Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 18

Jinsi Kazi za Ufalme Zinavyogharimiwa

Jinsi Kazi za Ufalme Zinavyogharimiwa

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Sababu zinazofanya watu wa Yehova wategemeze kazi ya Ufalme, na jinsi wanavyofanya hivyo

1, 2. (a) Ndugu Russell alimjibu jinsi gani mhudumu ambaye alitaka kujua jinsi ambavyo kazi za Wanafunzi wa Biblia ziliendeshwa? (b) Tutachunguza nini katika sura hii?

PINDI fulani, Ndugu Charles T. Russell alikaribiwa na mhudumu fulani wa Kanisa la Reformed ambaye alitaka kujua jinsi kazi za Wanafunzi wa Biblia zilivyogharimiwa.

“Hatuombi kamwe michango,” akaeleza Ndugu Russell.

“Mnapataje pesa?” mhudumu huyo akauliza.

“Hutaamini endapo nitakwambia ukweli wa mambo,” akajibu Russell. “Watu wanapokuja kwenye mikutano yetu, hawaoni kikapu [cha mchango] kikipitishwa kwa kila mtu. Lakini wanaona kwamba kuna matumizi ya pesa. Wanajiambia hivi, ‘Jumba hili linahitaji kugharimiwa . . . Ninaweza kuchangia jinsi gani?’”

Mhudumu huyo alimwangalia Ndugu Russell akiwa haamini aliyosikia.

Russell akaendelea kusema, “Ninakuambia ukweli mtupu. Huwa wananiuliza swali hili, ‘Ninaweza kuchangia jinsi gani?’ Mtu anapobarikiwa na ana pesa kiasi fulani, anataka kuitumia kwa ajili ya Bwana. Ikiwa hana pesa yoyote, kwa nini tumsukume kutoa?” *

2 Bila shaka, Ndugu Russell alikuwa akisema “ukweli mtupu.” Tangu zamani, watu wa Mungu wamekuwa wakitoa michango ya hiari ili kuitegemeza ibada ya kweli. Katika sura hii, tutachunguza baadhi ya mifano ya Kimaandiko kuhusu jambo hilo na pia jinsi tunavyofanya leo. Tunapochunguza jinsi ambavyo kazi za Ufalme zinagharimiwa leo, itafaa kila mmoja wetu ajiulize, ‘Ninaweza kuutegemeza Ufalme jinsi gani?’

‘Kila Mtu Mwenye Moyo Wenye Nia na Aulete Mchango’

3, 4. (a) Yehova anawaamini jinsi gani waabudu wake? (b) Waisraeli waliutegemezaje ujenzi wa maskani?

3 Yehova anawaamini waabudu wake wa kweli. Anajua kwamba wakipewa nafasi, watafurahi kuonyesha ujitoaji wao wa moyo wote kwa Mungu kwa kutoa kwa hiari. Fikiria mifano miwili kutoka katika historia ya Waisraeli.

4 Baada ya kuwakomboa Waisraeli kutoka Misri, Yehova aliwaambia wajenge hema, au maskani inayoweza kuhamishwa, kwa ajili ya ibada. Ujenzi na vyombo vyake vingehitaji pesa nyingi. Yehova alimwamuru Musa awape watu nafasi ya kuunga mkono mradi huo, aliposema: “Kila mtu mwenye moyo wenye nia na aulete ukiwa mchango wa Yehova.” (Kut. 35:5) Watu hao, ambao muda mfupi tu uliopita walikuwa “watumwa chini ya uonevu,” waliitikiaje? (Kut. 1:14) Waliutegemeza kwa kiwango kikubwa sana, walitoa kwa hiari dhahabu, fedha, na vitu vingine vyenye thamani—huenda vitu vingi kati ya hivyo walipata kutoka kwa mabwana wao wa zamani, Wamisri. (Kut. 12:35, 36) Waisraeli walitoa mchango mwingi zaidi kuliko ulivyohitajika hivi kwamba ililazimika ‘wazuiwe wasilete.’—Kut. 36:4-7.

5. Waisraeli waliitikiaje Daudi alipowapa nafasi ya kuchanga kwa ajili ya ujenzi wa hekalu?

5 Miaka 475 hivi baadaye, Daudi alitoa mchango kutoka kwenye ‘mali yake ya pekee’ ili kugharimia ujenzi wa hekalu, kituo cha kwanza cha kudumu cha ibada ya kweli duniani. Kisha akawapa Waisraeli wenzake nafasi ya kutoa, aliwauliza hivi: “Ni nani anayejitolea kuujaza mkono wake leo kwa zawadi kwa ajili ya Yehova?” Matokeo yakawa kwamba watu “walimtolea Yehova matoleo ya hiari kwa moyo kamili.” (1 Nya. 29:3-9) Akitambua chanzo halisi cha michango hiyo, Daudi alimwambia hivi Yehova katika sala: “Kila kitu hutoka kwako, nasi tumekupa kutoka katika mkono wako mwenyewe.”—1 Nya. 29:14.

