazuri katika kazi yako ya kuhubiri?

8 Kwa miaka mingi, tengenezo la Yehova limetumia mikusanyiko, na mikutano ya kutaniko, kama vile Mukutano wa Utumishi ili kuzoeza watu wa Mungu kwa ajili ya kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, kuanzia miaka ya 1940, ndugu ambao walikuwa wanaongoza kwenye makao makubwa walianza mipango ya kuzoeza watu wa Mungu kupitia masomo mbalimbali.

9 Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi. Kama vile tulijifunza katika sura ambayo ilitangulia, masomo hayo yalianza kuongozwa katika mwaka wa 1943. Kusudi la masomo hayo, ilikuwa nikuzoeza tu wanafunzi ili watoe hotuba nzuri kwenye mikutano ya kutaniko? Hapana. Tangu mwanzo, kusudi kubwa la masomo ilikuwa ni kuzoeza watu wa Mungu watumie zawadi yao ya kusema ili kumusifu Yehova katika mahubiri. (Zab. 150:6) Masomo hayo yaliwasaidia ndugu na dada wote ambao walijiandikisha kuwa wahubiri wa Ufalme wenye matokeo zaidi. Sasa mazoezi kama hayo yanatolewa kupitia mukutano wa katikati ya juma.

10, 11. Leo, ni nani anaweza kujiandikisha kwenye Masomo ya Gileadi, na masomo hayo yana kusudi gani?

10 Masomo ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Masomo ambayo yanajulikana leo kwa jina la Masomo ya Biblia ya Gileadi, yalianza Siku ya Kwanza tarehe 1 Mwezi 2, 1943. Mwanzoni masomo hayo yalianzishwa ili kuzoeza mapainia na watumishi wengine wa wakati wote ili waweze kufanya kazi ya umisionere kila mahali ambapo kuna lazima ya wahubiri duniani pote. Lakini kuanzia Mwezi wa 10, 2011, maagizo mapya yalitolewa ambayo yalionyesha kwamba, ni wale tu ambao wako tayari katika utumishi wa wakati wote ndio wanakubaliwa, ni kusema, mapainia wa pekee, waangalizi wenye kusafiri na wake zao, Wanabeteli, na wamisionere wengine ambao walikuwa hawajahuzuria masomo hayo.

11 Mazoezi ambayo yanatolewa kwenye Masomo ya Gileadi yana kusudi gani? Mwalimu mumoja ambaye amekuwa mwalimu kwa miaka mingi kwenye masomo hayo, anajibu hivi: “Kusudi la masomo hayo ni kutia nguvu imani ya wanafunzi kwa kujifunza sana Neno la Mungu na kuwasaidia wawe na sifa za kiroho ambazo wanahitaji ili kupambana na matatizo mbalimbali ambayo watakutana nayo katika migao yao. Pia, kusudi kubwa ni kuwafanya wanafunzi wawe na tamaa zaidi ya kufanya kazi ya kueneza injili.”—Efe. 4:11.

12, 13. Masomo ya Gileadi yamekuwa na matokeo gani mazuri juu ya kazi ya kuhubiri ya duniani pote? Toa mufano.

12 Masomo ya Gileadi yamekuwa na matokeo gani juu ya kazi ya kuhubiri ya duniani pote? Kuanzia mwaka wa 1943, ndugu na dada zaidi ya 8500 wamepata mazoezi kwenye masomo hayo, * na wamisionere hao wemetumikia katika inchi zaidi ya 170 duniani. Wamisionere wametumia vizuri mazoezi ambayo wamepata kwa kufanya kazi ya kuhubiri kwa bidii na pia kwa kuzoeza wengine wafanye hivyo. Mara nyingi, wamisionere waliongoza kazi ya kuhubiri katika maeneo ambayo yalikuwa na wahubiri wadogo ao maeneo ambayo hayakuwa hata na muhubiri mumoja wa Ufalme.

