Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 22

Ufalme Unatimiza Mapenzi ya Mungu Duniani

Ufalme Unatimiza Mapenzi ya Mungu Duniani

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Ufalme unatimiza ahadi zote za Mungu kuhusiana na wanadamu na dunia

1, 2. (a) Kwa nini nyakati nyingine inaweza kuwa vigumu kuiona Paradiso ikiwa halisi? (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia kuimarisha imani yetu katika ahadi za Mungu?

NDUGU mwaminifu anafika kwenye mkutano akiwa amechoka kwa sababu siku ilikuwa na mikazo mingi. Ametendewa isivyofaa na mwajiri anayetazamia mengi mno, ana mahangaiko ya jinsi atakavyoitunza familia yake, na ana wasiwasi kwa kuwa mke wake ni mgonjwa. Muziki wa wimbo wa kwanza unapoanza, anashusha pumzi na kufurahi kwamba yuko katika Jumba la Ufalme pamoja na ndugu na dada zake. Wimbo huo unahusu tumaini la uzima katika Paradiso, na maneno yake yanamhimiza ajiwazie akiwa katika Paradiso. Anaupenda sana wimbo huo na anapouimba pamoja na familia yake, tumaini la wakati ujao linamfariji.

2 Je, umewahi kuhisi hivyo? Wengi wetu tumewahi kuhisi hivyo. Hata hivyo, ukweli wa mambo ni kwamba maisha katika mfumo huu wa kale yanaweza kufanya iwe vigumu kuiona Paradiso inayokuja kuwa halisi. Hizi ni “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” na ulimwengu tunamoishi haufanani hata kidogo na paradiso. (2 Tim. 3:1) Ni nini kinachoweza kutusaidia tuone tumaini letu kuwa halisi? Tunajuaje kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utatawala wanadamu wote? Acheni tuchunguze baadhi ya unabii kutoka kwa Yehova ambao watu wake waliona ukitimizwa nyakati za kale. Kisha tutachunguza jinsi ambavyo unabii huo na unabii mwingine unaofanana nao unatimia kwa njia yenye kusisimua leo. Mwishowe, imani yetu ikiwa imeimarishwa, tutakazia fikira jinsi unabii huo unavyohusiana na wakati wetu ujao.

Jinsi Yehova Alivyotimiza Ahadi Zake Zamani za Kale

3. Ni ahadi gani iliyowafariji Wayahudi walioishi uhamishoni Babiloni?

3 Wazia jinsi maisha yalivyokuwa kwa Wayahudi walioishi uhamishoni huko Babiloni katika karne ya sita K.W.K. Wengi wao walizaliwa uhamishoni kama wazazi wao, na maisha yalikuwa magumu. Wababiloni waliwadhihaki kwa sababu ya imani yao katika Yehova. (Zab. 137:1-3) Kwa makumi ya miaka, Wayahudi washikamanifu walishikilia tumaini hili zuri la wakati ujao: Yehova aliahidi kuwakusanya watu wake na kuwarudisha katika nchi yao. Yehova alisema kwamba hali zingekuwa nzuri huko. Hata aliilinganisha nchi iliyorudishwa ya Yuda na bustani ya Edeni—paradiso! (Soma Isaya 51:3.) Ahadi hizo zilikusudiwa kuwatia moyo watu wa Mungu, na kuondoa shaka zozote ambazo huenda walikuwa nazo. Zilifanyaje hivyo? Chunguza baadhi ya unabii hususa.

4. Yehova aliwahakikishiaje Wayahudi kwamba wangepata usalama katika nchi yao?

4 Usalama. Wayahudi hao waliokuwa uhamishoni hawangerudi katika paradiso halisi, bali wangerudi katika nchi ya mbali ambayo ilikuwa imeachwa ukiwa kwa miaka 70, nchi ambayo ni watu wachache kati yao waliwahi kuiona. Katika siku hizo, kulikuwa na simba, mbwa-mwitu, chui, na wanyama wengine wawindaji katika nchi zinazotajwa katika Biblia. Huenda mwanaume mwenye familia angejiuliza, ‘Nitawalindaje mke na watoto wangu? Namna gani kondoo na ng’ombe wangu?’ Ni jambo la kawaida kuwa na mahangaiko kama hayo. Fikiria sasa kuhusu ahadi ya Mungu iliyoandikwa katika Isaya 11:6-9 na jinsi ambavyo iliwafariji Wayahudi. (Soma.) Akitumia maneno yenye kupendeza ya kishairi, Yehova aliwahakikishia watu waliokuwa uhamishoni kwamba wao na mifugo yao wangekuwa salama. Simba angekula majani katika maana ya kwamba hangewala ng’ombe wa Wayahudi. Wayahudi waaminifu hawangekuwa na sababu ya kuwaogopa wanyama hao wawindaji. Yehova aliahidi kwamba watu wake wangekuwa salama katika nchi iliyorudishwa ya Yuda, hata nyikani na katika misitu.—Eze. 34:25.

