Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 25

Amponya Mtu Mwenye Ukoma kwa Huruma

Amponya Mtu Mwenye Ukoma kwa Huruma

MATHAYO 8:1-4 MARKO 1:40-45 LUKA 5:12-16

  • YESU AMPONYA MTU MWENYE UKOMA

Yesu na wanafunzi wake wanne wanapoenda kuhubiri kwenye ‘masinagogi katika Galilaya yote,’ habari kuhusu miujiza ambayo Yesu anafanya zinaenea sana. (Marko 1:39) Habari kuhusu matendo yake zinafika katika jiji moja ambalo kuna mtu mwenye ukoma. Daktari Luka anaeleza kwamba mtu huyo ‘alikuwa amejaa ukoma.’ (Luka 5:12) Ugonjwa huo hatari unapokomaa, pole kwa pole huharibu viungo mbalimbali vya mwili.

Kwa hiyo mtu huyo mwenye ukoma ana hali mbaya sana na anapaswa kuishi mbali na watu wengine. Isitoshe, kama kuna watu karibu anapaswa kupaza sauti akisema, “Mimi si safi, mimi si safi!” ili wasije wakamkaribia sana nao wakaambukizwa. (Mambo ya Walawi 13:45, 46) Hata hivyo, mtu huyo mwenye ukoma anafanya nini? Anamkaribia Yesu na kuanguka mbele yake akiomba: “Bwana, ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.”—Mathayo 8:2.

Mtu huyo ana imani yenye nguvu katika Yesu! Na ugonjwa wake ni wenye kusikitisha sana! Yesu atatendaje? Ikiwa ungekuwa hapo, wewe ungefanyaje? Akichochewa na huruma, Yesu ananyoosha mkono wake na kumgusa mtu huyo. Yesu anamwambia: “Ninataka! Takasika.” (Mathayo 8:3) Ingawa huenda ikawa vigumu kwa watu wengine kuamini, papo hapo yule mtu anapona ukoma!

Je, wewe ungependa kuwa na mfalme mwenye huruma na uwezo kama Yesu? Njia anayomtendea mtu huyu mwenye ukoma inatuhakikishia kwamba Yesu anapokuwa Mfalme juu ya dunia yote, unabii huu wa Biblia utatimizwa: “Atamhurumia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataokoa uhai wa maskini.” (Zaburi 72:13) Naam, wakati huo Yesu atatimiza tamaa ya moyo wake ya kuwasaidia wote wanaoteseka.

Kumbuka kwamba hata kabla ya kumponya mtu huyo mwenye ukoma, huduma ya Yesu imekuwa ikifanya watu wawe na msisimko. Sasa watu watasikia kuhusu muujiza huu ambao amefanya. Hata hivyo, Yesu hataki watu wamwamini tu kupitia mambo yanayosemwa na watu. Anajua unabii unaosema, “hatafanya sauti yake isikike barabarani,” yaani, kwa njia fulani yenye kusisimua. (Isaya 42:1, 2) Pia anampa maagizo haya yule mtu aliyeponywa: “Usimwambie mtu yeyote, bali nenda, ukajionyeshe kwa kuhani, na utoe zawadi ambayo Musa aliagiza.”—Mathayo 8:4.

Kama unavyoweza kuwazia, mwanaume huyo ana furaha sana baada ya kuponywa hivi kwamba hawezi kujizuia kusema kuhusu jambo lililotokea. Anaondoka na kueneza habari hizo kila mahali. Jambo hilo linafanya watu wawe na udadisi na hamu ya kujua mengi. Inafikia hatua ya kwamba hata Yesu hawezi kutembea waziwazi jijini, hivyo kwa muda fulani anakaa katika maeneo yasiyo na watu ambako hakuna mtu anayeishi. Lakini bado watu wanatoka kila mahali ili kuja kufundishwa naye na kuponywa.