Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 21

Ufalme Wa Mungu Unaondoa Maadui Wake

Ufalme Wa Mungu Unaondoa Maadui Wake

WAZO KUBWA KATIKA SURA HII

Matukio ambayo yataongoza kwenye vita ya Har-magedoni

1, 2. (a) Ni ushuhuda gani unaonyesha kwamba Mufalme wetu alianza kutawala kuanzia mwaka wa 1914? (b) Tutachunguza nini katika sura hii?

KUZUNGUMUZIA mambo ambayo Ufalme wa Mungu umetimiza katikati ya maadui wake, bila shaka, kumetia imani yetu nguvu. (Zab. 110:2) Mufalme wetu ametokeza jeshi la wahubiri ambao wanajitoa kwa kupenda. Amesafisha na kutakasa wafuasi wake ili wawe safi kiroho na wawe na mwenendo safi. Maadui wa Ufalme wametumia nguvu zao zote ili kutugawanya, lakini sisi tunaishi kwa umoja katika dunia yote. Mambo hayo na mambo mengine ambayo Ufalme wa Mungu umetimiza ambayo tumejifunza ni ushuhuda wenye kusadikisha kwamba Mufalme wetu ameanza kutawala katikati ya maadui wa Ufalme kuanzia mwaka wa 1914.

2 Ufalme utafanya mambo mengi ya ajabu zaidi wakati unaokuja. ‘Utakuja’ ili ‘kuvunja na kukomesha [ao kuharibu]’ maadui wake wote. (Mt. 6:10; Dan. 2:44) Lakini, mbele jambo hilo, kutakuwa matukio mengine ya maana sana ambayo yatatokea. Ni matukio gani hayo? Unabii mbalimbali wa Biblia unatusaidia kupata jibu la ulizo hilo. Acha tuchunguze unabii fulani ili tujue matukio ambayo tungali tunangojea.

Tukio Ambalo Litatokea Mbele tu ya ‘Uharibifu wa Gafula’

3. Tunangojea tukio gani la kwanza?

3 Tangazo la amani. Katika barua ambayo mutume Paulo aliandikia Wathesalonike, alizungumuzia tukio la kwanza ambalo tunangojea. (Soma 1 Wathesalonike 5:2, 3.) Katika barua hiyo mutume Paulo anazungumuzia “siku ya Yehova.” Siku hiyo itaanza na shambulio la ‘Babiloni Mukubwa.’ (Ufu. 17:5) Hata hivyo, mbele tu ya siku hiyo kuanza, mataifa yatatangaza “amani na usalama!” Pengine maneno hayo yatatolewa katika tangazo moja tu ao yatakuwa matangazo mengi ya maana ambayo yatafuatana. Je, viongozi wa dini wataunga mukono tangazo hilo? Kwa sababu wao ni sehemu ya ulimwengu inawezekana watajiunga na mataifa katika kusema kwamba “kuna amani!” (Yer. 6:14; 23:16, 17; Ufu. 17:1, 2) Tangazo hilo la amani na usalama litakuwa alama ambayo itaonyesha kwamba siku ya Yehova iko karibu kuanza. Maadui wa Ufalme wa Mungu “hawataponyoka hata kidogo.”

4. Kuelewa maana ya unabii wa mutume Paulo kuhusu tangazo la amani na usalama kunatuletea faida gani?

4 Kuelewa maana ya unabii huo kunatuletea faida gani? Mutume Paulo anasema hivi: ‘Hamuko katika giza, hivi kwamba siku hiyo iwafikie ninyi kama vile ambavyo ingewafikia wezi.’ (1 Thes. 5:3, 4) Tofauti na watu wengi leo, tunajua ni wapi matukio ya leo yanatupeleka. Hata hivyo, namna gani unabii huo kuhusu amani na usalama utatimizwa? Tunapaswa kungojea ili kuona ni nini itatokea. Kwa hiyo, acheni ‘tukae macho na kutunza akili zetu.’​—1 Thes. 5:6; Sef. 3:8.

