Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA 22

Ufalme Unatimiza Mapenzi ya Mungu Duniani

Ufalme Unatimiza Mapenzi ya Mungu Duniani

WAZO KUBWA KATIKA SURA HII

Ufalme unatimiza ahadi zote za Mungu kuelekea wanadamu na dunia

1, 2. (a) Sababu gani wakati mwingine inaweza kuwa vigumu kuona kwamba Paradiso ni jambo la kweli? (b) Ni nini ambayo inaweza kutusaidia tuwe na imani yenye nguvu katika ahadi za Mungu?

FIKIRIA jambo hili: Ndugu fulani mwaminifu anafika kwenye mikutano, ni mwenye kuchoka kabisa kisha kuhangaika sana siku hiyo. Bwana wake wa kazi mwenye kulazimisha mambo mengi amemusumbua sana. Ana mahangaiko kuhusu namna atatunza familia yake, pia anahangaishwa kwa sababu bibi yake anateswa na magonjwa. Wakati anasikia muziki wa wimbo wa kufungua mikutano, anapumua kidogo ili kuonyesha kwamba anapata kitulizo. Anafurahi sana kuwa kwenye Jumba la Ufalme pamoja na ndugu na dada zake. Maneno ya wimbo huo yanazungumuzia tumaini la uzima katika Paradiso, na maneno hayo yanamusaidia aone namna tumaini hilo linatimia na yanamusaidia ajione katika paradiso. Kwa kawaida, ndugu huyo anapenda wimbo huo sana, na wakati anaimba wimbo huo na familia yake, tumaini la wakati ujao linamufariji.

2 Je, umekwisha kujisikia hivyo? Wengi kati yetu wamekwisha kujisikia hivyo. Ni kweli kwamba maisha katika dunia hii yanaweza kutuzuia tusione Paradiso ambayo inakuja kuwa ni jambo la kweli kabisa. Wakati wetu ni ‘nyakati za hatari zilizo ngumu kushugulika nazo,’ na dunia ambayo tunaishi ndani haifanane hata kidogo na Paradiso. (2 Tim. 3:1) Basi, ni nini inaweza kutusaidia tuone tumaini letu kuwa jambo ambalo litatimia kabisa? Namna gani tunajua kabisa kwamba karibuni Ufalme wa Mungu utatawala wanadamu wote? Acha tuzungumuzie unabii fulani mbalimbali ambao Yehova alitoa, unabii ambao watu wa Yehova waliona utimizo wake wakati wa zamani. Kisha tutaona namna gani unabii huo na mwingine unaendelea kutimia leo kwa namna yenye kufurahisha sana. Kisha, kwa sababu imani yetu itakuwa imetiwa nguvu, tutaona baraka ambazo tutapata wakati unabii huo mbalimbali utatimia.

Namna Yehova Alitimiza Ahadi Zake Wakati wa Zamani

3. Ni ahadi gani ambayo iliwatia moyo Wayahudi ambao walikuwa uhamishoni huko Babiloni?

3 Fikiria maisha ya Wayahudi wakati walikuwa uhamishoni huko Babiloni katika miaka ya 500 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. Wengi wao walikomalia huko Babiloni, kama vile wazazi wao pia, na maisha yalikuwa magumu sana. Wababiloni walikuwa wanawacheka kwa sababu ya imani yao kwa Yehova. (Zab. 137:1-3) Kwa muda wa miaka mingi, Wayahudi waliendelea kushikamana na tumaini nzuri ambalo Yehova aliwatolea: Yehova aliahidi kwamba atawakusanya watu wake katika inchi yao. Yehova aliahidi kwamba katika inchi hiyo hali zitakuwa nzuri sana. Hata alilinganisha inchi hiyo ya Yuda wakati watarudi na bustani ya Edeni, ni kusema, Paradiso! (Soma Isaya 51:3.) Mungu alikuwa ameandikisha ahadi hizo ili kuwapa watu wake tumaini, kuondoa mashaka ambayo yangeweza kuvuruga mioyo yao. Ni ahadi gani aliwapatia? Acha tuzungumuzie unabii fulani.

