Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 106

Anatoa Mifano Mbili Kuhusu Mashamba ya Mizabibu

Anatoa Mifano Mbili Kuhusu Mashamba ya Mizabibu

MATAYO 21:28-46 MARKO 12:1-12 LUKA 20:9-19

  • MUFANO KUHUSU WATOTO WAWILI

  • MUFANO KUHUSU WALIMAJI WA SHAMBA LA MIZABIBU

Kwenye hekalu, Yesu anatoka tu kuwavuruga wakubwa wa makuhani na wazee wa watu, wenye walimutega kwa kumuuliza ni kwa mamlaka ya nani anafanya mambo. Jibu la Yesu linawanyamazisha. Kisha anatoa mufano wenye kuonyesha namna wako kabisa.

Yesu anaeleza: “Mutu fulani alikuwa na watoto wawili. Akamuendea wa kwanza, akamuambia, ‘Mutoto wangu, leo uende kufanya kazi katika shamba la mizabibu.’ Huyu akamujibu na kusema, ‘Sitaenda,’ lakini kisha, akasikitika na akaenda. Akamukaribia wa pili na kumuambia jambo lilelile. Huyo akajibu, ‘Nitaenda, Bwana,’ lakini hakuenda. Kati ya hao wawili, ni nani alifanya mapenzi ya baba yake?” (Matayo 21:28-31) Jibu liko wazi: ni mutoto wa kwanza mwenye mwishowe alifanya mapenzi ya baba yake.

Basi Yesu anaambia wale wenye kumupinga: “Kwa kweli ninawaambia ninyi kwamba wakusanya-kodi na makahaba wanawatangulia ninyi kuingia katika Ufalme wa Mungu.” Mbele, wakusanya-kodi na makahaba hawakumutumikia Mungu. Lakini, kama ule mutoto wa kwanza, walifikia kutubu na sasa wanamutumikia. Tofauti na wao, viongozi wa dini wako kama ule mutoto wa pili, wanasema kuwa wao ni watu wenye kumutumikia Mungu, lakini wanashindwa kufanya hivyo kabisa. Yesu anawaambia: “Yohana alikuja kwenu na kuwaonyesha mambo yenye kuwa sawa, lakini hamukumuamini. Hata hivyo, wakusanya-kodi na makahaba walimuamini, na hata kisha ninyi kuona jambo hilo, hamukusikitika ili mumuamini.”—Matayo 21:31, 32.

Yesu analeta mufano mwengine tena. Mara hii, Yesu anaonyesha kwamba viongozi wa dini hawashindwe tu kumutumikia Mungu, lakini wao ni waovu. Yesu anaeleza: “Mutu fulani alipanda shamba la mizabibu na kulizungushia ukuta, akachimba shimo kwa ajili ya kikamulio cha divai na akasimamisha munara; kisha akalipangisha kwa walimaji na akasafiri kuenda katika inchi ingine. Wakati kipindi chake kilifika akatuma mutumwa kwa walimaji ili akusanye kutoka kwao sehemu fulani ya matunda ya shamba la mizabibu. Lakini wakamukamata, wakamupiga, na wakamufukuza mikono wazi. Tena akatuma mutumwa mwingine kwao, na huyo wakamupiga kwenye kichwa na kumukosea heshima. Na akatuma mwingine, na huyo wakamuua, na wengine wengi, wamoja wao wakawapiga na wengine wakawaua.”—Marko 12:1-5.

Je, watu wenye wanasikiliza Yesu wataelewa mufano huo? Pengine wanakumbuka maneno haya ya Isaya: “Shamba la mizabibu la Yehova wa majeshi ni nyumba ya Israeli; watu wa Yuda ndilo shamba lenye alikuwa anapenda sana. Aliendelea kutumaini haki, lakini angalia! kulikuwa ukosefu wa haki.” (Isaya 5:7) Ni kama tu mufano wa Yesu. Mwenye shamba ni Yehova, na shamba la mizabibu ni taifa la Israeli, lenye kukingwa na kulindwa na Sheria ya Mungu. Yehova alituma manabii ili kufundisha watu wake na kuwasaidia wazae matunda ya muzuri.

Lakini, “walimaji” walitesa na kuua “watumwa” wenye walitumwa kwao. Yesu anasema: “Mutu mumoja [mwenye shamba la mizabibu] mwenye alibakia naye alikuwa mwana wake mupendwa. Akamutuma wa mwisho, akisema: ‘Watamuheshimia mwana wangu.’ Lakini wale walimaji wakaambiana, ‘Huyu ndiye muriti. Mukuje, tumuue, na uriti utakuwa wetu. Basi wakamukamata na kumuua.”—Marko 12:6-8.

Sasa Yesu anauliza: “Mwenye shamba la mizabibu atafanya nini?” (Marko 12:9) Viongozi wa dini wanajibu: “Kwa sababu ni waovu, ataleta uharibifu mubaya juu yao na kupangisha shamba hilo la mizabibu kwa walimaji wengine, wenye watamupatia matunda kwa wakati wake.”—Matayo 21:41.

Kwa hiyo, bila kujua wanatangaza hukumu juu yao wenyewe, kwa sababu wako kati ya “walimaji” wa “shamba la mizabibu” la Yehova, ni kusema, taifa la Israeli. Matunda yenye Yehova anatazamia kwa wale walimaji inatia ndani imani katika Mwana wake, Masiya. Yesu anawaangalia viongozi hao wa dini na kuwaambia: “Je, hamujasoma hata siku moja andiko hili: ‘Jiwe lenye wajenzi walikataa ndilo limekuwa jiwe kubwa la pembe. Hili limetoka kwa Yehova, na ni la ajabu katika macho yetu’?” (Marko 12:10, 11) Kisha Yesu anawaambia waziwazi hivi: “Ndiyo sababu ninawaambia ninyi, Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.”—Matayo 21:43.

Waandishi na wakubwa wa makuhani wanatambua kama Yesu “alisema mufano huo juu yao.” (Luka 20:19) Sasa kuliko wakati mwengine wowote, wanataka kumuua mwenye kuwa na haki ya kuwa “muriti.” Lakini wanaogopa watu, wenye wanamuona Yesu kuwa nabii, kwa hiyo hawajaribu kumuua wakati huo.