Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 19

Kazi ya Ujenzi Ambayo Inamuletea Yehova Heshima

Kazi ya Ujenzi Ambayo Inamuletea Yehova Heshima

WAZO KUBWA KATIKA SURA HII

Kazi ya ujenzi ambayo inafanyika duniani pote inategemeza faida za Ufalme

1, 2. (a) Tokea zamani watumishi wa Yehova wamefurahia kufanya nini? (b) Ni jambo gani Yehova anaona kuwa la maana sana?

TOKEA zamani watumishi waaminifu wa Yehova wamefurahia kujenga majengo ambayo yanafanya jina lake lisifiwe. Kwa mufano, Waisraeli walifanya kazi ya kujenga hekalu kwa furaha na walitoa vitu vyao vya kimwili kwa ajili ya kazi hiyo.​—Kut. 35:30-35; 36:1, 4-7.

2 Yehova haone majengo hayo ya kimwili kuwa jambo la kwanza ambalo linamuletea heshima, wala haone majengo hayo kuwa jambo la maana sana. (Mt. 23:16, 17) Zawadi ambayo Yehova anaona kuwa ya maana sana na ambayo inamuletea heshima kuliko zawadi zote, ni ibada ambayo watumishi wake wanamutolea. Na pia roho yao ya kujipendea na bidii ya kazi ambayo wanaonyesha. (Kut. 35:21; Mk. 12:41-44; 1 Tim. 6:17-19) Jambo hilo ni la maana sana. Sababu gani? Kwa sababu siku fulani, majengo hayo yanaweza kubomolewa. Kwa mufano, ile hema ya kutaniko na ile hekalu, je, vingali mupaka leo? Hapana. Majengo hayo hayako tena, lakini Yehova anaendelea kukumbuka ukarimu na kazi ya jasho ambayo watumishi wake walifanya wakati wa ujenzi wa majengo hayo.​—Soma 1 Wakorintho 15:58; Waebrania 6:10.

3. Tutachunguza nini katika sura hii?

3 Pia, watumishi wa Yehova wa leo, wametumika sana ili kujenga Majumba ya Ufalme. Na kazi ambayo tumetimiza kwa uongozi wa Mufalme Yesu Kristo ni ya ajabu kabisa! Bila shaka, Yehova amebariki bidii yetu. (Zab. 127:1) Katika sura hii, tutachunguza kazi fulani ambazo zimefanywa na namna gani kazi hizo zimemuletea Yehova heshima. Tutasoma pia maelezo ya ndugu fulani ambao walishiriki katika kazi ya ujenzi.

Ujenzi wa Majumba ya Ufalme

4. (a) Sababu gani tuna lazima ya Majumba ya Ufalme zaidi? (b) Sababu gani biro za tawi mbalimbali zimeunganishwa? (Soma kisanduku “ Bujenzi wa Beteli Mbalimbali—Kulingana na Uhitaji Ambao Unaendelea Kuongezeka.”)

4 Kama vile tulijifunza katika Sura ya 16, Yehova anatuomba tukusanyike pamoja ili kumuabudu. (Ebr. 10:25) Mikutano yetu inatia nguvu imani yetu, na pia inatufanya tuwe na bidii sana katika kazi ya kuhubiri. Kwa sababu siku za mwisho zinasonga mbele, Yehova anaendelea kuharakisha kazi hiyo. Matokeo ni kwamba, kila mwaka maelfu ya watu wanamiminika katika tengenezo lake. (Isa. 60:22) Kwa sababu hesabu ya raia wa Ufalme inazidi kuongezeka, kuna lazima kubwa ya mashine za kuchapisha vichapo vyenye kutegemea Biblia. Pia, tuna lazima ya Majumba ya Ufalme zaidi.

