Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 36

Mukubwa Fulani wa Jeshi Anaonyesha Imani Kubwa

Mukubwa Fulani wa Jeshi Anaonyesha Imani Kubwa

MATAYO 8:5-13 LUKA 7:1-10

  • MUTUMWA WA MUKUBWA FULANI WA JESHI ANAPONYESHWA

  • WALE WENYE KUWA NA IMANI WATABARIKIWA

Kisha kufanya Mahubiri yake ya Mulimani, Yesu anaenda katika muji wa Kapernaumu. Wakati iko katika muji huo, wazee Wayahudi wanamukaribia. Wanaume hao wametumwa na mutu wa desturi ingine, ni kusema, mukubwa wa jeshi Muroma.

Mutumishi mupendwa wa mukubwa huyo wa jeshi ni mugonjwa sana na anakaribia kufa. Hata kama mukubwa huyo wa jeshi haiko Muyahudi, iko anatafuta Yesu amusaidie. Wayahudi wanaambia Yesu kuwa mutumishi wa mwanaume huyo “analala nyumbani, iko na ugonjwa wa kupooza na anateseka sana,” pengine iko na maumivu makali sana. (Matayo 8:6) Wazee Wayahudi wanamuhakikishia Yesu kuwa mukubwa huyo wa jeshi anastahili kabisa kutolewa musaada. Wanaeleza hivi: “Anapenda taifa letu na yeye mwenyewe alijenga sinagogi letu.”—Luka 7:4, 5.

Bila kukawia, Yesu anaondoka pamoja na wazee na kuenda kwa mukubwa huyo wa jeshi. Wakati wanafika karibu na nyumba yake, mukubwa huyo anatuma marafiki wake ili wamuambie Yesu hivi: “Bwana, usijisumbue, kwa maana mimi sistahili kukupokea katika nyumba yangu. Ndiyo sababu nilijiona sistahili kuja kwako.” (Luka 7:6, 7) Kwa mutu mwenye anazoea kupatia wengine maagizo, hayo ni maneno yenye kuonyesha unyenyekevu sana! Na hilo linaonyesha namna gani mwanaume huyo iko tofauti na Waroma wengine wenye kutendea watumwa kwa ukali sana.—Mathayo 8:9.

Bila shaka, mukubwa huyo wa jeshi anajua muzuri kuwa Wayahudi wanaepuka kushirikiana ao kujiunga pamoja na watu wenye hawako Wayahudi. (Matendo 10:28) Pengine mukubwa huyo wa jeshi anajua jambo hilo, ndiyo sababu anatuma marafiki wake wamuambie Yesu hivi: “Sema neno moja tu, na mutumishi wangu atapona.”—Luka 7:7.

Yesu anashangazwa kusikia maneno hayo na anasema hivi: “Ninawaambia ninyi, hata katika Israeli sijaona imani kubwa kama hii.” (Luka 7:9) Wakati wanarudia nyumbani kwa mukubwa huyo wa jeshi, marafiki wake wanatambua kuwa mutumishi mwenye alikuwa mugonjwa iko sasa na afya ya muzuri.

Kisha tu Yesu kufanya muujiza huo, anatumia nafasi hiyo ili kuhakikisha kuwa watu wenye hawako Wayahudi ambao wako na imani watapata baraka. Anasema hivi: “Watu wengi kutoka mashariki na mangaribi watakuja na kukaa kwenye meza pamoja na Abrahamu, Isaka, na Yakobo katika Ufalme wa mbinguni.” Halafu Wayahudi wenye kukosa imani? Yesu anasema kuwa “watatupwa inje katika giza. Ni kule watalia na kusaga meno yao.”—Matayo 8:11, 12.

Kwa hiyo, Wayahudi wa asili wenye wanakataa nafasi yenye ilitolewa kwanza kwao ya kuwa kati ya wale wenye watatawala pamoja na Kristo katika Ufalme wa mbinguni watakataliwa. Lakini wale wenye hawako Wayahudi watakaribishwa kwenye meza yake, “katika Ufalme wa mbinguni.”