Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 39

Ole kwa Kizazi Kisichotii

Ole kwa Kizazi Kisichotii

MATHAYO 11:16-30 LUKA 7:31-35

  • YESU ASHUTUMU MAJIJI FULANI

  • ANAFARIJI NA KUBURUDISHA

Yesu anamheshimu sana Yohana Mbatizaji, lakini watu wengi wanamwonaje Yohana? “Kizazi hiki,” Yesu anasema, “ni kama watoto walioketi sokoni wakiwapazia wenzao sauti, wakisema: ‘Tuliwapigia filimbi, lakini hamkucheza dansi; tuliomboleza, lakini hamkujipiga-piga kwa huzuni.’”—Mathayo 11:16, 17.

Yesu anamaanisha nini? Anafafanua wazo hilo: “Yohana hakuja akila wala kunywa, lakini watu wanasema, ‘Ana roho mwovu.’ Mwana wa binadamu alikuja akila na kunywa, lakini watu wanasema, ‘Tazama! Yeye ni mlafi na mwenye mazoea ya kunywa divai, rafiki ya wakusanya kodi na watenda dhambi.’” (Mathayo 11:18, 19) Kwa upande wake, Yohana ameishi maisha rahisi akiwa Mnadhiri, hata amejiepusha na divai, na bado kizazi hiki kinasema ana roho mwovu. (Hesabu 6:2, 3; Luka 1:15) Kwa upande mwingine, Yesu anaishi kama watu wengine. Anakula na kunywa kwa njia yenye usawaziko, lakini anashtakiwa kwamba anapita kiasi. Inaonekana haiwezekani kuwapendeza watu hao.

Yesu anafananisha kizazi hicho na watoto wadogo sokoni ambao wanakataa kucheza dansi watoto wengine wanapowapigia filimbi au kuhuzunika wengine wanapoomboleza. “Hata hivyo,” Yesu anasema, “hekima huthibitishwa kuwa yenye uadilifu kupitia kazi zake.” (Mathayo 11:16, 19) Naam, “kazi”—yaani, ushahidi unaotolewa na Yohana na Yesu—unathibitisha kwamba mashtaka dhidi yao ni ya uwongo.

Baada ya Yesu kuonyesha kwamba kizazi hicho si kitiifu, anataja kihususa majiji ya Korazini, Bethsaida, na Kapernaumu, ambako amefanya miujiza. Yesu anasema kwamba kama angefanya miujiza kama hiyo katika majiji ya Wafoinike huko Tiro na Sidoni, majiji hayo yangetubu. Pia, anataja Kapernaumu, ambako amekaa kwa muda fulani. Hata huko, watu wengi hawakuitikia vizuri. Yesu anasema hivi kuhusu jiji hilo: “Katika Siku ya Hukumu itakuwa afadhali zaidi kwa nchi ya Sodoma kuliko kwenu.”—Mathayo 11:24.

Kisha Yesu anamsifu Baba yake, ambaye huwaficha kweli za kiroho zenye thamani watu “wenye hekima na wenye elimu” lakini huyafunua mambo hayo kwa watu wanyenyekevu, walio kama watoto wadogo. (Mathayo 11:25) Anawatolea watu hao mwaliko huu wenye kupendeza: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu. Kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”—Mathayo 11:28-30.

Yesu anawaburudisha kwa njia gani? Viongozi wa kidini wamewatwika watu utumwa wa kufuata desturi, kama vile masharti yenye kulemea kuhusu Sabato. Lakini Yesu anawaburudisha kwa kuwafundisha ukweli wa Mungu, ambao haujachafuliwa na desturi hizo. Pia, anatoa faraja kwa wale wanaohisi kwamba wamepondwa kwa kukandamizwa na mamlaka za kisiasa na kwa wale waliolemewa na dhambi. Naam, Yesu anawafunulia jinsi wanavyoweza kusamehewa dhambi zao na jinsi wanavyoweza kuwa na amani pamoja na Mungu.

Wote wanaokubali nira yenye fadhili ya Yesu wanaweza kujiweka wakfu kwa Mungu na kumtumikia Baba yetu wa mbinguni mwenye huruma na rehema. Kufanya hivyo si mzigo mzito, kwa maana matakwa ya Mungu si yenye kulemea.—1 Yohana 5:3.