5. Sababu gani jina Jumba la Ufalme linafaa kabisa? (Soma pia kisanduku “ Kanisa la Nuru Mupya.”)

5 Historia ya watu wa Yehova wa leo, inaonyesha kwamba hapo mwanzoni Wanafunzi wa Biblia walianza kuona ulazima wa kuwa na mahali pao wenyewe pa mikutano. Inajulikana kwamba ni katika Mangaribi mwa muji wa Virginia, Amerika, katika mwaka wa 1890, ndipo palijengwa kwa mara ya kwanza mahali pa ibada. Kufikia miaka ya 1930, watu wa Yehova walikuwa wamejenga ao kutengeneza majumba fulani ya kutosha, lakini majumba hayo yalikuwa bado hayajapewa jina. Lakini, katika mwaka wa 1935, Ndugu Rutherford alitembelea inchi ya Hawaii, wakati huo jumba lenye kukamatana na biro ya tawi lilikuwa linajengwa. Wakati ndugu walimuuliza jumba hilo liitwe kwa jina gani, Ndugu Rutherford alijibu hivi: “Hamuone kwamba linapaswa kuitwa ‘Jumba la Ufalme,’ kwa sababu hiyo ndio kazi ambayo tunafanya, kuhubiri habari njema ya Ufalme?” (Mt. 24:14) Jumba hilo lingepewa jina hilo ambalo linafaa kabisa, lakini pia majumba mengine mengi ambayo makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yanatumia duniani pote kwa ajili ya mikutano yangeitwa kwa jina hilo.

6, 7. Ufundi wa kujenga Majumba ya Ufalme kwa haraka sana umekuwa na matokeo gani?

6 Kufikia miaka ya 1970, iliomba kuwa na Majumba ya Ufalme zaidi na zaidi. Kwa hiyo, ndugu katika Amerika walijifunza ufundi wa kujenga Majumba ya Ufalme kwa siku kidogo tu. Majumba yenye kuvutia, na ambayo hayaombe mambo mengi-mengi. Kufikia mwaka wa 1983, Majumba ya Ufalme karibu 200 kama hayo yalikuwa yamejengwa katika Amerika na Kanada. Ili kutimiza kazi hiyo, ndugu waliunda halmashauri za ujenzi wa eneo. Mupango huo ulisaidia kufanya kazi vizuri sana. Kwa hiyo, katika mwaka wa 1986, Baraza Lenye Kuongoza liliagiza mupango huo uanze kutumika mahali pote. Katika mwaka wa 1987, kulikuwa na Halmashauri za Ujenzi wa Eneo 60 katika Amerika. * Katika mwaka wa 1992, Halmashauri hizo ziliwekwa katika Afrika ya Kusini, Argentina, Australia, Hispania, Japani, Meksiko, Ufaransa, na Ujerumani. Bila shaka, tunapaswa kuunga mukono ndugu ambao wanajenga Majumba ya Ufalme na Majumba ya Mikusanyiko, kwa sababu kazi ambayo wanafanya ni sehemu ya utumishi mutakatifu.

7 Ufundi huo wa kujenga Majumba ya Ufalme kwa haraka ulitoa ushahidi muzuri kwa watu wa mahali ambapo ujenzi huo umefanyika. Kwa mufano, gazeti fulani la huko Hispania liliandika habari hii: “Imani Yenye Kuhamisha Milima.” Ili kuzungumuzia ujenzi kama huo wa Jumba la Ufalme katika muji wa Martos, gazeti hilo liliuliza hivi: “Namna gani inawezekana katika dunia ya leo, yenye kujaa watu wenye kujipenda wenyewe, kuwa na watu kutoka maeneo mbalimbali ya Hispania kukutana katika muji wa Martos ili kujenga tu jumba? Jumba hilo limejengwa kwa uharaka sana, vizuri sana na kwa mupangilio muzuri isivyo kawaida.” Gazeti hilo lilitoa jibu kwa ulizo hilo kwa kurudilia maneno ya Shahidi fulani ambaye alikuwa mufanya kazi mwenye kujipendea: “Inawezekana kwa sababu sisi ni watu ambao wamefundishwa na Yehova.”

