Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 63

Yesu Atoa Ushauri Kuhusu Kukwaza na Dhambi

Yesu Atoa Ushauri Kuhusu Kukwaza na Dhambi

MATHAYO 18:6-20 MARKO 9:38-50 LUKA 9:49, 50

  • USHAURI KUHUSU KUKWAZWA

  • IKIWA NDUGU ANATENDA DHAMBI

Yesu ametoka tu kuelezea mtazamo ambao wafuasi wake wanapaswa kuwa nao. Wanapaswa kujiona kama watoto, watu wa hali ya chini na wasio na cheo. Wanafunzi wanapaswa ‘kuwapokea watoto wadogo kama hao kwa msingi wa jina lake na hivyo kumpokea Yesu pia.’—Mathayo 18:5.

Hivi karibuni, mitume wamekuwa wakibishana kuhusu ni nani aliye mkuu zaidi, kwa hiyo wanaweza kuona maneno ya Yesu kuwa karipio. Basi mtume Yohana anataja jambo lingine ambalo limetoka tu kutukia: “Tulimwona mtu fulani akifukuza roho waovu kwa kutumia jina lako, tukajaribu kumzuia, kwa sababu hafuatani nasi.”—Luka 9:49.

Je, Yohana anafikiri kwamba mitume peke yao ndio wenye mamlaka ya kuwaponya wengine na kufukuza roho waovu? Ikiwa ndivyo, Myahudi huyo anawezaje kuwafukuza roho waovu? Inaonekana Yohana anahisi kwamba mwanamume huyo hapaswi kufanya miujiza kwa sababu hafuatani na Yesu na mitume.

Yohana anashangaa Yesu anaposema: “Msijaribu kumzuia, kwa maana hakuna yeyote atakayefanya matendo yenye nguvu kwa msingi wa jina langu atakayeweza kusema mambo mabaya kunihusu. Kwa maana yeyote ambaye hatupingi yuko upande wetu. Na yeyote anayewapa kikombe cha maji ya kunywa kwa sababu ninyi ni wa Kristo, kwa kweli ninawaambia hatapoteza kamwe thawabu yake.”—Marko 9:39-41.

Hapana, wakati huu mtu huyo hahitaji kuandamana na Kristo ili kuwa upande wa Yesu. Bado kutaniko la Kikristo halijaanzishwa, kwa hiyo, ingawa mwanamume huyo haandamani na Yesu, haimaanishi kwamba yeye ni mpinzani au anaunga mkono dini ya uwongo. Ni wazi kwamba mtu huyo anaamini jina la Yesu, na mambo ambayo Yesu anasema yanaonyesha kwamba mtu huyo hatapoteza thawabu yake.

Kwa upande mwingine, litakuwa jambo zito ikiwa mwanamume huyo atakwazwa na maneno na matendo ya mitume. Yesu anasema: “Yeyote anayemkwaza mmoja wa hawa wadogo walio na imani, ingekuwa afadhali ikiwa jiwe la kusagia ambalo huzungushwa na punda lingefungwa shingoni mwake kisha atupwe baharini.” (Marko 9:42) Kisha Yesu anasema kwamba wafuasi wake wanapaswa kuondoa hata kitu chenye thamani kama mkono, mguu, au jicho ikiwa kitu hicho kinawafanya wakwazike. Ni vema kutokuwa na kitu kama hicho chenye thamani na kuingia katika Ufalme wa Mungu kuliko kuwa nacho na kuishia Gehena (Bonde la Hinomu). Huenda mitume wameliona bonde hilo karibu na Yerusalemu ambako takataka huchomwa, basi wanaweza kuelewa kwamba linamaanisha uharibifu wa milele.

Pia, Yesu anaonya hivi: “Angalieni msimdharau mmoja wa hawa wadogo, kwa maana ninawaambia kwamba malaika zao mbinguni sikuzote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni.” Hao “wadogo” wana thamani gani mbele za Baba yake? Yesu anasimulia kuhusu mwanamume aliye na kondoo 100 lakini mmoja anapotea. Mtu huyo anawaacha wale 99 na kwenda kumtafuta yule mmoja aliyepotea, na anapompata anashangilia zaidi kuliko wale 99. Yesu anaongezea hivi: “Baba yangu aliye mbinguni hapendi hata mmoja wa hawa wadogo aangamie.”—Mathayo 18:10, 14.

Labda akifikiria mabishano ya mitume wake kuhusu ni nani atakayekuwa mkuu zaidi, Yesu anawaambia hivi: “Iweni na chumvi ndani yenu, na mdumishe amani kati yenu.” (Marko 9:50) Chumvi huongeza ladha kwenye chakula. Chumvi ya mfano hufanya iwe rahisi zaidi kwa watu kukubali mambo tunayosema na hivyo kusaidia kudumisha amani, lakini mabishano hayawezi kuleta amani.—Wakolosai 4:6.

Nyakati nyingine matatizo mazito hutokea, na Yesu anazungumzia jinsi ya kuyashughulikia. Yesu anasema: “Ndugu yako akitenda dhambi, nenda ufunue kosa lake kati yako na yeye peke yenu. Akikusikiliza, umempata ndugu yako.” Namna gani asiposikiliza? Yesu anashauri hivi: “Nenda pamoja na mtu mmoja au wawili, ili kwa ushahidi wa mashahidi wawili au watatu kila jambo lithibitishwe.” Ikiwa kufanya hivyo hakumalizi tatizo hilo, wanapaswa kuliambia “kutaniko,” yaani, wazee ambao wanaweza kufanya uamuzi. Namna gani ikiwa mkosaji huyo bado hasikilizi? “Na awe kwako kama mtu wa mataifa na kama mkusanya kodi,” watu ambao Wayahudi hawakushirikiana nao.—Mathayo 18:15-17.

Waangalizi wa kutaniko wanahitaji kufuata Neno la Mungu. Ikiwa wanampata mkosaji na hatia naye anahitaji kutiwa nidhamu, tayari hukumu yao ‘itakuwa imefungwa mbinguni.’ Lakini wasipompata na hatia, itakuwa ‘imefunguliwa mbinguni.’ Miongozo hiyo itakuwa msaada mkubwa kutaniko la Kikristo litakapoanzishwa. Katika mazungumzo hayo mazito, Yesu anasema: “Mahali wanapokusanyika wawili au watatu katika jina langu, nipo hapo kati yao.”—Mathayo 18:18-20.