Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 21

Ufalme wa Mungu Unaondoa Maadui Wake

Ufalme wa Mungu Unaondoa Maadui Wake

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Matukio yanayoongoza kwenye vita vya Har–Magedoni

1, 2. (a) Ni mambo gani yanayothibitisha kwamba Mfalme wetu amekuwa akitawala tangu mwaka wa 1914? (b) Tutazungumzia nini katika sura hii?

LIMEKUWA jambo lenye kuimarisha sana imani kuchunguza mambo ambayo Ufalme wa Mungu umetimiza katikati ya adui zake. (Zab. 110:2) Mfalme wetu amekusanya jeshi la wahubiri wa hiari. Amewatakasa na kuwasafisha wafuasi wake kiroho na kiadili. Na licha ya jitihada zote za maadui wa Ufalme kujaribu kutuletea migawanyiko, tunafurahia umoja wa ulimwenguni pote leo. Mambo hayo na mengine mengi yaliyotimizwa na Ufalme ambayo tumechunguza katika kitabu hiki yanatupa uhakika thabiti kwamba tangu mwaka wa 1914, Mfalme wetu amekuwa akitawala katikati ya maadui wa Ufalme.

2 Ufalme huo utafanya mambo yenye kustaajabisha hata zaidi hivi karibuni. ‘Utakuja’ ili ‘kuvunja na kukomesha’ maadui wake. (Mt. 6:10; Dan. 2:44) Hata hivyo, kabla ya wakati huo kufika, matukio mengine muhimu yatatukia. Ni matukio gani hayo? Unabii mwingi wa Biblia unazungumzia swali hilo. Acheni tuchunguze baadhi ya unabii huo ili tuone ni matukio gani ambayo bado yako mbele yetu.

Kitakachotokea Kabla tu ya “Uharibifu wa Ghafula”

3. Tunasubiri tukio gani la kwanza?

3 Tangazo la amani. Katika barua yake kwa Wathesalonike, mtume Paulo alielezea tukio la kwanza ambalo tunasubiri. (Soma 1 Wathesalonike 5:2, 3.) Katika barua hiyo Paulo anaitaja “siku ya Yehova,” ambayo itaanza kwa kushambuliwa kwa “Babiloni Mkubwa.” (Ufu. 17:5) Hata hivyo, kabla tu ya siku ya Yehova kuanza, mataifa yatakuwa yakisema, “Amani na usalama!” Huenda maneno hayo yakarejelea tangazo moja au mfululizo wa matangazo ya pekee. Je, viongozi wa dini watahusika? Kwa kuwa wao ni sehemu ya ulimwengu huu, huenda wakaungana na mataifa kusema, “Kuna amani!” (Yer. 6:14; 23:16, 17; Ufu. 17:1, 2) Tangazo hilo la amani na usalama litakuwa ishara ya kwamba siku ya Yehova iko karibu kuanza. Maadui wa Ufalme wa Mungu “hawataponyoka hata kidogo.”

4. Tunanufaikaje kwa kuelewa maana ya unabii wa Paulo kuhusu tangazo la amani na usalama?

4 Tunanufaika jinsi gani kwa kuelewa maana ya unabii huo? Paulo anasema hivi: “Hamko gizani, hivi kwamba siku hiyo iwafikie ninyi kama vile ambavyo ingewafikia wezi.” (1 The. 5:3, 4) Tofauti na watu wengi, sisi tunajua mambo yanayotukia leo yanaelekea wapi. Ni katika njia gani hususa unabii huo kuhusu amani na usalama utatimizwa? Tunapaswa kusubiri na kuona kile kitakachotukia. Kwa hiyo basi, acheni “tukae macho na kutunza akili zetu.”—1 The. 5:6; Sef. 3:8.

