Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 19

Kazi ya Ujenzi Inayomletea Yehova Sifa

Kazi ya Ujenzi Inayomletea Yehova Sifa

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Kazi ya ujenzi inayofanywa ulimwenguni pote inaendeleza kazi ya Ufalme

1, 2. (a) Tangu zamani watumishi wa Yehova wamefurahia kufanya nini? (b) Yehova anathamini nini?

TANGU zamani watumishi washikamanifu wa Yehova wamefurahia kujenga majengo yanayoliletea sifa jina lake. Kwa mfano, Waisraeli walishiriki kwa bidii kujenga maskani na kuchangia vifaa vya ujenzi.—Kut. 35:30-35; 36:1, 4-7.

2 Yehova haoni kwamba vifaa vya ujenzi ndivyo vitu pekee vinavyomletea sifa, wala havioni kuwa ndivyo muhimu zaidi. (Mt. 23:16, 17) Jambo ambalo Yehova anathamini sana, zawadi ambayo inamletea sifa zaidi kuliko jambo lingine lolote, ni ibada ya watumishi wake, kutia ndani roho yao ya kujitoa na bidii yao. (Kut. 35:21; Marko 12:41-44; 1 Tim. 6:17-19) Jambo hilo ni muhimu sana. Kwa nini? Kwa sababu majengo hayadumu milele. Kwa mfano, leo hakuna maskani wala hekalu. Ingawa majengo hayo hayapo leo, bado Yehova anakumbuka ukarimu na bidii ya watumishi wake washikamanifu ambao walisaidia katika ujenzi huo.—Soma 1 Wakorintho 15:58; Waebrania 6:10.

3. Tutapitia mambo gani katika sura hii?

3 Leo pia watumishi wa Yehova wamejitahidi sana kujenga majengo ya ibada. Yale ambayo tumetimiza chini ya mwelekezo wa Mfalme wetu Yesu Kristo ni yenye kustaajabisha sana! Kwa kweli, Yehova amebariki jitihada zetu. (Zab. 127:1) Katika sura hii, tutapitia baadhi ya kazi za ujenzi ambazo tumefanya na jinsi ambavyo zimemletea Yehova sifa. Pia tutaona maelezo ya baadhi ya wale ambao wameshiriki katika kazi hiyo.

Ujenzi wa Majumba ya Ufalme

4. (a) Kwa nini tunahitaji majengo zaidi ya ibada? (b) Kwa nini ofisi kadhaa za tawi zimeunganishwa? (Ona sanduku “Kujenga Ofisi za Tawi Kulingana na Mahitaji.”)

4 Kama tulivyoona katika Sura ya 16, Yehova anataka tukusanyike pamoja kwa ajili ya ibada. (Ebr. 10:25) Mikutano yetu haiimarishi tu imani yetu bali pia inachochea bidii yetu katika kazi ya kuhubiri. Kadiri siku za mwisho zinavyosonga, ndivyo Yehova anavyoendelea kuharakisha kazi hiyo. Matokeo ni kwamba mamia ya maelfu ya watu wanamiminika katika tengenezo lake kila mwaka. (Isa. 60:22) Kwa sababu ya ongezeko kubwa la raia wa Ufalme, kumekuwa na uhitaji mkubwa wa viwanda vya kuchapisha machapisho ya Biblia. Pia tunahitaji majengo zaidi ya ibada.

5. Kwa nini jina Jumba la Ufalme linafaa? (Ona pia sanduku “Kanisa la Nuru Mpya.”)

5 Mwanzoni mwa historia ya watu wa Yehova wa siku za kisasa, Wanafunzi wa Biblia walianza kuona uhitaji wa kuwa na mahali pao pa kufanyia mikutano. Inaonekana kwamba mojawapo ya majengo ya kwanza kujengwa kwa ajili ya ibada lilijengwa huko West Virginia, Marekani, mwaka wa 1890. Kufikia miaka ya 1930, watu wa Yehova walikuwa wamejenga au kukarabati majumba kadhaa, lakini majengo hayo ya ibada hayakuwa yamepewa jina hususa. Hata hivyo, katika mwaka wa 1935, Ndugu Rutherford alitembelea nchi ya Hawaii ambako jumba lilikuwa likijengwa pamoja na ofisi mpya ya tawi. Alipoulizwa jengo hilo linapaswa kuitwaje, Ndugu Rutherford alijibu hivi: “Unaonaje tukiliita ‘Jumba la Ufalme,’ kwa kuwa hiyo ndiyo kazi yetu, tunahubiri habari njema ya Ufalme?” (Mt. 24:14) Baada ya muda mfupi jina hilo linalofaa lingetumiwa katika jumba hilo na katika majengo mengi yanayotumiwa na makutaniko ya watu wa Yehova ulimwenguni pote.