13 Fikiria jambo ambalo lilitokea katika inchi ya Japani, ambako kazi ya kuhubiri ilikuwa kama yenye kusimamishwa wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu. Katika Mwezi wa 8, 1949, kulikuwa karibu wahubiri kumi katika inchi ya Japani. Lakini mwisho wa mwaka huo, wamisionere 13 ambao walipata mazoezi kwenye Gileadi walikuwa wanahubiri kwa bidii katika inchi ya Japani. Kisha, wamisionere wengine zaidi walitumwa katika inchi hiyo. Kwanza, walijikaza sana ili kuhubiri katika miji mikubwa-mikubwa; kisha wakaenda katika miji ingine. Wamisionere hao walitia moyo wanafunzi wao wa Biblia na pia wahubiri wengine kufanya kazi ya upainia. Bila shaka, bidii ambayo wamisionere hao walionyesha ilileta matokeo mazuri. Leo, kuna wahubiri wa Ufalme zaidi ya 216000 katika inchi ya Japani, na wahubiri karibu 40 juu ya 100 ni mapainia! *

14. Masomo mbalimbali ya kiteokrasi yanatoa ushuhuda gani wenye nguvu? (Soma pia kisanduku  “Masomo Mbalimbali Ambayo Yanazoeza Wahubiri wa Ufalme,” ukurasa wa188.)

14 Masomo mengine ya kiteokrasi. Masomo ya Mapainia, Masomo ya Biblia kwa Ajili ya Ndugu na Bibi zao, na Masomo ya Biblia kwa Ajili ya Ndugu Wasio na Bibi, yamesaidia ndugu na dada ambao wamealikwa kuwa na urafiki wenye nguvu pamoja na Yehova, na pia kuwa mufano muzuri katika kazi ya kueneza injili kwa bidii. * Masomo hayo yote ya kiteokrasi ni ushuhuda wenye nguvu kwamba Mufalme amezoeza wafuasi wake kutimiza kazi yao.​—2 Tim. 4:5.

Ndugu Wanazoezwa ili Kutimiza Migao ya Pekee

15. Ndugu walio na madaraka katika tengenezo wanapenda kumuiga Yesu namna gani?

15 Tukumbuke tena unabii wa Isaya ambao unasema kwamba Yesu anafundishwa na Mungu. Kwenye “masomo” hayo ya mbinguni, Mwana alijifunza namna ya kumujibu yeye aliyechoka kwa neno linalofaa. (Isa. 50:4) Yesu alitumikisha mafundisho hayo; wakati alikuwa hapa duniani, aliwapatia kitulizo wale ‘waliotaabika na kulemewa na mizigo.’ (Mt. 11:28-30) Kwa kuiga mufano wa Yesu, wanaume ambao wana madaraka fulani wanapenda kuwa watu ambao wanatolea ndugu na dada zao kitulizo. Ndio sababu masomo mbalimbali yemeanzishwa ili kusaidia ndugu wenye kustahili wapate matokeo mazuri wakati wanawatumikia ndugu na dada.

16, 17. Masomo ya Huduma ya Ufalme yana kusudi gani? (Soma pia maelezo mengine.)

16 Masomo ya Huduma ya Ufalme. Masomo hayo yalianzishwa tarehe 9 Mwezi wa 3, 1959, katika muji wa South Lansing, New York. Waangalizi wenye kusafiri na watumishi wa kutaniko (leo waratibu wa baraza la wazee) walialikwa ili kuhuzuria masomo hayo kwa muda wa mwezi moja. Kisha, habari ambazo walijifunza kwenye masomo hayo zilitafsiriwa katika luga zingine, na hatua kwa hatua ndugu wengine katika dunia yote walianza kupewa mazoezi kwenye masomo hayo. *

Ndugu Lloyd Barry anafundisha kwenye Masomo ya Huduma ya Ufalme katika inchi ya Japani, mwaka wa 1970

17 Kuhusu kusudi la Masomo ya Huduma ya Ufalme, Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1962 kilisema hivi: “Katika ulimwengu huu ambao watu wana mambo mengi ya kufanya, mwangalizi katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova anapaswa kuwa mwanaume ambaye anaweza kupanga maisha yake vizuri. Jambo hilo linaweza kumusaidia akazie uangalifu zaidi ndugu na dada wote katika kutaniko, na pia kumufanya awe baraka kwa kutaniko lote. Hapaswe kusahau familia yake kwa sababu ya kuhangaikia kutaniko, kwa hiyo, anapaswa kutumia akili nzuri. Bila shaka, watumishi wa makutaniko katika dunia yote wamepewa pendeleo kubwa sana la kuhuzuria Masomo ya Huduma ya Ufalme ili wapewe mazoezi ambayo yatawasaidia kufanya yote ambayo Biblia inasema mwangalizi anapaswa kufanya!”​—1 Tim. 3:1-7; Tito 1:5-9.