5. Ni unabii gani uliowasaidia Wayahudi waliokuwa wakirudi kwao wawe na uhakika kwamba Yehova angewaandalia mahitaji yao kwa wingi?

5 Maandalizi mengi. Huenda kukawa na mahangaiko mengine. ‘Je, nitaweza kuilisha familia yangu katika nchi hiyo iliyorudishwa? Tutaishi wapi? Je, kutakuwa na kazi ya kufanya, na je, kazi hiyo itakuwa bora kuliko kazi yenye kuchosha tuliyofanya uhamishoni chini ya watu waliotuteka?’ Kupitia unabii ulioongozwa na roho yake, kwa upendo Yehova alijibu maswali hayo pia. Yehova aliahidi kwamba watu wake watiifu wangepata mvua za kutosha; na hivyo udongo ungetokeza mkate “mnono na wenye mafuta,” hilo likionyesha kwamba udongo ungetokeza chakula kwa wingi. (Isa. 30:23) Kuhusu makao na kazi yenye kuridhisha, Yehova aliahidi hivi kuhusu watu wake: “Watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale.” (Isa. 65:21, 22) Naam, katika njia nyingi, maisha yangekuwa mazuri katika nchi ya Yuda yakilinganishwa na maisha ya uhamishoni huko Babiloni ya kipagani. Lakini vipi kuhusu matatizo yao mazito zaidi—matatizo ambayo yaliwafanya wapelekwe uhamishoni?

6. Kwa muda mrefu, watu wa Mungu walikuwa na matatizo gani ya kiroho, na Yehova aliwahakikishia nini Wayahudi waliokuwa wakirudi kutoka uhamishoni?

6 Hali ya kiroho. Miaka mingi kabla ya uhamisho wao, watu wa Mungu tayari walikuwa wagonjwa kiroho. Kupitia nabii Isaya, Yehova alisema hivi kuhusu watu wake: “Kichwa chote kimo katika hali ya ugonjwa, na moyo wote ni mnyonge.” (Isa. 1:5) Walikuwa vipofu na viziwi kiroho, kwa kuwa walikuwa wakiziba masikio yao yasisikilize shauri la Yehova na kufunga macho yao yasione nuru ambayo alikuwa akiwapa. (Isa. 6:10; Yer. 5:21; Eze. 12:2) Ikiwa Wayahudi hao waliokuwa wakirudi nchini kwao wangekabili tena matatizo hayo, wangekuwa na uhakika gani? Je, wangepoteza tena kibali cha Yehova? Ahadi hii ya Yehova iliwapa uhakika: “Katika siku hiyo viziwi hakika watasikia maneno ya kitabu, na kutoka katika mahali penye weusi na kutoka katika giza macho ya vipofu yataona.” (Isa. 29:18) Ndiyo, Yehova angewaponya kiroho watu wake waliotiwa nidhamu na kutubu. Maadamu wangesikiliza na kutii, angewapa mwongozo na nuru ambayo ingeokoa uhai wao.

7. Ahadi za Mungu kwa watu wake waliokuwa uhamishoni zilitimizwaje, na kwa nini utimizo huo unaimarisha imani yetu?

7 Je, Yehova alitimiza ahadi zake? Historia inajibu swali hilo. Wayahudi waliorudi katika nchi yao walipata usalama, maandalizi mengi, na hali nzuri ya kiroho. Kwa mfano, Yehova aliwalinda dhidi ya majirani wao waliokuwa wenye nguvu na wengi kuliko wao. Wanyama wawindaji hawakuangamiza mifugo ya Wayahudi. Ni kweli kwamba Wayahudi hao waliona utimizo mdogo tu wa unabii kuhusu paradiso ambao wanaume kama vile Isaya, Yeremia, na Ezekieli waliandika—lakini utimizo ambao watu wa Mungu waliona ulikuwa wenye kusisimua na ulitimia kwa wakati unaofaa. Tunapotafakari yale ambayo Yehova aliwatendea watu wake huko nyuma, imani yetu itaimarishwa zaidi. Ikiwa utimizo mdogo wa unabii huo ulikuwa wenye kusisimua, namna gani utimizo mkubwa? Fikiria yale ambayo Yehova ametufanyia leo.

