Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 67

“Hakuna Mutu Mwenye Amekwisha Kusema Kama Mutu Huyu”

“Hakuna Mutu Mwenye Amekwisha Kusema Kama Mutu Huyu”

YOHANA 7:32-52

  • WALINZI WANATUMWA ILI KUMUKAMATA YESU

  • NIKODEMO ANAMUSEMEA YESU

Yesu angali katika Yerusalemu kwa ajili ya Sikukuu ya Tabenakulo. Anafurahi kuona kuwa “wengi kati ya watu walimuamini.” Lakini hilo halifurahishe viongozi wa dini. Wanatuma walinzi, wenye wanatumika kama polisi wa dini, ili wamukamate. (Yohana 7:31, 32) Hata hivyo, Yesu hajaribu kujificha.

Lakini, Yesu anaendelea kufundisha mbele ya watu wengi katika Yerusalemu, kwa kusema hivi: “Nitaendelea kuwa pamoja na ninyi kwa wakati mufupi mbele niende kwa Ule mwenye alinituma. Mutanitafuta, lakini hamutanipata, na kwenye niko hamuwezi kuja.” (Yohana 7:33, 34) Wayahudi hawaelewe, ndiyo sababu wanajiambia kati yao wenyewe hivi: “Mutu huyu anakusudia kuenda wapi, na hivyo hatutamupata? Je, anakusudia kuenda kwa Wayahudi wenye walitawanyika kati ya Wagiriki na afundishe Wagiriki? Anamaanisha nini wakati anasema, ‘Mutanitafuta, lakini hamutanipata, na kwenye niko hamuwezi kuja’?” (Yohana 7:35, 36) Lakini, Yesu iko anazungumuzia kifo chake na ufufuo wake ili kuenda mbinguni, na maadui wake hawawezi kumufuata huko.

Siku ya saba ya sikukuu inafika. Kila asubui ya sikukuu hiyo, kuhani mumoja anamwanga maji yenye yanatoka katika Dimbwi la Siloamu, yenye yanatiririka kwenye musingi wa mazabahu ya hekalu. Pengine ili kukumbusha watu tabia hiyo, Yesu anasema kwa sauti kubwa hivi: “Kama mutu yeyote iko na kiu, akuje kwangu na akunywe. Kila mutu mwenye ananiamini, kama vile andiko lilisema: ‘Kutoka ndani yake kabisa, mito midogo ya maji ya uzima itatiririka.’”—Yohana 7:37, 38.

Yesu iko anazungumuzia kile kitatokea wakati wanafunzi wake watatiwa mafuta kwa roho takatifu na kupata mwaliko wa kuenda kuishi mbinguni. Jambo hilo la kutiwa mafuta litafanyika kisha kifo cha Yesu. Kuanzia siku ya Pentekoste ya mwaka wenye kufuata, mito midogo ya maji yenye kuleta uzima itaanza kutiririka wakati wanafunzi watiwa-mafuta watafanya kazi ya kuhubiria watu kweli.

Kuhusu mafundisho ya Yesu, wamoja wanasema hivi: “Kwa kweli huyu ni ule Nabii,” inawezekana wako wanafikiria ule nabii mwenye alitabiriwa ambaye ni mukubwa zaidi kuliko Musa. Wengine wanasema hivi: “Huyu ndiye Kristo.” Lakini wengine wanabisha kwa kusema: “Kristo hatakuja kutoka Galilaya, haiko vile? Je, andiko haliseme kwamba Kristo anakuja kutoka katika uzao wa Daudi na kutoka katika Betlehemu, kijiji kwenye Daudi alikuwa?”—Yohana 7:40-42.

Kwa hiyo, watu wanagawanyika. Hata kama watu fulani wanapenda Yesu akamatwe, hakuna hata mutu mumoja mwenye anapima kumukamata. Wakati walinzi wanarudia kwenye viongozi Wayahudi walikuwa pasipo Yesu, wakubwa wa makuhani na Mafarisayo wanawauliza hivi: “Sababu gani hamukumuleta?” Walinzi wanajibu hivi: “Hakuna mutu mwenye amekwisha kusema kama mutu huyu.” Kwa sababu ya kisirani, viongozi hao wa dini wanaanza kuzarau na kutukana kwa kusema: “Je, ninyi pia mumedanganywa? Hakuna hata mumoja wa watawala ao wa Wafarisayo mwenye amemuamini, haiko vile? Lakini watu hawa wenye hawajue sheria ni watu wenye kulaaniwa.”—Yohana 7:45-49.

Kwa hiyo, Nikodemo, Mufarisayo mumoja na ambaye ni mutu wa Sanhedrini, anapata ujasiri wa kumusemea Yesu. Miaka mbili na nusu mbele ya hapo, Nikodemo alikuja kumuona Yesu usiku na akaonyesha imani katika yeye. Sasa Nikodemo anasema hivi: “Sheria yetu haihukumu mutu mbele ya kumusikiliza na kujua jambo lenye anafanya, haiko vile?” Wanajibu namna gani ili kujitetea? Wanamuambia hivi: “Je, wewe pia umetoka Galilaya? Chunguza na uone kwamba hakuna nabii mwenye atainuliwa kutoka Galilaya.”—Yohana 7:51, 52.

Maandiko hayaseme moja kwa moja kuwa nabii fulani angetokea Galilaya. Hata hivyo, Neno la Mungu lilionyesha kuwa Kristo yeye angetokea Galilaya; lilitabiri kuwa “mwangaza mukubwa” ungeonekana katika “Galilaya ya mataifa.” (Isaya 9:1, 2; Matayo 4:13-17) Zaidi ya hilo, kama vile ilitabiriwa, Yesu alizaliwa katika Betlehemu, na ni mutu wa uzao wa Daudi. Hata kama Wafarisayo wanaweza kuwa wanajua jambo hilo, inaonekana kuwa ni wao ndio wanafanya watu wengi wakuwe na mawazo ya uongo juu ya Yesu.