Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 26

“Umesamehewa Dhambi Zako”

“Umesamehewa Dhambi Zako”

MATHAYO 9:1-8 MARKO 2:1-12 LUKA 5:17-26

  • YESU AMSAMEHE DHAMBI MTU ALIYEPOOZA KISHA AMPONYA

Watu kutoka sehemu mbalimbali wamesikia kumhusu Yesu. Wengi wanasafiri hadi maeneo ya mbali sana ili kumsikiliza akifundisha na kuona miujiza yake. Hata hivyo, baada ya siku chache, anarudi Kapernaumu, kituo chake cha kazi. Habari za kurudi kwake zinaenea haraka katika jiji hili lililo kando ya Bahari ya Galilaya. Kwa sababu hiyo, watu wengi wanakuja katika nyumba anayokaa. Baadhi yao ni Mafarisayo na walimu wa Sheria waliokuja kutoka sehemu mbalimbali za Galilaya na Yudea, kutia ndani Yerusalemu.

‘Watu wengi sana wanakuja hivi kwamba hakuna nafasi tena, hata mlangoni, naye anaanza kuwahubiria.’ (Marko 2:2) Sasa jambo la kustaajabisha sana linatokea. Ni tukio linaloweza kutusaidia kuelewa kwamba Yesu ana nguvu za kuondoa chanzo cha mateso ya wanadamu na kuwarudishia afya nzuri wale wote anaowachagua.

Yesu akiwa anafundisha katika chumba kilichojaa watu, watu wanne wanamleta mtu aliyepooza akiwa kitandani. Wanataka Yesu amponye rafiki yao. Lakini kwa sababu ya umati wanashindwa “kumleta moja kwa moja kwa Yesu.” (Marko 2:4) Wazia jinsi wanavyovunjika moyo. Wanapanda juu ya paa lililo tambarare la nyumba na kutoboa shimo kwenye vigae. Kisha wanashusha kitanda alicholalia mtu huyo aliyepooza hadi ndani ya nyumba.

Je, Yesu anakasirika kwa sababu ya kukatishwa? Hapana! Anafurahishwa sana na imani yao na kumwambia yule mtu aliyepooza: “Umesamehewa dhambi zako.” (Mathayo 9:2) Lakini je, kweli Yesu anaweza kusamehe dhambi? Waandishi na Mafarisayo wanakasirishwa na jambo hilo, wanajiuliza: “Kwa nini mtu huyu anasema hivyo? Anakufuru. Ni nani anayeweza kusamehe dhambi isipokuwa Mungu peke yake?”—Marko 2:7.

Akijua mawazo yao, Yesu anawaambia hivi: “Kwa nini mnawaza mambo hayo katika mioyo yenu? Ni jambo gani rahisi zaidi, kumwambia mtu huyu aliyepooza, ‘Umesamehewa dhambi zako,’ au kusema, ‘Simama, uchukue kitanda chako utembee’?” (Marko 2:8, 9) Naam, kwa msingi wa dhabihu ambayo baadaye Yesu atatoa, anaweza kusamehe dhambi za mtu huyo.

Kisha, Yesu anauonyesha umati pamoja na wale wanaomkosoa, kwamba ana mamlaka ya kusamehe dhambi duniani. Anamgeukia yule mtu aliyepooza na kumwamuru hivi: “Ninakuambia, Simama, chukua kitanda chako, uende nyumbani.” Mara moja mtu huyo anafanya hivyo, anatembea akiwa amebeba kitanda chake mbele ya macho ya wote waliopo. Watu wanashangaa sana! Wanamtukuza Mungu na kupaza sauti: “Hatujawahi kamwe kuona jambo kama hilo”!—Marko 2:11, 12.

Ni muhimu kutambua kwamba Yesu anataja dhambi kwa kuihusianisha na magonjwa na kwamba msamaha wa dhambi unaweza kuhusianishwa na afya ya kimwili. Biblia inafundisha kwamba mzazi wetu wa kwanza, Adamu, alitenda dhambi na kwamba sote tumerithi matokeo ya dhambi, yaani magonjwa na kifo. Lakini chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, Yesu atasamehe dhambi za watu wote wanaompenda na kumtumikia Mungu. Kisha magonjwa yataondolewa milele.—Waroma 5:12, 18, 19.