6. Kwa nini pesa zinahitajika ili kutimiza kazi ya Ufalme leo, na ni maswali gani yanatokea?

6 Musa na Daudi hawakuwalazimisha watu wa Mungu kutoa michango. Badala yake, watu walitoa kwa hiari kutoka moyoni. Namna gani leo? Tunajua vizuri kwamba kazi ambayo Ufalme wa Mungu unafanya inahitaji pesa. Inagharimu pesa nyingi kuchapisha na kugawanya Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia, kujenga na kudumisha mahali pa mikutano na majengo ya ofisi za tawi, na kutoa misaada ya dharura kwa waamini wenzetu katika nyakati za msiba. Kwa hiyo, maswali muhimu yanatokea: Pesa za kugharimia mambo hayo zinapatikanaje? Je, wafuasi wa Mfalme wanahitaji kusukumwa ili watoe?

“Halitawaomba Watu Wala Kuwasihi Kamwe Walitegemeze”

7, 8. Kwa nini watu wa Yehova hawaombi wala kuwasihi watu watoe pesa?

7 Ndugu Russell na washiriki wake hawakutaka kuiga mbinu za kuchangisha pesa ambazo zinatumiwa sana katika makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo. Katika toleo la pili la gazeti Mnara wa Mlinzi, chini ya kichwa “Je, Unalitaka ‘Zion’s Watch Tower’?” Russell alieleza hivi, “Tunaamini kwamba gazeti ‘Zion’s Watch Tower’ linategemezwa na YEHOVA, na maadamu hivyo ndivyo ilivyo halitawaomba watu wala kuwasihi kamwe walitegemeze. Yule anayesema: ‘Dhahabu na fedha yote ya milimani ni yangu,’ atakapoacha kutoa pesa zinazohitajiwa, tutajua kwamba huo ndio wakati wa kusimamisha uchapishaji wa gazeti hili.” (Hag. 2:7-9) Zaidi ya miaka 130 baadaye, gazeti Mnara wa Mlinzi na shirika linalochapisha gazeti hilo bado linaendelea kufanikiwa!

8 Watu wa Yehova hawaombi-ombi pesa. Hawapitishi vikapu vya michango au kutuma barua za kuomba pesa. Wala hawatumii minada au kupokea pesa kwa njia za simu ili kuchangisha pesa. Wanafuata yale yaliyosemwa kwenye Mnara wa Mlinzi miaka mingi iliyopita: “Hatujawahi kufikiria kamwe kuomba pesa kwa ajili ya Bwana, kama makanisa mengine yanavyofanya . . . Maoni yetu ni kwamba pesa zinazopatikana kwa kutumia mbinu mbalimbali za kuombaomba kwa jina la Bwana wetu zinamchukiza, hazikubaliki kwake, nazo hazileti baraka yake juu ya watoaji au kazi inayotimizwa.” *

“Kila Mmoja na Afanye Kama Alivyoazimia Moyoni Mwake”

9, 10. Ni sababu gani moja inayotufanya tutoe michango ya hiari?

9 Tukiwa raia wa Ufalme leo, hatupaswi kulazimishwa kutoa michango. Kinyume na hilo, tunatumia kwa shangwe pesa na mali zetu kutegemeza kazi ya Ufalme. Kwa nini tuko tayari kufanya hivyo kwa hiari? Fikiria sababu tatu.

10 Kwanza, tunatoa michango ya hiari kwa sababu tunampenda Yehova na tunataka kufanya “mambo yanayopendeza machoni pake.” (1 Yoh. 3:22) Kwa kweli, Yehova anapendezwa na waabudu wanaotoa kwa hiari kutoka moyoni. Acheni tuchunguze maneno ya mtume Paulo kuhusu utoaji wa Kikristo. (Soma 2 Wakorintho 9:7.) Mkristo wa kweli hatoi kwa kusitasita au kulazimishwa. Badala yake, anatoa kwa sababu ‘ameazimia moyoni mwake’ kufanya hivyo. * Hilo linamaanisha kwamba anatoa baada ya kufikiria uhitaji fulani na jinsi anavyoweza kutosheleza uhitaji huo. Yehova anampenda sana mtoaji wa namna hiyo, kwa maana “Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” Tafsiri nyingine inasema hivi: “Mungu huwapenda watu wanaopenda kutoa.”

