Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 76

Anakula Pamoja na Mufarisayo

Anakula Pamoja na Mufarisayo

LUKA 11:37-54

  • YESU ANALAUMU WAFARISAYO WANAFIKI

Wakati iko katika Yudea, Yesu anakubali mualiko wa Mufarisayo mumoja wa kula chakula kwake. Inawezekana ni wakati wa muchana. (Luka 11:37, 38; linganisha na Luka 14:12.) Mbele ya kula, Wafarisayo wananawa mikono mupaka kwenye kiwiko kulingana na desturi yao. Lakini Yesu hafanye hivyo. (Matayo 15:1, 2) Kufanya hivyo hakutavunja Sheria ya Mungu, na hata hivyo ni jambo lenye Mungu haombe watu wafanye.

Mufarisayo huyo anashangaa kuona vile Yesu hafuate desturi hiyo. Yesu anatambua jambo hilo na kusema hivi: “Sasa ninyi Wafarisayo, munasafisha upande wa inje wa kikombe na sahani, lakini ndani ninyi mumejaa pupa na uovu. Ninyi wapumbavu! Ule mwenye alifanya upande wa inje alifanya pia upande wa ndani, haiko vile?”—Luka 11:39, 40.

Kunawa mikono mbele ya kula haiko tatizo, lakini unafiki wa kidini ndilo tatizo. Wafarisayo na watu wengine wenye wananawa mikono yao kulingana na desturi wanashindwa kuondoa mambo ya mubaya yenye kuwa katika mioyo yao. Kwa hiyo Yesu anawashauria hivi: “Mutoe vitu vya ndani kuwa zawadi za rehema, na angalia! Kila kitu chenye kuwahusu kitakuwa safi.” (Luka 11:41) Ni kweli kabisa! Kutoa kunapaswa kufanywa kwa upendo, hapana kutoa ili wengine watuone kuwa sisi ni watu wenye kufanya mambo yenye kuwa sawa.

Haiko kusema kuwa wanaume hao hawatowake. Yesu anasema hivi: “Munatoa sehemu moja ya kumi (1/10) ya munanaa na muchicha na ya kila mboga ya majani, lakini munapuuza haki na upendo wa Mungu! Mambo haya, mulipaswa kuyafanya, bila kupuuza yale mengine.” (Luka 11:42) Sheria ya Mungu iliomba kutoa sehemu moja ya kumi ya mazao ya shamba. (Kumbukumbu la Torati 14:22) Matoleo hayo yalitia ndani munanaa na muchicha, majani ao mimea yenye ilitumiwa ili kufanya chakula kikuwe kitamu. Wafarisayo walijikaza sana kulipa sehemu moja ya kumi ya majani hayo, lakini walifanya nini kuhusu kuonyesha sifa za maana zenye kuombwa na Sheria, kama vile haki na kuwa wenye kiasi mbele ya Mungu?—Mika 6:8.

Yesu anaendelea kusema hivi: “Ole kwenu Wafarisayo, kwa sababu munapenda viti vya mbele katika masinagogi na salamu katika masoko! Ole kwenu, kwa sababu ninyi ni kama makaburi yenye hayaonekane muzuri, yenye watu wanatembea juu yake bila kujua!” (Luka 11:43, 44) Ndiyo, watu wangeweza kujikwaa kwenye makaburi hayo na kuwa watu wenye hawako safi kulingana na desturi. Yesu anatumia jambo hilo ili kukazia kuwa uchafu wa Wafarisayo hauonekane kwa inje.—Matayo 23:27.

Mwanaume mumoja mwenye kujua sana Sheria ya Mungu ananungunika na kusema: “Mwalimu, wakati unasema mambo hayo, unatutukana sisi pia.” Hata hivyo, watu hao wanapaswa kujua kwamba wako wanashindwa kusaidia watu. Kwa hiyo Yesu anasema hivi: “Ole kwenu pia ninyi wenye kujua sana Sheria, kwa sababu munabebesha watu mizigo mizito, lakini ninyi wenyewe hamuguse mizigo hiyo hata kwa kidole chenu kimoja! “Ole kwenu, kwa sababu munajenga makaburi ya manabii, lakini mababu zenu waliwaua!”—Luka 11:45-47.

Mizigo yenye Yesu anazungumuzia ni desturi zenye Wafarisayo wanaomba watu wafuate na namna yao ya kufasiria Sheria. Wanaume hao hawafanye maisha ya watu yakuwe mwepesi. Lakini, wanakaza watu wote wafuate mambo yenye ni mizigo mizito. Mababu zao waliua manabii wa Mungu, kuanzia Abeli na kuendelea. Sasa wao, wenye wanafanya ionekane kuwa wako wanaheshimia manabii kwa kuwajengea makaburi, wanaiga tabia na matendo ya mababu zao. Wako hata wanatafuta kuua Nabii mukubwa wa Mungu. Yesu alisema kuwa kizazi hiki kitatoa hesabu mbele ya Mungu. Na jambo hilo lilitimia kisha miaka karibu 38, ni kusema, katika mwaka wa 70 kisha kuzaliwa kwa Yesu.

Yesu anaendelea hivi: “Ole kwenu ninyi wenye kujua sana Sheria, kwa sababu mulitosha ufunguo wa ujuzi. Ninyi wenyewe hamukuingia, na wale wenye kuingia, munawazuia!” (Luka 11:52) Wanaume hao, wenye wanapaswa kusaidia watu waelewe maana ya Neno la Mungu, wao ndio wako wanazuia watu kupata nafasi ya kulijua na kulielewa.

Wafarisayo na waandishi wanatenda namna gani? Wakati Yesu anaanza kuondoka, wanaanza kumupinga na kumusumbua na maulizo. Hawako wanauliza juu wanapenda kujua. Lakini, wanapenda kumutega Yesu ili aseme jambo fulani lenye litawapatia nafasi ya kumukamata.