Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 5

Yesu Alizaliwa Wapi na Wakati Gani?

Yesu Alizaliwa Wapi na Wakati Gani?

LUKA 2:1-20

  • YESU ANAZALIWA BETLEHEMU

  • WACHUNGAJI WANAKUJA KUMUONA MUTOTO YESU

Kaisari Augusto, mutawala wa Serikali ya Roma, ametoa amri kwamba kila mutu anapaswa kujiandikisha. Kwa hiyo Yosefu na Maria wanapaswa kusafiri na kuenda kwenye Yosefu alizaliwa, kusini mwa Yerusalemu, katika muji wa Betlehemu.

Watu wengi wako Betlehemu ili kujiandikisha. Fasi moja tu ya kukaa yenye Yosefu na Maria wanapata ni mahali kwenye punda na wanyama wengine wanachungwa. Yesu anazaliwa mahali hapo. Maria anamufunga katika vitambaa na kumulalisha katika chombo cha kukulishia wanyama.

Mungu alipaswa kuwa aliongoza mambo ili Kaisari Augusto atoe sheria hiyo ya kujiandikisha. Sababu gani? Kwa sababu hilo lilifanya iwezekane Yesu azaliwe Betlehemu, muji wa babu yake Mufalme Daudi. Maandiko yalionyesha tangu zamani kwamba Mutawala mwenye kuahidiwa angezaliwa katika muji huo.—Mika 5:2.

Kwa kweli, usiku huo ni wa maana sana! Inje katika mashamba, mwangaza unaangazia kikundi cha wachungaji. Ni utukufu wa Yehova. Malaika moja anawaambia wachungaji hivi: “Musiogope, kwa maana muangalie! ninawatangazia ninyi habari njema yenye itafurahisha sana watu wote. Kwa sababu leo katika muji wa Daudi, mwokozi amezaliwa kwenu, mwenye ni Kristo Bwana. Na hii ndiyo alama kwenu: Mutamukuta mutoto mudogo amefungwa katika vitambaa na amelala katika chombo cha kulishia wanyama.” Mara moja, malaika wengi wanatokea na kusema: “Utukufu kwa Mungu kwenye nafasi za juu, na amani katika dunia kati ya watu wa nia njema.”—Luka 2:10-14.

Wakati malaika wanaenda, wachungaji wanaambiana hivi: “Tuende mara moja Betlehemu tuone jambo lenye limetendeka, lenye Yehova ametujulisha.” (Luka 2:15) Wanaenda haraka na kumukuta mutoto Yesu pale kwenye malaika aliwaambia wangemukuta. Wakati wachungaji wanaeleza mambo yenye malaika aliwaambia, wote wenye wanasikia jambo hilo wanashangaa. Maria anachukua maneno hayo yote kwa uzito na anafikiri sana juu ya maana yake katika moyo wake.

Watu wengi leo wanaamini kama Yesu alizaliwa tarehe 25 Mwezi wa 12. Lakini katika eneo la Betlehemu, Mwezi wa 12 ni mwezi wa mvua na baridi. Wakati fulani, kunakuwaka hata teluji (neige). Katika kipindi hicho cha mwaka, ni nguvu wachungaji wakuwe inje katika mashamba usiku wote na makundi yao. Tena, haingewezekana mutawala wa Serikali ya Roma awaombe watu wenye tayari walikuwa wanapinga utawala wake wasafiri siku nyingi katika kipindi cha baridi sana ili kuenda kujiandikisha. Ni wazi kwamba, Yesu alizaliwa tarehe fulani katika Mwezi wa 10.