Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 13

Jifunze Kutokana na Jinsi Yesu Alivyokabiliana na Vishawishi

Jifunze Kutokana na Jinsi Yesu Alivyokabiliana na Vishawishi

MATHAYO 4:1-11 MARKO 1:12, 13 LUKA 4:1-13

  • SHETANI AMJARIBU YESU

Mara tu baada ya kubatizwa na Yohana, roho ya Mungu inamwongoza Yesu kwenda kwenye nyika ya Yudea. Ana mambo mengi ya kufikiria. Yesu alipobatizwa ‘mbingu zilifunguliwa.’ (Mathayo 3:16) Kwa hiyo, anaweza kukumbuka mambo aliyojifunza na kufanya akiwa mbinguni. Kwa kweli, ana mambo mengi ya kutafakari!

Yesu anakaa nyikani kwa siku 40 mchana na usiku. Katika kipindi hicho hali chakula chochote. Ndipo, Yesu akiwa na njaa sana, Shetani Ibilisi anakuja kumjaribu, anasema: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, yaambie mawe haya yawe mikate.” (Mathayo 4:3) Yesu anajua ni kosa kutumia nguvu zake za kufanya miujiza ili kutosheleza tamaa zake za kibinafsi, hivyo anapinga kishawishi hicho.

Ibilisi anaendelea kumshawishi. Anajaribu njia nyingine. Anamshawishi Yesu ajitupe chini kutoka juu ya mnara wa hekalu. Lakini Yesu hakubali kujionyesha kwa njia hiyo yenye kustaajabisha. Akinukuu Maandiko, Yesu anaonyesha kwamba ni kosa kumjaribu Mungu kwa njia kama hiyo.

Kisha, katika kishawishi cha tatu, kwa njia fulani Ibilisi anamwonyesha Yesu “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo” na kumwambia: “Nitakupa vitu hivi vyote ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.” Tena, Yesu anakataa kabisa na kumwambia: “Nenda zako, Shetani!” (Mathayo 4:8-10) Hashawishiki kufanya makosa kwa kuwa anajua kwamba utumishi mtakatifu unapaswa kutolewa kwa Yehova peke yake. Naam, anachagua kuendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu.

Tunaweza kujifunza kutokana na vishawishi hivyo na jinsi Yesu alivyokabiliana navyo. Vishawishi hivyo vilikuwa halisi, na hilo linaonyesha kwamba Ibilisi si uovu tu kama watu fulani wanavyosema. Yeye ni mtu halisi, asiyeonekana. Simulizi hili linaonyesha pia kwamba serikali za ulimwengu ni mali ya Ibilisi; yeye ndiye anayeziongoza. Ikiwa serikali hizo hazingekuwa zake, je, kishawishi cha kumpa Kristo kingekuwa halisi?

Isitoshe, Ibilisi alisema kwamba alikuwa tayari kumthawabisha Yesu kwa ajili ya tendo moja la ibada, hata kumpa Yesu falme zote za ulimwengu. Ibilisi anaweza kutujaribu kwa njia kama hiyo, labda kwa kuweka mbele yetu nafasi zenye kushawishi za kupata mali za ulimwengu huu, mamlaka, au cheo. Tunatenda kwa hekima tunapofuata mfano wa Yesu kwa kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu hata iwe tumepata kishawishi cha aina gani! Lakini kumbuka kwamba Ibilisi alimwacha Yesu kwa muda, “mpaka wakati mwingine unaofaa.” (Luka 4:13) Inaweza kuwa hivyo pia kwetu, kwa hiyo tunahitaji kuendelea kuwa macho nyakati zote.