Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 16

Yesu Ana Bidii kwa Ajili ya Ibada ya Kweli

Yesu Ana Bidii kwa Ajili ya Ibada ya Kweli

YOHANA 2:12-22

  • YESU ASAFISHA HEKALU

Baada ya harusi huko Kana, Yesu anaelekea Kapernaumu. Mama ya Yesu na ndugu wa kambo wa Yesu​—Yakobo, Yosefu, Simoni, na Yuda—​wanasafiri pamoja naye.

Kwa nini Yesu anaenda Kapernaumu? Jiji hilo ni maarufu kuliko Nazareti au Kana na inaonekana ni kubwa zaidi. Vilevile, wengi kati ya wanafunzi wapya wa Yesu wanaishi Kapernaumu au maeneo ya karibu. Basi Yesu anaweza kuwazoeza wakiwa katika eneo lao la nyumbani.

Katika muda anaokaa huko Kapernaumu, Yesu pia anafanya miujiza. Basi watu wengi wa jiji hilo na maeneo yaliyo karibu wanasikia kuhusu mambo ambayo anafanya huko. Lakini Yesu na watu wanaoandamana naye, ni Wayahudi wanaomwogopa Mungu, na baada ya muda mfupi wanahitaji kwenda Yerusalemu ili kuhudhuria Pasaka ya mwaka wa 30 W.K.

Wakiwa hekaluni huko Yerusalemu, wanafunzi wa Yesu wanaona jambo fulani la kuvutia sana kumhusu Yesu, jambo ambalo ni tofauti na mambo ambayo tayari wameona.

Kulingana na Sheria ya Mungu, Waisraeli wanapaswa kutoa dhabihu za wanyama hekaluni, na wageni wanahitaji chakula kwa muda wanaokaa huko. Basi Sheria inakubali wale wanaosafiri kuja Yerusalemu kutoka mbali waje na pesa za kununua “ng’ombe, kondoo, mbuzi,” na vitu vingine wanavyohitaji kwa muda watakaokaa jijini. (Kumbukumbu la Torati 14:24-26) Kwa hiyo, wafanyabiashara huko Yerusalemu wanauza wanyama na ndege, ndani kabisa ya ua mkubwa wa hekalu. Baadhi yao wanawadangaya watu kwa kuwatoza pesa nyingi sana.

Akiwa amejawa na hasira, Yesu anamwaga sarafu za wale wanaobadili pesa, anapindua meza zao, na kuwafukuza wanaume hao. Kisha Yesu anasema: “Ondoeni vitu hivi hapa! Acheni kuifanya nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara!”—Yohana 2:16.

Wanafunzi wa Yesu wanapoona jambo hilo, wanakumbuka unabii ulioandikwa kumhusu Mwana wa Mungu: “Bidii kwa ajili ya nyumba yako itanila.” Lakini Wayahudi wanamuuliza: “Utatuonyesha ishara gani, kwa maana unafanya mambo haya?” Yesu anawajibu: “Libomoeni hekalu hili, na kwa siku tatu nitalisimamisha.”—Yohana 2:17-19; Zaburi 69:9.

Wayahudi wanafikiri Yesu anamaanisha hekalu halisi huko Yerusalemu, basi wanauliza: “Hekalu hili lilijengwa kwa miaka 46, je, wewe utalisimamisha kwa siku tatu?” (Yohana 2:20) Hata hivyo, Yesu anarejezea mwili wake kuwa hekalu. Miaka mitatu baadaye, wanafunzi wake wanakumbuka maneno hayo anapofufuliwa.