Dhiki Kuu Inaanza

5. Ni nini itakayokuwa sehemu ya kwanza ya ile “dhiki kuu”?

5 Dini inashambuliwa. Kumbuka kwamba Paulo aliandika: “Wakati watakapokuwa wakisema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao mara moja.” Kama vile ambavyo radi hufuatwa na mngurumo mkubwa, ndivyo tu tangazo la “Amani na usalama!” litafuatwa mara moja na “uharibifu wa ghafula.” Ni nini kitakachoharibiwa? Kwanza, “Babiloni Mkubwa,” miliki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo, pia anajulikana kama “yule kahaba.” (Ufu. 17:5, 6, 15) Uharibifu huo wa dini zinazodai kuwa za Kikristo na mashirika yote ya dini za uwongo ndio utakaokuwa mwanzo wa “dhiki kuu.” (Mt. 24:21; 2 The. 2:8) Kwa watu wengi, tukio hilo litakuja bila kutarajiwa. Kwa nini? Kwa sababu hadi wakati huo, yule kahaba atajiona kuwa “malkia” ambaye ‘hataona maombolezo kamwe.’ Lakini atagundua ghafla kwamba alijiamini isivyofaa. Ataondolewa haraka sana, kana kwamba “katika siku moja.”—Ufu. 18:7, 8.

6. Ni nini au ni nani atakayemshambulia “Babiloni Mkubwa”?

6 Ni nini au ni nani atakayemshambulia “Babiloni Mkubwa”? Ni “mnyama-mwitu” mwenye “pembe kumi.” Kitabu cha Ufunuo kinaonyesha kwamba mnyama-mwitu huyo anafananisha Umoja wa Mataifa (UM). Pembe hizo kumi zinawakilisha serikali zote za kisiasa zinazotawala sasa ambazo zinamuunga mkono yule “mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu.” (Ufu. 17:3, 5, 11, 12) Shambulizi hilo litakuwa kubwa kadiri gani? Mataifa ya UM yatapora utajiri wa yule kahaba, yatamrarua, na “kumteketeza kabisa kwa moto.”—Soma Ufunuo 17:16. *

7. Maneno ya Yesu kwenye Mathayo 24:21, 22 yalitimiaje katika karne ya kwanza W.K., na yatatimia jinsi gani hivi karibuni?

7 Kufupishwa kwa siku. Mfalme wetu alifunua mambo yatakayotukia katika kipindi hicho wakati wa dhiki kuu. Yesu alisema: “Kwa sababu ya wale waliochaguliwa siku hizo zitafupishwa.” (Soma Mathayo 24:21, 22.) Maneno ya Yesu yalitimia kwa kiwango kidogo katika mwaka wa 66 W.K., Yehova ‘alipofupisha’ shambulizi la jeshi la Roma dhidi ya Yerusalemu. (Marko 13:20) Kitendo hicho kiliwapa nafasi ya kuokoka Wakristo waliokuwa Yerusalemu na Yudea. Ni nini kitakachotokea ulimwenguni pote wakati wa ile dhiki kuu inayokuja? Yehova, akimtumia Mfalme wetu, ‘atafupisha’ shambulizi la Umoja wa Mataifa dhidi ya dini ili dini ya kweli isiharibiwe pamoja na dini ya uwongo. Hivyo, wakati mashirika ya dini za uwongo yatakapoharibiwa, dini moja tu ya kweli itaokoka. (Zab. 96:5) Acheni sasa tuchunguze ni matukio gani yatakayotokea baada ya sehemu hiyo ya dhiki kuu kupita.

Matukio Yanayoongoza Kwenye Har–Magedoni

8, 9. Huenda Yesu alikuwa akirejelea matukio gani, na watu watatendaje watakapoona matukio hayo?

8 Unabii wa Yesu kuhusu siku za mwisho unaonyesha kwamba matukio kadhaa muhimu yatatukia katika kipindi kinachoongoza kwenye Har–Magedoni. Matukio mawili ya kwanza tutakayochunguza yametajwa kwenye Injili ya Mathayo, Marko, na Luka.—Soma Mathayo 24:29-31; Marko 13:23-27; Luka 21:25-28.

9 Matukio yasiyo ya kawaida mbinguni. Yesu anatabiri hivi: “Jua litatiwa giza, na mwezi hautatoa nuru yake, nazo nyota zitakuwa zikianguka kutoka mbinguni.” Ni wazi kwamba watu hawatatafuta mwongozo kutoka kwa viongozi wa kidini. Je, Yesu alikuwa akirejelea pia kutokea kwa matukio yasiyo ya kawaida mbinguni? Huenda alirejelea matukio hayo. (Isa. 13:9-11; Yoe. 2:1, 30, 31) Watu watatendaje watakapoona matukio hayo? Watapata “maumivu makali” kwa sababu ya ‘kutojua njia ya kutokea.’ (Luka 21:25; Sef. 1:17) Naam, maadui wa Ufalme wa Mungu—‘wafalme kwa watumwa’—‘watazimia kwa woga na tarajio la mambo yanayokuja’ na kutafuta mahali pa kujificha. Hata hivyo, hawatapata mahali salama pa kujificha wanapoikimbia ghadhabu ya Mfalme wetu.—Luka 21:26; 23:30; Ufu. 6:15-17.

