Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 43

Mifano Kuhusu Ufalme wa Mbinguni

Mifano Kuhusu Ufalme wa Mbinguni

MATHAYO 13:1-53 MARKO 4:1-34 LUKA 8:4-18

  • YESU ATOA MIFANO KUHUSU UFALME

Huenda Yesu yuko Kapernaumu anapowakemea Mafarisayo. Baadaye siku hiyo, anaondoka nyumbani na kwenda kwenye Bahari ya Galilaya iliyo hapo karibu, ambako umati unakusanyika. Yesu anapanda kwenye mashua, kisha anasogea mbali kidogo na ufuo, na kuanza kuwafundisha watu kuhusu Ufalme wa mbinguni. Anawafundisha kwa kutumia mifano kadhaa. Wasikilizaji wa Yesu wanafahamu mambo au vitu vingi anavyotaja, na hivyo ni rahisi kwao kuelewa mambo mbalimbali kuhusu Ufalme.

Kwanza, Yesu anazungumza kuhusu mpandaji anayepanda mbegu. Mbegu fulani zinaanguka kando ya barabara na kuliwa na ndege. Mbegu nyingine zinaanguka kwenye miamba ambako hakuna udongo mwingi. Mizizi inayotokea haiwezi kufika chini, nayo mimea hiyo michanga inachomwa na jua na kunyauka. Nazo mbegu nyingine zinaanguka katikati ya miiba, ambayo inaisonga mimea michanga inapomea. Mwishowe, baadhi ya mbegu zinaanguka kwenye udongo mzuri. Hizo zinazaa matunda, “nyingine mara 100 zaidi, nyingine 60, na nyingine 30.”—Mathayo 13:8.

Katika mfano mwingine, Yesu anafananisha Ufalme na mtu anayepanda mbegu. Katika kisa hiki, iwe mtu huyu amelala au yuko macho, mbegu zinakua. “Naye hajui jinsi zinavyokua.” (Marko 4:27) Zinakua zenyewe na kutokeza nafaka, ambazo anaweza kuvuna.

Kisha Yesu anatoa mfano wa tatu kuhusu kupanda mbegu. Mtu fulani anapanda mbegu bora, lakini “watu walipokuwa wamelala usingizi,” adui anapanda magugu miongoni mwa ngano. Watumwa wa mtu huyo wanamuuliza ikiwa wanaweza kung’oa yale magugu. Anawajibu: “Hapana, ili mnapong’oa magugu, msije mkang’oa ngano pia. Acheni vikue pamoja mpaka wakati wa mavuno, na katika majira ya mavuno nitawaambia wavunaji: Kusanyeni magugu kwanza na kuyafunga matita-matita ili yateketezwe motoni; kisha mkusanye ngano ghalani mwangu.”—Mathayo 13:24-30.

Watu wengi wanaomsikiliza Yesu wanajua kazi ya ukulima. Pia, anazungumzia kitu kingine wanachofahamu sana, mbegu ndogo ya haradali. Inamea na kuwa mti mkubwa sana hivi kwamba ndege wanakaa kwenye matawi yake. Kuhusu mbegu hiyo, anasema: “Ufalme wa mbinguni ni kama mbegu ya haradali ambayo mtu aliichukua na kuipanda katika shamba lake.” (Mathayo 13:31) Hata hivyo, Yesu hafundishi kuhusu elimu ya mimea. Anafafanua ukuzi mkubwa, jinsi kitu kidogo sana kinavyoweza kukua au kupanuka na kuwa kikubwa sana.

Kisha, Yesu anazungumzia jambo linalofahamika na wasikilizaji wake wengi. Anafananisha Ufalme wa mbinguni na “chachu ambayo mwanamke aliichukua na kuchanganya na vipimo vikubwa vitatu vya unga.” (Mathayo 13:33) Ingawa chachu hiyo haionekani kwa macho, inasambaa kwenye donge lote na kulifanya liumuke. Inatokeza ukuzi na mabadiliko makubwa ambayo hayaonekani kwa macho.

Baada ya kutoa mifano hiyo, Yesu anauaga umati naye anarudi katika nyumba anayoishi. Baada ya muda mfupi wanafunzi wake wanamjia, wakitaka kujua kile alichomaanisha.

KUFAIDIKA KUTOKANA NA MIFANO YA YESU

Hapo awali wanafunzi walimsikia Yesu akitumia mifano, lakini si kama alivyofanya sasa. Wanamuuliza: “Kwa nini unazungumza nao kwa kutumia mifano?”—Mathayo 13:10.

Sababu moja ni ili kutimiza unabii wa Biblia. Simulizi la Mathayo linasema: “Hakuwa akizungumza nao bila mfano, ili kutimiza maneno haya yaliyosemwa kupitia nabii: ‘Nitafungua kinywa changu kwa mifano; nitatangaza mambo yaliyofichwa tangu kuwekwa msingi.’”—Mathayo 13:34, 35; Zaburi 78:2.