Watoto wetu nchini Msumbiji pia wanapenda kutoa

11. Ni nini kinachotuchochea tumpe Yehova zawadi bora kabisa?

11 Pili, tunatoa michango yetu kama njia ya kumshukuru Yehova kwa sababu ya baraka nyingi anazotupa. Fikiria kanuni inayopatikana katika Sheria ya Musa ambayo inatusaidia kujichunguza. (Soma Kumbukumbu la Torati 16:16, 17.) Walipokuwa wakihudhuria sherehe tatu za kila mwaka, kila mwanaume Mwisraeli alipaswa kutoa zawadi “kulingana na baraka za Yehova” ambazo alikuwa amempa. Hivyo, kabla ya kuhudhuria sherehe, kila mwanaume alipaswa kufikiria baraka ambazo amepata na kujichunguza, kisha aamue zawadi bora kabisa ya kutoa. Vivyo hivyo, tunapotafakari kuhusu baraka nyingi ambazo Yehova ametupa, tunachochewa kumpa zawadi bora kabisa. Zawadi yetu tunayotoa kwa moyo wote, ambayo inatia ndani michango yetu, inaonyesha jinsi ambavyo tunathamini sana baraka ambazo Yehova ametumwagia.—2 Kor. 8:12-15.

12, 13. Michango yetu ya hiari inaonyeshaje kwamba tunampenda Mfalme, na kila mtu anatoa kiasi gani?

12 Tatu, tunapotoa michango yetu ya hiari, tunaonyesha kwamba tunampenda Mfalme Yesu Kristo. Jinsi gani? Ona yale ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake katika usiku wa mwisho wa maisha yake duniani. (Soma Yohana 14:23.) Yesu alisema hivi, “Ikiwa yeyote ananipenda, atalishika neno langu.” “Neno” la Yesu linatia ndani amri ya kuhubiri habari njema ya Ufalme katika dunia yote. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Tunashika “neno” hilo kwa kufanya yote tuwezayo, yaani, kutumia wakati wetu, nguvu, na mali zetu, ili kuendeleza kazi ya kuhubiri Ufalme. Kwa kufanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunampenda Mfalme wa Kimasihi.

13 Naam, tukiwa raia washikamanifu wa Ufalme, tunataka kutegemeza kwa moyo wetu wote Ufalme kwa kutoa michango yetu ya pesa. Tunatoa kiasi gani? Huo ni uamuzi wa kibinafsi. Kila mtu anatoa kulingana na uwezo wake. Hata hivyo, wengi wa waamini wenzetu, hawana mali nyingi. (Mt. 19:23, 24; Yak. 2:5) Lakini waamini hao wanaweza kufarijika kujua kwamba Yehova na Mwana wake wanathamini sana hata michango kidogo inayotolewa kutoka moyoni.—Marko 12:41-44.

Pesa Hutolewaje?

14. Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova walitoaje machapisho yao?

14 Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova walitoa machapisho ya Biblia kwa kiasi fulani hususa cha mchango. Kiasi cha mchango kilichopendekezwa kilikuwa cha chini sana hivi kwamba hata watu ambao hawakuwa na pesa nyingi wangeweza kupata machapisho. Bila shaka, ikiwa mwenye nyumba alionekana kwamba anapendezwa lakini hana uwezo wa kuchangia, wahubiri wa Ufalme walikuwa tayari kabisa kumwachia machapisho. Tamaa yao kubwa ilikuwa kuwapatia machapisho watu wanyofu ambao wangeyasoma na kunufaishwa nayo.

15, 16. (a) Katika mwaka wa 1990, Baraza Linaloongoza lilifanya rekebisho gani kuhusu jinsi ya kutoa machapisho yetu? (b) Michango ya hiari inatolewaje? (Ona pia sanduku “ Michango Yetu Hutumiwaje?”)

15 Katika mwaka wa 1990, Baraza Linaloongoza lilianza kurekebisha njia yetu ya kutoa machapisho. Kuanzia mwaka huo nchini Marekani, machapisho yalianza kutolewa kwa msingi wa mchango wa hiari. Barua iliyotumwa kwa makutaniko yote nchini humo ilieleza hivi: “Wahubiri na watu wote wanaopendezwa watapewa magazeti na machapisho bila kuombwa au hata kutaja kwamba mchango fulani hususa utolewe ili kupata chapisho. . . . Mtu yeyote ambaye anapenda kuchanga ili kulipia gharama za kazi yetu ya kuwaelimisha watu anaweza kufanya hivyo, lakini wanaweza kupata machapisho iwe wametoa mchango au la.” Mpango huo ulikusudiwa kuonyesha wazi kwamba kazi yetu ni ya kidini na inafanywa kwa kujitolea na kwamba “sisi si wachuuzi wa neno la Mungu.” (2 Kor. 2:17) Baada ya muda, mpango wa michango ya hiari ulianza kufuatwa katika ofisi za tawi ulimwenguni pote.

16 Michango ya hiari hutolewaje? Katika Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova, kuna masanduku ya michango. Mtu yeyote anaweza kuweka mchango wake humo au anaweza kutuma moja kwa moja kwa mojawapo ya mashirika ya kisheria yanayotumiwa na Mashahidi wa Yehova. Kila mwaka makala moja katika gazeti Mnara wa Mlinzi inaelezea jinsi ambavyo michango hiyo ya hiari inaweza kutolewa.

Pesa Hizo Hutumiwaje?

17-19. Eleza jinsi ambavyo michango hutumiwa kwa ajili ya (a) kazi ya ulimwenguni pote, (b) ujenzi wa Majumba ya Ufalme ulimwenguni pote, na (c) gharama za kutaniko.

17 Kazi ya ulimwenguni pote. Pesa hizo zinatumiwa kulipia gharama zinazohusika katika kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. Gharama hizo zinatia ndani pesa zinazotumiwa kuchapisha na kusambaza machapisho hayo ulimwenguni pote, kujenga na kudumisha ofisi za tawi, na kuendesha shule mbalimbali za kitheokrasi. Zaidi ya yote, pesa hizo zinatumiwa kuwatunza wamishonari, waangalizi wanaosafiri, na mapainia wa pekee. Pia, michango yetu inatumiwa kuwapatia msaada wa dharura waamini wenzetu wakati wa msiba. *

18 Ujenzi wa Majumba ya Ufalme ulimwenguni pote. Pesa hizo zinatumiwa kusaidia makutaniko kujenga au kurekebisha Jumba la Ufalme. Michango zaidi inapopokewa, makutaniko mengine yanaweza kusaidiwa. *

19 Gharama za kutaniko. Pesa hizo zinatumiwa kulipia uendeshaji na udumishaji wa Jumba la Ufalme na kurudisha pesa zozote ambazo ofisi ya tawi ililipatia kutaniko ili lijenge au kukarabati mahali pake pa ibada. Huenda wazee wakapendekeza kwamba kiasi fulani cha pesa kitumwe ofisi ya tawi ili kuendeleza kazi ya ulimwenguni pote. Katika visa kama hivyo, wazee watapendekeza kutaniko lifanye azimio. Azimio hilo likipitishwa, pesa zilizopendekezwa zitatumwa ofisi ya tawi. Kila mwezi, ndugu anayeshughulikia hesabu za kutaniko anatayarisha ripoti ya hesabu, ambayo inasomwa kutanikoni.

20. Unawezaje kumheshimu Yehova kwa “vitu vyako vyenye thamani”?

20 Tunapotafakari mambo yote yanayohusika katika kutimiza kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kuwafanya watu kuwa wanafunzi duniani kote, tunachochewa sana ‘kumheshimu Yehova kwa vitu vyetu vyenye thamani.’ (Met. 3:9, 10) Vitu vyetu vyenye thamani vinatia ndani nguvu zetu za kimwili, kiakili, na vipawa vyetu vya kiroho. Bila shaka, tunataka kutumia vitu hivyo kwa ukamili katika kazi ya Ufalme. Hata hivyo, kumbuka kwamba vitu vyetu vyenye thamani pia vinatia ndani mali zetu. Acheni tuazimie kutoa kile tunachoweza, na wakati tunapoweza kufanya hivyo. Michango yetu ya hiari inamletea Yehova heshima na inaonyesha kwamba tunamuunga mkono Mfalme wa Kimasihi.

^ fu. 1 Gazeti Mnara wa Mlinzi, Julai 15, 1915, ukurasa wa 218-219.

^ fu. 8 Gazeti Mnara wa Mlinzi, Agosti 1, 1899, ukurasa wa 201.

^ fu. 10 Msomi mmoja anasema kwamba neno la Kigiriki linalotafsiriwa “azimia” “lina wazo la kuamua mapema.” Anaongezea kusema hivi, “Ingawa kuna shangwe unapotoa kwa hiari, bado utoaji unapaswa kufikiriwa mapema na kutolewa kwa mpango.”—1 Kor. 16:2.

^ fu. 17 Ona Sura ya 20 kwa habari zaidi kuhusu huduma ya msaada.

^ fu. 18 Ona Sura ya 19 kwa habari zaidi kuhusu ujenzi wa Majumba ya Ufalme.