10. Yesu atatoa hukumu gani, na wale wanaounga mkono Ufalme wa Mungu watatendaje, na wapinzani wa Ufalme wa Mungu watatendaje?

10 Kutolewa kwa hukumu. Maadui wote wa Ufalme wa Mungu hatimaye watalazimishwa kushuhudia tukio ambalo litazidisha maumivu yao. Yesu alisema: ‘Watamwona Mwana wa binadamu akija katika mawingu akiwa na nguvu nyingi na utukufu.’ (Marko 13:26) Wonyesho huo wa mamlaka unaopita uwezo wa mwanadamu utaashiria kwamba Yesu amekuja kuhukumu. Katika sehemu nyingine ya unabii huo kuhusu siku za mwisho, Yesu anatoa habari zaidi kuhusu hukumu hiyo itakayotolewa wakati huo. Tunapata habari hiyo katika mfano wa kondoo na mbuzi. (Soma Mathayo 25:31-33, 46.) Wale wanaounga mkono kwa ushikamanifu Ufalme wa Mungu watahukumiwa kuwa “kondoo” na ‘watainua vichwa vyao,’ wakitambua kwamba “ukombozi [wao] unakaribia.” (Luka 21:28) Hata hivyo, wapinzani wa Ufalme watahukumiwa kuwa “mbuzi,” nao ‘watajipiga-piga kwa huzuni,’ wakitambua kwamba hivi punde “watakatiliwa mbali milele.”—Mt. 24:30; Ufu. 1:7.

11. Tunapaswa kukumbuka nini tunapochunguza matukio yanayokuja?

11 Baada ya Yesu kutoa hukumu yake dhidi ya “mataifa yote,” bado matukio kadhaa muhimu yatatokea kabla ya vita vya Har–Magedoni kuanza. (Mt. 25:32) Tutachunguza matukio mawili kati ya hayo: shambulizi la Gogu na kukusanywa kwa watiwa-mafuta. Tunapochunguza matukio hayo mawili, ni muhimu kukumbuka kwamba Neno la Mungu halifunui wakati hususa wa matukio hayo. Kwa kweli, inaonekana kwamba huenda tukio moja litapishana na tukio lingine kwa kiasi fulani.

12. Ni shambulizi gani kali ambalo Shetani atafanya dhidi ya Ufalme?

12 Shambulizi kali. Gogu wa Magogu atawashambulia watiwa-mafuta ambao wangali duniani na waandamani wao, kondoo wengine. (Soma Ezekieli 38:2, 11.) Shambulizi hilo dhidi ya utawala wa Ufalme uliosimamishwa litakuwa ndilo pambano la mwisho katika vita ambavyo Shetani amekuwa akipigana dhidi ya watiwa-mafuta ambao wangali duniani tangu alipofukuzwa kutoka mbinguni. (Ufu. 12:7-9, 17) Hasa tangu watiwa-mafuta walipoanza kukusanywa katika kutaniko la Kikristo lililopangwa upya, Shetani amejaribu kuharibu hali yao nzuri ya kiroho, bila mafanikio yoyote. (Mt. 13:30) Hata hivyo, baada ya mashirika yote ya dini za uwongo kuharibiwa na watu wa Mungu kuonekana ni kana kwamba wanaishi “bila ukuta, nao hawana hata mapingo na milango,” Shetani ataona kwamba hiyo ni nafasi nzuri ya kuwashambulia. Atayachochea mataifa yaliyo chini ya nguvu zake yashambulie vikali wale wanaounga mkono Ufalme.

13. Yehova ataingiliaje kati kwa niaba ya watu wake?

13 Ezekieli anaeleza yale yatakayotokea. Kuhusu Gogu, unabii unasema hivi: “Utakuja kutoka mahali pako, kutoka sehemu za mbali zaidi za kaskazini, wewe na vikundi vingi vya watu pamoja nawe, hao wote wakiwa wamepanda farasi, kutaniko kubwa, naam, jeshi kubwa sana. Nawe utalazimika kupanda na kuja juu ya watu wangu.” (Eze. 38:15, 16) Yehova atachukua hatua gani dhidi ya uvamizi huo unaoonekana kana kwamba hauwezi kuzuiwa? “Ghadhabu yangu itapanda puani mwangu,” asema Yehova. “Nami nitaita upanga.” (Eze. 38:18, 21; soma Zekaria 2:8.) Yehova ataingilia kati kwa niaba ya watumishi wake duniani. Kuingilia kati huko ndiyo vita vya Har–Magedoni.

14, 15. Ni matukio gani mengine ambayo yatatokea wakati fulani baada ya kuanza kwa shambulizi kali la Shetani?

14 Kabla ya kuanza kuzungumzia jinsi Yehova atakavyowapigania watu wake wakati wa vita vya Har–Magedoni, acheni tutue kidogo na kuchunguza tukio lingine muhimu. Tukio hilo litatokea wakati fulani kati ya mwanzoni mwa shambulizi kali la Shetani na mwanzoni mwa Har–Magedoni wakati Yehova anapoingilia kati. Kama ilivyoelezwa katika fungu la 11, tukio hili la pili ni kukusanywa kwa watiwa-mafuta ambao wangali duniani.

15 Kukusanywa kwa watiwa-mafuta. Mathayo na Marko waliandika kwamba maneno ya Yesu kuhusu ‘watu waliochaguliwa,’ yaani, Wakristo watiwa-mafuta, ni sehemu ya mfululizo wa matukio ambayo yatatokea kabla ya Har–Magedoni kuanza. (Ona fungu la 7.) Yesu alisema hivi alipokuwa akizungumza kujihusu akiwa Mfalme: “Ndipo atakapowatuma malaika na kuwakusanya pamoja watu wake waliochaguliwa kutoka zile pepo nne, kutoka mwisho wa dunia mpaka mwisho wa mbingu.” (Marko 13:27; Mt. 24:31) Yesu anarejelea kukusanywa kwa aina gani katika mistari hiyo? Hazungumzi kuhusu kupigwa muhuri wa mwisho kwa Wakristo watiwa-mafuta ambao wangali duniani, ambako kutatukia muda mfupi tu kabla ya dhiki kuu kuanza. (Ufu. 7:1-3) Badala yake, Yesu anarejelea tukio fulani ambalo litatukia wakati wa dhiki kuu inayokuja. Hivyo, huenda wakati fulani baada ya kuanza kwa shambulizi kali la Shetani dhidi ya watu wa Mungu, watiwa-mafuta ambao wangali duniani watakusanywa na kwenda mbinguni.

16. Watiwa-mafuta waliofufuliwa watashiriki kufanya nini katika vita vya Har–Magedoni?

16 Kukusanywa kwa watiwa-mafuta ambao wangali duniani kunahusianaje na tukio ambalo litafuata, yaani, Har–Magedoni? Kipindi hicho cha kukusanywa kinaonyesha kwamba watiwa-mafuta wote watakuwa mbinguni kabla ya vita vya Mungu vya Har–Magedoni kuanza. Wakiwa mbinguni, wale 144,000 watakaotawala pamoja na Kristo watapokea mamlaka ili washiriki pamoja na Yesu kutumia “fimbo ya chuma” kuwaharibu maadui wa Ufalme wa Mungu. (Ufu. 2:26, 27) Kisha, wakiwa pamoja na malaika wenye nguvu, watiwa-mafuta hao waliofufuliwa watamfuata Kristo, Mfalme-Shujaa, anapoanza kulikabili “jeshi kubwa sana” la maadui ambalo linavizia windo lao, yaani, watu wa Yehova. (Eze. 38:15) Wakati makabiliano hayo makali yanapotokea, vita vya Har–Magedoni vinaanza!—Ufu. 16:16.

Mwisho Wenye Utukufu wa Dhiki Kuu

Vita Vya Har-magedoni vinaanza!

17. Ni nini kitakachowapata “mbuzi” wakati wa Har–Magedoni?

17 Kutekelezwa kwa hukumu. Vita vya Har–Magedoni ndivyo vitakavyokuwa mwisho wa dhiki kuu. Wakati huo, Yesu atafanya kazi nyingine ya ziada. Mbali na kuwa Hakimu wa “mataifa yote,” atakuwa pia mtekelezaji hukumu juu ya mataifa, yaani, atatekeleza hukumu juu ya watu wote ambao mapema alikuwa amewahukumu kuwa “mbuzi.” (Mt. 25:32, 33) Akiwa na “upanga mrefu mkali,” Mfalme wetu ‘atayapiga mataifa.’ Ndiyo, wale wote walio mfano wa mbuzi—kuanzia “wafalme” hadi “watumwa”—“watakatiliwa mbali milele.”—Ufu. 19:15, 18; Mt. 25:46.