Lakini kuna sababu nyingine zinazofanya Yesu atumie mifano. Inasaidia kufunua mtazamo wa watu. Wengi wao wanapendezwa na Yesu kama tu mtu mwenye ustadi wa kusimulia hadithi na kufanya miujiza. Hawamwoni kuwa mtu wanayepaswa kumtii akiwa Bwana na kumfuata bila ubinafsi. (Luka 6:46, 47) Hawataki kubadili maoni yao au njia yao ya maisha. Hawataki ujumbe uwaguse kwa kina sana.

Akijibu swali la wanafunzi, Yesu anasema: “Ndiyo maana ninazungumza nao kwa kutumia mifano, kwa sababu, wanatazama lakini hawaoni, wanasikiliza lakini hawasikii, wala hawaelewi. Na unabii wa Isaya unatimia kuwahusu unaosema: ‘. . . Mioyo ya watu hawa imekuwa migumu.’”—Mathayo 13:13-15; Isaya 6:9, 10.

Hata hivyo, hilo halihusu wale wote wanaomsikiliza Yesu. Anaeleza hivi: “Macho yenu ni yenye furaha kwa sababu yanaona na masikio yenu kwa sababu yanasikia. Kwa kweli ninawaambia, manabii wengi na watu waadilifu walitamani kuona mambo mnayoona lakini hawakuyaona, na kusikia mambo mnayosikia lakini hawakuyasikia.”—Mathayo 13:16, 17.

Naam, wale mitume 12 na wanafunzi wengine washikamanifu wana moyo msikivu. Hivyo, Yesu anasema: “Ninyi mmepewa uwezo wa kuzielewa siri takatifu za Ufalme wa mbinguni, lakini wao hawajapewa.” (Mathayo 13:11) Kwa kuwa wanatamani kwa unyoofu kuelewa, Yesu anawafafanulia wanafunzi wake maana ya mfano wa mpandaji.

Yesu anasema: “Mbegu ni neno la Mungu.” (Luka 8:11) Nao udongo ni moyo. Hiyo ndiyo siri ya kuelewa maana ya mfano wake.

Kuhusu mbegu iliyopandwa kwenye udongo mgumu ulio kando ya barabara, Yesu anasema hivi: “Ibilisi huja na kuliondoa lile neno mioyoni mwao ili wasiamini na kuokolewa.” (Luka 8:12) Anapozungumza kuhusu mbegu iliyopandwa kwenye miamba, Yesu anamaanisha watu wanaolipokea neno kwa shangwe lakini neno halitii mizizi katika mioyo yao. “Dhiki au mateso yakitokea kwa sababu ya lile neno,” wanakwazika. Naam, “wanapojaribiwa,” labda kupitia upinzani kutoka kwa watu wa familia au watu wengine, wanaanguka.—Mathayo 13:21; Luka 8:13.

Namna gani mbegu zilizoanguka katikati ya miiba? Yesu anawaambia wanafunzi wake kwamba zinamaanisha watu ambao wamelisikia neno. Hata hivyo, wanasongwa na “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu za utajiri.” (Mathayo 13:22) Walikuwa na neno mioyoni mwao, lakini sasa limesongwa nalo halizai matunda.

Udongo wa mwisho ambao Yesu anazungumzia ni udongo mzuri. Huu unamaanisha wale wanaolisikia neno na kulikubali katika mioyo yao na kulielewa. Matokeo ni nini? “[Wanazaa] matunda.” Kwa sababu ya hali zao, kama vile umri au afya hawawezi kupata matokeo yaleyale; mmoja anazaa mara 100 zaidi, mwingine 60 zaidi, na mwingine 30 zaidi. Naam, baraka za kumtumikia Mungu huja kwa “wale wenye moyo mzuri na mwema, ambao baada ya kulisikia neno hulihifadhi na kuzaa matunda kwa uvumilivu.”—Luka 8:15.

Maneno hayo lazima yanawavutia hasa wanafunzi ambao wamemtafuta Yesu ili wapate ufafanuzi wa mafundisho yake! Sasa wanaelewa mengi zaidi kuhusu mifano hiyo. Yesu anataka waelewe mifano yake ili nao pia wawafundishe wengine ukweli. Anawauliza: “Je, taa huletwa na kuwekwa chini ya kikapu au chini ya kitanda? Je, hailetwi na kuwekwa juu ya kinara cha taa?” Basi, Yesu anawashauri hivi: “Yeyote aliye na masikio ya kusikiliza, na asikilize.”—Marko 4:21-23.

WAPOKEA MAFUNDISHO ZAIDI

Baada ya kupata ufafanuzi wa mfano wa Yesu wa mpandaji, wanafunzi wanataka kujifunza mengi zaidi. Wanaomba hivi: “Tufafanulie ule mfano wa magugu katika shamba.”—Mathayo 13:36.