4. Namna gani Yehova aliwahakikishia Wayahudi kwamba wataishi kwa amani katika inchi yao?

4 Kuishi katika usalama. Wayahudi ambao walikuwa uhamishoni, wangerudi, si kabisa katika Paradiso ya kweli, lakini katika inchi ya mbali ambayo ilikuwa imebaki ukiwa kwa muda wa miaka 70. Kati yao, ni wadogo tu ndio walikuwa wamekwisha kuona inchi hiyo. Zamani katika inchi kama vile Palestina ilikuwa kawaida kukutana na simba, mbwa-mwitu, chui na wanyama wengine wakali. Kwa hiyo, baba wa familia angeweza kujiuliza, ‘Namna gani nitalinda bibi yangu na watoto wangu? Namna gani nitalinda kondoo wangu na ngombe zangu?’ Haikuwa vibaya mutu kuwa na mahangaiko kama hayo. Fikiria sasa ahadi ya Mungu ambayo inapatikana katika andiko la Isaya 11:6-9 na uone namna gani ingepaswa kumufariji mutu. (Soma.) Kwa maneno hayo mazuri yenye kuonyesha upendo, Yehova alihakikishia Wayahudi kwamba wao na mifugo yao wangeishi katika usalama. Simba angekula majani, katika maana ya kwamba haingekula tena ngombe zao. Wayahudi waaminifu hawangeogopa wanyama wakali kama hao. Yehova aliahidi kwamba watu wake wangeishi kwa usalama katika inchi ya Yuda ambayo wangerudilia tena, hata katika jangwa ao misitu wangekuwa na usalama.​—Eze. 34:25.

5. Ni unabii gani mbalimbali ulisaidia Wayahudi ambao walirudi kuwa na uhakika kwamba Yehova angewatolea kila kitu kwa uwingi?

5 Kuwa na vitu tele. Mutu angeweza kuwa na mahangaiko mengine kama haya: ‘Katika inchi hiyo nitaweza kabisa kulisha familia yangu? Tutaishi wapi? Nitakuwa na kazi, na kazi hiyo itakuwa nzuri kuliko kazi hii ya jasho ambayo tunafanya katika utumwa na kusukumwa-sukumwa na Wababiloni?’ Kupitia unabii mbalimbali ambao uliongozwa na roho yake, Yehova alijibia maulizo hayo pia. Yehova alikuwa ameahidi kwamba watu wake waaminifu wangekuta inchi yenye kuwa na mvua kwa wakati wake; na kwa hiyo, udongo ungewazalia mukate ‘munono [ao kwa uwingi] na wenye mafuta.’ (Isa. 30:23) Kuhusu nyumba na kazi nzuri, Yehova alikuwa ameahidi watu wake hivi: ‘Watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mutu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mutu mwingine ale.’ (Isa. 65:21, 22) Kwa kweli, katika njia nyingi maisha yao yangekuwa mazuri sana kulinganishwa na maisha yao ya uhamishoni katika inchi ya wapagani ya Babiloni. Lakini, ingekuwa namna gani kuhusu matatizo yao makubwa sana, matatizo ambayo hasa kabisa ndio yalifanya waende katika uhamisho?

6. Zamani sana watu wa Mungu walikuwa wamegonjwa ugonjwa gani, na Yehova aliwahakikishia nini wale ambao walipaswa kurudi kutoka uhamishoni?

6 Kuabudu Yehova kama inavyofaa. Zamani sana mbele ya kuenda uhamishoni, watu wa Mungu waligonjwa sana kiroho. Kupitia nabii Isaya, Yehova aliwaambia watu wake hivi: ‘Kichwa chote kimo katika hali ya ugonjwa, na moyo wote ni munyonge [ao mugonjwa].’ (Isa. 1:5) Katika njia ya kiroho, walikuwa vipofu na viziwi, kwa sababu walifunga masikio yao wasisikie shauri la Yehova, na walifunga macho yao wasione mwangaza ambao alikuwa anawatolea. (Isa. 6:10; Yer. 5:21; Eze. 12:2) Ikiwa wale ambao wangerudi wangebaki katika hali hiyohiyo, wangelikuwa kabisa na usalama? Yehova angewakubali tena? Ahadi ya Yehova iliwahakikishia hivi: “Na katika siku hiyo viziwi hakika watasikia maneno ya kitabu, na kutoka katika mahali penye weusi na kutoka katika giza macho ya vipofu yataona.” (Isa. 29:18) Bila shaka, Yehova angeponesha watu wake kiroho, watu ambao walikuwa wameazibiwa, lakini walitubu. Wakati wote ambao wangeendelea kumusikiliza Yehova na kumutii, yeye angewatolea muongozo na nuru ambayo ingewasaidia waendelee kuishi.

