Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 50

Tayari Kuhubiri Licha ya Mateso

Tayari Kuhubiri Licha ya Mateso

MATHAYO 10:16–11:1 MARKO 6:12, 13 LUKA 9:6

  • YESU AWAZOEZA MITUME NA KUWATUMA

Yesu anawapa mitume wake maagizo bora kuhusu jinsi ya kufanya kazi ya kuhubiri, nao wanaenda wawili wawili. Hata hivyo, anawaambia mambo mengine pia. Kwa fadhili anawaonya kuhusu wapinzani: “Tazama! Ninawatuma kama kondoo katikati ya mbwamwitu . . . Jihadharini na watu, kwa maana watawapeleka mahakamani na kuwapiga mijeledi katika masinagogi yao. Nanyi mtapelekwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu.”—Mathayo 10:16-18.

Naam, wafuasi wa Yesu huenda watakabili mateso makali, lakini anawapa ahadi hii yenye kutia moyo: “Mtakapopelekwa, msihangaike kuhusu jambo mtakalosema au jinsi mtakavyolisema, kwa sababu mtapewa jambo la kusema katika saa hiyo; kwa maana si ninyi tu mnaosema, bali ni roho ya Baba yenu inayosema kupitia ninyi. Yesu anaendelea kusema: “Mtu atamtoa ndugu yake auawe, na baba atamtoa mtoto wake, na watoto watainuka dhidi ya wazazi na kufanya wauawe. Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu, lakini yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”—Mathayo 10:19-22.

Kwa sababu kazi ya kuhubiri ni muhimu sana, Yesu anawahimiza wafuasi wake wawe na busara, ili waendelee kufanya kazi hiyo kwa uhuru. Anasema: “Mnapoteswa katika jiji moja, kimbilieni jiji lingine; kwa kweli ninawaambia, hamtamaliza kamwe kuzunguka majiji ya Israeli kabla ya Mwana wa binadamu kufika.”—Mathayo 10:23.

Yesu anawatia moyo mitume wake 12 na kuwapa maagizo na maonyo hayo yaliyo bora sana! Hata hivyo, inaeleweka kwamba, maneno hayo yanawahusu pia wale ambao watafanya kazi ya kuhubiri baada ya Yesu kufa na kufufuliwa. Hilo linathibitishwa na maneno ambayo Yesu alisema, kwamba wanafunzi wake ‘watachukiwa na watu wote,’ bali si wale tu ambao mitume walitumwa kuwahubiria. Isitoshe, haijaandikwa kwamba mitume walipelekwa mbele ya magavana na wafalme katika kampeni hii fupi ya kuhubiri huko Galilaya, wala kwamba watu wa familia zao waliwatoa ili wauawe.

Ni wazi kwamba Yesu anafikiria wakati ujao anapowaambia mitume mambo hayo. Fikiria maneno aliyosema, kwamba wanafunzi wake hawatamaliza “kuzunguka majiji ya Israeli kabla ya Mwana wa binadamu kufika.” Yesu anaonyesha kuwa mitume wake hawatamaliza kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu kabla ya Mfalme aliyetukuzwa, Yesu Kristo kufika akiwa hakimu wa Mungu.

Mitume wanapofanya kazi ya kuhubiri, hawapaswi kushangaa wanapokabili upinzani, kwa sababu Yesu anasema: “Mwanafunzi hamzidi mwalimu wake, wala mtumwa hamzidi bwana wake.” Jambo analosema Yesu liko wazi. Yeye anatendewa vibaya na kuteswa kwa sababu ya kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu, wao pia watatendewa hivyo. Hata hivyo, Yesu anawahimiza: “Msiwaogope wale wanaoua mwili lakini hawawezi kuua nafsi; badala yake, mwogopeni yule anayeweza kuangamiza nafsi na mwili katika Gehena.”—Mathayo 10:24, 28.

Yesu anaweka mfano mzuri katika jambo hili. Bila woga, alivumilia kufa, ili asivunje ushikamanifu wake kwa Yehova, aliye na nguvu zote. Mungu Mweza-Yote ndiye anayeweza kuangamiza “nafsi” ya mtu (matarajio yake ya kuishi wakati ujao) au kumfufua ili afurahie uzima wa milele. Jambo hilo linawatia moyo sana mitume!

Yesu anatoa mfano huu ili kuonyesha jinsi Mungu anavyowapenda na kuwajali wafuasi wake: “Shore wawili huuzwa kwa sarafu ya thamani ndogo, sivyo? Lakini hakuna hata mmoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua. . . . Kwa hiyo msiogope; ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.”—Mathayo 10:29, 31.

Ujumbe ambao wanafunzi wa Yesu wanahubiri utasababisha mgawanyiko katika familia, baadhi ya watu katika familia watakubali na wengine watakataa. Yesu anaeleza: “Msifikiri nilikuja kuleta amani duniani.” Naam, mtu anahitaji ujasiri katika familia ili akubali kweli ya Biblia. Yesu anasema: “Yeyote anayempenda baba au mama kuliko anavyonipenda hanistahili; na yeyote anayempenda mwana au binti kuliko anavyonipenda hanistahili.”—Mathayo 10:34, 37.

Hata hivyo, baadhi ya watu watawakaribisha wanafunzi wake. Anasema: “Yeyote anayempa mmoja wa hawa wadogo kikombe tu cha maji baridi ya kunywa kwa sababu ni mwanafunzi wangu, kwa kweli ninawaambia, hatapoteza kamwe thawabu yake.”—Mathayo 10:42.

Wakiwa wametayarishwa vizuri kwa kupewa maagizo, maonyo, na kutiwa moyo na Yesu, mitume wanaenda “katika eneo hilo kutoka kijiji mpaka kijiji, wakitangaza habari njema na kuponya wagonjwa kila mahali.”—Luka 9:6.