Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 72

Yesu Awatuma Wanafunzi 70 Wakahubiri

Yesu Awatuma Wanafunzi 70 Wakahubiri

LUKA 10:1-24

  • YESU ACHAGUA WANAFUNZI 70 NA KUWATUMA WAKAHUBIRI

Sasa ni mwishoni mwa mwaka wa 32 W.K., karibu miaka mitatu tangu Yesu alipobatizwa. Hivi karibuni, yeye na wanafunzi wake walikuwa kwenye Sherehe ya Vibanda huko Yerusalemu. Huenda bado wako karibu na Yerusalemu. (Luka 10:38; Yohana 11:1) Kwa kweli, Yesu anatumia kipindi kinachobaki cha miezi sita ya huduma yake huko Yudea au ng’ambo ya Mto Yordani katika wilaya ya Perea. Anahitaji kuhubiri katika maeneo hayo pia.

Mapema, baada ya Pasaka ya mwaka wa 30 W.K., Yesu alitumia miezi kadhaa akihubiri huko Yudea na kusafiri kupitia Samaria. Kisha karibu na Pasaka ya mwaka wa 31 W.K., Wayahudi huko Yerusalemu wakajaribu kumuua. Kwa mwaka mmoja na nusu uliofuata, Yesu alihubiri hasa kaskazini, huko Galilaya. Katika kipindi hicho, alipata wafuasi wengi. Huko Galilaya, Yesu aliwazoeza mitume wake kisha akawatuma na kuwapa maagizo haya: “Hubirini mkisema: ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’” (Mathayo 10:5-7) Sasa anapanga kampeni ya kuhubiri huko Yudea.

Ili kuanza kampeni hiyo, Yesu anawachagua wanafunzi 70 na kuwatuma wawili wawili. Kwa hiyo, kuna vikundi 35 vya wahubiri wa Ufalme katika eneo hilo, ambalo “mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.” (Luka 10:2) Wanapaswa kutangulia kwenda kwenye maeneo ambayo huenda baadaye Yesu ataenda. Wale 70 watawaponya wagonjwa na kutangaza ujumbe ambao Yesu amekuwa akihubiri.

Wanafunzi hao hawatakazia fikira kuhubiri katika masinagogi tu. Yesu anawaambia waende kwenye nyumba za watu. Anawaagiza hivi: “Mkiingia katika nyumba yoyote, kwanza semeni: ‘Nyumba hii na iwe na amani.’ Na kama humo kuna rafiki wa amani, amani yenu itakaa naye.” Watatangaza ujumbe gani? Yesu anawaambia: “[Waambieni]: ‘Ufalme wa Mungu umekuja karibu nanyi.’”—Luka 10:5-9.

Maagizo ambayo Yesu anawapa wale 70 ni kama yale aliyotoa alipowatuma mitume 12 karibu mwaka mmoja uliopita. Anawaonya kwamba si watu wote watakaowakaribisha. Ingawa hivyo, jitihada zao zitawatayarisha wanaotaka kusikiliza ili Yesu atakapofika muda mfupi baadaye, wengi wawe na hamu ya kukutana na Bwana na kujifunza kutoka kwake.

Baada ya muda, wale wahubiri 70 wa Ufalme wanarudi kwa Yesu. Kwa shangwe wanamwambia: “Bwana, hata tunawatiisha roho waovu kwa kutumia jina lako.” Bila shaka, ripoti hiyo nzuri inamsisimua Yesu, kwa maana anasema: “Ninamwona Shetani akiwa tayari ameanguka kutoka mbinguni kama radi. Tazama! Nimewapa mamlaka ya kukanyaga nyoka na nge.”—Luka 10:17-19.

Kwa hiyo, Yesu anawahakikishia wafuasi wake kwamba watashinda mambo hatari, kwa njia ya mfano watakanyaga nyoka na nge. Isitoshe, wanaweza kuwa na uhakika kwamba wakati ujao Shetani ataanguka kutoka mbinguni. Pia, Yesu anawasaida wale 70 kuona jambo ambalo hasa litakuwa muhimu mwishowe. Anasema: “Msishangilie kwa sababu mnawatiisha roho waovu, bali shangilieni kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.”—Luka 10:20.

Yesu anashangilia na kumsifu Baba yake hadharani kwa kuwatumia kwa njia kubwa hivyo watumishi hao wake wanyenyekevu. Akiwageukia wanafunzi wake, anawaambia: “Yenye furaha ni macho yanayoona mambo mnayoona. Kwa maana ninawaambia, manabii na wafalme wengi walitamani kuona mambo mnayoona lakini hawakuyaona, na kusikia mambo mnayosikia lakini hawakuyasikia.”—Luka 10:23, 24.