Kupitia ombi hilo, wanaonyesha kwamba wana mtazamo tofauti na wa umati uliokuwa ufuoni. Ni wazi kwamba watu hao wanasikia lakini hawatamani kujifunza maana na matumizi ya mifano hiyo. Wanaridhika tu na muhtasari wa mambo yanayotajwa kwenye mifano hiyo. Yesu anaonyesha tofauti kati ya umati uliokuwa ufuoni na wanafunzi wake wanaotaka kujua mengi zaidi, anaposema:

“Sikilizeni kwa makini mambo mnayosikia. Kwa kipimo mnachopima, ndicho mtakachopimiwa, ndiyo, mtaongezewa hata zaidi.” (Marko 4:24) Wanafunzi wanasikiliza kwa makini mambo wanayosikia kutoka kwake. Wanafunzi hao wanampimia Yesu kwa wingi kwa kupendezwa sana na kusikiliza kwa makini, nao wanabarikiwa kwa kupokea mafundisho zaidi, na nuru zaidi. Kwa hiyo, akijibu ombi la wanafunzi kuhusu mfano wa ngano na magugu, Yesu anaeleza hivi:

“Mpandaji aliyepanda mbegu nzuri ni Mwana wa binadamu; lile shamba ni ulimwengu. Nazo mbegu nzuri ni wana wa Ufalme, lakini magugu ni wana wa yule mwovu, na adui aliyepanda magugu ni Ibilisi. Mavuno ni umalizio wa mfumo wa mambo, na wavunaji ni malaika.”—Mathayo 13:37-39.

Baada ya kufafanua kila sehemu ya mfano wake, Yesu anaeleza matokeo. Anasema kwamba wakati wa umalizio wa mfumo wa mambo, wavunaji, au malaika, watawatenganisha Wakristo wa uwongo wanaofananishwa na magugu na “wana wa [kweli wa] Ufalme.” “Waadilifu” watakusanywa na hatimaye watang’aa kwa wangavu “katika Ufalme wa Baba yao.” Namna gani “wana wa yule mwovu”? Matokeo yao ni kuangamizwa, na hapo ndipo “watalia na kusaga meno yao.”—Mathayo 13:41-43.

Kisha Yesu anawaambia wanafunzi wake mifano mitatu zaidi. Kwanza, anasema: “Ufalme wa mbinguni ni kama hazina iliyofichwa katika shamba, ambayo mtu fulani aliipata na kuificha; na kwa sababu ya shangwe aliyo nayo, anaenda na kuuza kila kitu alicho nacho na kununua shamba hilo.”—Mathayo 13:44.

Anaongezea hivi: “Ufalme wa mbinguni ni kama mfanyabiashara anayesafiri akitafuta lulu nzuri. Alipopata lulu moja yenye thamani kubwa, alienda na mara moja akauza vitu vyote alivyokuwa navyo na kuinunua.”—Mathayo 13:45, 46.

Kwa kutumia mifano yote miwili, Yesu anakazia utayari wa mtu kujidhabihu kwa ajili ya mambo yenye thamani zaidi. Mfanyabiashara anauza haraka “vitu vyote alivyokuwa navyo” ili kupata lulu moja yenye thamani kubwa. Wanafunzi wa Yesu wanaweza kuelewa mfano huo kuhusu lulu yenye thamani. Na mtu anayepata hazina iliyofichwa shambani anauza “kila kitu” ili kuipata. Katika visa vyote, kuna kitu fulani chenye thamani, ambacho kinapaswa kumilikiwa na kuthaminiwa sana. Jambo hilo linaweza kulinganishwa na jinsi ambavyo mtu anajidhabihu ili kutosheleza uhitaji wake wa kiroho. (Mathayo 5:3) Baadhi ya wale wanaomsikiliza Yesu akitoa mifano hiyo wameonyesha utayari wa kufanya jitihada za kutosheleza uhitaji wao wa kiroho na kuwa wafuasi wake wa kweli.—Mathayo 4:19, 20; 19:27.

Mwishowe Yesu anafananisha Ufalme wa mbinguni na wavu wa kukokotwa unaovua samaki wa kila aina. (Mathayo 13:47) Samaki wanapotenganishwa, wale wazuri huwekwa katika vyombo, lakini wale wasiofaa hutupwa. Yesu anasema kwamba ndivyo itakavyokuwa katika umalizio wa mfumo wa mambo—malaika watawatenganisha waovu kutoka kwa waadilifu.

Yesu mwenyewe alikuwa akifanya uvuvi wa kiroho alipowaita wanafunzi wake wa kwanza wawe “wavuvi wa watu.” (Marko 1:17) Hata hivyo, anasema kwamba mfano wake kuhusu wavu wa kukokota unahusu wakati ujao, “katika umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 13:49) Hivyo mitume na wanafunzi wengine wanaomsikiliza Yesu wanaweza kutambua kwamba mambo mengi yenye kupendeza yatatokea wakati ujao.

Wale waliosikia mifano ikitolewa kutoka kwenye mashua wanafaidika zaidi. Yesu anaonyesha utayari wake wa ‘kuwafafanulia wanafunzi wake faraghani mambo yote.’ (Marko 4:34) Yeye ni “kama bwana wa nyumba, ambaye hutoa katika hazina yake vitu vipya na pia vya zamani.” (Mathayo 13:52) Yesu anapotoa mifano hiyo, si kwamba anataka kujionyesha kwamba ana uwezo wa kufundisha. Badala yake anashiriki na wanafunzi wake kweli ambazo ni kama hazina yenye thamani. Kwa kweli ni “mwalimu wa watu wote” asiye na kifani.