Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 30

Uhusiano Kati ya Yesu na Baba Yake

Uhusiano Kati ya Yesu na Baba Yake

YOHANA 5:17-47

  • MUNGU NI BABA YA YESU

  • AHADI YA UFUFUO

Wayahudi fulani wanapomshutumu Yesu kwamba anavunja Sabato kwa kumponya mtu, Yesu anawajibu: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa, nami ninaendelea kufanya kazi.”—Yohana 5:17.

Jambo ambalo Yesu anafanya halijakatazwa na Sheria ya Mungu kuhusu Sabato. Kwa kuhubiri na kuponya, Yesu anaiga kazi njema za Mungu. Basi Yesu anaendelea kufanya mambo mema kila siku. Anapowajibu wale wanaomshutumu, wanakasirika hata zaidi, nao wanataka kumwua Yesu. Kwa nini?

Zaidi ya kuwa na maoni yenye makosa kwamba Yesu anavunja Sabato kwa kuwaponya watu, wanakasirika sana anaposema kwamba yeye ni Mwana wa Mungu. Wanaona kwamba anakufuru kwa kusema Mungu ni Baba yake, kana kwamba Yesu anaposema Yehova ni Baba yake anamaanisha kwamba analingana na Mungu. Hata hivyo, Yesu haogopi na anaendelea kuwaeleza kuhusu uhusiano wake wa pekee pamoja na Mungu. Anasema: “Baba anampenda Mwana na humwonyesha mambo yote anayofanya.”—Yohana 5:20.

Baba ndiye Mpaji-Uhai, na ameonyesha hivyo nyakati zilizopita kwa kuwawezesha wanadamu kuwafufua wafu. Yesu anaendelea kusema: “Kama vile Baba anavyowafufua wafu na kuwafanya kuwa hai, ndivyo Mwana pia anavyowafanya kuwa hai wale anaotaka.” (Yohana 5:21) Maneno hayo muhimu yanatoa tumaini zuri ajabu kwa ajili ya wakati ujao! Hata sasa, Mwana anawafufua watu waliokufa kiroho. Basi Yesu anasema: “Yeyote ambaye husikia neno langu na kumwamini Yule aliyenituma ana uzima wa milele, naye hahukumiwi bali amevuka kutoka katika kifo na kuingia kwenye uzima.”—Yohana 5:24.

Kufikia sasa Yesu hajamfufua mtu yeyote aliyekufa, lakini anawaeleza wale wanaomshtumu kwamba atawafufua watu kihalisi. Anasema: “Saa inakuja ambayo wote walio katika makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.”—Yohana 5:28, 29.

Ingawa Yesu ana jukumu la pekee, anaonyesha waziwazi kwamba yuko chini ya Mungu anaposema: “Siwezi kufanya jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe. . . . Sitafuti mapenzi yangu mwenyewe, bali mapenzi ya yule aliyenituma.” (Yohana 5:30) Hata hivyo, Yesu anafafanua jukumu lake muhimu katika kusudi la Mungu, anafanya hivyo hadharani, jambo ambalo hakuwa amefanya kufikia wakati huo. Lakini wale wanaomshutumu Yesu wana ushahidi mwingine mbali na ushahidi wa Yesu. Yesu anawakumbusha: “Mmewatuma watu kwa Yohana [Mbatizaji], naye ametoa ushahidi kuhusu kweli.”—Yohana 5:33.

Huenda wale wanaomshutumu Yesu walisikia kwamba miaka miwili iliyopita, Yohana alikuwa amewaambia viongozi wa dini ya Kiyahudi kuhusu Yule anayekuja baada yake—aliyeitwa “Nabii” na “Kristo.” (Yohana 1:20-25) Akiwakumbusha wale wanaomshutumu jinsi wakati fulani walivyomheshimu Yohana ambaye sasa amefungwa gerezani, Yesu anasema: “Kwa wakati mfupi mlikuwa tayari kufurahia sana mwangaza wake.” (Yohana 5:35) Lakini Yesu anatoa ushahidi mkubwa hata kuliko Yohana.

“Kazi hizi ninazofanya [kutia ndani uponyaji ambao amefanya hivi punde] zinatoa ushahidi kwamba Baba alinituma.” Zaidi ya hilo, Yesu anasema: “Baba aliyenituma ametoa ushahidi kunihusu.” (Yohana 5:36, 37) Kwa mfano, Yesu alipobatizwa Mungu alitoa ushahidi kumhusu.—Mathayo 3:17.

Kwa kweli wale wanaomshutumu Yesu hawana sababu ya kumkataa. Maandiko wanayodai kwamba wanayachunguza yanatoa ushahidi kumhusu Yesu. Yesu anamalizia kwa kusema: “Ikiwa mngemwamini Musa mngeniamini pia, kwa sababu aliandika kunihusu. Lakini ikiwa hamwamini mambo aliyoandika, mnawezaje kuamini mambo ninayosema?”—Yohana 5:46, 47.