Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 56

Ni Nini Hasa Kinachomchafua Mtu?

Ni Nini Hasa Kinachomchafua Mtu?

MATHAYO 15:1-20 MARKO 7:1-23 YOHANA 7:1

  • YESU AFUNUA DESTURI ZA WANADAMU

Pasaka ya mwaka wa 32 W.K. inapokaribia, Yesu anahubiri kwa bidii huko Galilaya. Kisha huenda anaelekea Yerusalemu kwa ajili ya Pasaka, kulingana na Sheria ya Mungu. Lakini Yesu anafanya hivyo kwa tahadhari kwa sababu Wayahudi wanataka kumuua. (Yohana 7:1) Baada ya hapo anarudi Galilaya.

Huenda Yesu yuko Kapernaumu Mafarisayo na waandishi wanapomjia kutoka Yerusalemu. Kwa nini wamefunga safari hiyo? Wanatafuta msingi wa kumshtaki Yesu kwamba amefanya kosa la kidini. Wanauliza: “Kwa nini wanafunzi wako huvunja mapokeo ya mababu zetu? Kwa mfano, hawanawi mikono kabla ya kula.” (Mathayo 15:2) Mungu hakuwaamuru kamwe watu wake wafuate desturi ya ‘kunawa mikono yao mpaka kwenye kiwiko.’ (Marko 7:3) Lakini Mafarisayo wanaona kutofanya hivyo ni kosa zito.

Badala ya kujibu mashtaka yao moja kwa moja, Yesu anaonyesha jinsi wanavyovunja kimakusudi Sheria ya Mungu. “Kwa nini ninyi pia huvunja amri ya Mungu kwa sababu ya mapokeo yenu?” anawauliza. “Kwa mfano, Mungu alisema, ‘Mheshimu baba yako na mama yako,’ na, ‘Yeyote anayemtukana baba yake au mama yake anapaswa kuuawa.’ Lakini ninyi mnasema, ‘Yeyote anayemwambia baba yake au mama yake: “Chochote nilicho nacho ambacho kingekusaidia ni zawadi iliyowekwa wakfu kwa Mungu,” anakosa kabisa kumheshimu baba yake.’”—Mathayo 15:3-6; Kutoka 20:12; 21:17.

Mafarisayo wanadai kwamba pesa, mali, au kitu kingine kilichowekwa wakfu kwa Mungu ni mali ya hekalu, basi hakiwezi kutumiwa kwa kusudi lingine. Hata hivyo, ukweli ni kwamba bado mtu huyo anamiliki zawadi iliyowekwa wakfu. Huenda mwana akasema kwamba pesa au mali yake ni “korbani,” zawadi iliyowekwa wakfu kwa Mungu au kwa hekalu, kana kwamba tayari zawadi hiyo ni mali ya hekalu. Bado pesa au mali hiyo inaweza kutumiwa na mwana huyo, lakini anadai kwamba hawezi kuitumia kuwasaidia wazazi wake waliozeeka na wenye uhitaji. Kwa hiyo anahepa jukumu lake kuwaelekea.—Marko 7:11.

Kwa kweli, Yesu anakasirishwa na njia hiyo ya kupotosha Sheria ya Mungu naye anasema: “Mmelibatilisha neno la Mungu kwa sababu ya mapokeo yenu. Ninyi wanafiki, kwa kufaa Isaya alitabiri kuwahusu aliposema: ‘Watu hawa huniheshimu kwa midomo yao, lakini mioyo yao iko mbali nami. Wao huniabudu bure, kwa maana wanafundisha amri za wanadamu kuwa mafundisho.’” Mafarisayo wanashindwa kujibu baada ya Yesu kuwakosoa kwa uthabiti. Basi anauita umati ukaribie. “Sikilizeni na kuelewa maneno haya,” anasema. “Mtu hachafuliwi na kile kinachoingia kinywani mwake, bali huchafuliwa na kile kinachotoka kinywani mwake.”—Mathayo 15:6-11; Isaya 29:13.

Baadaye Yesu akiwa katika nyumba, wanafunzi wanamuuliza: “Unajua kwamba Mafarisayo walikwazika waliposikia mambo uliyosema?” Anawajibu: “Kila mmea ambao Baba yangu wa mbinguni hakuupanda utang’olewa. Waacheni. Wao ni viongozi vipofu. Basi, kipofu akimwongoza kipofu, wote wawili watatumbukia ndani ya shimo.”—Mathayo 15:12-14.

Inaonekana Yesu anashangaa wakati Petro, kwa niaba ya wanafunzi, anapoomba afafanuliwe zaidi kuhusu mambo yanayomchafua mtu. Yesu anajibu: “Je, hamjui kwamba chochote kinachoingia kinywani hupita tumboni kisha hutoka na kuingia chooni? Hata hivyo, mambo yanayotoka kinywani hutoka moyoni, nayo ndiyo yanayomchafua mtu. Kwa mfano, moyoni hutoka mawazo mabaya, mauaji, uzinzi, uasherati, wizi, ushahidi wa uwongo, na makufuru. Hayo ndiyo mambo yanayomchafua mtu; lakini kula bila kunawa mikono hakumchafui mtu.”—Mathayo 15:17-20.

Yesu hasemi kwamba watu wasizingatie usafi, wala hapingi kwamba mtu anapaswa kunawa mikono kabla ya kutayarisha au kula chakula. Badala yake, anashutumu unafiki wa viongozi wa kidini ambao wanajaribu kuepuka sheria za Mungu zenye uadilifu na kufuata desturi za wanadamu. Ukweli ni kwamba matendo maovu yanayotoka moyoni ndiyo yanayomchafua mtu.