18. Watu wote wa Mungu wanafaidika na Masomo ya Huduma ya Ufalme namna gani?

18 Watu wote wa Mungu wamefaidika na Masomo ya Huduma ya Ufalme. Namna gani? Wakati wazee na watumishi wa huduma wanatumia mambo ambayo wamefundishwa kwenye masomo hayo, kama Yesu, wanakuwa chanzo cha kitulizo kwa ndugu na dada zao katika makutaniko. Haufurahie wakati wazee ao watumishi wa huduma wanatumia maneno ya upole, wakati wanakusikiliza kwa uangalifu ao wakati wanakutembelea ili kukutia moyo? (1 Tes. 5:11) Wanaume hao wenye kustahili ni baraka kubwa kwa makutaniko!

19. Ni masomo gani mengine ambayo Halmashauri ya Ufundishaji inasimamia, na masomo hayo yote yana kusudi gani?

19 Masomo mengine ya kiteokrasi. Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Lenye Kuongoza inasimamia masomo mengine ambayo yanapatia mazoezi ndugu walio na madaraka katika tengenezo. Masomo hayo yote yana kusudi la kusaidia ndugu wenye madaraka, kama vile wazee wa kutaniko, waangalizi wenye kusafiri, na ndugu wa Halmashauri ya Tawi ili waweze kutimiza kazi yao vizuri. Mazoezi hayo ambayo yanategemea Biblia yanawatia ndugu hao moyo waendelee kulinda hali yao nzuri ya kiroho wakati wanasaidia kondoo za Yehova ambao amewapatia wachunge.​—1 Pet. 5:1-3.

Masomo ya Mazoezi ya Kihuduma ambayo yalifanywa kwa mara ya kwanza katika inchi ya Malawi, mwaka wa 2007

20. Sababu gani Yesu alisema kweli wakati alisema kwamba sisi wote ‘tunafundishwa na Yehova,’ na umeazimia kufanya nini?

20 Ni wazi kwamba Masiya-Mufalme amehakikisha kwamba wafuasi wake wanazoezwa vizuri. Mazoezi hayo yote yametoka juu mbinguni: Yehova alimuzoeza Mwana wake, na Mwana wake anawazoeza wanafunzi wake. Kwa hiyo, alisema kweli wakati alisema kwamba sisi wote ‘tunafundishwa na Yehova.’ (Yoh. 6:45; Isa. 54:13) Acheni tuazimie kupata faida kabisa ya mafundisho yote ambayo Mufalme ametupatia. Pia acheni tukumbuke kwamba kusudi kubwa la mazoezi yote ambayo tunapewa ni kutusaidia tuendelee kuwa wenye nguvu kiroho ili tuweze kutimiza kazi yetu kwa ukamilifu.

^ fu. 5 Tunajua namna gani kwamba Baba alimufundisha Mwana wake namna ya kufundisha? Fikiria jambo hili: Yesu alitumia mifano mingi katika mafundisho yake ili kutimiza unabii ambao uliandikwa miaka mingi mbele ya kuzaliwa kwake. (Zab. 78:2; Mt. 13:34, 35) Kwa kweli, Yehova ambaye aliandikisha unabii huo, alijua vizuri mbele ya wakati kwamba Mwana wake atatumia mifano katika mafundisho yake.​—2 Tim. 3:16, 17.

^ fu. 6 Kisha miezi fulani, Yesu ‘akachagua wengine 70 na akawatuma wawili-wawili’ katika mahubiri. Aliwapatia pia mazoezi.​—Lu. 10:1-16.

^ fu. 12 Wamisionere fulani walihuzuria Masomo ya Gileadi zaidi ya mara moja.

^ fu. 13 Ili kujua zaidi juu ya kazi ambayo imetimizwa duniani na wamisionere ambao wamezoezwa kwenye Gileadi, soma sura ya 23 ya kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu.

^ fu. 14 Masomo ya Biblia kwa Ajili ya Ndugu na Bibi zao, na Masomo ya Biblia kwa Ajili ya Ndugu Wasio na Bibi, yamechangwa pamoja na sasa yanaitwa Masomo kwa Ajili ya Waeneza Injili wa Ufalme.

^ fu. 16 Leo, wazee wote wanafaidika na Masomo ya Huduma ya Ufalme. Muda wa masomo hayo unabadilika kila mara, na masomo hayo yanafanywa kisha miaka fulani. Kuanzia mwaka wa 1984, watumishi wa huduma wamepewa pia mazoezi kupitia masomo hayo.