Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 36

Imani Kubwa ya Ofisa wa Jeshi

Imani Kubwa ya Ofisa wa Jeshi

MATHAYO 8:5-13 LUKA 7:1-10

  • MTUMWA WA OFISA WA JESHI APONYWA

  • WALE WALIO NA IMANI WATABARIKIWA

Baada ya kumaliza Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu anaelekea katika jiji la Kapernaumu. Akiwa huko, baadhi ya wazee Wayahudi wanakuja kuongea naye. Wametumwa na mtu wa nchi nyingine—ofisa wa jeshi Mroma, msimamizi wa kikosi cha wanajeshi.

Mtumwa mpendwa wa ofisa huyo wa jeshi ni mgonjwa sana na anakaribia kufa. Ingawa ofisa huyo si Myahudi, anatafuta msaada wa Yesu. Wayahudi wanamwambia Yesu kwamba mtumwa wa mtu huyo “amelala nyumbani na ana ugonjwa wa kupooza, naye anateseka sana,” labda ana maumivu makali. (Mathayo 8:6) Wazee Wayahudi wanamhakikishia Yesu kwamba ofisa huyo anastahili kupewa msaada huo, wanaeleza hivi: “Analipenda taifa letu na yeye ndiye aliyetujengea sinagogi.”—Luka 7:4, 5.

Baada ya muda mfupi Yesu anaondoka pamoja na wale wazee kuelekea kwenye nyumba ya yule ofisa. Wanapoikaribia, yule ofisa anawatuma rafiki zake wakaseme: “Bwana, usijisumbue, kwa maana mimi sistahili uingie ndani ya nyumba yangu. Ndiyo sababu niliona sistahili kuja kwako.” (Luka 7:6, 7) Hayo ni maneno ya unyenyekevu sana kutoka kwa mtu aliyezoea kutoa maagizo! Na yanaonyesha jinsi mtu huyo alivyo tofauti na Waroma ambao huwatendea watumwa kwa ukali.—Mathayo 8:9.

Bila shaka, yule ofisa anajua kwamba Wayahudi huepuka kushirikiana na watu wasio Wayahudi. (Matendo 10:28) Labda akifikiria jambo hilo, yule ofisa anawaambia rafiki zake wamsihi Yesu hivi: “Sema tu neno, na mtumishi wangu atapona.”—Luka 7:7.

Yesu anashangaa kusikia maneno hayo naye anasema: “Ninawaambia, hata katika Israeli sijaona imani kubwa kama hii.” (Luka 7:9) Wanaporudi katika nyumba ya yule ofisa, rafiki zake wanatambua kwamba yule mtumwa aliyekuwa mgonjwa sana sasa amepona.

Baada ya kufanya muujiza huo, Yesu anatumia pindi hiyo kuthibitisha kwamba watu wasio Wayahudi watapata baraka, anaposema: “Wengi watakuja kutoka mashariki na magharibi na kuketi mezani pamoja na Abrahamu, Isaka, na Yakobo katika Ufalme wa mbinguni.” Namna gani Wayahudi wasio na imani? Yesu anasema kwamba “watatupwa nje gizani. Huko ndiko watalia na kusaga meno yao.”—Mathayo 8:11, 12.

Hivyo, Wayahudi wa asili wanaokataa nafasi wanayopewa kwanza ya kuwa sehemu ya Ufalme pamoja na Kristo watakataliwa. Lakini watu wa mataifa watakaribishwa kuketi mezani, kwa njia ya mfano, “katika Ufalme wa mbinguni.”