Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 9

Maisha ya Utotoni Huko Nazareti

Maisha ya Utotoni Huko Nazareti

MATHAYO 13:55, 56 MARKO 6:3

  • FAMILIA YA YOSEFU NA MARIA YAONGEZEKA

  • YESU ANAJIFUNZA KAZI

Yesu analelewa huko Nazareti, mji mdogo, usio maarufu. Mji huo uko kaskazini, katika eneo lenye vilima liitwalo Galilaya, upande wa magharibi wa ziwa kubwa lijulikanalo kama Bahari ya Galilaya.

Yesu ameletwa hapa na Yosefu na Maria kutoka Misri labda akiwa na umri wa miaka miwili. Inaonekana wakati huu, yeye ndiye mtoto wao pekee. Hata hivyo, ndugu zake wa kambo wanazaliwa baadaye—Yakobo, Yosefu, Simoni, na Yuda. Pia Yosefu na Maria wanazaa watoto wa kike, dada za kambo wa Yesu. Naam, Yesu ana angalau ndugu na dada sita wadogo.

Hapana shaka kwamba Yesu ana watu wengine wa ukoo. Tayari tunajua kuhusu Elisabeti na mwana wake Yohana. Anaishi kilomita nyingi upande wa kusini, huko Yudea. Anayeishi karibu zaidi nao huko Galilaya ni Salome ambaye inaonekana ni dada yake Maria na hivyo ni shangazi ya Yesu. Mume wa Salome ni Zebedayo. Inaelekea wana wao wawili, Yakobo na Yohana, ni binamu wa Yesu. Hatujui ikiwa Yesu alitumia muda mwingi na wavulana hao walipokuwa wakikua, lakini mwishowe wanakuwa waandamani wake wa karibu, wakiwa wawili kati ya mitume wake.

Yosefu anahitaji kufanya kazi kwa bidii ili kuitegemeza familia yake inayoongezeka. Yeye ni seremala. Yosefu anamlea Yesu kama mwana wake mwenyewe, hivyo Yesu anaitwa “mwana wa yule seremala.” (Mathayo 13:55) Yosefu pia anamfundisha Yesu kazi ya useremala, naye Yesu anajifunza vizuri sana. Ndiyo maana baadaye watu wanasema hivi kumhusu Yesu: “Je, huyu si yule seremala?”—Marko 6:3.

Familia ya Yosefu inajihusisha sana na ibada ya Yehova. Kulingana na Sheria ya Mungu, Yosefu na Maria wanawafundisha watoto wao mambo ya kiroho ‘wanapoketi nyumbani mwao na wanapotembea barabarani na wanapolala na wanapoamka.’ (Kumbukumbu la Torati 6:6-9) Huko Nazareti kuna sinagogi. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yosefu anaipeleka familia yake huko kwa ukawaida ili kuabudu. Baadaye inasemwa kwamba “kulingana na desturi yake siku ya Sabato,” Yesu alienda katika sinagogi. (Luka 4:16) Familia hiyo pia ilifurahia sana kusafiri kwa ukawaida kwenda Yerusalemu kwenye hekalu la Yehova.