Kuanza kwa ile Ziki Kubwa

5. Ni tukio gani ambalo litaonyesha kwamba ni mwanzo wa ile ziki kubwa?

5 Kushambuliwa kwa dini. Usisahau maneno haya ya mutume Paulo: ‘Wakati watakapokuwa wakisema, Amani na usalama! ndipo uharibifu wa gafula utakapokuwa juu yao.’ Kama vile umeme wa radi unaonekana mbele tu ya radi kupiga, ndivyo kutangazwa kwa “Amani na usalama” kutafuatwa na ‘uharibifu wa gafula.’ Ni nini itaharibiwa? Kwanza, ‘Babiloni Mukubwa,’ ni kusema, dini zote za uongo, ambazo zinaitwa pia “kahaba.” (Ufu. 17:5, 6, 15) Uharibifu huo wa dini zinazojiita kuwa za Kikristo na dini zingine zote za uongo utakuwa ndio mwanzo wa ile ‘ziki kubwa.’ (Mt. 24:21; 2 Thes. 2:8) Kwa watu wengi, tukio hilo litakuja bila wao kutazamia. Sababu gani? Kwa sababu wakati huo kahaba huyo atakuwa mwenye kufikiri kwamba yeye ni “malkia” ambaye ‘hataona maombolezo kamwe.’ Lakini kwa gafula kahaba huyo atatambua kwamba tumaini lake lilikuwa la uongo. Kahaba huyo ataharibiwa haraka sana kama “katika siku moja.”​—Ufu. 18:7, 8.

6. Ni nani ambaye atashambulia ‘Babiloni Mukubwa’?

6 Ni nani ambaye atamushambulia ‘Babiloni Mukubwa’? Ni ‘munyama-mwitu’ mwenye “pembe kumi.” Kitabu cha Ufunuo kinatusaidia kuelewa kwamba munyama huyo ni Umoja wa Mataifa (UM). Zile pembe kumi ni serikali zote za kisiasa za leo ambazo zinaunga mukono ‘munyama-mwitu mwenye rangi nyekundu.’ (Ufu. 17:3, 5, 11, 12) Uharibifu huo utakuwa mukubwa kadiri gani? Mataifa ambayo yanaunda Umoja wa Mataifa yatanyanganya mali yote ya kahaba huyo, yatamukula-kula na, ‘kumuteketeza kabisa kwa moto.’​—Soma Ufunuo 17:16. *

7. Maneno ya Yesu ambayo yanapatikana katika andiko la Mathayo 24:21, 22 yalitimia namna gani wakati wa mitume, na yatatimia namna gani wakati unaokuja?

7 Siku zitafupishwa. Mufalme wetu Yesu alionyesha jambo ambalo litatokea wakati huo wa ziki kubwa. Alisema hivi: “Kwa sababu ya wale waliochaguliwa siku hizo zitafupishwa.” (Soma Mathayo 24:21, 22.) Maneno hayo ya Yesu yalitimia kwa kiasi kidogo katika mwaka wa 66, wakati Yehova ‘alifupisha’ shambulio la jeshi la Roma juu ya Yerusalemu. (Mk. 13:20) Jambo hilo lilisaidia Wakristo wa Yerusalemu na Yudea waweze kuokoka. Kwa hiyo, ni nini itatokea duniani pote wakati wa ile ziki kubwa? Yehova, kupitia Mufalme wetu ‘atafupisha’ shambulio la Umoja wa Mataifa juu ya dini ili dini ya kweli isiweze kuhabiriwa pamoja na dini za uongo. Kwa hiyo, dini zote za uongo zitaharibiwa, lakini dini moja ya kweli tu ndio itaokoka. (Zab. 96:5) Acheni sasa tuchunguze matukio ambayo yatafanyika kisha kupita kwa sehemu hii ya kwanza ya ziki kubwa.

Matukio Ambayo Yatatokea Mbele ya Har-magedoni

8, 9. Yesu alikuwa anazungumuzia matukio gani ya ajabu, na watu watafanya nini wakati wataona mambo hayo?

8 Unabii wa Yesu kuhusu siku za mwisho unaonyesha matukio ya maana ambayo yatatokea mbele ya vita ya Har-magedoni. Matukio mawili ambayo tutachunguza kwanza yanatajwa katika Injili ya Mathayo, Marko, na Luka.​—Soma Mathayo 24:29-31; Mk. 13:23-27; Lu. 21:25-28.

9 Mambo ya ajabu yataonekana katika mbingu. Yesu alitabiri hivi: “Jua litatiwa giza, nao mwezi hautatoa nuru yake, nazo nyota zitaanguka kutoka mbinguni.” Bila shaka, watu hawatatafuta tena nuru kutoka kwa viongozi wa dini, kwa sababu hawatakuwa tena viongozi. Yesu alikuwa anazungumuzia pia mambo fulani ya ajabu ambayo yatatukia katika mbingu? Pengine. (Isa. 13:9-11; Yoe. 2:1, 30, 31) Watu watafanya nini wakati wataona mambo hayo? Watapatwa na “maumivu makali” kwa sababu ‘hawatajua njia ya kutokea.’ (Lu. 21:25; Sef. 1:17) Bila shaka, maadui wa Ufalme wa Mungu, kuanzia kwa wafalme mupaka watumwa, ‘watazimia kwa woga na tarajio la mambo yanayokuja’ na watakimbia ili kuenda kutafuta mahali pa kujificha. Lakini hawatapata mahali penye usalama pa kujificha ili waepuke hasira ya Mufalme wetu.​—Lu. 21:26; 23:30; Ufu. 6:15-17.

