Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 21

Kwenye Sinagogi ya Nazareti

Kwenye Sinagogi ya Nazareti

LUKA 4:16-31

  • YESU ANASOMA KATIKA KITABU CHA KUKUNJWA CHA ISAYA

  • WATU WA NAZARETI WANAJARIBU KUMUUA YESU

Bila shaka, watu wa Nazareti wako na furaha nyingi. Mbele aende kubatizwa na Yohana kumepita zaidi ya mwaka moja hivi, Yesu alikuwa anafanya kazi ya useremala huku Nazareti. Lakini sasa anajulikana kuwa mutu mwenye kufanya miujiza. Watu wa Nazareti wanangojea kwa hamu kuona Yesu anawafanyia miujiza fulani.

Hamu yao inaongezeka wakati wanasikia kuwa Yesu anaenda kwenye sinagogi ya Nazareti, kulingana na desturi yake. Utumishi wenye kufanywa katika sinagogi unatia ndani sala na kusoma katika vitabu vya Musa, kama vile inafanywa “katika masinagogi kila sabato.” (Matendo 15:21) Sehemu za vitabu vya unabii zinasomwa pia. Wakati Yesu anasimama ili kusoma, inawezekana anatambua watu fulani wenye alizoea kuona wakati alikuwa anaenda katika sinagogi hiyo. Wanamupatia kitabu cha kukunjwa cha nabii Isaya. Anapata andiko lenye kuzungumuzia Ule mwenye ametiwa mafuta kupitia roho ya Yehova, andiko lenye kupatikana leo katika Isaya 61:1, 2.

Yesu anasoma juu ya namna Mutu huyo mwenye kuahidiwa atahubiria wafungwa wa vita uhuru, vipofu kufunguliwa kabisa kwa macho, na kuja kwa mwaka wenye kukubaliwa na Yehova. Yesu anarudishia mutumishi kwenye sinagogi kitabu cha kukunjwa na anakaa. Watu wote wanamukazia macho. Kisha anasema, pengine kwa muda murefu kidogo, na maelezo yake yanatia ndani maneno haya ya maana: “Leo andiko hili lenye mumesikia limetimia.”—Luka 4:21.

Watu wanashangazwa na “maneno yenye kupendeza yenye kutoka katika kinywa chake,” na wanaambiana hivi: “Huyu ni mwana wa Yosefu, haiko vile?” Lakini, wakati Yesu anatambua kuwa wanapenda kumuona anafanya miujiza kama ile walikuwa wanasikia, Yesu anaendelea kuwaambia hivi: “Bila shaka mutatumia mufano huu kunihusu, ‘Munganga, ujiponyeshe wewe mwenyewe. Fanya pia katika eneo lako la nyumbani mambo yenye tulisikia yalifanyika kule Kapernaumu.’” (Luka 4:22, 23) Pengine majirani wa zamani wa Yesu wanawaza kuwa kuponyesha watu kunapaswa kuanzia nyumbani, kwanza kwa faida ya watu wake mwenyewe. Kwa hiyo, pengine wanawaza kuwa Yesu amewazarau.

Wakati Yesu anatambua mawazo yao, anataja matukio fulani katika historia ya Israeli. Yesu anaeleza kuwa katika Israeli kulikuwa wajane wengi katika siku za Eliya, lakini Eliya hakutumwa hata kwa mujane moja kati yao. Lakini, alitumwa kwa mujane mwenye haiko Mwisraeli katika Sarefati, muji wenye kuwa karibu na Sidoni, kwenye Eliya alifanya muujiza wenye kuokoa uzima. (1 Wafalme 17:8-16) Na katika siku za Elisha, kulikuwa watu wengi wenye ukoma, lakini nabii Elisha alisafisha tu Naamani Musiria.—2 Wafalme 5:1, 8-14.

Watu wa Nazareti wanatenda namna gani wakati wanasikia maneno hayo yenye kulinganisha matukio ya zamani yenye wanaona kuwa hayafae na yenye yanafunua wazi kuwa wanajipenda wenyewe na kuwa hawana imani? Watu wenye kuwa katika sinagogi wanakasirika, wanasimama, na wanamutosha haraka inje ya muji. Wanamupeleka kwenye sehemu ya juu kabisa ya mulima kwenye muji wa Nazareti ulijengwa, na wanajaribu kumutupa chini. Lakini Yesu anawaponyoka na kuenda kwa usalama. Sasa Yesu anashuka kuenda Kapernaumu, upande wa kaskazini-mashariki pembeni ya Bahari ya Galilaya.