7. Namna gani ahadi za Mungu kwa watu wake ambao walikuwa uhamishoni zilitimia, na sababu gani utimizo huo unatia imani nguvu?

7 Je, Yehova alitimiza ahadi zake? Mambo ambayo yalitokea katika historia ya taifa lake yanajibu ulizo hilo. Wayahudi ambao walirudia katika inchi yao, waliishi katika usalama, walikuwa na vitu tele, na walimuabudu Yehova kama inavyofaa. Kwa mufano, Yehova aliwalinda ili wasishambuliwe na mataifa jirani ambayo yalikuwa yenye nguvu sana na ambayo yalikuwa na watu wengi kuliko wao. Nyama zao za kufugwa hazikuliwa na wanyama wakali. Ni kweli, Wayahudi hao waliona tu utimizo mudogo wa unabii mbalimbali ambao unazungumuzia Paradiso, unabii ambao nabii Isaya, Yeremia na Ezekieli waliandika. Utimizo wa unabii huo ambao watu wa Mungu waliona ulifurahisha sana na hilo ndilo jambo ambalo walihitaji kwa wakati huo. Tukitafakari juu ya mambo ambayo Yehova alifanyia watu wake zamani, imani yetu itakuwa nguvu. Kwa sababu, hapo zamani utimizo mudogo wa unabii huo ulikuwa wenye kufurahisha sana, hauone kama itakuwa ajabu wakati wa utimizo wake mukubwa? Fikiria mambo ambayo Yehova ametutimizia leo.

Namna Yehova Ameanza Kutimiza Ahadi Zake Leo

8. Watu wa Mungu wanafurahia leo ‘inchi’ ya aina gani?

8 Leo, watu wa Yehova hawafanyize taifa moja la kimwili, wala hawaishi katika inchi moja fulani. Lakini, Wakristo watiwa-mafuta wanafanyiza taifa la kiroho, “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16) Watiwa-mafuta na ndugu zao wa “kondoo wengine” wanakutana katika tengenezo la Yehova ambalo linafananishwa na inchi ambamo wanamuabudu Yehova kwa umoja. Ibada hiyo ni sehemu ya maana sana katika maisha yao. (Yoh. 10:16; Isa. 66:8) Na ni ‘inchi’ ya aina gani Yehova amewapatia? Ni paradiso ya kiroho. Katika paradiso hiyo, ahadi za Mungu kuhusu hali za Edeni zimetimizwa kiroho kwa namna ya ajabu. Tuchukue mifano fulani.

9, 10. (a) Namna gani unabii ambao unapatikana katika andiko la Isaya 11:6-9 unatimia leo? (b) Ni nini inaonyesha kwamba watu wa Mungu wanaishi kwa amani?

9 Kuishi katika usalama. Unabii ambao uliandikwa katika Isaya 11:6-9, unazungumuzia hali nzuri sana yenye kuonyesha upatano na amani​—kati ya wanyama na wanadamu na pia kati ya wanyama wao wa kufugwa. Unabii huo unatimizwa kiroho leo? Ndiyo! Katika mustari wa 9, tunajifunza sababu gani viumbe kama hivyo havitaleta hasara wala kuharibisha: ‘Kwa maana dunia hakika itajaa na kumujua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.’ Kwa hiyo, ulizo ni hili, ‘kumujua Yehova’ kunaweza kubadilisha tabia za wanyama? Hapana, ni watu ndio wanaweza kubadilisha tabia zao wakati wanamujua Mungu Aliye Juu Zaidi, na wakati wanajifunza kuiga njia zake za amani. Ndiyo sababu leo, katika paradiso yetu ya kiroho, tunaona utimizo wenye kufurahisha wa unabii huo. Katika utawala wa Ufalme, wafuasi wa Kristo wanaachana kabisa na tabia za jeuri, na tabia zingine za kinyama na wanaishi kwa amani na kwa umoja na ndugu na dada zao.

10 Kwa mufano, katika kitabu hiki tumezungumuzia jambo la Wakristo kutokujiingiza katika mambo ya siasa ao mambo ya vita. Tulizungumuzia sababu zinazotoka katika Biblia na mateso ambayo watu wa Mungu walipambana nayo kwa sababu ya musimamo wao kuhusu jambo hilo. Hauone kwamba ni jambo lenye kufurahisha sana kujua kwamba katika ulimwengu huu wenye kujaa jeuri kuna “taifa” kubwa la watu ambao wanakataa kujiingiza katika jeuri yoyote hata kama wanaambiwa kwamba watauawa? Hiyo ni alama ya ajabu ambayo inaonyesha kwamba raia wa Masiya Mufalme wanafurahia ile amani ambayo ilizungumuziwa katika andiko la Isaya! Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangejulikana kwa upendo ambao wangekuwa nao wao kwa wao. (Yoh. 13:34, 35) Katika kutaniko, kwa uvumilivu Kristo anatumia ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara’ kuwafundisha Wakristo wote wa kweli kuwa watu wa amani, wenye upendo, na wenye tabia nzuri.​—Mt. 24:45-47.

11, 12. Leo, watu wa ulimwengu wana njaa ya namna gani, lakini namna gani Yehova ametolea watu wake chakula kwa uwingi?

11 Kuwa na vitu tele. Watu wa ulimwengu wana njaa sana ya kiroho. Biblia inasema hivi: ‘Tazama! Siku zinakuja, asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, Nami nitaleta njaa katika inchi, wala si njaa ya mukate, nami nitaleta kiu, wala si kiu ya maji, bali ya kuyasikia maneno ya Yehova.’ (Amo. 8:11) Ujiulize, raia wa Ufalme wa Mungu nao wana njaa ya kiroho? Yehova alitabiri kwamba hali ya watu wake itakuwa tofauti na hali ya maadui wao. Alitabiri hivi: ‘Watumishi wangu watakula, lakini ninyi mutakuwa na njaa. Tazama! Watumishi wangu watakunywa, lakini ninyi mutakuwa na kiu. Tazama! Watumishi wangu watashangilia, lakini ninyi mutaona aibu [haya].’ (Isa. 65:13) Umejionea utimizo wa maneno hayo?

12 Tunapewa chakula cha kiroho kwa uwingi. Jambo hilo linafananishwa na muto mukubwa sana na wenye kujaa sana. Tuna vichapo ambavyo vinategemea Biblia, tuna habari mbalimbali ambazo zimerekodiwa na pia tuna video; mikutano na mikusanyiko; habari mbalimbali zenye kupatikana kwenye Internete. Mambo yote hayo yanafanyiza muto mukubwa ambao unaendelea kutiririka, ni kusema, tunapata miongozo mingi ya kiroho katika ulimwengu huu wenye kuwa na njaa kali ya kiroho. (Eze. 47:1-12; Yoe. 3:18) Wewe haufurahi kuona utimizo wa ahadi ya Yehova ya kutolea watu wake chakula cha kiroho kwa uwingi katika siku zetu? Unahakikisha kwamba unakula kwa kawaida kwenye meza ya Yehova?

Makutaniko yetu yanatusaidia ili tuwe wenye kulishwa vizuri kiroho, kuishi katika usalama na kuwa na afya nzuri kiroho

13. Namna gani umejionea utimizo wa ahadi ya Yehova ambayo inasema macho ya vipofu yatafunguliwa na masikio ya viziwi yatafunguliwa?

13 Kuabudu Yehova kama inavyofaa. Leo, watu wengi ni vipofu na viziwi kiroho, na jambo hilo linaenea sana kama ugonjwa wa kuambukiza. (2 Kor. 4:4) Hata hivyo, Kristo anaendelea kuponya ulema mbalimbali na ugonjwa mbalimbali wa kiroho. Je, umekwisha kuona namna macho ya vipofu na masikio ya viziwi yamefunguka? Ikiwa umeona namna watu wamefikia kujua Neno la kweli la Mungu, wameachana na mafundisho ya uongo ya dini ambayo yaliwafanya wasione na kusikia kweli, basi umejionea utimizo wa ahadi hii: “Katika siku hiyo viziwi hakika watasikia maneno ya kitabu, na kutoka katika mahali penye weusi na kutoka katika giza macho ya vipofu yataona.” (Isa. 29:18) Katika dunia yote, kila mwaka maelfu ya watu wanaponyeshwa kiroho. Kila mutu ambaye anaachana na Babiloni Mukubwa na ambaye anajiunga na sisi ili kumuabudu Yehova katika paradiso yetu ya kiroho ni ushuhuda wenye nguvu kwamba ahadi za Yehova zimetimia!

14. Kutafakari juu ya mambo gani kutasaidia imani ya mutu kuwa nguvu?

14 Kila sura ya kitabu hiki ina ushuhuda wenye nguvu ambao unaonyesha kwamba Kristo ameingiza wafuasi wake katika paradiso ya kiroho katika siku hizi za mwisho. Kwa hiyo, acha tuendelee kutafakari juu ya njia mbalimbali ambazo zinaonyesha kwamba tunabarikiwa katika paradiso leo. Tukifanya hivyo, imani yetu katika ahadi za Yehova itaendelea kuwa nguvu.

‘Ufalme Wako Uje’

15. Sababu gani tunaweza kuwa hakika kwamba dunia itakuwa Paradiso?

15 Tokea zamani kusudi la Yehova limekuwa la kuifanya dunia yote kuwa paradiso. Aliwaweka Adamu na Eva katika bustani, na akawapatia amri ya kuzaa watoto na kuijaza dunia na kutunza viumbe vyake vyote. (Mwa. 1:28) Lakini, Adamu na Eva walifuata Shetani katika uasi wake na wakaingiza watoto wao wote katika hali ya kukosa kukamilika, katika zambi, na kifo. Hata hivyo, kusudi la Mungu halikubadilika. Mungu akiisha kusema, lazima maneno yake yatimie. (Soma Isaya 55:10, 11.) Kwa hiyo, tunapaswa kuwa hakika kwamba watoto wa Adamu na Eva wataijaza dunia na kuitiisha, watachunga kwa upendo viumbe vya Yehova katika Paradiso ambayo itaenea katika dunia yote. Wakati huo, unabii mbalimbali ambao ulipewa kwa Wayahudi ambao walikuwa uhamishoni, unabii ambao ulizungumuzia maisha katika paradiso utatimia kwa ukamili! Fikiria mifano hii.

16. Namna gani Biblia inazungumuzia hali ya usalama ambayo tutafurahia katika Paradiso?

16 Kuishi katika usalama. Kwa mwisho, maneno yenye kugusa moyo ambayo yanapatikana katika andiko la Isaya 11:6-9 yatatimia kwa ukamili, si katika hali ya kiroho tu, lakini pia katika hali ya kimwili. Wanaume, wanawake, na watoto wataishi katika usalama, na hawataogopa kitu mahali kote ambako watakuwa duniani. Hakuna kiumbe kitakachotia maisha ya mwengine katika hatari, iwe mwanadamu ao munyama. Fikiria wakati utaona dunia nzima kuwa makao yako, ambako unaweza kuogelea katika muto, ziwa, na bahari kubwa; mahali utaweza kusafiri kwa usalama kabisa kwenye milima mbalimbali na kwenye maeneo ya porini. Na wakati usiku unaingia hautaogopa kitu. Maneno ya andiko la Ezekieli 34:25 yatatimia kabisa-kabisa. Kwa hiyo, itawezekana kwa watu wa Mungu ‘kukaa katika nyika [ao jangwa] kwa usalama na kulala katika misitu [ao pori].’

17. Sababu gani tunaweza kuwa hakika kwamba Yehova atatutolea vitu kwa uwingi wakati Ufalme utatawala juu ya dunia nzima?