Kazi ya Ujenzi Katika Inchi Masikini

8. Katika mwaka wa 1999, Baraza Lenye Kuongoza lilianzisha mupango mupya gani, na kwa sababu gani?

8 Mwisho-mwisho wa miaka ya 1990, katika inchi masikini watu walimiminika katika tengenezo la Yehova. Makutaniko ya inchi hizo yalijikaza kujenga mahali pa kukusanyikia. Lakini, katika inchi fulani ndugu zetu walichekwa na kubaguliwa kwa sababu majumba yao hayakuwa mazuri wakati yalilinganishwa na majengo ya makanisa mengine. Hata hivyo, kuanzia mwaka wa 1999, Baraza Lenye Kuongoza lilianzisha mupango wa kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme katika inchi masikini. Feza ambazo zilitoka katika inchi tajiri zilitumiwa ili kuwe na “usawaziko” kuhusiana na ujenzi wa Majumba ya Ufalme. (Soma 2 Wakorintho 8:13-15.) Na pia, ndugu na dada wa inchi zingine walijitolea ili kusaidia katika kazi hiyo.

9. Ni mupango gani ambao ulionekana kuwa hautawezekana, lakini ni kazi gani ambayo ilifanywa?

9 Mwanzoni, mupango huo ulionekana kuwa hautawezekana. Katika mwaka wa 2001, ripoti fulani ilionyesha kwamba inchi masikini 88 zilikuwa na lazima ya Majumba ya Ufalme zaidi ya 18300. Kwa musaada wa roho ya Mungu na Mufalme wetu Yesu Kristo, hakuna jambo ambalo haliwezekane. (Mt. 19:26) Katika miaka 15 hivi, ni kusema, kuanzia mwaka wa 1999 mupaka mwaka wa 2013, kupitia mupango huo watu wa Mungu wamejenga Majumba ya Ufalme 26849. * Yehova anaendelea kubariki kazi ya kuhubiri, kwa hiyo, katika mwaka wa 2013 kulikuwa bado na lazima ya Majumba ya Ufalme zaidi ya 6500 katika inchi masikini, na kwa wakati huu, kila mwaka kuna lazima ya mamia ya Majumba mengine ya Ufalme.

Kazi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme katika inchi masikini ina matatizo yake

10-12. Namna gani kazi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme imeheshimisha jina la Yehova?

10 Namna gani ujenzi wa Majumba hayo mapya ya Ufalme umeheshimisha jina la Yehova? Ripoti fulani kutoka kwenye Beteli ya Zimbabwe ilisema hivi: “Mwezi moja tu kisha kujengwa kwa Jumba la Ufalme, kwa kawaida huzurio kwenye mikutano linaongezeka mara mbili.” Inaonekana kwamba katika inchi fulani watu wanaanza kukusanyika wakati jumba nzuri kwa ajili ya ibada linajengwa. Wakati Jumba la Ufalme linajengwa, kisha muda kidogo, watu wanakuwa wengi zaidi, na hivyo kunakuwa lazima ya jumba lingine. Hata hivyo, si namna Majumba ya Ufalme yanajengwa tu ndio inafanya watu wamukaribie Yehova. Lakini pia, watu wanabadilisha mawazo yao kuhusu tengenezo la Mungu wakati wanaona upendo wa kweli wa Kikristo ambao unaonyeshwa na ndugu ambao wanajenga majumba hayo. Tuchukue mifano fulani.

11 Indonesia. Mwanaume fulani alikuwa anaangalia namna ndugu walikuwa wanajenga Jumba la Ufalme. Wakati alijua kwamba ndugu wote ni wafanyakazi wa kujitolea, alisema hivi: “Nyinyi ni watu wa ajabu! Nimeona namna kila mumoja wenu anatumika kwa moyo wote na kwa furaha, hata ikiwa hamulipwe feza. Ninafikiri hakuna dini ambayo inalingana na dini yenu!”

