Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 17

Amfundisha Nikodemo Usiku

Amfundisha Nikodemo Usiku

YOHANA 2:23–3:21

  • YESU AZUNGUMZA NA NIKODEMO

  • MAANA YA ‘KUZALIWA TENA’

Akiwa Yerusalemu kwa ajili ya Pasaka ya mwaka wa 30 W.K., Yesu anafanya ishara au miujiza yenye kustaajabisha. Kwa hiyo, watu wengi wanamwamini. Nikodemo ambaye ni Farisayo na mshiriki wa mahakama kuu ya Kiyahudi inayoitwa Sanhedrini, anavutiwa. Akitaka kujifunza mengi zaidi, anamtembelea Yesu usiku, labda kwa sababu anaogopa kwamba jina lake litaharibika machoni pa viongozi wa Kiyahudi iwapo ataonekana.

Nikodemo anamwambia: “Rabi, tunajua kwamba wewe ni mwalimu na umetoka kwa Mungu, kwa maana hakuna anayeweza kufanya miujiza kama unayofanya isipokuwa Mungu awe pamoja naye.” Naye Yesu anamwambia Nikodemo kwamba ili kuingia katika Ufalme wa Mungu, ni lazima mtu ‘azaliwe tena.’—Yohana 3:2, 3

Hata hivyo, mtu anawezaje kuzaliwa tena? “Hawezi kuingia tumboni mwa mama yake mara ya pili na kuzaliwa, sivyo?” Nikodemo anauliza.—Yohana 3:4.

Hapana, kuzaliwa tena hakumaanishi hivyo. Yesu anafafanua hivi: “Mtu asipozaliwa kwa maji na roho, hawezi kuingia katika Ufalme wa Mungu.” (Yohana 3:5) Yesu alipobatizwa na roho takatifu ikashuka juu yake, alizaliwa “kwa maji na roho.” Wakati huo, kulikuwa pia na tangazo kutoka mbinguni: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:16, 17) Kwa njia hiyo, Mungu alitangaza kwamba sasa Yesu amekuwa mwana wake wa kiroho aliye na tumaini la kuingia katika Ufalme wa mbinguni. Baadaye katika Pentekoste ya 33 W.K., roho takatifu itamwagwa juu ya wengine waliobatizwa, nao watakuwa wamezaliwa tena wakiwa wana wa kiroho wa Mungu.—Matendo 2:1-4.

Ni vigumu kwa Nikodemo kuelewa mambo ambayo Yesu anamfundisha kuhusu Ufalme. Basi Yesu anampa habari zaidi kuhusu jukumu lake la pekee akiwa Mwana wa kibinadamu wa Mungu. Yesu anasema: “Kama vile Musa alivyoinua nyoka nyikani, ndivyo Mwana wa binadamu atakavyoinuliwa, ili kila mtu anayemwamini apate uzima wa milele.”—Yohana 3:14, 15.

Zamani Waisraeli walioumwa na nyoka wenye sumu walipaswa kumwangalia nyoka wa shaba ili waokolewe. (Hesabu 21:9) Vivyo hivyo, wanadamu wote wanapaswa kumwamini Mwana wa Mungu ili waokolewe kutokana na hali yao ya kufa na wapate uzima wa milele. Akikazia jukumu lenye upendo ambalo Yehova alitimiza kuhusiana na jambo hilo, Yesu anamwambia Nikodemo: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Miezi sita baada ya kuanza huduma yake, sasa akiwa Yerusalemu, Yesu anaonyesha wazi kwamba yeye ndiye njia ya wanadamu kupata wokovu.

Yesu anamwambia Nikodemo: “Mungu hakumtuma Mwanawe ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu.” Hilo linamaanisha hakutumwa auhukumu ulimwengu kwamba una hatia, akiwahukumu wanadamu wote waangamizwe. Badala yake, kama Yesu anavyosema, alitumwa ili “ulimwengu uokolewe kupitia kwake.”—Yohana 3:17.

Kwa sababu ya woga, Nikodemo amekuja kumwona Yesu usiku. Inapendeza kwamba Yesu anamalizia mazungumzo yao kwa kusema: “Basi huu ndio msingi wa hukumu: kwamba nuru [ambayo ni Yesu kupitia maisha na mafundisho yake] imekuja ulimwenguni, lakini watu wamependa giza badala ya nuru, kwa maana matendo yao yalikuwa maovu. Kwa maana yeyote ambaye huzoea kutenda mambo maovu huchukia nuru na haji kwenye nuru, ili matendo yake yasikaripiwe. Lakini yeyote ambaye hufanya yaliyo ya kweli huja kwenye nuru, ili matendo yake yafunuliwe kwamba yamefanywa kulingana na Mungu.”—Yohana 3:19-21.

Sasa Nikodemo ambaye ni Farisayo na mwalimu katika Israeli, anapaswa kutafakari mambo ambayo amesikia kuhusu jukumu la Yesu katika kusudi la Mungu.