17 Kuwa na vitu tele. Piga picha akilini na uone wakati hakutakuwa tena umasikini, njaa, mutu kukosa kula chakula kizuri, ao mashirika ya kutoa misaada. Chakula kingi cha kiroho ambacho watu wa Mungu wanafurahia leo ni uhakikisho kwamba Masiya Mufalme atalisha kabisa watu wake, hawatakosa kitu. Wakati Yesu alikuwa hapa duniani, alionyesha kwa kiasi kidogo kwamba ana uwezo wa kutimiza ahadi hizo, kwa sababu alilisha maelfu ya watu kwa mikate kidogo na samaki kidogo tu. (Mt. 14:17, 18; 15:34-36; Mk. 8:19, 20) Wakati Ufalme wa Mungu utatawala dunia yote, unabii mbalimbali kama huu utatimia katika hali ya kimwili: ‘Ataleta mvua kwa ajili ya mbegu yako unayoipanda katika udongo, na mukate kuwa mazao ya udongo, ambao utakuwa munono [ao mwingi] na wenye mafuta. Mifugo yako italisha katika siku hiyo katika malisho mapana.’​—Isa. 30:23.

18, 19. (a) Unabii ambao uliandikwa katika andiko la Isaya 65:20-22 unamaanisha nini kwako? (b) Inamaanisha nini wakati Biblia inasema kwamba siku zetu zitakuwa ‘kama siku za muti’?

18 Leo, watu wengi wanaweza kufikiri kwamba haiwezekane mutu kuwa na nyumba nzuri ao kufanya kazi nzuri ambayo inaweza kumufanya mutu afurahie maisha. Katika dunia hii mbovu, watu wengi wanaona kwamba wanatumika sana na wanatumia nguvu nyingi, lakini wao na familia zao hawapate faida kabisa, lakini watu matajiri na wenye pupa ndio wanavuna mambo yote mazuri. Fikiria sasa vile maisha itakuwa wakati unabii huu utatimia duniani pote: ‘Watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mutu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mutu mwingine ale. Kwa maana siku za watu wangu zitakuwa kama siku za muti; na watu wangu waliochaguliwa wataitumia kazi ya mikono yao wenyewe kikamilifu.’​—Isa. 65:20-22.

19 Biblia inamaanisha nini wakati inasema kwamba siku zetu zitakuwa ‘kama siku za muti’? Wakati unasimama mbele ya muti mukubwa, haushangazwe wakati unafikiria miaka ambayo muti huo umefanya hapo​​—pengine uko hapo mbele ya wazazi wa wazazi wako kuzaliwa? Bila shaka, ikiwa ungeendelea kuwa katika hali yako ya kutokamilika, wewe ungekufa na muti huo ungeendelea kuongeza siku zake, kuishi kwa amani wakati wewe umekuwa katika hali ya kukumbukwa tu. Hauone kwamba Yehova ni mwema kabisa kwa kutuhakikishia kwamba katika Paradiso, siku zetu zitakuwa nyingi na zenye amani? (Zab. 37:11, 29) Siku inakuja ambayo hata miti ambayo inaishi maisha marefu, itaonekana kuwa inaishi maisha mafupi kama majani. Itakuja na itapita na sisi tutaendelea kuishi milele!

20. Ni nini itasaidia raia wa Ufalme kuwa na afya yenye kukamilika?

20 Afya yenye kukamilika. Leo, katika dunia hii hakuna mutu ambaye anaweza kuepuka ugonjwa na kifo. Kwa njia fulani, sisi wote ni wagonjwa​​—tuna ugonjwa ambao mwanadamu hawezi kuponyesha. Ugonjwa huo unaitwa zambi. Dawa ya ugonjwa huo ni zabihu ya ukombozi ya Kristo tu. (Rom. 3:23; 6:23) Katika Utawala wa Miaka Elfu Moja, Yesu na wale watatawala pamoja naye watasaidia watu kupata faida kabisa na zabihu ya ukombozi. Hatua kwa hatua watamaliza matokeo yote ya zambi ambayo yanawasumbua wanadamu waaminifu. Unabii wa Isaya utatimia katika maana yake kamili: ‘Hakuna mukaaji atakayesema: Mimi ni mugonjwa. Watu wanaokaa katika inchi hiyo watakuwa wamesamehewa kosa lao.’ (Isa. 33:24) Fikiria wakati ambao hakutakuwa na mutu ambaye ni kipofu, kiziwi, ao kilema. (Soma Isaya 35:5, 6.) Hakuna ugonjwa ambao utamushinda Yesu, iwe wa kimwili, kiakili ao wa kimoyoni. Raia wa Ufalme duniani watafurahia kuwa na afya yenye kukamilika!