12 Ukrainia. Mwanamuke fulani ambaye alikuwa anapita kila siku mahali Jumba la Ufalme lilikuwa linajengwa alitambua mara moja kwamba wafanyakazi wote ni Mashahidi wa Yehova na kwamba jengo hilo lingekuwa Jumba la Ufalme. Alisema hivi: “Nilijua mambo fulani juu ya Mashahidi wa Yehova kupitia dada yangu mudogo ambaye pia ni Shahidi. Wakati niliona namna ndugu walikuwa wanafanya kazi hii ya ujenzi, mimi pia niliamua kuwa katika familia hii ya kiroho. Hapa nimeona namna upendo unaonyeshwa.” Mwanamuke huyo alikubali funzo la Biblia na alibatizwa katika mwaka wa 2010.

13, 14. (a) Maneno ya bibi na bwana ambao walikuwa wanaangalia namna Jumba la Ufalme lilikuwa linajengwa yanakufundisha nini? (b) Unaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba Jumba lenu la Ufalme linaheshimisha jina la Yehova?

13 Arjentina. Bwana fulani na bibi yake walimukaribia ndugu aliyekuwa anasimamia kazi ya ujenzi wa Jumba la Ufalme. Bwana huyo alisema hivi: “Tumewaangalia sana namna munaendelea kujenga jumba lenu, na . . . tumeamua kwamba tutajifunza kuhusu Mungu katika jumba hili.” Kisha akauliza hivi: “Tunapaswa kufanya nini ili tuhuzurie mikutano yenu?” Ndugu waliwaomba wajifunze Biblia. Bwana huyo na bibi yake walisema kwamba watakubali kujifunza Biblia ikiwa tu familia yao yote itakubaliwa pia kujiunga nao katika funzo. Ndugu walikubali ombi hilo kwa furaha.

14 Pengine haukupata pendeleo la kusaidia katika ujenzi wa Jumba lenu la Ufalme, lakini unaweza kufanya mengi katika kusaidia ili Jumba lenu la Ufalme liheshimishe jina la Yehova. Kwa mufano, unaweza kumualika kwa furaha mutu ambaye munajifunza naye Biblia kuhuzuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Unaweza pia kualika watu ambao unarudilia na watu wengine. Unaweza tena kusaidia wakati wa kusafisha na kutengeneza Jumba lenu la Ufalme. Ukipanga mambo yako vizuri, unaweza kutoa muchango wa kujipendea ili kutengeneza Jumba lenu la Ufalme ao kusaidia ili majumba mengine yajengwe katika sehemu zingine za dunia. (Soma 1  Wakorintho 16:2.) Kazi hizo mbalimbali zinasaidia kuheshimisha jina la Yehova.

Wafanyakazi Ambao Wanajitoa kwa Kupenda

15-17. (a) Ni nani ambao wanafanya kazi ya ujenzi? (b) Maelezo ya bibi na bwana ambao wamefanya kazi ya ujenzi katika inchi zingine yamekufundisha nini?

15 Ni ndugu na dada wa mahali ndio wanajenga Majumba ya Ufalme, Majumba ya Mikusanyiko, na majengo ya Beteli. Hata hivyo, mara nyingi wanasaidiwa na ndugu na dada ambao wanatoka katika inchi zingine, na ambao wana uzoefu katika kazi ya kujenga. Kati ya ndugu na dada hao wenye kujitolea, wamoja wamepanga mambo yao vizuri ili waweze kufanya kazi ya ujenzi ambayo inafanywa katika inchi zingine kwa majuma mengi. Wengine wamejitolea ili kutumikia kwa miaka mingi; wakati wanamaliza ujenzi mahali fulani wanapewa mugao wa kuenda kujenga mahali pengine.

Ndugu Timo na bibi yake Lina Lappalainen(ona fungo la 16)

