Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 49

Kuhubiri Galilaya na Kuwazoeza Mitume

Kuhubiri Galilaya na Kuwazoeza Mitume

MATHAYO 9:35–10:15 MARKO 6:6-11 LUKA 9:1-5

  • YESU ATEMBELEA TENA GALILAYA

  • AWATUMA MITUME WAKAHUBIRI

Yesu amekuwa akihubiri kwa bidii kwa miaka miwili. Je, sasa ni wakati wa kupunguza bidii na kupumzika? La, badala yake, Yesu anapanua kazi yake ya kuhubiri kwa kuanza “kutembelea majiji na vijiji vyote [vya Galilaya], akifundisha katika masinagogi yao na kuhubiri habari njema ya Ufalme na kuponya kila aina ya ugonjwa na kila aina ya udhaifu.” (Mathayo 9:35) Mambo anayoona yanamsadikishia kwamba kuna uhitaji wa kupanua kazi ya kuhubiri. Lakini atafanyaje hivyo?

Anaposafiri, Yesu anaona watu wanaohitaji kuponywa kiroho na kufarijiwa. Wao ni kama kondoo wasio na mchungaji, waliochunwa ngozi na kutupwa huku na huku. Anawasikitikia na kuwaambia wanafunzi wake hivi: “Ndiyo, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.”—Mathayo 9:37, 38.

Yesu anajua jambo litakalosaidia. Anawaita wale mitume 12 na kuwapanga katika vikundi sita vya wawili wawili. Kisha anawapa maagizo yaliyo wazi: “Msiende katika barabara ya mataifa, wala msiingie katika jiji lolote la Wasamaria; badala yake, nendeni kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. Mnapoenda, hubirini mkisema: ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’”—Mathayo 10:5-7.

Ufalme ambao wanapaswa kuutangaza, ni ufalme aliotaja Yesu katika sala ya kielelezo. ‘Ufalme umekaribia’ katika maana ya kwamba Yesu Kristo ambaye ni Mfalme aliyechaguliwa na Mungu, sasa yuko hapo. Hata hivyo, ni nini kitakachothibitisha kwamba wanafunzi wake wanawakilisha Ufalme huo? Yesu anawapa nguvu za kuwaponya wagonjwa na kuwafufua wafu, bila malipo. Basi, mitume watashughulikiaje mahitaji yao, kama vile chakula cha kila siku?

Yesu anawaambia wanafunzi wake wasitayarishe vitu watakavyohitaji katika safari hii ya kuhubiri. Hawapaswi kubeba dhahabu, fedha, au shaba kwenye mikoba yao. Hata hawahitaji mfuko wa chakula, wala mavazi ya ndani ya ziada au viatu. Kwa nini? Yesu anawahakikishia: “Mfanyakazi anastahili chakula chake.” (Mathayo 10:10) Watu watakaowapata ambao wanathamini ujumbe watawapa wanafunzi mahitaji yao ya lazima. Yesu anasema: “Mtakapoingia katika nyumba yoyote, kaeni humo mpaka mtakapoondoka huko.”—Marko 6:10.

Yesu anawapa pia maagizo kuhusu jinsi ya kuwahubiria watu ujumbe wa Ufalme, anasema: “Mnapoingia katika nyumba, wasalimuni watu wa nyumba hiyo. Ikiwa nyumba hiyo inastahili, amani mnayoitakia na iwe juu yake; lakini kama haistahili, amani yenu na iwarudie ninyi. Popote pale ambapo mtu hawakaribishi au kusikiliza maneno yenu, mnapotoka katika nyumba hiyo au jiji hilo, kung’uteni mavumbi yaliyo kwenye miguu yenu.”—Mathayo 10:12-14.

Hata inawezekana kwamba jiji lote au kijiji chote kitakataa ujumbe wao. Itakuwaje kwa jiji au kijiji kama hicho? Yesu anafunua kwamba watahukumiwa vikali. Anaeleza hivi: “Kwa kweli ninawaambia, katika Siku ya Hukumu itakuwa afadhali zaidi kwa Sodoma na Gomora kuliko kwa jiji hilo.”—Mathayo 10:15.