6, 7. Ujenzi wa haraka wa Majumba ya Ufalme umekuwa na matokeo gani?

6 Kufikia miaka ya 1970, uhitaji wa Majumba ya Ufalme ulikuwa ukiongezeka haraka sana. Ili kutosheleza uhitaji huo, akina ndugu nchini Marekani walibuni mbinu ya kujenga Majumba ya Ufalme mazuri kwa siku chache. Kufikia mwaka wa 1983, Majumba ya Ufalme 200 hivi yalikuwa yamejengwa nchini Marekani na Kanada. Ili kutimiza kazi hiyo akina ndugu walianzisha halmashauri za ujenzi za mkoa. Mbinu hiyo ilikuwa na matokeo mazuri hivi kwamba mwaka wa 1986, Baraza Linaloongoza liliuweka rasmi mpango huo, na kufikia mwaka wa 1987, kulikuwa na Halmashauri za Ujenzi za Mkoa (RBC) 60 nchini Marekani. * Kufikia mwaka wa 1992, kulikuwa pia na Halmashauri za Ujenzi za Mkoa katika nchi za Afrika Kusini, Argentina, Australia, Hispania, Japani, Mexico, Ufaransa, na Ujerumani. Kwa kweli, ndugu zetu wenye bidii wanaojenga Majumba ya Ufalme na Majumba ya Kusanyiko wanahitaji utegemezo wetu, kwa kuwa kazi wanayofanya ni sehemu ya utumishi mtakatifu.

7 Majumba hayo ya Ufalme yaliyojengwa haraka yalitoa ushahidi mzuri katika maeneo ambayo yalijengwa. Kwa mfano, nchini Hispania, gazeti moja la habari lilikuwa na kichwa hiki: “Imani Yahamisha Milima.” Likizungumzia ujenzi wa Jumba la Ufalme katika mji wa Martos, gazeti hilo lilisema hivi: “Inawezekanaje katika ulimwengu huu wenye ubinafsi, wajitoleaji wasio na ubinafsi kutoka maeneo mbalimbali [ya Hispania] wasafiri hadi Martos ili kujenga jengo ambalo limevunja rekodi zote kwa kujengwa kwa kasi, kwa ustadi, na kwa utaratibu mzuri?” Makala hiyo ilijibu swali hilo kwa kunukuu maneno haya ya Shahidi aliyejitolea: “Hilo linawezekana tu kwa sababu sisi ni watu wanaofundishwa na Yehova.”

Ujenzi Katika Nchi Zisizo na Uwezo Mkubwa wa Kifedha

8. Katika mwaka wa 1999, programu gani mpya ambayo Baraza Linaloongoza liliikubali, na kwa nini?

8 Mwishoni mwa karne ya 20, watu wengi walimiminika kwenye tengenezo la Yehova katika nchi ambazo ndugu zetu wasio na uwezo mkubwa wa kifedha. Ndugu wenyeji walifanya yote waliyoweza ili kujenga mahali pa kufanyia mikutano. Hata hivyo, katika baadhi ya nchi walihitaji kuvumilia dhihaka na ubaguzi kwa sababu Majumba yao ya Ufalme yalikuwa ya hali ya chini yakilinganishwa na majengo mengine ya ibada. Hata hivyo, kuanzia mwaka wa 1999, Baraza Linaloongoza lilikubali programu ya kuharakisha ujenzi wa Majumba ya Ufalme katika nchi zinazoendelea. Ili kuwe na ‘usawaziko’ pesa kutoka katika nchi tajiri zilitumiwa. (Soma 2 Wakorintho 8:13-15.) Ndugu na dada kutoka nchi nyingine walijitolea kusaidia katika ujenzi.

9. Ni kazi gani ambayo ilionekana kuwa kubwa sana, lakini ilitimizwa jinsi gani?

9 Mwanzoni, kazi hiyo ilionekana kuwa kubwa sana. Ripoti moja ya mwaka wa 2001 ilifunua kwamba Majumba ya Ufalme zaidi ya 18,300 yalikuwa yanahitajika katika nchi 88 zinazoendelea. Hata hivyo, kwa msaada wa roho ya Mungu na Mfalme wetu Yesu Kristo hakuna jambo lisilowezekana. (Mt. 19:26) Katika kipindi cha miaka 15 hivi, kuanzia mwaka wa 1999 hadi 2013, watu wa Mungu walikuwa wamejenga Majumba ya Ufalme 26,849 yakiwa sehemu ya programu hiyo. * Yehova anaendelea kubariki kazi ya kuhubiri, hivi kwamba kufikia mwaka wa 2013, kulikuwa na uhitaji wa Majumba ya Ufalme 6,500 hivi katika nchi hizo, na sasa, mamia ya Majumba ya Ufalme yanahitajika kila mwaka.

