Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 14

Yesu Aanza Kufanya Wanafunzi

Yesu Aanza Kufanya Wanafunzi

YOHANA 1:29-51

  • WANAFUNZI WA KWANZA WA YESU WAJIUNGA NAYE

Baada ya kukaa nyikani siku 40 na kabla ya kurudi Galilaya, Yesu anarudi kwa Yohana ambaye alimbatiza. Yesu anapokaribia, Yohana anamtambulisha na kuwatangazia hivi wale walio hapo: “Ona, Mwanakondoo wa Mungu ambaye huondoa dhambi ya ulimwengu! Huyu ndiye niliyesema kumhusu: ‘Nyuma yangu anakuja mwanamume ambaye amenitangulia, kwa sababu alikuwapo kabla yangu.’” (Yohana 1:29, 30) Ingawa Yohana amemzidi Yesu umri kidogo, anajua kwamba Yesu aliishi kabla yake akiwa kiumbe wa roho huko mbinguni.

Majuma machache mapema, Yesu alipokuja ili abatizwe, Yohana hakuwa na uhakika kwamba Yesu ndiye angekuwa Masihi. “Hata mimi sikumjua,” Yohana anakiri, “lakini nilikuja kubatiza katika maji ili afunuliwe kwa Israeli.”—Yohana 1:31.

Yohana anaendelea kuwasimulia watu wanaomsikiliza mambo yaliyotukia alipombatiza Yesu: “Niliona roho ikishuka kama njiwa kutoka mbinguni, nayo ikakaa juu yake. Hata mimi sikumjua, bali Yule aliyenituma nikabatize katika maji aliniambia: ‘Yeyote ambaye utaona roho ikishuka na kukaa juu yake, huyo ndiye anayebatiza kwa roho takatifu.’ Mimi nimeona, nami nimetoa ushahidi kwamba huyo ndiye Mwana wa Mungu.”—Yohana 1:32-34.

Kesho yake Yesu anapokuja tena, Yohana yuko pamoja na wawili kati ya wanafunzi wake. Yohana anasema: “Ona, Mwanakondoo wa Mungu!” (Yohana 1:36) Papo hapo, wanafunzi hao wawili wa Yohana Mbatizaji wanamfuata Yesu. Mmoja wao anaitwa Andrea. Huenda yule mwingine ndiye aliyeandika kuhusu tukio hili, naye anaitwa Yohana. Inaonekana kwamba Yohana huyo ni binamu wa Yesu, yeye ni mwana wa Salome. Inaelekea Salome ni dada yake Maria, na mume wake ni Zebedayo.

Anapogeuka na kuwaona Andrea na Yohana wakimfuata, Yesu anawauliza: “Mnatafuta nini?”

Wanamuuliza: “Rabi unakaa wapi?”

Yesu anawajibu: “Njooni, nanyi mtaona.”—Yohana 1:37-39.

Ni alasiri, saa kumi hivi, na Andrea na Yohana wanakaa pamoja na Yesu siku hiyo. Andrea amefurahi sana hivi kwamba anapompata Simoni ndugu yake, ambaye pia anaitwa Petro, anamwambia: “Tumempata Masihi.” (Yohana 1:41) Andrea anampeleka Petro kwa Yesu. Matukio ya baadaye yanaonyesha kwamba hata Yohana alimpata Yakobo ndugu yake na kumleta kwa Yesu; hata hivyo, anapoandika matukio hayo, Yohana haandiki kuhusu jambo hilo alilofanya.

Siku inayofuata, Yesu anampata Filipo, ambaye anatoka Bethsaida. Mji huo uko karibu na ufuo wa kaskazini wa Bahari ya Galilaya na Andrea na Petro wanatoka huko pia. Yesu anamwalika Filipo: “Njoo uwe mfuasi wangu.”—Yohana 1:43.

Filipo naye anampata Nathanaeli, ambaye pia anaitwa Bartholomayo, na kusema: “Tumempata yule ambaye Musa, katika Sheria, na Manabii waliandika kumhusu: Yesu, mwana wa Yosefu, kutoka Nazareti.” Lakini Nathanaeli anatilia shaka na kumuuliza Filipo: “Je, kitu chochote kizuri kinaweza kutoka Nazareti?”

Filipo anamhimiza: “Njoo uone.” Yesu anapomwona Nathanaeli akija anasema: “Ona, Mwisraeli kwa hakika ambaye hamna udanganyifu ndani yake.”

“Umenijuaje?” Nathanaeli anauliza.

Yesu anamjibu: “Nilikuona ulipokuwa chini ya mtini, kabla ya Filipo kukuita.”

Nathanaeli anamwambia kwa mshangao: “Rabi, wewe ni Mwana wa Mungu, wewe ni Mfalme wa Israeli.”

“Je, unaamini kwa sababu nimekuambia nilikuona chini ya mtini?” Yesu anauliza. “Utaona mambo makubwa kuliko haya.” Kisha Yesu anaahidi: “Kwa kweli ninawaambia, mtaona mbingu imefunguliwa na malaika wa Mungu wakipanda na kushuka kwa Mwana wa binadamu.”—Yohana 1:45-51.

Muda mfupi baadaye, Yesu pamoja na wanafunzi wake wapya, wanaondoka katika Bonde la Yordani na kwenda Galilaya.