Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza

Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza

Wahubiri wa Ufalme Wapendwa:

HEBU jiwazie ukiwa mshiriki wa familia ya Betheli ya Brooklyn Ijumaa asubuhi, Oktoba 2, 1914. Umeketi mahali pako kwenye meza ukimngojea Ndugu C. T. Russell awasili. Ghafla mlango wa chumba cha kulia chakula unafunguliwa na Ndugu Russell anaingia. Kama kawaida yake, anatua kidogo na kwa uchangamfu anaisalimu familia ya Betheli hivi, “Hamjambo nyote!” Kisha, kabla hajaketi, anapiga makofi na kutoa tangazo hili lenye kusisimua: “Nyakati za Mataifa zimekwisha; siku za wafalme wao zimekwisha!” Unajawa na shangwe kwa kuwa umekuwa ukiitazamia siku hii kwa siku nyingi! Wewe pamoja na washiriki wengine wa familia ya Betheli mnafurahia habari hiyo kwa kupiga makofi kwa muda mrefu.

Miaka mingi imepita tangu Ndugu Russell aliposema maneno hayo yenye kusisimua. Ufalme umetimiza nini tangu wakati huo? Mambo mengi! Kupitia mpango wa Ufalme, Yehova amekuwa akiwasafisha na kuwazoeza hatua kwa hatua watu wake ambao walikuwa maelfu kadhaa katika mwaka wa 1914 na sasa ni zaidi ya milioni saba na nusu. Wewe binafsi umenufaikaje na mazoezi hayo?

Leo mara nyingi sisi husikia ndugu zetu wakisema, “Gari la kimbingu la Yehova liko mwendoni!” na hilo ni kweli. Hata hivyo, ukweli wa mambo ni kwamba tangu mwaka wa 1914, gari hilo la kimbingu ambalo linafananisha sehemu isiyoonekana ya tengenezo la Yehova, limekuwa likisonga kwa mwendo wa kasi sana, kama vile utakavyoona unaposoma kwa makini kitabu hiki. Ili wahubiri habari njema ulimwenguni pote, wahubiri wa Ufalme wametumia mbinu mbalimbali, kutia ndani magazeti ya habari, maandamano ya kutangaza habari, sinema, kadi za ushuhuda, gramafoni, redio, na hata Intaneti.

Kwa sababu ya baraka za Yehova, sasa tunaweza kuchapisha machapisho yetu yenye kupendeza yanayotegemea Biblia katika zaidi ya lugha 670 na kuwapa watu bila malipo. Wajitoleaji wenye kujidhabihu husaidia kujenga Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na majengo ya ofisi za tawi, katika nchi tajiri na nchi zisizo na uwezo mkubwa kifedha. Na kunapokuwa na misiba, kwa upendo ndugu na dada zetu huwasaidia haraka wale walioathiriwa na hivyo kuthibitisha kwamba kwa kweli ‘wamezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.’—Met. 17:17.

Nyakati nyingine, viongozi wa kidini na wapinzani wengine wametunga “matatizo kwa njia ya amri,” lakini imani yetu inaimarishwa tunapoona tena na tena jinsi ambavyo jitihada zao zenye nia mbaya ‘zimeendeleza mbele habari njema.’—Zab. 94:20; Flp. 1: 12.

Ni pendeleo kushirikiana nanyi, ‘watumishi wenzetu wa nyumbani.’ Tunawahakikishia kwamba tunawapenda sana. Tunasali kwamba habari zilizo katika kitabu hiki zitawasaidia kuthamini hata zaidi urithi wenu wa kiroho.—Mt. 24:45.

Tunawatakia mema,

Ndugu zenu,

Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova