Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 100

Mfano wa Mina Kumi

Mfano wa Mina Kumi

LUKA 19:11-28

  • MFANO WA YESU WA MINA KUMI

Ingawa Yesu anaelekea Yerusalemu, huenda bado yuko nyumbani kwa Zakayo akiwa pamoja na wanafunzi wake. Wanaamini kwamba “Ufalme wa Mungu” utasimamishwa hivi karibuni Yesu akiwa Mfalme wake. (Luka 19:11) Wanaelewa jambo hilo vibaya, kama tu wanavyokosa kuelewa kwamba lazima Yesu afe. Basi anatoa mfano ili kuwasaidia kuelewa kwamba bado Ufalme uko mbali.

Anasema: “Mtu fulani wa familia mashuhuri alitaka kusafiri kwenda nchi ya mbali ili apokee mamlaka ya kifalme kisha arudi.” (Luka 19:12) Safari kama hiyo inaweza kuchukua muda mrefu. Ni wazi kwamba Yesu ndiye ‘mtu wa familia mashuhuri’ anayesafiri kwenda “nchi ya mbali,” yaani, mbinguni, ambako Baba yake atampa mamlaka ya kifalme.

Katika mfano huo, kabla yule ‘mtu wa familia mashuhuri’ hajaondoka, anawaita watumwa kumi na kumpa kila mmoja wao mina ya fedha na kuwaambia: “Fanyeni nazo biashara mpaka nitakaporudi.” (Luka 19:13) Kihalisi, mina za fedha ni kiasi fulani cha pesa zenye thamani. Mina moja inalingana na mshahara wa miezi mitatu wa mtu anayefanya kazi shambani.

Huenda wanafunzi wakatambua kwamba wao ni kama wale watumwa kumi katika ule mfano, kwa maana hapo awali Yesu alikuwa amewafananisha na wavunaji. (Mathayo 9:35-38) Bila shaka hajawaagiza walete mavuno ya nafaka. Badala yake, wanahitaji kuvuna wanafunzi wengine ambao wanaweza kupata nafasi katika Ufalme wa Mungu. Wanafunzi wanatumia kila kitu walicho nacho ili kutokeza warithi wengine wa Ufalme.

Yesu anafunua mambo gani mengine katika mfano huo? Anasema kwamba raia “walimchukia [yule mtu wa familia mashuhuri] nao wakatuma mabalozi wamfuate na kusema, ‘Hatutaki mtu huyu awe mfalme wetu.’” (Luka 19:14) Wanafunzi wanajua kwamba Wayahudi hawamkubali Yesu—hata baadhi yao wanataka kumuua. Baada ya Yesu kufa na kwenda mbinguni, kwa ujumla Wayahudi wanaonyesha maoni yao kumhusu kwa kuwatesa wanafunzi wake. Wapinzani hao wanaonyesha wazi kwamba hawataki Yesu awe Mfalme wao.—Yohana 19:15, 16; Matendo 4:13-18; 5:40.

Namna gani wale watumwa kumi, wanatumiaje mina zao hadi yule ‘mtu wa familia mashuhuri’ anapopokea “mamlaka ya kifalme” na kurudi? Yesu anaeleza: “Mwishowe aliporudi baada ya kupokea mamlaka ya kifalme, aliwaita watumwa aliokuwa amewapa pesa, ili ajue faida waliyopata kwa kufanya biashara. Basi wa kwanza akaja na kusema, ‘Bwana, mina yako moja imeleta faida ya mina kumi.’ Akamwambia, ‘Umefanya vema, mtumwa mwema! Kwa kuwa umekuwa mwaminifu katika jambo dogo sana, utatawala majiji kumi.’ Kisha wa pili akaja na kusema, ‘Bwana, mina yako moja, imeleta faida ya mina tano.’ Vilevile akamwambia, ‘Wewe pia, utatawala majiji matano.’”—Luka 19:15-19.

Ikiwa wanafunzi wanaelewa kwamba wao ni kama wale watumwa wanaotumia kila kitu walicho nacho ili kufanya wanafunzi zaidi, wanaweza kuwa na uhakika kwamba Yesu atafurahi. Nao wanaweza kuwa na uhakika atawathawabisha kwa sababu ya bidii yao. Bila shaka, wanafunzi wote wa Yesu hawana hali, fursa, na uwezo unaolingana. Hata hivyo, Yesu ambaye anapokea “mamlaka ya kifalme,” atatambua na kubariki jitihada zao za ushikamanifu za kufanya wanafunzi.—Mathayo 28:19, 20.

Hata hivyo, ona tofauti anayoonyesha Yesu anapomalizia mfano wake: “Lakini [mtumwa] mwingine akaja, akasema, ‘Bwana, hii hapa mina yako, niliifunga kwa kitambaa nikaificha. Nilikuogopa kwa sababu wewe ni mtu mkali; wewe huchukua kile ambacho hukuweka akiba, na kuvuna kile ambacho hukupanda.’ Akamwambia, ‘Ninakuhukumu kwa maneno yako mwenyewe, mtumwa mwovu. Ulijua, sivyo, kwamba mimi ni mtu mkali, ambaye huchukua kile ambacho sikuweka akiba na kuvuna kile ambacho sikupanda? Basi kwa nini hukuziweka pesa zangu benki? Kisha baada ya kurudi, ningezichukua zikiwa na faida.’ “Ndipo akawaambia wale waliokuwa wamesimama hapo, ‘Chukueni mina hiyo mkampe yule aliye na mina kumi.’”—Luka 19:20-24.

Kwa sababu hakufanya kazi ili kuongeza mali ya ufalme wa bwana wake, mtumwa huyo anapata hasara. Mitume wanatazamia kwamba Yesu atatawala katika Ufalme wa Mungu. Basi, kutokana na mambo anayosema kumhusu mtumwa huyo wa mwisho, inaelekea wanatambua kwamba ikiwa hawatakuwa na bidii, hawatapata nafasi katika Ufalme huo.

Bila shaka, maneno ya Yesu yanawachochea wanafunzi washikamanifu kuongeza bidii. Anamalizia hivi: “Ninawaambia, kila mtu aliye na kitu, ataongezewa, lakini yule asiye na kitu, hata kile alicho nacho kitachukuliwa.” Pia, anasema kwamba maadui wake ambao hawakutaka awe “mfalme wao,” watauawa. Kisha Yesu anaendelea na safari yake ya kwenda Yerusalemu.—Luka 19:26-28..