Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 12

Yesu Abatizwa

Yesu Abatizwa

MATHAYO 3:13-17 MARKO 1:9-11 LUKA 3:21, 22 YOHANA 1:32-34

  • YESU ABATIZWA NA KUTIWA MAFUTA

  • YEHOVA ATANGAZA KWAMBA YESU NI MWANA WAKE

Miezi sita hivi baada ya Yohana Mbatizaji kuanza kuhubiri, Yesu, ambaye sasa ana umri wa miaka 30 hivi, anamjia katika Mto Yordani. Kwa sababu gani? Si kumtembelea kirafiki. Wala si kwa sababu tu Yesu anataka kuona jinsi kazi ya Yohana inavyoendelea. Hapana, Yesu amekuja kumwomba Yohana ambatize.

Hata hivyo, Yohana anakataa: “Mimi ndiye ninayehitaji kubatizwa na wewe, nawe unakuja kwangu?” (Mathayo 3:14) Yohana anajua kwamba Yesu ni Mwana wa kipekee wa Mungu. Kumbuka kwamba Yohana alipokuwa bado tumboni mwa mama yake, aliruka kwa shangwe Maria ambaye alikuwa na mimba ya Yesu, alipomtembelea Elisabeti, mama ya Yohana. Bila shaka baadaye Elisabeti alimwambia Yohana kuhusu jambo hilo. Na huenda Yohana alijua pia kuhusu tangazo lililotolewa na malaika kuhusiana na kuzaliwa kwa Yesu na vilevile kuhusu malaika waliowatokea wachungaji usiku aliozaliwa Yesu.

Yohana anajua kwamba ubatizo anaofanya ni kwa ajili ya wale wanaotubu dhambi zao. Hata hivyo Yesu hana dhambi. Ingawa Yohana anakataa, Yesu anasisitiza: “Acha iwe hivyo wakati huu, kwa maana kwa njia hiyo inafaa tufanye yote yaliyo ya uadilifu.”—Mathayo 3:15.

Kwa nini inafaa Yesu abatizwe? Yesu habatizwi ili kuonyesha kwamba ametubu dhambi. Ubatizo wake unaonyesha kwamba amejitoa ili kufanya mapenzi ya Baba yake. (Waebrania 10:5-7) Yesu alikuwa seremala, lakini sasa wakati umefika wa kuanza huduma ambayo Baba yake wa mbinguni alimtuma afanye duniani. Je, unafikiri Yohana anatarajia jambo lisilo la kawaida litokee anapombatiza Yesu?

Baadaye Yohana anaripoti hivi: “Yule aliyenituma nikabatize katika maji aliniambia: ‘Yeyote ambaye utaona roho ikishuka na kukaa juu yake, huyo ndiye anayebatiza kwa roho takatifu.’” (Yohana 1:33) Basi, Yohana anatazamia kwamba roho ya Mungu itashuka juu ya mtu fulani atakayembatiza. Kwa hiyo, mara tu Yesu anapotoka kwenye maji, Yohana hashangai anapoona “roho ya Mungu ikishuka kama njiwa, ikija juu [ya Yesu].”—Mathayo 3:16.

Lakini zaidi ya hilo mambo mengine pia yanatokea Yesu anapobatizwa. ‘Mbingu zinafunguliwa’ kwa Yesu. Hilo linamaanisha nini? Huenda inamaanisha kwamba Yesu anapobatizwa, anaanza tena kukumbuka maisha yake huko mbinguni kabla ya kuwa mwanadamu. Kwa hiyo, sasa Yesu anakumbuka maisha yake akiwa mwana wa kiroho wa Yehova kutia ndani kweli ambazo Mungu alimfundisha huko mbinguni kabla ya kuja duniani.

Vilevile, Yesu anapobatizwa sauti kutoka mbinguni inatangaza: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:17) Hiyo ni sauti ya nani? Si sauti ya Yesu; kwa kuwa yuko hapo pamoja na Yohana. Hiyo ni sauti ya Mungu. Ni wazi kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu. Yeye si Mungu mwenyewe.

Yesu ni mwana wa kibinadamu wa Mungu, kama alivyokuwa mwanadamu wa kwanza, Adamu. Baada ya mwanafunzi Luka kueleza kuhusu ubatizo wa Yesu, anaandika hivi: “Yesu alikuwa na umri wa miaka 30 hivi alipoanza kazi yake, akiwa mwana, kama alivyoonwa, wa Yosefu, mwana wa Heli, . . . mwana wa Daudi, . . . mwana wa Abrahamu, . . . mwana wa Noa, . . . mwana wa Adamu, mwana wa Mungu.”—Luka 3:23-38.

Kama Adamu alivyokuwa ‘mwana wa kibinadamu wa Mungu,’ ndivyo Yesu alivyo. Yesu anapobatizwa anakuwa na uhusiano mpya na Mungu, anakuwa Mwana wake wa kiroho. Hivyo, Yesu anaweza kufundisha kweli kumhusu Mungu na kuwaonyesha watu njia ya uzima. Yesu anaanza maisha ambayo hatimaye yatamfanya atoe uhai wake wa kibinadamu uwe dhabihu kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi.