Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 85

Kushangilia Mtenda Dhambi Anapotubu

Kushangilia Mtenda Dhambi Anapotubu

LUKA 15:1-10

  • MFANO WA KONDOO ALIYEPOTEA NA MFANO WA SARAFU ILIYOPOTEA

  • MALAIKA MBINGUNI HUSHANGILIA

Yesu amekazia umuhimu wa unyenyekevu pindi mbalimbali katika huduma yake. (Luka 14:8-11) Angependa kupata wanaume na wanawake wanaotamani kumtumikia Mungu kwa unyenyekevu. Kufikia sasa, huenda baadhi yao bado ni watenda dhambi sugu.

Mafarisayo na waandishi wanatambua kwamba watu hao—ambao wanawaona kuwa hawafai—wanampenda Yesu na ujumbe wake. Wanalalamika hivi: “Mtu huyu huwakaribisha watenda dhambi na kula pamoja nao.” (Luka 15:2) Mafarisayo na waandishi wanajiona kuwa bora na wanawatendea watu wa kawaida kama mavumbi kwenye miguu yao. Wanapowataja watu hao, viongozi hao hutumia neno la Kiebrania ‛am ha·’aʹrets, yaani, “watu wa ardhi” ili kuonyesha jinsi wanavyowadharau.

Tofauti nao, Yesu anawatendea watu wote kwa heshima, fadhili, na huruma. Basi watu wengi wa hali ya chini, kutia ndani baadhi yao wanaojulikana kuwa watenda dhambi, wanatamani kumsikiliza Yesu. Hata hivyo, Yesu anahisije kuhusu lawama anazopata kwa sababu ya kuwasaidia watu hao wa hali ya chini, naye anakabilianaje nazo?

Jibu linakuwa wazi anapotoa mfano wenye kugusa moyo, unaofanana na ule aliokuwa ametoa hapo awali huko Kapernaumu. (Mathayo 18:12-14) Yesu anazungumzia mambo kana kwamba Mafarisayo ni waadilifu na wako salama katika zizi la Mungu. Tofauti na hilo, anawazungumzia watu wa hali ya chini kama watu walioacha njia na waliopotea. Yesu anasema:

“Ikiwa mmoja wenu ana kondoo 100, naye ampoteze mmoja, je, hatawaacha wale 99 nyikani aende kumtafuta yule aliyepotea mpaka ampate? Na baada ya kumpata, anambeba mabegani na kushangilia. Na anapofika nyumbani anawaita rafiki zake na jirani zake, na kuwaambia, ‘Shangilieni pamoja nami, kwa kuwa nimempata kondoo wangu aliyekuwa amepotea.’”—Luka 15:4-6.

Yesu anafafanuaje mfano huo? Anaeleza hivi: “Vivyo hivyo, ninawaambia kwamba kutakuwa na shangwe nyingi mbinguni kwa sababu ya mtenda dhambi mmoja anayetubu kuliko kwa waadilifu 99 ambao hawahitaji kutubu.”—Luka 15:7.

Yesu anapotaja kutubu, jambo hilo linawashangaza Mafarisayo. Wanajiona kuwa waadilifu na wanafikiri kwamba hawahitaji kutubu. Baadhi yao walipomshutumu Yesu miaka kadhaa mapema kwa kula pamoja na wakusanya kodi na watenda dhambi, aliwajibu hivi: “Sikuja kuwaita waadilifu, bali watenda dhambi.” (Marko 2:15-17) Mafarisayo wanaojiona kuwa waadilifu hawatambui kwamba wanahitaji kutubu, na hivyo hawaleti shangwe yoyote mbinguni. Hali inakuwa tofauti watenda dhambi wanapotubu kikweli.

Ili kukazia kwamba watenda dhambi wanapotubu kunakuwa na shangwe kubwa mbinguni, Yesu anatoa mfano mwingine, unaomhusu mama nyumbani: “Mwanamke aliye na sarafu kumi za drakma akipoteza drakma moja, je, hatawasha taa, afagie nyumba yake na kuitafuta kwa makini mpaka aipate? Na baada ya kuipata, anawaita rafiki zake na jirani zake na kuwaambia, ‘Shangilieni pamoja nami, kwa kuwa nimeipata sarafu ya drakma niliyokuwa nimepoteza.’”—Luka 15:8, 9.

Ufafanuzi ambao Yesu anatoa unafanana na ule aliotoa baada ya kusimulia mfano wa kondoo aliyepotea. Anasema: “Vivyo hivyo, ninawaambia kwamba malaika wa Mungu hushangilia mtenda dhambi mmoja anapotubu.”—Luka 15:10.

Hebu wazia, malaika wa Mungu wanapendezwa sana na watenda dhambi wanaotubu! Jambo hilo ni la pekee kwa sababu watenda dhambi wanaotubu na kupata nafasi katika Ufalme wa mbinguni wa Mungu watakuwa na cheo kikubwa kuliko malaika wenyewe! (1 Wakorintho 6:2, 3) Hata hivyo malaika hawana wivu. Basi tunapaswa kuhisije mtenda dhambi anapotubu kikweli na kumrudia Mungu?