Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 65

Kufundisha Akiwa Safarini Kwenda Yerusalemu

Kufundisha Akiwa Safarini Kwenda Yerusalemu

MATHAYO 8:19-22 LUKA 9:51-62 YOHANA 7:2-10

  • JINSI NDUGU ZA YESU WANAVYOMWONA

  • HUDUMA YA UFALME NI MUHIMU KADIRI GANI?

Kwa muda fulani, Yesu amefanya kazi yake hasa katika Galilaya, ambako watu wameitikia vizuri kuliko huko Yudea. Isitoshe, alipomponya mwanamume siku ya Sabato huko Yerusalemu, ‘Wayahudi walizidi kutafuta njia ya kumuua.’—Yohana 5:18; 7:1

Sasa ni majira ya kupukutika ya mwaka wa 32 W.K., na Sherehe ya Vibanda inakaribia. Sherehe hii hufanywa kwa siku saba, na siku ya nane kunakuwa na kusanyiko takatifu. Sherehe hiyo hufanyika mwishoni mwa mwaka wa kilimo na ni pindi yenye shangwe sana na ya kutoa shukrani.

Ndugu wa kambo wa Yesu—Yakobo, Simoni, Yosefu, na Yuda—wanamhimiza: “Ondoka hapa uende Yudea.” Jiji la Yerusalemu ndilo kitovu cha kidini nchini. Katika zile sherehe tatu za kila mwaka, jiji hilo hujaa watu. Ndugu za Yesu wanasema: “Mtu yeyote anayetaka kujulikana hadharani hafanyi jambo lolote kisiri. Ikiwa unafanya mambo haya jionyeshe kwa ulimwengu.”—Yohana 7:3, 4.

Kwa kweli ndugu hawa wanne “hawakuwa wakimwamini” kwamba yeye ni Masihi. Hata hivyo, wanataka wale waliokuja kwenye sherehe waone akifanya miujiza. Yesu anajua kufanya hivyo ni hatari, anawaambia: “Ulimwengu hauna sababu ya kuwachukia ninyi, lakini unanichukia mimi kwa sababu ninatoa ushahidi kuuhusu kwamba matendo yake ni maovu. Ninyi nendeni kwenye sherehe; mimi bado siendi kwenye sherehe hiyo, kwa sababu bado wakati wangu haujafika kikamili.”—Yohana 7:5-8.

Siku chache baada ya ndugu za Yesu kuondoka pamoja na kikundi kikubwa cha wasafiri, Yesu na wanafunzi wake wanaondoka kisiri, bila kuonwa na watu. Wanatumia njia ya moja kwa moja inayopitia Samaria, badala ya njia inayotumiwa na watu wengi iliyo karibu na Mto Yordani. Yesu na wanafunzi wake watahitaji mahali pa kulala huko Samaria, basi anawatuma wajumbe watangulie na kufanya matayarisho. Watu wa eneo fulani wanakataa kuwakaribisha wala kuwaonyesha ukarimu kama ilivyo kawaida kwa sababu Yesu anaelekea Yerusalemu kwa ajili ya sherehe ya Kiyahudi. Kwa hasira, Yakobo na Yohana wanauliza: “Bwana unataka tuagize moto utoke mbinguni uwaangamize?” (Luka 9:54) Yesu anawakemea kwa kutoa maoni hayo, nao wanaendelea na safari.

Wakiwa njiani, mwandishi mmoja anamwambia Yesu: “Mwalimu, nitakufuata popote utakapoenda.” Yesu anamwambia: “Mbweha wana mapango na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali pa kulaza kichwa chake.” (Mathayo 8:19, 20) Anamaanisha kwamba mwandishi huyo atakabili hali ngumu iwapo atakuwa mfuasi wa Yesu. Na inaonekana mwandishi huyo ana kiburi sana hivi kwamba hawezi kukubali maisha kama hayo. Kwa hiyo, kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza: ‘Mimi niko tayari kadiri gani kumfuata Yesu?’

Yesu anamwambia mtu mwingine hivi: “Njoo, uwe mfuasi wangu.” Mtu huyo anajibu: “Bwana, niruhusu kwanza niende nikamzike baba yangu.” Yesu akijua hali za mtu huyo, anamwambia: “Waache wafu wawazike wafu wao, lakini wewe nenda ukatangaze Ufalme wa Mungu kila mahali.” (Luka 9:59, 60) Inawezekana kwamba baba yake bado hajafa. Ikiwa angekuwa amekufa, mwana huyo hangekuwa hapo akizungumza na Yesu. Mwana huyo hayuko tayari kutanguliza Ufalme wa Mungu maishani mwake.

Wanapoendelea kushuka kuelekea Yerusalemu, mtu mwingine anamwambia Yesu: “Bwana nitakufuata, lakini niruhusu kwanza nikawaage watu wa nyumbani kwangu.” Yesu anajibu: “Yeyote anayeshika jembe la ng’ombe na kutazama vitu vilivyo nyuma hastahili Ufalme wa Mungu.”—Luka 9:61, 62.

Wale wanaotaka kuwa wanafunzi wa kweli wa Yesu lazima wakaze macho yao kwenye kazi ya Ufalme. Mkulima asipoendelea kutazama mbele, inawezekana kwamba mtaro anaochimba utaenda kombo. Akiliweka jembe chini ili atazame vitu vilivyo nyuma, hatamaliza kazi shambani. Vivyo hivyo, yeyote anayeangalia nyuma na kutazama ulimwengu huu wa kale, anaweza kukwazika na kuiacha barabara inayoongoza kwenye uzima wa milele.