Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 45

Iko na Mamlaka Juu ya Pepo Wengi Wachafu

Iko na Mamlaka Juu ya Pepo Wengi Wachafu

MATAYO 8:28-34 MARKO 5:1-20 LUKA 8:26-39

  • ANAFUKUZA PEPO WACHAFU NA KUWATUMA KATIKA NGURUWE

Wakati wanafunzi wanafika upande mwengine wa bahari kisha kupatwa na hali yenye kuogopesha, wanaona jambo fulani lenye kushangaza sana. Wanaume wawili wakali sana, wenye kuwa na pepo wachafu, wanatoka katika makaburi yenye kuwa pembeni na kukimbia mupaka kwenye Yesu iko! Maandiko yanakazia uangalifu mwanaume mumoja kati ya wanaume hao, pengine ni kwa sababu ni mukali sana na amekuwa akitawaliwa na pepo wachafu kwa miaka mingi.

Mwanaume huyo amekuwa akitembea bila nguo. Usiku na muchana, “anafanya makelele katikati ya makaburi na kwenye milima na kujikatakata kwa majiwe.” (Marko 5:5) Iko mukali sana hivi kwamba watu wako wanaogopa kupitia barabara kwenye alikuwa. Watu fulani walijaribu kumufunga, lakini alivunja minyororo na pingu zenye zilikuwa kwenye miguu yake. Hakuna mutu mwenye amekuwa na nguvu za kumuzuia.

Wakati mwanaume huyo anamukaribia Yesu na kuanguka kwenye miguu yake, pepo wachafu wenye kumutawala wanafanya alalamike: “Niko na shida gani na wewe, Yesu, Mwana wa Mungu Mwenye Kuwa Juu Zaidi? Ninakuapisha mbele ya Mungu, usinitese.” Yesu anaonyesha kama iko na mamlaka juu ya pepo wachafu kwa kusema hivi: “Toka ndani ya mutu huyu, wewe roho muchafu.”—Marko 5:7, 8.

Kwa kweli, pepo wengi wachafu wanatawala mutu huyo. Wakati Yesu anauliza, “Jina lako nani?” anajibu hivi: “Jina langu Lejioni, kwa sababu tuko wengi.” (Marko 5:9) Katika jeshi la Roma, Lejioni inafanyizwa na maelfu ya maaskari; kwa hiyo, pepo wengi wachafu wanatawala mwanaume huyo na kufurahia mateso yake. Wanamuomba Yesu “asiwaamuru waende katika abiso.” Inaonekana wanatambua mambo yenye yatawapata huko mbele pamoja na kiongozi wao, Shetani.—Luka 8:31.

Karibu na mahali hapo kunapatikana nguruwe 2000 hivi, wanyama wenye hawako safi kulingana na Sheria na wenye Wayahudi hawapaswe kuwa nao. Pepo hao wachafu wanasema hivi: “Ututume ndani ya wale nguruwe, ili tuingie ndani yao.” (Marko 5:12) Yesu anawaambia waende, nao wanaingia katika nguruwe. Kwa hiyo, nguruwe wote 2000 wanakimbia na kuruka kwenye poromoko na kuzama ndani ya bahari.

Wakati wale wenye walikuwa wanachunga nguruwe hao wanaona jambo hilo, wanakimbia haraka ili kupeleka habari katika muji na kwenye eneo la mashamba. Watu wanakuja ili kuona jambo lenye limefanyika. Wakati wanafika, wanaona kama ule mwanaume mwenye pepo wachafu walitoka ndani yake anatenda kama mutu wa kawaida. Sasa ni mwenye kuvaa nguo na anakaa pembeni ya Yesu!

Watu wenye wanasikia jambo hilo ao wanaona mwanaume huyo wanaogopa sana, wanajiuliza ni mambo gani mengine yenye Yesu anaweza kufanya kwa ajili yao. Wanamuomba Yesu atoke katika eneo lao. Wakati Yesu anapanda katika mashua ili kuenda, ule mwanaume mwenye alikuwa na pepo wachafu anaomba aende pamoja na Yesu. Lakini Yesu anaambia mwanaume huyo hivi: “Uende nyumbani kwa watu wa jamaa yako, na uwaelezee mambo yote yenye Yehova amekufanyia na namna amekuonyesha rehema.”—Marko 5:19.

Kwa kawaida Yesu anaambia wale wenye anaponyesha wasiambie mutu yeyote kwa sababu hapendi watu wamuamini kupitia habari za kusikiliza zenye kutiwa chumvi. Lakini katika hali hii, mutu huyo mwenye alikuwa na pepo wachafu ni ushuhuda wa kweli kabisa kwamba Yesu iko na mamlaka, na mutu huyo anaweza kutoa ushahidi kwa watu wenye pengine Yesu mwenyewe hatakutana nao. Ushuhuda wake pia unaweza kupinga habari za uongo kuhusu jambo lenye lilifanya nguruwe wapotee. Kwa hiyo mwanaume huyo anaenda na kuanza kutangaza katika eneo lote la Dekapoli mambo yenye amemufanyia.