Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 3

Yule Atakayetayarisha Njia Azaliwa

Yule Atakayetayarisha Njia Azaliwa

LUKA 1:57-79

  • YOHANA MBATIZAJI AZALIWA NA KUPEWA JINA

  • ZEKARIA ATABIRI JUKUMU LA WAKATI UJAO LA YOHANA

Elisabeti yuko karibu kujifungua. Kwa miezi mitatu, Maria mtu wake wa ukoo amekuwa akiishi pamoja naye. Sasa wakati umefika wa Maria kuondoka na kufunga safari ndefu kuelekea kaskazini kwenda nyumbani kwao huko Nazareti. Baada ya miezi sita hivi, yeye pia atazaa mwana.

Muda mfupi baada ya Maria kuondoka, Elisabeti anajifungua. Inafurahisha kwamba anajifungua bila matatizo, na Elisabeti na mtoto wana afya nzuri! Elisabeti anapowaonyesha majirani na watu wa ukoo yule mtoto, wanashangilia pamoja naye.

Sheria ya Mungu kwa Israeli ilisema kwamba siku nane baada ya kuzaliwa, mtoto wa kiume alipaswa kutahiriwa, na pia kupewa jina. (Mambo ya Walawi 12:2, 3) Baadhi ya watu wanafikiri kwamba mwana wa Zekaria anapaswa kupewa jina la baba yake. Hata hivyo, Elisabeti anaeleza maoni yake kwa kusema: “Hapana! ataitwa Yohana.” (Luka 1:60) Kumbuka kwamba malaika Gabrieli alisema kuwa mtoto huyo anapaswa kuitwa Yohana.

Majirani na watu wa ukoo wanalalamika wakisema: “Hakuna mtu wenu wa ukoo anayeitwa jina hilo.” (Luka 1:61) Wakitumia ishara wanamuuliza Zekaria jina analotaka kumpa mwanawe. Zekaria anaomba kibao na kuandika jibu lake: “Yohana ndilo jina lake.”—Luka 1:63.

Papo hapo, kimuujiza Zekaria anaanza tena kuongea. Huenda unakumbuka kwamba alipoteza uwezo wake wa kuongea alipokosa kuamini maneno ya malaika—kwamba Elisabeti atapata mwana. Basi sasa, Zekaria anapozungumza, majirani wake wanashangaa na kujiuliza: “Mtoto huyu atakuwa mtu wa aina gani?” (Luka 1:66) Wanaona mkono wa Mungu kupitia jinsi Yohana alivyopewa jina.

Kisha, akiwa amejaa roho takatifu, Zekaria anatangaza: “Asifiwe Yehova Mungu wa Israeli, kwa sababu amewakumbuka watu wake na kuwaletea ukombozi. Naye ametuinulia pembe ya wokovu katika nyumba ya Daudi mtumishi wake.” (Luka 1:68, 69) Anaposema “pembe ya wokovu,” anamaanisha Bwana Yesu, ambaye bado hajazaliwa. Zekaria anasema kwamba kupitia huyo, Mungu “atatukomboa kutoka mikononi mwa adui, na kutupatia pendeleo la kumtolea utumishi mtakatifu bila woga kwa ushikamanifu na uadilifu mbele zake siku zetu zote.”—Luka 1:74, 75.

Kuhusu mwanawe, Zekaria anatabiri hivi: “Lakini wewe, mtoto mchanga, utaitwa nabii wa Aliye Juu Zaidi, kwa maana utaenda mbele za Yehova ili kutayarisha njia zake, kuwapa watu wake ujuzi wa wokovu kupitia kusamehewa dhambi zao, kwa sababu ya huruma nyororo za Mungu wetu. Kwa huruma hizo tutapata mapambazuko kutoka juu, ili kuwapa nuru wale wanaokaa gizani na katika kivuli cha kifo na kuongoza hatua zetu kwenye njia ya amani.” (Luka 1:76-79) Unabii huo unatia moyo kwelikweli!

Kufikia wakati huo, Maria ambaye inaonekana bado hajaolewa, amefika nyumbani huko Nazareti. Itakuwaje kwake itakapojulikana kwamba ana mimba?