Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 90

“Ufufuo na Uzima”

“Ufufuo na Uzima”

YOHANA 11:17-37

  • YESU ANAWASILI BAADA YA KIFO CHA LAZARO

  • “UFUFUO NA UZIMA”

Baada ya kutoka Perea, Yesu anafika kwenye ukingo wa kijiji cha Bethania, kilicho karibu kilomita tatu upande wa mashariki wa Yerusalemu. Maria na Martha, dada za Lazaro, wanaomboleza kifo cha Lazaro. Watu wengi wamekuja kuwafariji.

Kisha mtu fulani anamwambia Martha kwamba Yesu anakaribia, naye anakimbia kwenda kumlaki. Martha anamwambia Yesu jambo ambalo huenda yeye na dada yake wamekuwa wakifikiria kwa siku nne: “Bwana, kama ungekuwa hapa ndugu yangu hangekufa.” Hata hivyo, si kwamba hana imani. Martha anasema: “Ninajua kwamba chochote utakachomwomba Mungu, Mungu atakupa.” (Yohana 11:21, 22) Anahisi kwamba bado Yesu anaweza kumsaidia ndugu yake.

Yesu anajibu hivi: “Ndugu yako atafufuka.” Martha anafikiri kwamba anazungumzia ufufuo wa wakati ujao duniani, tumaini ambalo Abrahamu na wengine walikuwa nalo. Naye anaonyesha anaamini kwamba jambo hilo litatendekea anaposema: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.”—Yohana 11:23, 24.

Lakini je, inawezekana kwamba Yesu anaweza kuleta kitulizo pindi hii? Anamkumbusha Martha kwamba Mungu amempa mamlaka juu ya kifo anaposema: “Yule anayeniamini, hata akifa, ataishi tena; na kila mtu aliye hai na ananiamini hatakufa kamwe.”—Yohana 11:25, 26.

Yesu hamaanishi kwamba wanafunzi wake walio hai wakati huo hawatakufa kamwe. Hata yeye lazima afe, kama alivyowaambia mitume wake. (Mathayo 16:21; 17:22, 23) Yesu anakazia kwamba mtu anayemwamini anaweza kupata uzima wa milele. Kwa watu wengi, uhai kama huo utapatikana kupitia ufufuo. Hata hivyo, mfumo huu utakapofika mwisho inawezekana kwamba watu waaminifu walio hai hawatakufa kamwe. Vyovyote vile, kila mtu anayemwamini anaweza kuwa na uhakika kwamba hatakufa kamwe milele.

Lakini je, Yesu ambaye ametoka kusema, “Mimi ndiye ufufuo na uzima,” anaweza kumsaidia Lazaro, ambaye amekufa kwa siku nne? Yesu anamuuliza Martha: “Je, unaamini hilo?” Anajibu: “Ndiyo Bwana, ninaamini kwamba wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu, yule anayekuja ulimwenguni.” Akiwa na imani kwamba Yesu anaweza kufanya jambo fulani siku hiyo, Martha anakimbia nyumbani na kumwambia hivi dada yake faraghani: “Mwalimu amefika naye anakuita.” (Yohana 11:25-28) Papo hapo, Maria anatoka ndani ya nyumba kisha watu wengine wanamfuata, wakifikiri kwamba anaenda kwenye kaburi la Lazaro.

Badala yake, Maria anaenda kwa Yesu, anaanguka miguuni pake akilia, kisha anarudia maneno ambayo dada yake alisema: “Bwana, kama ungekuwa hapa, ndugu yangu hangekufa.” Baada ya kuona Maria na umati ukilia, Yesu anaugua, anataabika, na hata anatokwa na machozi. Jambo hilo linawagusa moyo watu wanaotazama. Lakini baadhi yao wanauliza: ‘Ikiwa Yesu alimfungua macho yule kipofu, je, hangeweza kuzuia huyu asife?’—Yohana 11:32, 37.