Jinsi Ambavyo Yehova Ameanza Kutimiza Ahadi Zake Katika Siku Zetu

8. Watu wa Mungu leo wanafurahia “nchi” ya aina gani?

8 Leo watu wa Yehova hawafanyizi taifa halisi, wala wote hawaishi katika nchi moja. Badala yake, Wakristo watiwa-mafuta wanafanyiza taifa la kiroho, “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16) “Kondoo wengine” ambao ni waandamani wao wanajiunga nao katika “nchi” ya kiroho, yaani, tengenezo lake linaloweza kufananishwa na nchi ambamo wanamwabudu Mungu kwa umoja. Ibada hiyo ni njia yao ya maisha. (Yoh. 10:16; Isa. 66:8) Yehova ametupatia “nchi” ya aina gani? Ni paradiso ya kiroho. Katika paradiso hiyo, ahadi za Mungu kuhusu hali zinazofanana na zile zilizokuwa Edeni zimetimia katika njia ya kiroho yenye kustaajabisha. Fikiria mifano michache.

9, 10. (a) Unabii ulio kwenye Isaya 11:6-9 unatimizwaje leo? (b) Tunaona uthibitisho gani kwamba kuna amani miongoni mwa watu wa Mungu?

9 Usalama. Katika unabii ulioandikwa kwenye Isaya 11:6-9, tunapata picha ya upatano na amani—kati ya wanyama-mwitu na wanadamu pamoja na wanyama wao wa kufugwa. Je, picha hiyo inatimizwa kwa njia ya kiroho leo? Ndiyo! Katika mstari wa 9, tunajifunza ni kwa nini wanyama hao hawatasababisha madhara wala uharibifu: “Kwa maana dunia hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.” Je, “kumjua Yehova” kunabadili tabia za wanyama? Hapana. Watu ndio wanaobadilika wanapomjua Mungu Aliye Juu Zaidi na kujifunza kuiga njia zake zenye amani. Hiyo ndiyo sababu katika paradiso yetu ya kiroho leo, tunaweza kuona jinsi ambavyo unabii huo umetimizwa katika njia inayochangamsha moyo. Chini ya utawala wa Ufalme, wafuasi wa Kristo wanajifunza kuacha tabia zao za kikatili na za kinyama na kuishi kwa amani na upatano pamoja na ndugu na dada zao wa kiroho.

10 Kwa mfano, katika kitabu hiki, tumezungumza kuhusu msimamo wa Wakristo wa kutounga mkono upande wowote—tumezungumzia msingi wa Kimaandiko wa uelewaji wetu na jinsi ambavyo watu wa Mungu wameteswa kwa sababu ya kushikilia msimamo huo. Je, haishangazi kwamba katika ulimwengu huu wenye jeuri, kuna “taifa” la watu wengi kiasi ambao hukataa, hata wanapotishwa kuuawa, kujihusisha katika jeuri ya aina yoyote? Huo ni uthibitisho wa kutosha kuonyesha kwamba raia wa Ufalme wa Kimasihi kwa kweli wanafurahia amani kama ile iliyotajwa na Isaya! Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangetambuliwa kwa upendo ambao wangekuwa nao miongoni mwao. (Yoh. 13:34, 35) Katika kutaniko, kwa subira, Kristo anamtumia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” kuwafundisha Wakristo wote wa kweli kuwa wenye kufanya amani, upendo, na wapole.—Mt. 24:45-47.

11, 12. Ni njaa ya aina gani inayoukumba ulimwengu leo, hata hivyo, Yehova amewaandaliaje watu wake kwa wingi?