10. Yesu atatoa hukumu gani, na wale ambao wanaunga mukono Ufalme wa Mungu watafanya nini, na wapinzani wa Ufalme wa Mungu watafanya nini?

10 Kutoa hukumu. Maadui wote wa Ufalme wa Mungu watalazimika kujionea tukio ambalo litaongeza maumivu yao. Kuhusu jambo hilo Yesu alisema hivi: ‘Watamuona Mwana wa binadamu akija katika mawingu akiwa na nguvu nyingi na utukufu.’ (Mk. 13:26) Tukio hilo la ajabu na lisilo la kawaida litaonyesha kwamba Yesu amekuja kuhukumu. Katika sehemu nyingine ya unabii huo wa Yesu kuhusu siku za mwisho, Yesu anatoa habari zaidi kuhusu hukumu ambayo itatolewa wakati huo. Habari hiyo inapatikana katika mufano wa kondoo na mbuzi. (Soma Mathayo 25:31-33, 46.) Wale ambao wanaunga mukono Ufalme wa Mungu kwa ushikamanifu watahukumiwa na kuonwa kama “Kondoo” na ‘watainua vichwa vyao,’ kwa sababu wakati huo watatambua kwamba ‘ukombozi wao unakaribia.’ (Lu. 21:28) Lakini, maadui wa Ufalme watahukumiwa na kuonwa kama “mbuzi,” na ‘watajipiga-piga wenyewe kwa kuomboleza’ kwa sababu wakati huo watatambua kwamba ‘watakatiliwa mbali milele.’​—Mt. 24:30; Ufu. 1:7.

11. Wakati tunaendelea kuzungumuzia matukio ambayo tunangojea, tunapaswa kukumbuka jambo gani?

11 Kisha Yesu kutoa hukumu juu ya “mataifa yote,” kutakuwa matukio mengine mengi ya maana ambayo yatatokea mbele ya vita ya Har-magedoni. (Mt. 25:32) Tutazungumuzia tu matukio mawili, ni kusema, shambulio la Gogu na kukusanywa kwa watiwa-mafuta. Wakati tunaendelea kuzungumuzia matukio hayo, tukumbuke kwamba Neno la Mungu halifunue ni wakati gani kabisa kila tukio litatokea. Hata hivyo, inaonekana kuwa matukio hayo mawili yatatokea kwa wakati mumoja kwa kadiri fulani.

12. Shambulio kubwa la Shetani juu ya Ufalme litakuwa namna gani?

12 Shambulio kubwa. Gogu wa Magogu atashambulia mabaki ya watiwa-mafuta na ndugu zao kondoo wengine. (Soma Ezekieli 38:2, 11.) Shambulio hilo juu ya Ufalme ambao unatawala litakuwa ndilo shambulio la mwisho katika vita ambayo Shetani anapiganisha mabaki ya watiwa-mafuta tangu kufukuzwa kwake mbinguni. (Ufu. 12:7-9, 17) Zaidi sana tangu Wakristo watiwa-mafuta walianza kukusanywa katika kutaniko la Kikristo ambalo lilianza tena kufanya kazi, Shetani amejaribu sana kuharibu utajiri wao wa kiroho, lakini hakuweza. (Mt. 13:30) Hata hivyo, wakati dini zote za uongo zitakuwa zimeharibiwa, watu wa Mungu wataonekana kuwa ‘wanakaa bila ukuta, [bila] mapingo ao milango.’ Kwa hiyo, Shetani ataona kwamba huo ndio wakati muzuri wa kuwashambulia. Atawachochea watumishi wake kufanya shambulio kubwa juu ya wale ambao wanaunga mukono Ufalme wa Mungu.

