Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 67

‘Hakuna Mtu Mwingine Ambaye Amewahi Kuzungumza Hivyo’

‘Hakuna Mtu Mwingine Ambaye Amewahi Kuzungumza Hivyo’

YOHANA 7:32-52

  • MAOFISA WATUMWA WAKAMKAMATE YESU

  • NIKODEMO AMTETEA YESU

Bado Yesu yuko Yerusalemu kwa ajili ya Sherehe ya Vibanda. Anafurahi kwamba ‘wengi katika umati wanamwamini.’ Hata hivyo, viongozi wa kidini hawafurahishwi na jambo hilo. Wanawatuma maofisa, ambao ni askari wa kidini ili wakamkamate. (Yohana 7:31, 32) Hata hivyo, Yesu hajifichi.

Badala yake, Yesu anaendelea kufundisha hadharani huko Yerusalemu akisema: “Nitakuwa pamoja nanyi kwa muda mfupi kisha nitarudi kwa Yule aliyenituma. Mtanitafuta lakini hamtanipata, na mahali nilipo hamwezi kuja.” (Yohana 7:33, 34) Wayahudi hawaelewi anachomaanisha, kwa hiyo wanaulizana: “Mtu huyu anakusudia kwenda wapi, hivi kwamba hatutampata? Je, anakusudia kwenda kwa Wayahudi waliotawanyika kati ya Wagiriki ili awafundishe Wagiriki? Anamaanisha nini anaposema, ‘Mtanitafuta, lakini hamtanipata, na mahali nilipo hamwezi kuja’?” (Yohana 7:35, 36) Hata hivyo, Yesu anazungumza kuhusu kifo chake na jinsi atakavyofufuliwa na kwenda mbinguni ambako maadui wake hawawezi kumfuata.

Siku ya saba ya sherehe inafika. Kila asubuhi ya sherehe, kuhani amekuwa akimwaga maji yaliyotekwa kwenye Dimbwi la Siloamu, ili yatiririke chini ya madhabahu. Huenda Yesu anawakumbusha watu kuhusu zoea hilo anapopaza sauti na kusema: “Ikiwa yeyote ana kiu, na aje kwangu anywe maji. Yeyote anayeniamini, kama andiko linavyosema: ‘Vijito vya maji ya uzima vitatiririka kutoka ndani yake.’”—Yohana 7:37, 38.

Yesu anazungumzia jambo litakalotokea wanafunzi wake watakapotiwa mafuta kwa roho takatifu na kupata tumaini la kwenda mbinguni. Wanatiwa mafuta baada ya kifo cha Yesu. Kuanzia siku ya Pentekoste mwaka unaofuata, vijito vya maji yanayotoa uhai vinaanza kutiririka wanafunzi waliotiwa mafuta kwa roho wanapowaeleza watu ukweli.

Baada ya kusikiliza mafundisho ya Yesu, baadhi yao wanasema: “Kwa kweli huyu ndiye Nabii,” inaelekea wanarejelea nabii aliyetabiriwa ambaye angekuwa mkuu kuliko Musa. Wengine wanasema: “Huyu ndiye Kristo.” Lakini wengine wanapinga na kusema: “Kristo hatakuja kutoka Galilaya, sivyo? Je, andiko halisemi kwamba Kristo atatoka katika uzao wa Daudi na atatoka Bethlehemu, kijiji alichoishi Daudi?”—Yohana 7:40-42.

Basi umati umegawanyika. Ingawa baadhi yao wanataka Yesu akamatwe, hakuna anayemgusa. Maofisa wanaporudi kwa viongozi wa kidini bila kumkamata Yesu, wakuu wa makuhani na Mafarisayo wanawauliza: “Kwa nini hamkumleta?” Maofisa wanajibu: “Hakuna mtu mwingine yeyote ambaye amewahi kuzungumza hivyo.” Kwa hasira viongozi wa kidini wanaanza kuwadhihaki na kuwatukana: “Je, ninyi pia mmepotoshwa? Je, kuna yeyote kati ya watawala au Mafarisayo ambaye amemwamini? Lakini umati huu usiojua Sheria ni watu waliolaaniwa.”—Yohana 7:45-49.

Hapo ndipo Nikodemo, ambaye ni Farisayo na mshiriki wa Sanhedrini, anapoanza kumtetea Yesu. Miaka miwili na nusu mapema, Nikodemo alimtembelea Yesu usiku na kuonyesha kwamba anamwamini. Sasa Nikodemo anasema: “Kulingana na Sheria yetu, kabla ya kumhukumu mtu, tunapaswa kumsikiliza ili tujue anachofanya, sivyo?” Wanajitetea hivi: “Je, wewe pia umetoka Galilaya? Chunguza uone kwamba hakuna nabii atakayeinuliwa kutoka Galilaya.”—Yohana 7:51, 52.

Maandiko hayasemi moja kwa moja kwamba nabii angetokea Galilaya. Hata hivyo Neno la Mungu lilionyesha kwamba Kristo angetokea huko; lilitabiri kwamba “nuru kuu” ingeonekana katika “Galilaya ya mataifa.” (Isaya 9:1, 2; Mathayo 4:13-17) Isitoshe, kama ilivyotabiriwa, Yesu alizaliwa huko Bethlehemu, naye ni mzao wa Daudi. Ingawa huenda Mafarisayo wanajua mambo hayo, inawezekana kwamba wao ndio wanaoeneza habari za uwongo kumhusu Yesu.