Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 80

Mchungaji Mwema na Mazizi ya Kondoo

Mchungaji Mwema na Mazizi ya Kondoo

YOHANA 10:1-21

  • YESU AZUNGUMZIA KUHUSU MCHUNGAJI MWEMA NA MAZIZI YA KONDOO

Yesu anapoendelea kufundisha huko Yudea, sasa anazungumzia jambo ambalo wasikilizaji wake wanaweza kulielewa kwa urahisi—kondoo na mazizi. Lakini analizungumzia kwa kutumia mfano. Huenda Wayahudi wanakumbuka maneno haya ya Daudi: “Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote. Hunilaza katika malisho yenye majani mengi.” (Zaburi 23:1, 2) Katika zaburi nyingine, Daudi alilihimiza hivi taifa hilo: “Na tupige magoti mbele za Yehova Muumba wetu. Kwa maana yeye ni Mungu wetu, na sisi ni watu wa malisho yake.” (Zaburi 95:6, 7) Naam, chini ya Sheria, kwa muda mrefu Waisraeli walilinganishwa na kundi la kondoo.

“Kondoo” hao wamekuwa katika “zizi” katika maana ya kwamba walizaliwa chini ya agano la Sheria ya Musa. Sheria ilikuwa kama ukuta, uliowatenganisha na matendo maovu ya watu ambao hawakuwa katika mpango huo. Hata hivyo, baadhi ya Waisraeli, walilitendea vibaya kundi la Mungu. Yesu anasema: “Kwa kweli ninawaambia, mtu asiyeingia katika zizi la kondoo kupitia mlango, bali anapanda na kuingia kupitia njia nyingine, ni mwizi na mporaji. Lakini yule anayeingia kupitia mlango ndiye mchungaji wa kondoo.”—Yohana 10:1, 2.

Huenda watu wakafikiri kuhusu watu waliodai kwamba wao ni Masihi, au Kristo. Hao ni kama wezi na waporaji. Watu hawapaswi kuwafuata wadanganyifu hao. Badala yake, wanapaswa kumfuata “mchungaji wa kondo,” ambaye Yesu anasema hivi kumhusu:

“Mlinzi wa mlango humfungulia, nao kondoo huisikiliza sauti yake. Naye huwaita kondoo wake kwa majina na kuwatoa nje. Baada ya kuwatoa kondoo wake wote nje, yeye huwatangulia, nao kondoo humfuata kwa sababu wanaijua sauti yake. Hawatamfuata mgeni kamwe bali watamkimbia, kwa sababu hawajui sauti ya wageni.”—Yohana 10:3-5.

Hapo awali, Yohana Mbatizaji, aliye kama mlinzi wa mlango, alimtambulisha Yesu kuwa yule ambaye kondoo wa mfano chini ya Sheria wanapaswa kumfuata. Na baadhi ya kondoo, huko Galilaya na huku Yudea wameitambua sauti ya Yesu. ‘Atawatoa nje’ kwenda wapi? Na wanapomfuata kutakuwa na matokeo gani? Baadhi ya watu wanaosikiliza mfano huo huenda wakashangaa, kwa sababu ‘hawaelewi anachowaambia.’—Yohana 10:6.

Yesu anafafanua hivi: “Kwa kweli ninawaambia, mimi ndiye mlango wa kondoo. Wote ambao wamekuja wakidai kwamba wao ni mimi, ni wezi na waporaji; lakini kondoo hawakuwasikiliza. Mimi ndiye mlango; yeyote anayeingia kupitia kwangu ataokolewa, naye ataingia na kutoka na kupata malisho.”—Yohana 10:7-9.

Ni wazi kwamba Yesu anazungumza kuhusu jambo jipya. Wasikilizaji wake wanajua kwamba yeye si mlango wa kuelekea kwenye agano la Sheria, ambalo limekuwepo kwa karne nyingi. Basi, lazima awe anamaanisha kwamba kondoo ‘anaowatoa nje’ wanapaswa kuingia kwenye zizi lingine. Matokeo yatakuwa nini?

Akifafanua zaidi kuhusu jukumu lake, Yesu anasema: “Nimekuja ili wapate uzima na waupate kwa wingi. Mimi ndiye mchungaji mwema; mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo.” (Yohana 10:10, 11) Hapo awali, Yesu alikuwa amewafariji wanafunzi wake kwa kusema: “Msiogope, ninyi kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa Ufalme.” (Luka 12:32) Kwa kweli, wale wanaofanyiza “kundi dogo” ndio ambao Yesu atawaingiza katika zizi jipya, ili “wapate uzima na waupate kwa wingi.” Ni baraka kubwa kuwa katika kundi hilo!

Hata hivyo, Yesu hamalizii mazungumzo hayo hapo. Anasema: “Nina kondoo wengine, ambao si wa zizi hili; hao pia nitawaleta, nao wataisikiliza sauti yangu, nao watakuwa kundi moja, mchungaji mmoja.” (Yohana 10:16) “Kondoo [hao] wengine” si “wa zizi hili.” Hivyo basi, lazima wawe wa zizi lingine tofauti na “kundi dogo” ambao wataurithi Ufalme. Mazizi hayo mawili ya kondoo yana matarajio tofauti. Lakini kondoo kutoka mazizi yote mawili watafaidika kutokana na jukumu la Yesu. Yesu anasema: “Kwa sababu hiyo, Baba ananipenda, kwa kuwa ninautoa uhai wangu.”—Yohana 10:17.

Wengi katika umati wanasema hivi: “Ana roho mwovu naye ana wazimu.” Lakini wengine wanaonyesha kwamba wanasikiliza kwa makini na wanataka kumfuata Mchungaji Mwema. Wanasema: “Haya si maneno ya mtu mwenye roho mwovu. Je, roho mwovu anaweza kufungua macho ya vipofu?” (Yohana 10:20, 21) Ni wazi kwamba wanarejelea jinsi hapo awali Yesu alivyomponya mtu aliyezaliwa kipofu.