Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 53

Mtawala Anayeweza Kudhibiti Nguvu za Asili

Mtawala Anayeweza Kudhibiti Nguvu za Asili

MATHAYO 14:22-36 MARKO 6:45-56 YOHANA 6:14-25

  • WATU WANATAKA KUMFANYA YESU AWE MFALME

  • YESU ATEMBEA JUU YA MAJI, ATULIZA UPEPO

Watu wanachochewa sana na uwezo wa Yesu wa kulisha maelfu ya watu kimuujiza. Wanafikia mkataa kwamba “kwa kweli huyu ndiye Nabii aliyepaswa kuja ulimwenguni,” yule Masihi, na kwamba kwa hakika atakuwa mtawala anayefaa. (Yohana 6:14; Kumbukumbu la Torati 18:18) Basi watu wanapanga kumkamata Yesu ili wamfanye kuwa mfalme.

Hata hivyo, Yesu anatambua jambo ambalo watu wanapanga. Anauaga umati na kuwaagiza wanafunzi wake warudi kwenye mashua. Wanaelekea wapi? Wataelekea Bethsaida kisha waende Kapernaumu. Lakini Yesu anaenda mlimani ili kusali akiwa peke yake usiku huo.

Muda mfupi kabla ya mapambazuko, kupitia mwangaza wa mwezi, Yesu anaiona ile mashua kwa mbali. Mawimbi ya bahari yanapigwa na upepo wenye nguvu, nao mitume ‘wanataabika kupiga makasia kwa kuwa upepo unavuma kinyume chao.’ (Marko 6:48) Yesu anashuka kutoka mlimani na kuanza kutembea juu ya mawimbi kuwaelekea wanafunzi. Kufikia sasa ‘wamepiga makasia umbali wa karibu kilomita tano au sita.’ (Yohana 6:19) Wanafunzi wanaona kwamba Yesu anataka kuwapita, basi wanapaza sauti kwa woga: “Ni mzuka!”—Marko 6:49.

Yesu anawafariji kwa kuwaambia: “Jipeni moyo! Ni mimi; msiogope.” Lakini Petro anasema: “Bwana, ikiwa ni wewe, niamuru nije kwako nikitembea juu ya maji.” Yesu anajibu: “Njoo!” Papo hapo Petro anatoka kwenye mashua na kwa kweli anatembea juu ya maji kumwelekea Yesu. Lakini Petro anapoitazama ile dhoruba ya upepo, anaogopa na kuanza kuzama. Anapaza sauti: “Bwana, niokoe!” Yesu anaunyoosha mkono wake na kumshika Petro kisha anasema: “Wewe mwenye imani ndogo, kwa nini umekuwa na shaka?”—Mathayo 14:27-31.

Petro na Yesu wanapanda kwenye mashua, na ule upepo unatulia. Wanafunzi wanashangaa, lakini je, wanapaswa kushangaa? Kama wangeelewa “maana ya ule muujiza wa mikate,” ambao Yesu alifanya saa kadhaa mapema alipolisha maelfu, hawangeshangaa kwamba anaweza kutembea juu ya maji na kuutuliza upepo. Sasa wanamsujudia wakisema: “Kwa kweli wewe ni Mwana wa Mungu.”—Marko 6:52; Mathayo 14:33.

Baada ya muda mfupi wanafika kwenye eneo maridadi, tambarare, na lenye rutuba la Genesareti, upande wa kusini wa Kapernaumu. Wanaegesha mashua na kwenda ufuoni. Watu wanamtambua Yesu, na pamoja na watu wengine kutoka maeneo jirani, wanamletea wagonjwa. Watu hao wanapogusa tu pindo za mavazi ya nje ya Yesu, wanapona kabisa.

Wakati huohuo, umati uliomwona Yesu akilisha maelfu ya watu kimuujiza unatambua kwamba Yesu ameondoka. Basi mashua ndogo kutoka Tiberia zinapofika, watu wanapanda na kuelekea Kapernaumu ili kumtafuta Yesu. Wanapompata, wanamuuliza: “Rabi, ulifika hapa wakati gani?” (Yohana 6:25) Akiwa na sababu nzuri, Yesu anawakemea, kama tutakavyoona.