11 Maandalizi mengi. Ulimwengu una njaa ya kiroho. Biblia ilionya hivi: “‘Tazama! Siku zinakuja,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘nami nitaleta njaa katika nchi, wala si njaa ya mkate, nami nitaleta kiu, wala si kiu ya maji, bali ya kuyasikia maneno ya Yehova.’” (Amo. 8:11) Je, raia wa Ufalme wa Mungu wanasumbuliwa na njaa pia? Yehova alitabiri tofauti hii kati ya watu wake na maadui wake: “Watumishi wangu watakula, lakini ninyi mtakuwa na njaa. Tazama! Watumishi wangu watakunywa, lakini ninyi mtakuwa na kiu. Tazama! Watumishi wangu watashangilia, lakini ninyi mtaona aibu.” (Isa. 65:13) Je, umejionea utimizo wa maneno hayo?

12 Maandalizi ya kiroho yanamiminika kwetu kama mto ambao unazidi kupanuka na kuongezeka kina. Machapisho yetu yanayotegemea Biblia—na pia rekodi za sauti na video, mikutano na makusanyiko yetu, na habari ambazo zimechapishwa kwenye Tovuti yetu—yote hayo ni mafuriko ya chakula cha kiroho tunachopata katika ulimwengu huu unaokufa njaa. (Eze. 47:1-12; Yoe. 3:18) Je, unasisimuka kuona Yehova akitimiza ahadi ya maandalizi mengi katika maisha yako ya kila siku? Je, unahakikisha kwamba unajilisha kwa ukawaida katika meza ya Yehova?

Makutaniko yetu yanatusaidia kulishwa vizuri, kuwa salama, na wenye afya kiroho

13. Ni katika njia gani umeona utimizo wa ahadi ya Yehova kuhusu macho ya vipofu yakifunguliwa na masikio ya viziwi yakizibuliwa?

13 Hali ya kiroho. Leo, watu wengi ni vipofu na viziwi kiroho. (2 Kor. 4:4) Hata hivyo, Kristo anaponya udhaifu na magonjwa ulimwenguni pote. Je, umeona macho ya vipofu yakifunguliwa na masikio ya viziwi yakizibuliwa? Ikiwa umeona watu wakipata ujuzi sahihi wa kweli ya Neno la Mungu, wakiacha uwongo wa kidini ambao hapo awali uliwafanya wawe vipofu na viziwi wa ile kweli, basi umeona ahadi hii ikitimia: “Katika siku hiyo viziwi hakika watasikia maneno ya kitabu, na kutoka katika mahali penye weusi na kutoka katika giza macho ya vipofu yataona.” (Isa. 29:18) Kila mwaka, mamia ya maelfu ya watu ulimwenguni pote wanaponywa kiroho. Kila mtu anayemuacha Babiloni Mkubwa na kujiunga nasi ili tuabudu katika paradiso yetu ya kiroho ni uthibitisho wa kwamba ahadi za Yehova zimetimia!

14. Imani yetu inaimarishwa tunapotafakari kuhusu uthibitisho gani?

14 Kila sura ya kitabu hiki ina uthibitisho wenye nguvu kwamba Kristo amewaleta wafuasi wake katika paradiso ya kiroho ya kweli katika siku hizi za mwisho. Acheni tuendelee kutafakari baraka nyingi tunazopata katika paradiso hiyo leo. Tukifanya hivyo, imani yetu katika ahadi za Yehova za wakati ujao itaendelea kuimarishwa.

“Ufalme Wako na Uje”

15. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba dunia itakuwa paradiso?

15 Tangu zamani, kusudi la Yehova limekuwa kuifanya dunia kuwa paradiso. Aliwaweka Adamu na Hawa katika bustani ya Edeni, na kuwaamuru wazaane na kuijaza dunia na kuwatunza viumbe wote. (Mwa. 1:28) Hata hivyo, Adamu na Hawa walimfuata Shetani katika uasi na kuwatumbukiza wazao wao wote katika hali ya kutokamilika, dhambi, na kifo. Licha ya hayo, kusudi la Mungu halikubadilika kamwe. Yehova hutimiza kwa ukamili kila neno analosema. (Soma Isaya 55:10, 11.) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba wazao wa Adamu na Hawa wataijaza dunia hii na kuitiisha, na kuwatunza kwa upendo viumbe wa Yehova katika paradiso itakayokuwa duniani kote. Wakati huo, ahadi ambazo Yehova alitoa kwa Wayahudi waliokuwa uhamishoni kuhusu kuishi chini ya hali za kiparadiso zitatimia kwa ukamili! Ona mifano ifuatayo.

16. Biblia inaelezaje usalama tutakaofurahia katika Paradiso?

16 Usalama. Hatimaye, maneno yenye kuchangamsha moyo yanayopatikana kwenye Isaya 11:6-9 yatatimia kwa ukamili katika njia halisi. Wanaume, wanawake, na watoto watakuwa salama salimini mahali popote duniani. Hakuna kiumbe yeyote, iwe mwanadamu au mnyama, atakayewatisha. Hebu wazia wakati ambapo dunia nzima itakuwa makao yako na utaweza kuogelea katika mito, maziwa, na bahari; kupanda milima; na kutembea mbugani bila woga wowote. Na wakati wa usiku, hutakuwa na wasiwasi wowote. Maneno ya Ezekieli 34:25 yatatimia, hivi kwamba watu wa Mungu wataweza ‘kukaa nyikani kwa usalama na kulala katika misitu.’

17. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatuandalia mahitaji yetu kwa wingi Ufalme utakapotawala dunia nzima?

17 Maandalizi mengi. Hebu wazia wakati ambapo hakutakuwa na umaskini, utapiamlo, njaa, wala uhitaji wa kuwa na mifumo ya kutoa huduma za jamii bure. Maandalizi mengi ya kiroho ambayo watu wa Mungu wanafurahia leo ni uhakikisho wa kwamba Mfalme wa Kimasihi atawalisha raia wake katika kila njia. Yesu alipokuwa duniani, alionyesha kwa kiwango kidogo kwamba anaweza kutimiza ahadi hizo, kwa kuwa aliwalisha maelfu ya watu wenye njaa kwa mikate na samaki wachache tu. (Mt. 14:17, 18; 15:34-36; Marko 8:19, 20) Ufalme wa Mungu utakapotawala dunia nzima, unabii mwingi kama huu utatimizwa kihalisi: “Ataleta mvua kwa ajili ya mbegu yako unayoipanda katika udongo, na mkate kuwa mazao ya udongo, ambao utakuwa mnono na wenye mafuta. Mifugo yako italisha katika siku hiyo katika malisho mapana.”—Isa. 30:23.

18, 19. (a) Unabii ulio kwenye Isaya 65:20-22 una maana gani kwako? (b) Ni katika maana gani siku zetu zitakuwa “kama siku za mti”?

18 Leo watu wengi hawana tumaini la kuwa na nyumba nzuri au kazi yenye kuridhisha. Katika ulimwengu huu wenye ufisadi, watu wengi wanahisi kwamba wao na familia zao hawafaidiki na kazi ngumu ambayo wanafanya kwa saa nyingi, bali matajiri na wenye pupa ndio wanaofaidika. Hebu wazia maisha yatakavyokuwa wakati unabii huu utakapotimia ulimwenguni pote: “Watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale. Kwa maana siku za watu wangu zitakuwa kama siku za mti; na watu wangu waliochaguliwa wataitumia kazi ya mikono yao wenyewe kikamilifu.”—Isa. 65:20-22.

19 Inamaanisha nini kwamba siku zetu zitakuwa “kama siku za mti”? Unaposimama chini ya mti mkubwa, je, wewe hustaajabu unapowazia mti huo umekuwa hapo kwa miaka mingapi? Huenda mti huo umekuwapo hata kabla ya mababu zako kuzaliwa. Huenda ukawazia kwamba ikiwa utaendelea kuwa katika hali ya kutokamilika, mti huo utaendelea kuishi kwa miaka mingi sana hata baada ya wewe kufa na kusahauliwa. Ni jambo la fadhili kwamba Yehova anatuhakikishia kuwa katika Paradiso inayokuja, tutaishi muda mrefu na kwa amani! (Zab. 37:11, 29) Siku moja, miti inayoishi miaka mingi sana itaonekana kama nyasi ambazo humea na kunyauka haraka, kwa sababu tutaishi milele!