16 Kazi ya kuenda kusaidia katika ujenzi katika inchi zingine ina matatizo yake, lakini pia ina baraka zake. Kwa mufano, ndugu Timo na bibi yake Lina, walienda katika inchi za Asia, Ulaya, na Amerika ya Kusini ili kusaidia katika kazi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme, Majumba ya Mikusanyiko, na Beteli mbalimbali. Ndugu Timo anasema hivi: “Kwa miaka 30 ambayo imepita, karibu kisha miaka miwili nimebadilishwa mugao.” Dada Lina, ambaye alioana na Timo kumekwisha kupita miaka 25, anasema hivi: “Tumetumika na Timo katika inchi 10. Inaomba wakati na kujikaza sana ili kujiambatanisha na hali mupya ya hewa, kuzoea chakula, luga mupya na eneo mupya la kuhubiri, na pia kujifanyia marafiki wapya.” * Kulikuwa na faida yoyote ya kufanya hivyo? Dada Lina anasema hivi: “Yale ambayo yalionekana kuwa matatizo yaligeuka kuwa baraka nyingi. Tumeona upendo wa Kikristo na ukaribishaji na tumeona namna Yehova ametuhangaikia kwa upendo. Pia tumeona utimizo wa ahadi ambayo Yesu alipatia wanafunzi wake, ambayo inapatikana katika andiko la Marko 10:29, 30. Tumepata ndugu, dada na mama wa kiroho mara mia zaidi.” Ndugu Timo anasema hivi: “Tumejisikia kuwa wenye kutosheka sana kwa sababu tunatumia uwezo wetu mbalimbali ili kufanya kazi iliyo nzuri kuliko zote, ni kusema, kufanya mali ya Mufalme iendelee kuongezeka.”

17 Ndugu Darren na bibi yake Sarah, wametumika katika kazi ya ujenzi katika Afrika, Amerika ya Kati, Amerika ya Kusini, Asia, Pasifiki ya Kusini, na Ulaya. Wanasema kwamba, baraka ambazo wamepata ni nyingi kuliko kazi ambayo wamefanya. Hata kama wamepata magumu fulani, ndugu Darren anasema hivi: “Imekuwa pendeleo kutumika pamoja na ndugu wa sehemu mbalimbali za dunia. Nimeona namna upendo wetu kwa Yehova unatuunganisha katika dunia yote.” Dada Sarah anasema pia hivi: “Nimejifunza mambo mengi kutoka kwa ndugu na dada wa sehemu mbalimbali za dunia! Wakati ninaona namna wanajikaza sana kumutumikia Yehova ninachochewa niendelee kumutumikia kwa nguvu zangu zote.”

18. Unabii ambao unapatikana katika andiko la Zaburi 110:1-3 unatimia namna gani?

18 Mufalme Daudi alitabiri kwamba, hata kama raia wa Ufalme wa Mungu watapatwa na magumu, “watajitoa kwa hiari [ao kwa kupenda]” ili kuunga mukono faida za Ufalme. (Soma Zaburi 110:1-3.) Wale wote ambao wanafanya kazi ambayo inaunga mukono Ufalme wanatimiza maneno hayo ya unabii. (1 Kor. 3:9) Hesabu ya Beteli mbalimbali, mamia ya Majumba ya Mikusanyiko, na maelfu ya Majumba ya Ufalme ambayo yanapatikana katika dunia yote, yanaonyesha wazi-wazi kwamba Ufalme wa Mungu ni jambo la kweli kabisa, na kwamba unatawala leo. Bila shaka, tuko na pendeleo kubwa la kumutumikia Mufalme Yesu Kristo, kwa kufanya kazi ambayo inamuletea Yehova heshima ambayo anastahili kabisa!

^ fu. 6 Katika mwaka wa 2013, zaidi ya wajitoleaji 230000 walikubaliwa kutumika katika Halmashauri za Ujenzi wa Eneo 132 katika inchi ya Amerika. Katika inchi hiyo, Halmashauri hizo za Ujenzi zilisimamia ujenzi wa Majumba ya Ufalme mapya karibu 75, na zilisaidia kutengeza Majumba karibu 900 kila mwaka.

^ fu. 9 Majumba mengine mengi ya Ufalme ambayo yalijengwa katika inchi ambazo hazipatikane katika mupango huo hayako katika hesabu hiyo.

^ fu. 16 Wafanyakazi kutoka inchi mbalimbali na wajitoleaji wengine wanatumia muda wao mwingi katika kazi ya ujenzi, lakini mwisho wa juma ao mangaribi, wanaunga mukono makutaniko ya eneo ambamo wanajenga katika kazi ya kuhubiri.