Kujenga Majumba ya Ufalme katika nchi zisizo na uwezo mkubwa wa kifedha kuna matatizo ya kipekee

10-12. Ujenzi wa Majumba ya Ufalme umelileteaje sifa jina la Yehova?

10 Ujenzi huo wa Majumba mapya ya Ufalme umelileteaje sifa jina la Yehova? Ripoti moja kutoka ofisi ya tawi ya Zimbabwe ilisema hivi: “Katika kipindi cha mwezi mmoja baada ya Jumba jipya la Ufalme kujengwa, kwa kawaida hudhurio la mikutano huongezeka mara mbili.” Katika nchi nyingi, inaonekana kwamba watu wanasita kuhudhuria mikutano yetu hadi tujenge mahali pazuri pa ibada. Hata hivyo, mara tu Jumba la Ufalme linapojengwa, hudhurio linaongezeka haraka na jumba lingine linahitajika. Hata hivyo, si jumba tu linalowavuta watu kwa Yehova. Upendo wa kweli wa Kikristo unaoonyeshwa na wajenzi hubadili pia maoni ya watu kuhusu tengenezo lake. Fikiria mifano michache.

11 Indonesia. Mwanaume mmoja ambaye alikuwa akitazama ujenzi wa Jumba fulani la Ufalme alipotambua kwamba wafanyakazi wote walikuwa wamejitolea, alisema hivi: “Mnastaajabisha sana! Nimeona kila mmoja wenu akifanya kazi kwa moyo wote na kwa shangwe, hata ingawa hampati mshahara. Nafikiri hakuna dini nyingine kama yenu!”

12 Ukrainia. Mwanamke aliyekuwa akipita kila siku mahali ambapo Jumba la Ufalme lilikuwa likijengwa, alikata shauri kwamba wafanyakazi walikuwa Mashahidi wa Yehova na jengo lingekuwa Jumba la Ufalme. Alisema: “Dada yangu ambaye alikuja kuwa Shahidi alinieleza kuhusu Mashahidi wa Yehova. Baada ya kujionea kazi hiyo ya ujenzi, nilitaka kuwa sehemu ya familia hiyo ya kiroho. Nimeona jinsi wanavyopendana.” Mwanamke huyo alikubali kufundishwa Biblia na alibatizwa mwaka wa 2010.

13, 14. (a) Umejifunza nini kutokana na jinsi wenzi fulani wa ndoa walivyoitikia baada ya kuona ujenzi wa Jumba la Ufalme? (b) Unaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba mahali penu pa ibada panaliletea sifa jina la Yehova?

13 Argentina. Wenzi fulani wa ndoa walimfikia ndugu aliyekuwa akisimamia ujenzi wa Jumba la Ufalme. Mume alisema: “Tumekuwa tukiwatazama mkijenga Jumba hili la Ufalme, na . . . tumeamua kwamba tungependa kujifunza kuhusu Mungu mahali hapa.” Kisha akauliza: “Tunapaswa kufanya nini ili tustahili kuhudhuria mikutano hapa?” Wenzi hao walikubali kujifunza Biblia, ikiwa tu familia nzima ingeshiriki. Akina ndugu walikubali sharti hilo kwa furaha.

14 Hata kama hukupata pendeleo la kusaidia ujenzi wa Jumba la Ufalme ambalo mnatumia, bado unaweza kufanya mengi ili mahali penu pa ibada paliletee sifa jina la Yehova. Kwa mfano, unaweza kuwaalika kwa uchangamfu wanafunzi wako wa Biblia, watu ambao unawafanyia ziara za kurudia, na watu wengine wahudhurie mikutano pamoja nawe kwenye Jumba la Ufalme. Una fursa pia za kusaidia kusafisha na kutunza mahali penu pa ibada. Pia unaweza kutenga kiasi fulani cha pesa ili kuchangia utunzaji wa Jumba la Ufalme au kuchangia ujenzi wa majengo ya ibada katika nchi nyingine. (Soma 1 Wakorintho 16:2.) Kazi zote hizo zinachangia kuliletea sifa jina la Yehova.

Wafanyakazi ‘Wanaojitoa Wenyewe kwa Hiari’

15-17. (a) Sehemu kubwa ya kazi ya ujenzi inafanywa na nani? (b) Umejifunza nini kutokana na masimulizi ya wenzi wa ndoa ambao wameshiriki katika miradi ya ujenzi ya kimataifa?