20. Raia washikamanifu wa Ufalme watafurahia jinsi gani afya kamilifu?

20 Afya kamilifu. Leo, magonjwa na kifo humwathiri kila mtu katika ulimwengu huu. Kwa njia fulani, sisi sote ni wagonjwa—tumeambukizwa ugonjwa hatari sana unaosababisha kifo, ambao unaitwa dhambi. Tiba pekee ni dhabihu ya fidia ya Kristo. (Rom. 3:23; 6:23) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja, Yesu pamoja na watawala wenzake watawasaidia watu wanufaike kikamili na dhabihu hiyo kwa kuondoa hatua kwa hatua dhambi zote kutoka kwa wanadamu waaminifu. Unabii huu wa Isaya utatimia kwa ukamili: “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’ Watu wanaokaa katika nchi hiyo watakuwa wamesamehewa kosa lao.” (Isa. 33:24) Hebu wazia wakati ambapo hakuna mtu atakayekuwa kipofu, kiziwi, au mlemavu. (Soma Isaya 35:5, 6.) Hakuna ugonjwa wowote utakaopita uwezo wa Yesu wa kuponya—iwe ni ugonjwa wa kimwili, kiakili, au kihisia. Raia washikamanifu wa Ufalme watafurahia afya kamilifu!

21. Kifo kitafanywa nini, na kwa nini ahadi hiyo inakufariji?

21 Namna gani matokeo ya kawaida ya ugonjwa, matokeo yasiyoweza kuepukika ya dhambi, yaani, kifo? Kifo ndiye ‘adui yetu wa mwisho,’ ambaye huwashinda wanadamu wote wasio wakamilifu. (1 Kor. 15:26) Lakini, je, kifo ni adui asiyeshindwa machoni pa Yehova? Ona yale ambayo Isaya alitabiri: “Atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.” (Isa. 25:8) Unaweza kuwazia wakati huo? Hakutakuwa na mazishi, makaburi, wala machozi ya huzuni! Badala yake, kutakuwa na machozi ya furaha Yehova anapotimiza ahadi yake yenye kusisimua ya kuwafufua wafu! (Soma Isaya 26:19.) Hatimaye, maumivu yote yaliyosababishwa na kifo yataondolewa.

22. Ni nini kitakachotokea Ufalme wa Kimasihi utakapokuwa umetimiza mapenzi ya Mungu duniani?

22 Kufikia mwisho wa ile Miaka Elfu Moja, Ufalme utakuwa umetimiza mapenzi ya Mungu duniani, na Kristo atamrudishia Baba yake utawala. (1 Kor. 15:25-28) Wanadamu wote, wakiwa wamefikia ukamilifu, watakuwa tayari kwa ajili ya lile jaribu la mwisho Shetani anapofunguliwa kutoka katika hali ya kutotenda, inayofananishwa na abiso. Baada ya jaribu hilo, Kristo atamponda yule nyoka mwovu na wale wote wanaomuunga mkono. (Mwa. 3:15; Ufu. 20:3, 7-10) Lakini wote wanaompenda Yehova watakuwa na tarajio zuri sana. Pengine hakuna maneno yanayoweza kuleta picha ya tarajio hilo kuliko maneno tunayopata katika Biblia. Inaahidi kwamba watu waaminifu watakuwa na “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Rom. 8:21.

Ufalme utatimiza ahadi zote za Yehova kuhusiana na wanadamu na dunia

23, 24. (a) Kwa nini tuna uhakika kwamba ahadi za Mungu zitatimia? (b) Unaazimia kufanya nini?

23 Ahadi hizo si matumaini yasiyo na msingi au ndoto tu. Kwa hakika ahadi za Yehova zitatimia! Kwa nini? Kumbuka maneno ya Yesu tuliyozungumzia katika sura ya kwanza ya kitabu hiki. Aliwafundisha wafuasi wake wasali hivi kwa Yehova: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mt. 6:9, 10) Ufalme wa Mungu si jambo la kuwaziwa tu. Ni halisi! Sasa unatawala mbinguni. Kwa karne moja sasa, umetimiza ahadi za Yehova kwa njia ambazo tunaziona wazi katika kutaniko la Kikristo. Kwa hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba ahadi zote za Yehova zitatimia wakati Ufalme wa Mungu unapokuja kuitawala dunia nzima!

24 Tunajua kwamba Ufalme wa Mungu utakuja. Tunajua kwamba kila neno ambalo Yehova ameahidi litatimia. Kwa nini? Kwa sababu UFALME WA MUNGU UNATAWALA! Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Je, Ufalme unanitawala mimi?’ Acheni tufanye yote tuwezayo kuishi tukiwa raia washikamanifu wa Ufalme huo sasa, ili tunufaike milele na utawala wake mkamilifu na usio na ubaguzi!