Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 76

Kula Mlo Pamoja na Farisayo

Kula Mlo Pamoja na Farisayo

LUKA 11:37-54

  • YESU AWASHUTUMU MAFARISAYO WANAFIKI

Akiwa Yudea, Yesu anakubali Farisayo fulani anapomwalika kwenye mlo. Inawezekana ni mlo wa mchana, si mlo wa jioni. (Luka 11:37, 38; linganisha na Luka 14:12.) Kabla ya kula, Mafarisayo wanafuata desturi ya kunawa mikono hadi kwenye kiwiko. Lakini Yesu hafanyi hivyo. (Mathayo 15:1, 2) Kunawa mikono kwa njia hiyo hakuvunji Sheria ya Mungu, hata hivyo si takwa la Mungu.

Farisayo huyo anashangaa kwamba Yesu hafuati desturi hiyo. Yesu anagundua jambo hilo naye anasema: “Ninyi Mafarisayo, husafisha upande wa nje wa kikombe na sahani, lakini ndani yenu mmejaa pupa na uovu. Enyi wapumbavu! Yule aliyetengeneza nje ndiye aliyetengeneza ndani pia, sivyo?”—Luka 11:39, 40.

Kunawa mikono kabla ya kula si tatizo, bali tatizo ni unafiki wa kidini. Mafarisayo na wengine ambao hunawa mikono yao kidesturi, hawasafishi uovu ulio katika mioyo yao. Basi Yesu anawashauri hivi: “Toeni vitu vilivyo ndani viwe zawadi za rehema, na tazama! mtakuwa safi katika mambo mengine yote.” (Luka 11:41) Hilo ni kweli kabisa! Mtu anapaswa kutoa akichochewa na moyo wenye upendo, bali si tamaa ya kuwafurahisha wengine kwa kujifanya mwadilifu.

Si kwamba watu hao hawatoi.Yesu anasema hivi: “Mnatoa sehemu ya kumi ya mnanaa na mchicha na kila aina ya mboga, lakini mnapuuza haki na kumpenda Mungu! Mlipaswa kufanya mambo hayo, bila kupuuza yale mengine.” (Luka 11:42) Sheria ya Mungu iliwataka watoe fungu la kumi la mazao. (Kumbukumbu la Torati 14:22) Hilo lilitia ndani mnanaa na mchicha, mboga au mimea iliyotumiwa kuongeza ladha kwenye chakula. Mafarisayo walitoa kikamili fungu la kumi la mimea hiyo, lakini namna gani kuhusu mambo muhimu zaidi yaliyo katika Sheria, kama vile kutenda haki na kuwa wenye kiasi mbele za Mungu?—Mika 6:8.

Yesu anaongezea hivi: “Ole wenu Mafarisayo, kwa sababu mnapenda viti vya mbele katika masinagogi na kusalimiwa sokoni! Ole wenu, kwa sababu ninyi ni kama makaburi yasiyoonekana, ambayo watu hutembea juu yake bila kujua!” (Luka 11:43, 44) Kwa kweli, watu wanaweza kuanguka juu ya makaburi hayo na hivyo wasiwe safi kisherehe. Yesu anataja jambo hilo ili kukazia kwamba uchafu wa Mafarisayo hauonekani waziwazi.—Mathayo 23:27.

Mtu fulani mwenye ujuzi wa Sheria ya Mungu analalamika hivi: “Mwalimu, unaposema mambo hayo, unatutukana sisi pia.” Hata hivyo, watu hao wanapaswa kutambua kwamba hawawasaidii watu. Yesu anasema: “Ole wenu pia ninyi mlio na ujuzi wa Sheria, kwa sababu mnawatwika watu mizigo mizito, lakini ninyi wenyewe hamwigusi hata kwa kidole kimoja! Ole wenu, kwa sababu mnajenga makaburi ya manabii ambao mababu zenu waliwaua!”—Luka 11:45-47.

Mizigo ambayo Yesu anazungumzia ni jinsi Mafarisayo wanavyofafanua Sheria na mapokeo yanayosimuliwa. Watu hao wanafanya maisha ya watu yawe magumu. Wanasisitiza kwamba watu wote wanapaswa kufuata sheria zilizo kama mizigo mizito. Mababu zao waliwaua manabii wa Mungu, kuanzia Abeli na kuendelea. Sasa wao, ambao wanaonekana kana kwamba wanawaheshimu manabii kwa kuwajengea makaburi, wanaiga mtazamo na matendo ya mababu zao. Hata wanataka kumuua Nabii mkuu wa Mungu. Yesu anasema kwamba Mungu atakihukumu kizazi hicho. Na jambo hilo lilitimizwa miaka 38 hivi baadaye, mwaka wa 70 W.K.

Yesu anaendelea kusema: “Ole wenu ninyi wenye ujuzi wa Sheria, kwa sababu mliuondoa ufunguo wa ujuzi. Ninyi hamkuingia, na mnawazuia wale wanaoingia!” (Luka 11:52) Watu hao ambao wanapaswa kufundisha maana ya Neno la Mungu, wanawanyima watu fursa ya kulijua na kulielewa Neno la Mungu.

Mafarisayo na waandishi wanatendaje? Yesu anapoondoka, wanaanza kumpinga kwa hasira na kumshambulia kwa maswali. Hawaulizi wakiwa na nia ya kujifunza. Badala yake, wanataka kumtega Yesu aseme jambo ambalo wanaweza kumshtaki ili akamatwe.