18. (a) Hali ya “kondoo” itabadilika jinsi gani? (b) Yesu atakamilishaje ushindi wake?

18 Kwa kweli, hali zitabadilika sana kwa wale ambao Yesu alikuwa amewahukumu kuwa “kondoo”! Badala ya kukanyagwa-kanyagwa na jeshi kubwa sana la Shetani la “mbuzi,” “umati mkubwa” wa “kondoo” ambao wanaonekana kwamba hawawezi kujipigania utaokoka shambulizi la maadui na ‘utatoka katika ile dhiki kuu.’ (Ufu. 7:9, 14) Kisha, baada ya Yesu kuwashinda na kuwaondoa wanadamu wote ambao ni maadui wa Ufalme wa Mungu, atamtupa Shetani na roho wake waovu ndani ya abiso. Wakiwa humo watakuwa wamewekwa katika hali kama ya wafu, yaani, hali ya kutotenda kwa miaka elfu moja.—Soma Ufunuo 6:2; 20:1-3.

Tunaweza Kujitayarisha Jinsi Gani?

19, 20. Tunaweza kutumiaje mambo tunayojifunza kwenye Isaya 26:20 na 30:21?

19 Tunaweza kujitayarisha jinsi gani kwa ajili ya matukio yenye kushtua ambayo yako mbele yetu? Gazeti Mnara wa Mlinzi lilisema hivi miaka kadhaa iliyopita: “Wokovu utategemea utii.” Kwa nini? Jibu linapatikana katika onyo ambalo Yehova aliwapa Wayahudi waliokuwa wakiishi uhamishoni katika Babiloni la kale. Yehova alitabiri kwamba Babiloni lingeharibiwa, hata hivyo, watu wa Mungu walipaswa kufanya nini ili kujitayarisha kwa ajili ya tukio hilo? Yehova alisema hivi: “Nendeni, watu wangu, ingia katika vyumba vyako vya ndani, na ufunge milango nyuma yako. Jifiche kwa kitambo kidogo mpaka hukumu itakapopita.” (Isa. 26:20) Ona maneno yanayotumiwa katika mstari huo: “nendeni,” “ingia,” “ufunge,” “jifiche”—maneno yote hayo ni amri. Wayahudi ambao walitii amri hizo wangekaa ndani ya nyumba zao, mbali kabisa na wanajeshi waliokuwa wakishambulia barabarani. Hivyo, wokovu wao ulitegemea kutii maagizo ya Yehova. *

20 Tunajifunza nini? Kama ilivyokuwa kwa watumishi hao wa zamani wa Mungu, ili tuokoke matukio yanayokuja tunapaswa kutii maagizo ya Yehova. (Isa. 30:21) Tunapata maagizo hayo kupitia mpango wa kutaniko. Kwa hiyo, tunataka kutii kutoka moyoni mwongozo tunaopata. (1 Yoh. 5:3) Tukifanya hivyo leo, itakuwa rahisi zaidi kutii kutoka moyoni wakati ujao na hivyo kulindwa na Baba yetu, Yehova, na Mfalme wetu, Yesu. (Sef. 2:3) Ulinzi huo kutoka kwa Mungu utatuwezesha kuona moja kwa moja jinsi ambavyo Ufalme wa Mungu utaondoa kabisa maadui wake. Hilo litakuwa tukio ambalo hatutasahau milele!

^ fu. 6 Ni jambo linalopatana na akili kwamba uharibifu wa “Babiloni Mkubwa” unarejelea hasa uharibifu wa mashirika ya kidini, si mauaji ya watu wote wanaofuata dini. Kwa hiyo, watu wengi ambao zamani walikuwa wafuasi wa Babiloni hawataharibiwa wakati huo, na huenda wakajaribu, hata hadharani, kujitenga na dini, kama inavyoonyeshwa kwenye Zekaria 13:4-6.

^ fu. 19 Kwa habari zaidi, ona Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote I, ukurasa wa 282-283.