15 Kazi nyingi zinazofanywa katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na majengo ya ofisi za tawi zinafanywa na ndugu na dada wenyeji. Hata hivyo, mara nyingi wanasaidiwa na ndugu na dada kutoka nchi nyingine ambao wana uzoefu katika ujenzi. Baadhi ya wajitoleaji hao wanapanga mambo yao vizuri ili waweze kufanya kazi ya ujenzi katika nchi nyingine kwa majuma kadhaa. Wengine wamekuwa tayari kutumikia kwa miaka mingi, wakihama kutoka sehemu moja ya ujenzi hadi nyingine.

Timo na Lina Lappalainen (Ona fungu la 16)

16 Ujenzi wa Kimataifa una matatizo ya kipekee, lakini pia una thawabu nyingi. Kwa mfano, Timo na Lina wamefanya kazi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na ofisi za tawi katika nchi mbalimbali barani Amerika Kusini, Asia, na Ulaya. Timo anasema: “Kwa kipindi cha miaka 30 iliyopita mgawo wangu umebadilishwa kila baada ya miaka miwili hivi.” Lina, ambaye aliolewa na Timo miaka 25 iliyopita anasema hivi: “Nimetumikia na Timo katika nchi kumi tofauti. Inahitaji wakati na jitihada nyingi kuzoea chakula cha kigeni, hali ya hewa, eneo jipya la kuhubiri, na kuanzisha marafiki wapya.” * Je, jitihada zao ni za bure? Lina anasema hivi: “Tumepata baraka nyingi licha ya hali ngumu. Ndugu zetu wametuonyesha upendo na ukarimu wa Kikristo na tumeona jinsi ambavyo Yehova ametutunza kwa upendo. Tumejionea pia utimizo wa ahadi ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake kwenye Marko 10:29, 30. Tumepata mara mia zaidi ndugu, dada, na mama wa kiroho.” Timo anasema hivi: “Tunaridhika sana kwa kutumia ustadi wetu kwa ajili ya kusudi bora zaidi, yaani, kushiriki katika kupanua mali za Mfalme.”

17 Darren na Sarah ambao wamesaidia katika miradi ya ujenzi barani Afrika, Amerika ya Kati, Amerika ya Kusini, Asia, Pasifiki ya Kusini, na Ulaya wanahisi kwamba wamepokea zaidi ya kile walichotoa. Licha ya hali ngumu walizokabili, Darren anasema hivi: “Limekuwa pendeleo kubwa sana kufanya kazi pamoja na ndugu kutoka sehemu mbalimbali za ulimwengu. Nimeona kwamba upendo wetu kwa Yehova ni kama kamba inayotuunganisha ulimwengu pote.” Sarah anasema: “Nimejifunza mambo mengi kutoka kwa ndugu na dada wenye tamaduni tofauti-tofauti! Kuona jinsi wanavyojidhabihu ili kumtumikia Yehova kunanichochea niendelee kutoa kilicho bora.”

18. Unabii wa andiko la Zaburi 110:1-3 unatimizwaje?

18 Mfalme Daudi alitabiri kwamba hata ingawa raia wa Ufalme wa Mungu wangekabili hali ngumu, ‘wangejitoa kwa hiari’ ili kuendeleza kazi ya Ufalme. (Soma Zaburi 110:1-3.) Wale wote wanaofanya kazi inayotegemeza Ufalme wanashiriki kutimiza unabii huo. (1 Kor. 3:9) Majengo mengi ya ofisi za tawi, mamia ya Majumba ya Kusanyiko, na makumi ya maelfu ya Majumba ya Ufalme ulimwenguni pote ni uthibitisho unaoonekana wazi kwamba Ufalme wa Mungu ni halisi na unatawala sasa. Ni pendeleo kubwa sana kumtumikia Mfalme Yesu Kristo katika kazi inayomletea Yehova sifa anayostahili kabisa.

^ fu. 6 Katika mwaka wa 2013, wajitoleaji zaidi ya 230,000 walikubaliwa kufanya kazi katika Halmashauri za Ujenzi za Mkoa 132 nchini Marekani. Katika nchi hiyo, halmashauri hizo zilisimamia ujenzi wa Majumba mapya ya Ufalme 75 hivi kwa mwaka na kusaidia kukarabati majumba 900 hivi.

^ fu. 9 Idadi hiyo haihusishi Majumba mengi ya Ufalme yaliyojengwa katika nchi ambazo haziko katika mpango huo.

^ fu. 16 Watumishi na wajitoleaji wa kimataifa wanatumia muda wao mwingi kwenye maeneo ya ujenzi, lakini pia wanayaunga mkono makutaniko katika kazi ya kuhubiri mwishoni mwa juma au jioni.