Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 24

Apanua Huduma Yake Huko Galilaya

Apanua Huduma Yake Huko Galilaya

MATHAYO 4:23-25 MARKO 1:35-39 LUKA 4:42, 43

  • YESU ANATEMBEA HUKO GALILAYA PAMOJA NA WANAFUNZI WAKE WANNE

  • MAHUBIRI YAKE NA KAZI ZAKE ZAJULIKANA NA WATU WENGI

Yesu na wanafunzi wake wanne wamekuwa na siku yenye shughuli nyingi huko Kapernaumu. Jioni, watu wa Kapernaumu wanamletea wagonjwa ili awaponye. Yesu hajapata muda wa kutosha wa faragha.

Basi, asubuhi, siku inayofuata, kukiwa bado na giza, Yesu anaamka na kwenda nje akiwa peke yake. Anatafuta mahali patulivu ambapo anaweza kusali kwa Baba yake faraghani. Hata hivyo, faragha ya Yesu inakuwa ya muda mfupi. “Simoni na wenzake” wanapotambua kwamba Yesu hayupo, wanaenda kumtafuta. Huenda Petro ndiye anayewaongoza kwa sababu Yesu alikuwa nyumbani kwake.—Marko 1:36; Luka 4:38.

Wanapompata Yesu, Petro anamwambia: “Kila mtu anakutafuta.” (Marko 1:37) Ni wazi kwamba watu wa Kapernaumu wanataka Yesu aendelee kukaa pamoja nao. Wanathamini sana mambo ambayo amefanya, hivyo wanajaribu “kumzuia asiondoke.” (Luka 4:42) Hata hivyo, je, sababu ya msingi ya Yesu kuja duniani ni kufanya miujiza hiyo ya kuponya? Na je, atafanya kazi yake katika eneo hilo tu? Anasemaje kuhusu jambo hilo?

Yesu anawajibu wanafunzi wake hivi: “Twendeni mahali pengine, katika miji iliyo karibu, ili nihubiri huko pia, kwa maana nilikuja kwa kusudi hilo.” Kwa kweli, Yesu hata anawaambia hivi watu wanaotaka aendelee kukaa nao: “Ni lazima pia nitangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu katika majiji mengine, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.”—Marko 1:38; Luka 4:43.

Naam, sababu kubwa iliyofanya Yesu aje duniani ni kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. Ufalme huo utalitakasa jina la Baba yake na kuondoa kabisa matatizo yote ya wanadamu. Yesu anafanya miujiza ya kuponya ili kuthibitisha kwamba alitumwa na Mungu. Vivyo hivyo, karne nyingi mapema, Musa alifanya miujiza ili kuthibitisha kwamba alitumwa na Mungu.—Kutoka 4:1-9, 30, 31.

Kwa hiyo, Yesu anaondoka Kapernaumu ili akahubiri katika majiji mengine, na wanafunzi wake wanne wanamfuata. Wanne hao ni Petro na Andrea ndugu yake na pia Yohana na Yakobo ndugu yake. Yesu aliwaalika wawe wafanyakazi wenzake juma moja lililopita.

Safari ya Yesu ya kuhubiri huko Galilaya pamoja na wanafunzi hawa wanne inakuwa na mafanikio makubwa! Kwa kweli, habari kumhusu Yesu zinaenea kila mahali. “Habari kumhusu [zinaenea] katika Siria yote,” katika eneo la majiji kumi liitwalo Dekapoli, na mpaka ng’ambo ya Mto Yordani. (Mathayo 4:24, 25) Umati mkubwa kutoka maeneo hayo, na pia kutoka Yudea unamfuata Yesu na wanafunzi wake. Watu wengi wanamletea wale wanaotaka kuponywa. Yesu hawavunji moyo—anaponya wagonjwa na kufukuza roho waovu kutoka kwa wale walio na roho waovu.