13. Namna gani Yehova atapigania watu wake?

13 Nabii Ezekieli anaonyesha jambo ambalo litatokea. Kuhusu Gogu unabii huo unasema hivi: ‘Nawe hakika utakuja kutoka mahali pako, kutoka sehemu za mbali zaidi za kaskazini, wewe na vikundi vingi vya watu pamoja nawe, hao wote wakiwa wamepanda farasi, kutaniko kubwa, ndiyo, jeshi kubwa sana. Nawe utalazimika kupanda na kuja juu ya watu wangu, kama mawingu ili kuifunika inchi.’ (Eze. 38:15, 16) Yehova atafanya nini kuhusu shambulio hilo ambalo litaonekana kuwa haliwezi kuzuiliwa? Yehova anasema hivi: ‘Gazabu [ao hasira] yangu itapanda.’ Tena anasema hivi: “Nami nitaita upanga.” (Eze. 38:18, 21; soma Zekaria 2:8.) Yehova atawapigania watumishi wake walio hapa duniani. Na hiyo ndio itakuwa vita ya Har-magedoni.

14, 15. Ni tukio gani lingine litatokea wakati fulani kisha kuanza kwa shambulio kubwa la Shetani?

14 Mbele ya kuchunguza namna Yehova atapigania watu wake wakati wa vita ya Har-magedoni, acheni tuone kwanza tukio lingine la maana sana. Tukio hilo litafanyika katika kipindi fulani kilicho katikati ya mwanzo wa shambulio kubwa la Shetani juu ya watu wa Mungu na mwanzo wa vita ya Yehova, ni kusema, Har-magedoni. Kama vile tumeona kwenye fungu la 11, tukio la pili ni kukusanywa kwa mabaki ya watiwa-mafuta.

15 Kukusanywa kwa watiwa-mafuta. Mathayo na Marko waliandika tukio ambalo Yesu alizungumuzia kuhusu kukusanywa kwa ‘wale ambao wamechaguliwa,’ ni kusema, Wakristo waliotiwa mafuta na roho. Yesu alionyesha kwamba tukio hilo ni sehemu moja ya mufuatano wa matukio ambayo yatatokea mbele ya Har-magedoni kuanza. (Ona fungu la 7.) Akijizungumuzia yeye mwenyewe katika cheo chake cha Mufalme, Yesu alitabiri hivi: ‘Naye atawatuma malaika zake pamoja na muvumo [ao mulio] mukubwa wa tarumbeta, nao watawakusanya pamoja watu wake waliochaguliwa kutoka kwenye zile pepo ine, kutoka mwisho mumoja wa mbingu mupaka mwisho wake.’ (Mk. 13:27; Mt. 24:31) Yesu anazungumuzia kukusanywa kwa namna gani? Hazungumuzie kuhusu kutiwa muhuri wa mwisho kwa mabaki watiwa-mafuta, jambo hilo litatokea mbele tu ya kuanza kwa ile ziki kubwa. (Ufu. 7:1-3) Yesu anazungumuzia tukio ambalo litatendeka wakati wa ile ziki kubwa. Kwa hiyo, inaonekana kwamba wakati fulani kisha kuanza kwa shambulio kubwa la Shetani juu ya watu wa Mungu, Wakristo watiwa-mafuta ambao watakuwa wangali duniani watakusanywa na kuenda mbinguni.

16. Watiwa-mafuta watasaidia namna gani wakati wa vita ya Har–Magedoni?

16 Kukusanywa kwa mabaki ya watiwa-mafuta, kutamalizika mbele ya tukio ambalo litafuata, ni kusema, Har-magedoni? Wakati ambao umetiwa ili kukusanya watiwa-mafuta unaonyesha kwamba wote watakuwa mbinguni mbele ya kuanza kwa vita ya Mungu, ni kusema, vita ya Har-magedoni. Wale 144000 ambao watatawala mbinguni pamoja na Yesu, watasaidiana na Kristo kutumia “fimbo ya chuma” ya kuharibu maadui wote wa Ufalme wa Mungu. (Ufu. 2:26, 27) Kisha, malaika wenye nguvu pamoja na Wakristo watiwa-mafuta ambao walifufuliwa watamufuata Kristo, Mufalme-Mupiganaji, ili kushambulia “jeshi kubwa” la maadui ambao watakuwa karibu kuharibu watu wa Yehova. (Eze. 38:15) Mapambano ya majeshi hayo mawili itakuwa ndio mwanzo wa vita ya Har-magedoni!​—Ufu. 16:16.

Mwisho Muzuri wa ile Ziki Kubwa

Kuanza kwa vita ya Har_Magedoni!

17. Wakati wa Har-magedoni, watu walio mufano wa “mbuzi” watapatwa na nini?

17 Kutimiza hukumu. Vita ya Har-magedoni ndio itakuwa mwisho wa ile ziki. Wakati huo, Yesu atachukua daraka lingine. Zaidi ya kuwa Muamuzi wa “mataifa yote” atakuwa pia Yule ambaye anatimiza hukumu juu ya mataifa, ni kusema, juu ya watu wote ambao walikuwa wamehukumiwa na kuonwa kama “mbuzi.” (Mt. 25:32, 33) Mufalme wetu “atayapiga mataifa” kwa ‘upanga murefu mukali.’ Bila shaka wale wote ambao wanafananishwa na mbuzi, kuanzia kwa “wafalme” mupaka “watumwa,” wote “watakatiliwa mbali milele.”​—Ufu. 19:15, 18; Mt. 25:46.

18. (a) Hali itabadilika namna gani kwa watu walio mufano wa “kondoo”? (b) Namna gani Yesu atakamilisha ushindi wake?

18 Hali itabadilika kabisa kwa wale ambao walihukumiwa na kuonwa kama “kondoo”! Kuliko kuangamizwa na jeshi kubwa la Shetani, la wale walio kama “mbuzi,” mukutano “mukubwa” ambao ulionekana kama “kondoo” ambao hawana musaada wowote, wataokoka shambulio la adui na ‘watatoka katika ile ziki kubwa.’ (Ufu. 7:9, 14) Kisha, wakati Yesu atamaliza kuondoa maadui wote wa Ufalme wa Mungu, atamutupa Shetani na mashetani wake katika abiso. Katika abiso hiyo, Shetani na mashetani wake watabaki katika hali ya kutotenda ambayo inafananishwa na kifo kwa muda wa miaka elfu moja.​—Soma Ufunuo 6:2; 20:1-3.

Namna Gani Tunaweza Kujitayarisha

19, 20. Namna gani tunaweza kutumikisha maneno ambayo yanapatikana katika andiko la Isaya 26:20na 30:21?

19 Namna gani tunaweza kujitayarisha kwa ajili ya matukio hayo ambayo yataogopesha sana watu? Miaka fulani iliyopita gazeti Munara wa Mulinzi lilisema hivi: “Wale tu ambao wanaonyesha utii ndio wataokoka.” Sababu gani? Jibu la ulizo hilo linapatikana katika maneno ambayo Yehova aliwaambia Wayahudi ambao walikuwa katika uhamisho Babiloni. Yehova alitabiri kwamba Babiloni itashindwa. Kwa hiyo, watu wa Mungu wangefanya nini ili kujitayarisha mbele ya tukio hilo? Yehova aliwaambia hivi: ‘Muende, watu wangu, muingie katika vyumba vyenu vya ndani, na mufunge milango nyuma yenu. Mujifiche kwa kitambo kidogo mupaka hukumu itakapopita.’ (Isa. 26:20) Andiko hilo linatumia maneno kama vile, ‘Muende,’ ‘muingie,’ ‘mufunge,’ na ‘mujifiche.’ Maneno hayo yote ni amri; Wayahudi ambao wangetii maneno hayo, wangepaswa kubaki katika nyumba zao ili wasiuawe na maaskari ambao walishinda muji wa Babiloni, ambao walikuwa wakitembea-tembea katika mabarabara. Bila shaka, wale tu ambao wangeonyesha utii ndio wangeokoka. *

20 Mufano huo unatufundisha nini? Kama watumishi hao wa Mungu wa zamani sisi pia tutaokoka matukio yote ambayo yako mbele yetu ikiwa tu tunaendelea kutii maagizo ya Yehova. (Isa. 30:21) Yehova anatupatia maagizo hayo kupitia kutaniko. Kwa hiyo, tujifunze kuwa na moyo wa kutii maagizo ambayo tunapewa. (1 Yoh. 5:3) Ikiwa tunajikaza kufanya hivyo leo, wakati unaokuja, tutakuwa pia tayari kutii kutoka moyoni, na bila shaka, Baba yetu Yehova na Mufalme wetu Yesu watatulinda. (Sef. 2:3) Ulinzi huo wa Mungu utatusaidia tujionee namna Ufalme wa Mungu utaharibu kabisa maadui wake wote. Bila shaka, litakuwa jambo ambalo hatutaweza kusahau!

^ fu. 6 Ni jambo la akili kufikiri kwamba kuharibiwa kwa ‘Babiloni Mukubwa’ ni kuharibiwa kwa mashirika ya kidini wala si kuuawa kwa watu wa dini. Watu wengi wa Babiloni wataokoka uharibifu huo, na wakati huo watajaribu kuonyesha kijuu-juu kwamba wanajiepusha kabisa na mambo ya dini kama vile andiko la Zekaria 13:4-6 linaonyesha.

^ fu. 19 Ili upate maelezo zaidi, soma Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote I, ukurasa wa 282-283.