21. Kifo kitapatwa na nini, na sababu gani ahadi hiyo ni yenye kutia moyo?

21 Lakini, itakuwa namna gani juu ya matokeo ya kawaida ya magonjwa, matokeo ambayo hayaepukike ya zambi, ni kusema, kifo? Huyo ndiye “adui [wetu] wa mwisho,” ambaye mwanadamu asiye mukamilifu hawezi kumushinda, iwe anaishi miaka mingi ao miaka kidogo. (1 Kor. 15:26) Lakini, je, kifo ni adui mwenye kuogopesha kwa Yehova? Fikiria yale nabii Isaya alitabiri: “Atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.” (Isa. 25:8) Jaribu kupiga picha katika akili na kuona wakati huo! Hakuna tena sherehe za maziko, hakuna tena makaburi, hakuna tena machozi ya huzuni! Tofauti na hilo, wakati Yehova atatimiza ahadi yake yenye kufurahisha sana ya kufufua watu waliokufa, kutakuwa na machozi ya furaha! (Soma Isaya 26:19.) Mwisho wa yote, mateso yote ambayo yaliletwa na kifo yatakwisha.

22. Namna gani Ufalme wa Masiya utafikia kutimiza mapenzi ya Mungu kuelekea dunia?

22 Wakati ile miaka Elfu Moja itafikia mwisho wake, Ufalme utakuwa umetimiza mapenzi ya Mungu kuelekea dunia, na Kristo atamurudishia Baba yake Ufalme. (1 Kor. 15:25-28) Kwa sababu wanadamu watakuwa wakamilifu, watakuwa tayari kupambana na jaribu la mwisho wakati Shetani atafunguliwa kutoka abiso, ni kusema, hali ya kutotenda. Kisha, Kristo atamuponda nyoka huyo na wote ambao wanamuunga mukono. (Mwa. 3:15; Ufu. 20:3, 7-10) Lakini, wote ambao wanamupenda Yehova na ambao ni waaminifu kwake, ndio watakuwa na wakati muzuri sana mbele yao. Ni katika Biblia tu, tunaweza kupata maneno yenye kuonyesha vizuri zaidi hali ambayo itakuwa katika dunia mupya. Maneno hayo yanaonyesha kwamba watu waaminifu watakuwa “na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”​—Rom. 8:21.

Ufalme utatimiza ahadi zote za Yehova kuelekea wanadamu na dunia

23, 24. (a) Sababu gani ahadi za Mungu zitatimia bila shaka? (b) Unaazimia kufanya nini?

23 Ahadi hizo zote si matumaini ya bure ao ndoto tu. Ahadi za Yehova zitatimia bila shaka! Sababu gani tuko hakika hivyo? Kumbuka maneno ya Yesu ambayo tulizungumuzia katika sura ya kwanza ya kitabu hiki. Alifundisha wafuasi wake kumuomba Yehova hivi: ‘Ufalme wako uje. Mapenzi yako yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.’ (Mt. 6:9, 10) Ufalme wa Mungu si wazo ambalo mwanadamu fulani ametunga. Ni jambo la kweli kabisa! Leo, unatawala mbinguni. Kwa miaka mia moja sasa, umetimiza ahadi za Yehova kwa njia mbalimbali ambazo zinaonekana wazi katika kutaniko la Kikristo. Kwa hiyo, tunaweza kuwa hakika kwamba ahadi zote za Yehova zitatimia wakati Ufalme wa Mungu utakuja kutumikisha mamlaka yake yote juu ya dunia nzima!

24 Tunajua kabisa kama Ufalme wa Mungu utakuja. Tunajua kwamba kila neno la Yehova litatimia. Sababu gani? Kwa sababu UFALME WA MUNGU UNATAWALA SASA! Ulizo ambalo kila mumoja wetu anapaswa kujiuliza ni hili: Ufalme wa Mungu unanitawala mimi?’ Acha tufanye yote ambayo tunaweza ili kuwa na maisha yenye kuonyesha kwamba, leo, sisi ni raia wa Ufalme wa Mungu, ili tuweze kupata faida ya milele katika utawala wake wenye kukamilika, na wenye haki!