Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 74

Anafundisha Kuhusu Ukaribishaji-Wageni na Kuhusu Sala

Anafundisha Kuhusu Ukaribishaji-Wageni na Kuhusu Sala

LUKA 10:38–11:13

  • YESU ANATEMBELEA MARTA NA MARIA

  • KUENDELEA KUSALI NI KWA MAANA

Upande wa mashariki wa Mulima wa Mizeituni, kwenye karibu kilometre 3 kutoka Yerusalemu, kunapatikana kijiji cha Betania. (Yohana 11:18) Yesu anaenda huko na anaingia katika nyumba ya dada wawili, Marta na Maria. Dada hawa pamoja na ndugu yao, Lazaro, ni marafiki wa Yesu, na wanamukaribisha kwa furaha.

Ni pendeleo kukaribisha Masiya nyumbani. Marta iko na hamu ya kumukaribisha Yesu muzuri, kwa hiyo anatumika sana ili kutayarisha chakula chenye kuwa na mambo mengi. Wakati Marta iko anafanya kazi, Maria anakaa kwenye miguu ya Yesu na kumusikiliza. Kisha muda fulani, Marta anamuambia Yesu: “Bwana, haikusumbue kwamba dada yangu ameniacha nifanye kazi peke yangu? Umuambie akuje kunisaidia.”—Luka 10:40.

Kuliko kumulaumu Maria, Yesu anashauria Marta kwa sababu ya kuhangaikia sana vitu vya kimwili. Anamuambia hivi: “Marta, Marta, unahangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi. Lakini, mambo kidogo ndiyo yanahitajiwa, ao hata jambo moja tu. Maria alichagua sehemu ya muzuri, na haitaondolewa kwake.” (Luka 10:41, 42) Ndiyo, Yesu anaonyesha kwamba haiko jambo la lazima kutumia wakati mwingi ili kutayarisha chakula mbalimbali. Chakula chenye hakina mambo mengi kinatosha.

Marta iko na nia ya muzuri. Anapenda kuwa mukaribishaji-wageni. Lakini kuhangaikia tu chakula kunaonyesha kuwa iko anapoteza mafundisho ya maana kutoka kwa Mwana wa Mungu! Yesu anakazia kama Maria alikamata uamuzi wa muzuri, uamuzi wenye utamusaidia kupata baraka za milele. Pia, ni somo la maana kwa sisi wote lenye tunapaswa kukumbuka.

Wakati mwengine, Yesu anatoa somo lingine tofauti lakini la maana. Mwanafunzi mumoja anamuomba Yesu hivi: “Bwana, utufundishe kusali, kama vile Yohana pia alifundisha wanafunzi wake.” (Luka 11:1) Yesu amekwisha kufanya hivyo kwenye Mahubiri ya Mulimani kumepita karibu mwaka moja na nusu. (Matayo 6:9-13) Hata hivyo, pengine mwanafunzi huyo hakukuwa hapo wakati huo, kwa hiyo Yesu anarudilia mambo makubwa. Kisha anatoa mufano ili kukazia kwamba ni jambo la lazima kuendelea kusali.

Anasema hivi: “Tuseme mumoja wenu iko na rafiki, na anaenda kwake katikati ya usiku na kumuambia, ‘Rafiki, unikopeshe mikate tatu (3), kwa sababu rafiki yangu mumoja amenitembelea kutoka katika safari na sina kitu cha kumupatia.’ Lakini ule anamujibu akiwa ndani: ‘Acha kunisumbua. Tayari mulango umefungwa, na watoto wangu wadogo wako pamoja na mimi katika kitanda. Siwezi kuamuka nikupatie kitu chochote.’ Ninawaambia ninyi, hata kama hataamuka na kumupatia kitu chenye anaomba kwa sababu yeye ni rafiki yake, lakini kwa sababu anaendelea kuomba kwa uhodari, ataamuka na kumupatia kitu chochote chenye iko nacho lazima.”—Luka 11:5-8.

Yesu hatake kusema kuwa Yehova haiko tayari kujibia sala zetu, kama vile ule rafiki hakukuwa tayari kujibia ombi la rafiki yake. Lakini, iko anaonyesha kwamba ikiwa mutu mwenye haiko tayari kusaidia anafikia kusaidia rafiki yake mwenye ameendelea kumuomba, bila shaka Baba yetu wa mbinguni atajibu sala zenye kutoka moyoni za watumishi wake waaminifu! Yesu anaendelea: “Ninawaambia ninyi, muendelee kuomba, na mutapewa; muendelee kutafuta, na mutapata; muendelee kupiga hodi, na watawafungulia. Kwa maana kila mutu mwenye anaomba anapokea, na kila mutu mwenye anatafuta anapata, na kila mutu mwenye anapiga hodi, watamufungulia.”—Luka 11:9, 10.

Kisha Yesu anakazia maneno yake kwa kulinganisha jambo hilo na namna wazazi wanadamu wanatenda. Anasema hivi: “Ni baba gani kati yenu, kama mwana wake anaomba samaki atamupatia nyoka kuliko kumupatia samaki? Ao pia kama anaomba yai, atamupatia nge? Kwa hiyo, ikiwa ninyi, hata kama muko waovu, munajua kupatia watoto wenu zawadi za muzuri, Baba yenu wa mbinguni atawapatia hata zaidi roho yake takatifu wale wenye kumuomba!” (Luka 11:11-13) Kwa kweli, hilo linatuhakikishia kuwa Baba yetu iko tayari kutusikia na kututimizia mahitaji yetu!